Je! Wewe Una Akili ya Kristo?
“Sasa Mungu anayetoa uvumilivu na faraja na awajalie mwe miongoni mwenu na mwelekeo wa akili ule ule aliokuwa nao Kristo Yesu.”—WARUMI 15:5, NW.
1. Ikiwa mtu anadai kuwa ni Mkristo, ni maulizo gani yanayotaka jibu?
WATU zaidi ya bilioni moja katika sehemu zote za ulimwengu wanasemwa kuwa ni Wakristo. Hiyo inatokeza wazo gani? Kwamba angalau kwa jina, wao wanaamini Yesu Kristo na kudai kuwa ni wafuasi, au wanafunzi wake. (Mathayo 10:24, 25) Lakini ni nini kinachohitajiwa ili kufuata mfano wa Kristo, au kielelezo cha maisha? Kwa wazi, inakupasa umjue yeye. Je! wewe ni mtu anayejua kweli kweli Yesu wa Nazareti? Je! wewe una wazo sahihi juu ya yeye alikuwa mtu wa aina gani alipokuwa angali hapa duniani? Au juu ya jinsi alivyoitikia watu katika hali tofauti-tofauti? Je! wewe una “akili ya Kristo”?—1 Wakorintho 2:16; Waefeso 4:13, NW.
2, 3. Tunaweza kupataje kuijua akili ya Kristo?
2 Tunaweza kupataje kujua mtu aliyeishi karibu miaka elfu mbili iliyopita na ambaye maisha yake ya peupe yalikuwa na urefu upatao miaka mitatu na nusu? Katika habari ya Yesu kuna historia nne zenye kutegemeka juu ya maisha yake ambazo zinasaidia kukuza picha ya akilini juu ya yeye alikuwa mtu wa aina gani. Kwa kusoma kwa uangalifu masimulizi hayo manne ya Injili, tunaweza pia kufahamu kielelezo cha kufikiri kilichosukuma vitendo vyake. Kwa sababu hiyo, ili mtu awe Mkristo wa kweli badala ya kuwa wa jina tu, ni jambo gani linalohitajiwa kabisa? Yesu alilieleza hivi: “Hii ndiyo maana ya uzima wa milele, wapate maarifa ya kukujua wewe, Mungu wa kweli mmoja tu, na ya yeye uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3, NW; 2 Petro 3:18.
3 Hivyo, kila Mkristo anapaswa awe na maarifa na ufahamu wenye kina kirefu juu ya Baba, Yehova, na juu ya maisha na mafundisho ya Mwana, Kristo Yesu. Haitoshi mtu kujiita shahidi Mkristo wa Yehova. Ili tuwe na akili ya Kristo, ni lazima kwa ukawaida tujaze akili zetu ufahamu juu ya maisha na mfano wa Yesu. Hiyo inamaanisha tunahitaji funzo la ukawaida na la kikweli juu ya Maandiko pamoja na misaada ya kujifunzia Biblia inayosaidia kuelewesha maana na habari zinazozunguka wazo. Inahitaji pia kuwa na hali ya akilini inayofaa ili tuweze kufahamu na kukubali daraka la Kristo katika makusudi ya Mungu.—Yohana 5:39-47; Mathayo 24:45-47.
Mwanamume Mwenye Hisia
4. Yesu alikuwa mwanamume wa aina gani?
4 Yesu, mwanamume mtendaji mwenye afya nzuri, alifanya huduma yake alipokuwa katika mwanzo-mwanzo wa umri wa miaka 30. (Luka 3:23) Lakini yeye alikuwa mwanamume wa aina gani? Je! yeye alikuwa mtu asiyejali wengine na asiyetaka ukaribu nao? Kwa kinyume, yeye akiwa ni Myahudi wa Mashariki ya Kati, alikuwa mwenye kueleza maoni yake. Yeye hakuwa mtu wa kufungia maoni yake kwa ndani na kuelekeza mawazo yake yawe ya ubinafsi tu. Yeye alidhihirisha peupe namna nyingi za maoni ya moyoni ya kibinadamu, kuanzia masikitiko na huruma mpaka uchungu wenye uadilifu na hasira.—Marko 6:34; Mathayo 23:13-36.
5. Yesu aliitikiaje aliposikia juu ya kifo cha Lazaro?
5 Kwa mfano, Yesu aliitikiaje wakati alipokuta Martha na Mariamu wakilia machozi juu ya kupoteza Lazaro ndugu yao? Usimulizi wa Yohana unatuambia hivi: “Yeye alivutwa kindani na kwa njia yenye kuonekana, na kutaabika sana katika roho,” naye “akabubujika machozi.” (Yohana 11:33-36, The New Testament, ya William Barclay) Yeye alishiriki hisia zake pamoja na rafiki hao wa karibu. Yeye hakuona aibu kulia machozi pamoja nao. Ingawa yeye alikuwa “Mwana wa Mungu,” alifunua maoni ya kibinadamu sana aliyokuwa nayo moyoni. (Yohana 1:34) Lazima jambo hilo liwe liliwagusa sana Martha na Mariamu!—Linganisha Luka 19:41-44.
6. Kwa nini Yesu hakuwa goigoi kwa sababu alilia machozi?
6 Ijapokuwa hivyo, huenda wengine leo wakakata shauri kwamba Yesu alikuwa goigoi kwa sababu alilia machozi peupe akiwa na wanawake hao. Kwa kweli, mtungaji vitabu Mkatoliki Hilaire Belloc alimwita Yesu “goigoi.” Je! hiyo ni kweli? Je! Yesu alikuwa namna ya mtu asiyefanya kiume anayeonyeshwa mara nyingi katika picha zilizochorwa na Jumuiya ya Wakristo? Hapana, machozi si ishara ya unyonge kwa lazima. Ni kama vile jarida moja la kitiba lilivyoeleza jambo hilo: “Katazo la wonyesho unaofaa wa maoni mororo ya moyoni halipatani na kufikiri kuzuri tena lina madhara . . . Wonyesho wa maoni mororo ya moyoni, hasa kulia, ni sifa moja ambayo wanadamu ndio walio nayo kwa njia isiyo na kifani.”—Linganisha 2 Samweli 13:36-38; Yohana 11:35.
7. Ni kwa njia gani mbalimbali mfano wa Yesu wa huruma ya kibinadamu unaweza kutusaidia leo?
7 Maitikio ya Yesu kwa taabu yalikuwa ya kibinadamu na yenye huruma ya kibinadamu. Yanatusaidia sisi tuwe kama yeye na akili yake. Sisi hatufuati dude fulani la kihadithi tu lisilo na utu bali tunafuata mfano mkamilifu wa kibinadamu aliyetumwa kutoka kwa Mungu, “Mwana wa Mungu aliye hai.” (Mathayo 16:16; Yohana 3:16, 17; 6:68, 69) Huyo ni kiolezo kama nini kwa Wakristo wote leo, hasa wazee Wakristo, wanaolazimika mara nyingi kutoa faraja na kuonyesha hisia-mwenzi (kujihusisha katika shida za wengine) katika nyakati za kufiwa na kukazwa! Ndiyo, kuwa na akili na moyo wa Yesu katika pindi hizo kunaweza kufanyiza tofauti kubwa.—1 Wathesalonike 2:7, 8.
Mwanamume Mjasiri wa Vitendo
8. Yesu alionyeshaje ushujaa na kitendo la ujasiri?
8 Yesu alijionyesha pia kuwa mwanamume mwenye kufuata kwa ushujaa mambo aliyosadiki na mwenye msukumo mwingi wa vitendo. Kwa mfano, katika pindi mbili yeye aliwafukuza kwa jitihada nyingi wauzaji mifugo na wabadilishaji fedha watoke hekaluni. (Marko 11:15-17; Yohana 2:13-17) Yeye hakusita pia kufunua peupe unafiki wa waandishi na Mafarisayo wenye kujionyesha kuwa waadilifu. Katika shutumu lake la ujasiri, yeye alionya hivi: “Ole wenu, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! kwa kuwa mmefanana na makaburi yaliyopakwa chokaa, nayo kwa nje yaonekana kuwa mazuri, bali ndani yamejaa mifupa ya wafu, na uchafu wote.” Kwa uhakika, huo haukuwa ugoigoi!—Mathayo 23:27, 28; Luka 13:14-17.
9, 10. (a) Kwa sababu gani Yesu hakutenda dhambi kwa kuonyesha ghadhabu? (b) Mfano wa Kristo unapasa uwe na matokeo gani juu ya mzee Mkristo?
9 Je! ghadhabu ya Yesu ilikuwa ushuhuda wa ukosefu wa kujiweza? Petro mwandani wa karibu wa Yesu wakati wa huduma yake, anasema hivi: “Yeye hakutenda dhambi.” (1 Petro 2:22) Mtume Paulo aliandika hivi: “Kwa kuwa hatuna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi” (Waebrania 4:15) Pana tofauti kati ya ghadhabu yenye uadilifu yenye kuongozwa vizuri na hasira isiyoongozwa vizuri.—Linganisha Mithali 14:17; Waefeso 4:26.
10 Basi, ingawa mzee Mkristo, kwa mfano hangekuwa “mwenye kuhamaki,” kwa uhakika inampasa awe na nguvu za kiadili za kuweza ‘kukaripia wale wanaopinganisha,’ hata “kwa ukali” ikihitajiwa kabisa. Ni lazima awe anastahili ‘kukaripia, kukemea, na kutia moyo.’ (Tito 1:7-13; 2 Timotheo 4:1, 2, NW) Huenda pia hali fulani zikaamsha ghadhabu yake yenye uadilifu, hasa ikiwa yeye anaona tisho lenye utovu wa adabu kwa umoja wa kundi, hali ya kiroho, au usafi wa kiadili. Kama vile Paulo alivyosema, nyakati nyingine “inahitajiwa kabisa kufunga vinywa” vya “wasemaji wasioleta faida. . . na wadanganyaji akili” ambao ‘wanapindua jamaa nzima-nzima kwa kufundisha mambo wasiopaswa ili wapate faida ya ukosefu wa unyofu.’ Katika visa hivyo, kuwa na akili ya Kristo kutasaidia wazee wawe hodari, wenye usawaziko, na wenye kukata maneno.—Ona 1 Wakorintho 5:1-5; Ufunuo 2:20-23; 3:19.
11. Ni maulizo gani yanayohusu jinsi tunavyopaswa kuiga Kristo?
11 Alipokuwa akiendelea na safari zake kupitia Galilaya, Samaria, na Yudea, Yesu alikutana na watu wa aina zote—wanaume, wanawake, watoto, wagonjwa, na wale waliomwona kuwa adui yao wa mwisho. Yeye alishughulikaje nao? Je! alijionyesha kuwa mtu wa maana na kukaa mbali na watu, au alikuwa mwenye kufikika? Je! yeye angeweza kujihusisha na matatizo na vishawishi vya watu? Je! alikuwa asiyesamehe au alikuwa mwenye rehema? Majibu kwa maulizo hayo yanahusu kwa njia fulani jinsi sisi tunavyopaswa kuiga Kristo katika vitendo na maitikio yetu wenyewe ya kila siku.—Warumi 15:5; Wafilipi 2:5.
Yesu Aliitikiaje Watoto?
12. Wafuasi pamoja na Yesu waliitikiaje watoto katika pindi moja?
12 Tunapata usimulizi wa kupendeza sana juu ya jinsi Yesu alivyotenda kuelekea watoto kwenye Marko sura ya 10, mistari 13-16 (NW). Inasema hivi: “Sasa watu wakaanza kumletea yeye watoto wadogo ili yeye awaguse hao;lakini wafuasi wakawakemea.” Usimulizi huo hausemi ni sababu gani iliyowafanya wafuasi watende kwa njia hiyo. Huo ulikuwa mwaka 33 W.K., na Yesu alikuwa safarini kwenda Galilaya kupitia Perea kwenye ile ambayo ingekuwa ndiyo huduma yake ya mwisho ya peupe katika Yerusalemu na kando-kando ya mji huo. Labda wao walikifiri kwamba Yesu alikuwa mtu wa maana mno au mwenye shughuli nyingi mno asiweze kuwajali watoto wakati huu. Hata hivyo, je! yeye mwenyewe alionyesha kwamba alikuwa mwenye shughuli nyingi mno? “Kwa kuona hivyo Yesu alikuwa na uchungu na kuwaambia [wale wafuasi]: ‘Acheni watoto wadogo wanijie; msijaribu kuwaachisha, kwa maana ufalme wa Mungu ni wa walio kama hao. . . . Na yeye akawachukua watoto katika mikono yake akaanza kuwabariki, akiweka mikono yake juu yao.”
13. Watu waliitikiaje Yesu?
13 Sasa ni jambo gani jingine tunalofundishwa na kisa hicho juu ya akili ya Kristo? Kinatoa mfano wa uthabiti aliowaonyesha wafuasi wake wenye kukosea na mwelekeo wenye huruma ya kibinadamu aliokuwa nao kwa walio wadogo kwa cheo. Yeye alifahamu ni jambo gani lililofanya wazazi wakusudie kumletea watoto wao. Wao walitaka awaguse na kuwabariki watoto wao. Na jambo hilo linatuambia nini juu ya Yesu? Kwamba watu hawakumwogopa wala hawakuwa na hofu nyingi juu yake. Yeye alikuwa rafiki wa watu, na watu walitaka kuwa pamoja naye. Hata watoto waliona starehe walipokuwa katika kuwapo kwake—naye aliona starehe alipokuwa katika kuwapo kwa watoto. Je! watu, kutia na watoto, wanastareheka katika kuwapo kwako?—Marko 1:40-42; Mathayo 20:29-34
14. Kwa habari ya kuwa wenye kufikika, ni nani hasa wanaopaswa kufuata mfano wa Yesu?
14 Yesu alionyesha shauku ya upendo mchangamfu na fadhili. (Marko 9:36, 37) Alikuwa mtu wa kukaribika na kufikika. Wewe ukiwa mfuasi wa Kristo, je! una akili yake katika jambo hilo? Waangalizi Wakristo walio katika wilaya, mizunguko, makundi, na afisi za matawi ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi katika sehemu zote za ulimwengu wangepaswa kujiuliza wenyewe hivi: Je! mimi ni mwenye kushikilia tu maoni yangu na asiyepindika? Au nafanya wengine, hata watoto, wahisi wamestarehe wakiwa pamoja nami? Je! mimi ni mwenye kufikika kweli kweli?—Mithali 12:18; Mhubiri 7:8.
Shughuli za Yesu Pamoja na Wanawake
15, 16. Yesu alikuwaje tofauti na Wayahudi wengine katika shughuli zake na wanawake?
15 Sisi wazee, watumishi, na akina ndugu katika kundi la Kikristo, je! tuna akili ya Kristo tunaposhughulika na dada zetu Wakristo na wanawake kwa ujumla? Je! Kristo, mseja, aliitikiaje chini ya hali zenye kutofautiana alipokutana na wanawake wa siku zake?
16 Katika jamii hiyo ya Kiyahudi ambamo shughuli zilitawalwa na wanaume, Yesu alikuwa mwalimu asiye wa kawaida katika jambo la kwamba yeye alikuwa na nia ya kuongea na wanawake, hata wanawake wasio Wayahudi. (Yohana 4:7-30) Kwa mfano, wakati yeye alipokuwa akitembelea nyumba moja katika eneo la watu wa Mataifa wa Tiro na Sidoni, mwanamke Mgiriki alimwomba amsaidie binti yake mwenye mashetani. Kwa kawaida, Myahudi halisi hangeshughulika na mwanamke huyo hata kidogo. Lakini Yesu alisikiliza na akaijaribu imani yake, akisema: “Kwanza acha watoto [wa Kiyahudi] waridhike, kwa maana si sawa kuchukua mkate wa watoto na kuutupa kwa mbwa wadogo [wa watu wa Mataifa].” Je! namna ya sauti ya Yesu ilikomesha jambo hilo? Je! yeye alishikilia tu maoni yake hata akazuia mazungumzo yasiendelee? Haionekani kuwa hivyo, kwa maana mwanamke yule alijibu hivi kwa busara: “Naam, Bwana, lakini mbwa hula walio chini ya meza makombo ya watoto.” Yesu alivutwa na maneno hayo, naye akaponya binti ya mwanamke huyo.—Marko 7:24-30.
17. Tunaweza kujifunza nini kutokana na njia ambayo Yesu alishughulika na mwanamke fulani aliyekuwa mtenda dhambi?
17 Yesu aliendelea kuwa na akili iliyofunguka kuhusiana na wanawake na hakuhukumu kwa kutegemea sura za nje, (Mathayo 22:16) Katika pindi nyingine, alipokuwa akila katika nyumba ya Farisayo mmoja, yeye aliruhusu mtenda dhambi aliyejulikana, labda malaya, aoshe miguu yake kisha aipake mafuta. Kwa vitendo vyake, mwanamke huyo alionyesha mwelekeo wa kutubu kuhusu mwendo wake wenye dhambi. (Luka 7:36-50) Yesu hakumhesabu moja kwa moja kuwa asiyefaa na kumfukuza kwa hukumu ya bila kufikiria hali yake binafsi ati kwa sababu yeye alikuwa mwanamke mkosefu wa adili. (Ona pia Yohana 4:7-30.) Yeye alimsamehe ‘kwa kuwa alipenda sana.’ Hiyo inaonyesha nini juu ya akili ya Kristo? Yeye alikuwa mwenye huruma na ufahamu kuelekea mwanamke yule. Je! sisi hatuwezi kutenda vile vile katika kundi na katika huduma yetu?—Luka 19:1-10; Warumi 14:10-13; 1 Wakorintho 6:9-11.
Shughuli za Yesu Pamoja na Wanafunzi Wake
18. (a) Wengine wanawaitikiaje wale wanaofanya kazi chini yao? (b) Yesu alitendeaje wafuasi wake na wengine? (Marko 6:54-56)
18 Nyakati nyingine watu walio katika mamlaka wanahisi cheo chao kikitishwa na wadogo wao. Bila kujua sana kwamba wanafanya hivyo, wanahisi wagandamize jambo ambalo wanadhani limefanywa kwa kusudi la kushindana nao. Kiburi ndicho kinachotangulia. Wao wanafanya haraka kulaumu na kukawia kusifu wale wanaofanya kazi chini yao. Maneno yao ya kupuuza mambo yanakuwa hayaheshimu fahari ya kibinafsi ya wengine. Lakini namna gani Yesu—yeye alitendeaje wale waliokuwa chini yake, wafuasi wake? Je! wao walifanywa wahisi wakiwa duni, wasioweza kitu, au wapumbavu? Au, badala ya hivyo, wao walihisi wakiwa wamestarehe kufanya kazi pamoja na Yesu?—Linganisha Mathayo 11:28-30; 25:14-23.
19. Andiko la Yohana 13:1-17 linatufundisha nini juu ya Kristo?
19 Katika jambo hilo, moja la masomo ya kutokeza ambayo Yesu alifundisha wafuasi wake linapatikana katika Yohana sura ya 13. Tunadokeza kwamba usome mistari 1 mpaka 17. Siku hizo barabara zilikuwa zenye mavumbi- mavumbi, na ilikuwa desturi kuagiza mtumishi mmoja aoshe miguu ya wageni. Yesu alijitwika kazi hiyo ya hali ya chini. Ni sifa gani aliyokazia kwa kuosha miguu ya wafuasi wake? Yeye aliwapa somo lenye mafaa la unyenyekevu. Sisi tunajifunza nini hapa juu ya akili ya Kristo? Maneno ya Yesu yanatoa jibu: “Mtumwa si mkuu kuliko bwana wake; wala mtume si mkuu kuliko yeye aliyempeleka. Mkiyajua hayo, [wenye furaha] ninyi mkiyatenda.”—Yohana 13:16, 17.
20. Ni uchanganuzi gani wa kibinafsi tunaoweza kutumia tuone kama sisi tuna akili ya Kristo?
20 Je! sisi tuna akili ya Kristo katika jambo hilo? Je! sisi tuna nia ya kufanya kazi za unyenyekevu, za hali ya chini nyumbani na kundini? Au sisi tunataka kufanya mambo yale tu yanayoonekana kama kwamba ni “ya maana” au yatakayotufanya tuonekane kwamba sisi ni watu “wa pekee”? Je! sisi tuna nia ya kushiriki kazi ya kuhubiri habari njema nyumba kwa nyumba ambayo nyakati nyingine ni ya kunyenyekeza mtu? Au tunataka migawo ya kuwa katika jukwaa tu la Jumba la Ufalme? Kwa kweli, kuwa na akili ya Kristo kutaendelea kutufanya wanyenyekevu na wenye kufikika kama Yesu alivyokuwa.—Warumi 12:3.
21. Yesu alionyeshaje hisia-mwenzi kuelekea wanafunzi wake? Kuelekea umati?
21 Katika pindi moja, baada ya shughuli ya pekee ya kuhubiri, Yesu alionyesha fikira kubwa kwa ajili ya mitume. Ingawa alikuwa mkamilifu, Yesu hakutazamia ukamilifu kutoka kwa wengine. Mwishoni mwa shughuli ya kuhubiri, yeye hakusisitiza kwamba mitume warudie papo hapo kazi yao ya kuhubiri wakafanye vizuri hata zaidi. Yeye alifikiria uhitaji wao wa kupumzika na akawapeleka mahali pa upekee wapate faragha. Lakini wakati umati ulipowafuata, je! Yesu aliudhika na kukosa subira? Hapana, kwa maana ‘aliwahurumia,’ usimulizi huo unatuambia.—Marko 6:30-34.
22. Ni jambo gani litakalotusaidia zaidi tuifahamu akili ya Kristo?
22 Kwa kuwekewa mfano mzuri sana kama huo, je! ni ajabu kwamba walio wengi wa mitume walikuwa wafuasi waaminifu wa Kristo? Kwa uhakika Petro alivutwa na mambo aliyojifunza kwa kushirikiana kwa ukaribu pamoja na Yesu. Labda yeye ndiye aliyemgawia Marko nyingi za habari za kuweka katika usimulizi wake wa Injili. Na Petro alijirekebisha akapatana na akili ya Kristo kwa uthabiti ingawa ilikuwa polepole. Kuchunguza kidogo barua yake ya kwanza kutatusaidia tufuate mfano wa Kristo kwa ukaribu zaidi.—Mathayo 16:15-17, 21-23.
Je! Wewe Unakumbuka?
◻ Sisi tunaweza kuwaje na akili ya Kristo?
◻ Yesu alikuwa mwanamume wa aina gani?
◻ Yesu aliwaitikiaje watoto? Wanawake?
◻ Sisi tunajifunza nini kutokana na njia ambayo Yesu alishughulika na wafuasi wake?
[Picha katika ukurasa wa 10]
Yesu alikuwa mwenye huruma na hakuficha hisia zake
[Picha katika ukurasa wa 12]
Yesu alikuwa mwanamume wa vitendo vya ushujaa
[Picha katika ukurasa wa 15]
Yesu aliweka mfano wenye kutokeza wa unyenyekevu