Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ct sura 9 kur. 144-164
  • Mwalimu Mkuu Atudhihirishia Muumba Zaidi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mwalimu Mkuu Atudhihirishia Muumba Zaidi
  • Je, Kuna Muumba Anayekujali?
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mwanamke Msamaria
  • Maoni ya Mvuvi
  • Kwa Nini Yesu Alikufa?
  • Mwanafunzi Aliyetambua Upendo
  • Yesu Aliyefufuliwa—Ufunguo wa Maisha Yenye Umaana
  • Yesu Kristo Ni Nani?
    Biblia Inatufundisha Nini?
  • Yesu Kristo Ni Nani?
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Ukristo—Je! Yesu Alikuwa Ndiye Njia ya Kuongoza kwa Mungu
    Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu
  • Yesu Kristo—Maswali Yetu Yajibiwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
Pata Habari Zaidi
Je, Kuna Muumba Anayekujali?
ct sura 9 kur. 144-164

Sura Ya Tisa

Mwalimu Mkuu Atudhihirishia Muumba Zaidi

WATU wa Palestina ya karne ya kwanza ‘walikuwa na tarajio.’ Walikuwa wakitarajia nini? “Kristo,” au “Mesiya,” aliyetabiriwa na manabii wa Mungu karne nyingi zilizopita. Watu walikuwa na uhakika wa kwamba Biblia iliandikwa chini ya uelekezo wa Mungu na kwamba ilikuwa inasema mambo ya wakati ujao. Unabii mmoja kama huo, ulio katika kitabu cha Danieli, ulielekezea kufika kwa Mesiya mapema katika karne yao.—Luka 3:15; Danieli 9:24-26.

Lakini, wao walihitaji kutahadhari kwa sababu watu wenye kujifanya mesiya wangetokea. (Mathayo 24:5) Mwanahistoria Myahudi Yosefo ataja baadhi yao: Theudasi, aliyewaongoza wafuasi wake hadi Mto Yordani na kudai eti maji yake yangegawanyika; mtu fulani kutoka Misri ambaye aliongoza watu hadi Mlima wa Mizeituni, akisisitiza kwamba ukuta wa Yerusalemu ungeanguka kwa amri yake; na mlaghai mmoja wa wakati wa Gavana Festo aliyeahidi kwamba angewaondolea watu matatizo.—Linganisha Matendo 5:36; 21:38.

Tofauti na wafuasi hao waliodanganyika, kikundi kilichokuja kuitwa “Wakristo” kilimtambua Yesu wa Nazareti kuwa mwalimu mkuu aliye pia Mesiya wa kweli. (Matendo 11:26; Marko 10:47) Yesu hakuwa mesiya bandia; alikuwa na sifa za kumstahilisha kabisa, kama inavyothibitishwa vizuri katika vitabu vinne vya kihistoria viitwavyo Gospeli.a Kwa mfano, Wayahudi walijua kwamba Mesiya angezaliwa Bethlehemu, angekuwa wa uzao wa Daudi, naye angefanya matendo ya ajabu. Yesu alitimiza hayo yote, kama inavyoonyeshwa hata na ushuhuda wa wapinzani. Ndiyo, Yesu alitimiza sifa za Mesiya wa Biblia.—Mathayo 2:3-6; 22:41-45; Yohana 7:31, 42.

Umati wa watu waliokutana na Yesu walitazama matendo yake yenye kutokeza, walisikia maneno yake ya kipekee yenye hekima, na kutambua busara yake, walisadiki kwamba alikuwa ndiye Mesiya. Katika huduma yake (29-33 W.K.), uthibitisho wenye kutegemeza Umesiya wake uliongezeka. Hata akathibitika kuwa zaidi ya Mesiya. Mwanafunzi mmoja aliyefahamu mambo yake alikata kauli ya kwamba “Yesu ndiye Kristo Mwana wa Mungu.”b—Yohana 20:31.

Kwa sababu Yesu alikuwa na uhusiano wa karibu sana na Mungu, angeweza kueleza na kufunua vile Muumba alivyo. (Luka 10:22; Yohana 1:18) Yesu alitoa ushuhuda wa kwamba ukaribu wake na Baba yake ulianza akiwa mbinguni, ambako alifanya kazi pamoja na Mungu katika kutokeza vitu vingine vyote, vyenye uhai na visivyo na uhai.—Yohana 3:13; 6:38; 8:23, 42; 13:3; Wakolosai 1:15, 16.

Biblia yaripoti kwamba huyo Mwana alihamishwa kutoka makao ya roho “akaja kwa namna ya wanadamu.” (Wafilipi 2:5-8) Tukio kama hilo si la kawaida, lakini je, lawezekana? Wanasayansi wanathibitisha kwamba elementi ya asili, kama vile urani, yaweza kubadilishwa kuwa elementi nyingine; wao hata hupiga hesabu ya matokeo wakati masi inapobadilishwa kuwa nishati (E=mc2). Basi kwa nini tutilie shaka wakati Biblia isemapo kwamba kiumbe wa roho alibadilishwa ili aishi kama binadamu?

Tukitoa mfano mwingine, ebu fikiria kile ambacho baadhi ya matabibu hufanya katika utungaji wa mimba nje ya mwili. Uhai unaoanza katika “tesitubu” unaingizwa katika mwanamke na baadaye unazaliwa ukiwa mtoto mchanga. Katika kisa cha Yesu, Biblia yatuhakikishia ya kwamba kwa “nguvu ya Aliye Juu Zaidi Sana,” uhai wake uliingizwa ndani ya bikira aliyeitwa Maria. Yeye alikuwa wa nasaba ya Daudi, basi Yesu angekuwa mrithi wa daima wa Ufalme wa Mesiya ulioahidiwa Daudi.—Luka 1:26-38; 3:23-38; Mathayo 1:23.

Kwa msingi wa uhusiano wake wa karibu pamoja na Muumba na kufanana kwao, Yesu alisema: “Yeye ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” (Yohana 14:9) Pia alisema hivi: “Ya kwamba Baba ni nani, hakuna ajuaye ila Mwana, na yeye ambaye Mwana anapenda kumfunulia.” (Luka 10:22) Kwa hiyo, tujifunzapo kile ambacho Yesu alifundisha na kufanya duniani, twaweza kuona utu wa Muumba vizuri zaidi. Ebu tufikirie hili, tukitumia mambo waliyojionea wanaume na wanawake ambao walishughulika na Yesu.

Mwanamke Msamaria

“Huyu labda ndiye Kristo, sivyo?” akauliza mwanamke Msamaria baada ya kuzungumza na Yesu kwa muda fulani. (Yohana 4:29) Hata akawahimiza wengine katika mji ulio karibu wa Sikari waje kumwona Yesu. Ni nini kilichomfanya amkubali Yesu kuwa Mesiya?

Mwanamke huyo alikutana na Yesu wakati Yesu alipokuwa akipumzika baada ya kutembea asubuhi yote kwenye barabara zenye vumbi katika vilima vya Samaria. Ingawa Yesu alikuwa amechoka, alizungumza na mwanamke huyo. Akiona upendezi wake wa kiroho wenye makini, Yesu alimweleza kweli zenye kustaajabisha kuhusu uhitaji wa ‘kumwabudu Baba kwa roho na kweli.’ Baadaye akamfunulia kwamba kwa kweli yeye ndiye Kristo, jambo ambalo bado hakuwa amekiri peupe.—Yohana 4:3-26.

Huyo mwanamke Msamaria alipata mazungumzo yake na Yesu kuwa yenye umaana sana. Ibada yake ya awali ilitegemea kuabudu kwenye Mlima Gerizimu na kutegemea vile vitabu vitano tu vya kwanza vya Biblia. Wayahudi waliwaepuka Wasamaria, wengi wao wakiwa wa uzao mchanganyiko wa kati ya makabila kumi ya Israeli na watu wengine. Yesu alikuwa tofauti kama nini! Kwa hiari, alimfundisha Msamaria huyo, hata ingawa alitumwa kuwaendea “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” (Mathayo 15:24) Hapo Yesu alionyesha utayari wa Yehova wa kukubali watu wanyoofu wa mataifa yote. (1 Wafalme 8:41-43) Ndiyo, Yesu na Yehova hawana uhasama wa kidini ambao umejaa ulimwenguni leo. Kujua jambo hilo kwapasa kutuvutia kwa Muumba na Mwana wake.

Kuna somo jingine tuwezalo kupata katika utayari wa Yesu wa kumfundisha mwanamke huyu. Wakati huo huyo mwanamke alikuwa akiishi na mwanamume ambaye hakuwa mume wake. (Yohana 4:16-19) Lakini, Yesu hakuacha jambo hilo limzuie asiseme naye. Unafahamu kwamba ni lazima mwanamke huyo alithamini kutendewa kwa staha. Na si yeye pekee aliyetendewa hivyo. Viongozi fulani wa Kiyahudi (Mafarisayo) walipomchambua Yesu kwa kula pamoja na watenda-dhambi wenye kutubu, yeye alisema: “Watu wenye afya hawahitaji tabibu, bali wenye kuugua wahitaji. Nendeni, basi, na mjifunze kile ambacho hili lamaanisha, ‘Mimi nataka rehema, wala si dhabihu.’ Kwa maana nilikuja kuita, si watu waadilifu, bali watenda-dhambi.” (Mathayo 9:10-13) Yesu aliwapa msaada watu waliokuwa wakiugua kwa mzigo wa dhambi zao—za kukiuka sheria au viwango vya Mungu. Ni jambo lenye kuchangamsha moyo kama nini kujifunza kwamba Mungu na Mwana wake watasaidia wale ambao wana matatizo yatokanayo na mwenendo wao wa zamani!—Mathayo 11:28-30.c

Tusipuuze jambo la kwamba pindi hii katika Samaria, Yesu alizungumza na mwanamke kwa fadhili na kwa njia yenye msaada. Kwa nini hilo ni jambo muhimu? Wakati huo wanaume Wayahudi walifundishwa kwamba wanapaswa kuepuka kuzungumza na wanawake peupe, hata wake zao wenyewe. Marabi wa Kiyahudi waliwaona wanawake kuwa hawangeweza kufahamu mambo ya ndani ya kiroho na kuwaona kuwa “wenye akili ndogo.” Wengine walisema: “Ni afadhali maneno ya sheria yachomwe kuliko kuwaambia wanawake juu yake.” Wanafunzi wa Yesu walilelewa katika mazingira kama hayo; basi waliporudi, “wakaanza kustaajabu kwa sababu alikuwa akisema na mwanamke.” (Yohana 4:27) Masimulizi hayo—ambayo ni mojawapo ya mengi—yaonyesha kwamba Yesu alifanana na Baba yake, ambaye aliwaumba na kuwapa heshima wanaume na wanawake.—Mwanzo 2:18.

Baadaye yule mwanamke Msamaria aliwasadikisha wakazi wenzake wa mji kumsikiliza Yesu. Wengi waliyachunguza mambo wakawa waamini, wakisema: “Twajua kwamba mtu huyu kwa hakika ndiye mwokozi wa ulimwengu.” (Yohana 4:39-42) Kwa kuwa sisi ni sehemu ya “ulimwengu” wa wanadamu, Yesu ni muhimu katika wakati wetu ujao pia.

Maoni ya Mvuvi

Sasa ebu tumchunguze Yesu kupitia maoni ya washiriki wake wawili wa karibu—Petro kisha Yohana. Wavuvi hao wa kawaida walikuwa miongoni mwa wafuasi wake wa kwanza. (Mathayo 4:13-22; Yohana 1:35-42) Mafarisayo waliwaona kuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu,” wakiwa baadhi ya watu wa hali ya chini (ʽam-ha·ʼaʹrets), ambao walidharauliwa kwa sababu hawakusoma kama marabi. (Matendo 4:13; Yohana 7:49) Watu wengi kama hao, waliokuwa ‘wakimenyeka na kulemezwa mzigo’ na nira ya washika-mapokeo wa kidini, walitamani kupata nuru ya kiroho. Profesa Charles Guignebert wa Sorbonne alisema kwamba “mioyo yao ilikuwa ya Yahweh [Yehova] kabisa.” Yesu hakuwapuuza watu hao wanyenyekevu kwa kupendelea wenye mali au walio mashuhuri. Badala yake, aliwafunulia Baba kupitia mafundisho na matendo yake.—Mathayo 11:25-28.

Petro alijionea mtazamo wa Yesu wa kujali. Punde tu baada ya kujiunga na Yesu katika huduma, mama-mkwe wa Petro akawa mgonjwa kwa homa. Akija nyumbani kwa Petro, Yesu akamshika mama huyo kwa mkono, na homa ikaisha! Huenda tusijue hasa njia hiyo ya tiba, kama vile tu leo wanatiba hawawezi kueleza vizuri jinsi ambavyo baadhi ya tiba hutokea, lakini homa ilimwondoka mwanamke huyo. Jambo kubwa zaidi kuliko kujua njia yake ya tiba ni kuthamini kwamba kwa kuponya wagonjwa na wenye mapigo, Yesu alionyesha jinsi alivyowasikitikia. Kwa kweli alitaka kuwasaidia watu, na ndivyo ilivyo na Baba yake. (Marko 1:29-31, 40-43; 6:34) Kutokana na mambo aliyojionea akiwa na Yesu, Petro angeweza kuona kwamba Muumba amwona kila mtu kuwa astahili kutunzwa.—1 Petro 5:7.

Baadaye, Yesu alikuwa katika Ua wa Wanawake katika hekalu la Yerusalemu. Aliwatazama watu wakiweka michango katika masanduku ya hazina. Matajiri waliweka sarafu nyingi. Akiwa makini, Yesu aliona mjane maskini akitumbukiza sarafu mbili zenye thamani kidogo sana. Yesu akawaambia Petro, Yohana, na wengine: “Kwa kweli nawaambia nyinyi kwamba mjane maskini huyu alitumbukiza ndani zaidi ya wote wale waliokuwa wakitumbukiza fedha ndani ya masanduku ya hazina; kwa maana wote walitumbukiza ndani kutokana na ziada yao, lakini yeye, kutokana na uhitaji wake, alitumbukiza ndani vyote alivyokuwa navyo.”—Marko 12:41-44.

Unaweza kuona kwamba Yesu aliangalia sifa nzuri za watu naye alithamini jitihada za kila mtu. Unafikiri hilo liliwavutiaje Petro na mitume wengine? Kwa kutazama kutokana na kielelezo cha Yesu jinsi Yehova alivyo, Petro alinukuu zaburi moja: “Macho ya Yehova yako juu ya waadilifu, na masikio yake yaelekea dua zao.” (1 Petro 3:12; Zaburi 34:15, 16) Je, wewe huvutiwi na Muumba na Mwana wake ambao hutaka kuona wema wako na ambao watasikiliza dua zako?

Baada ya miaka miwili hivi ya kushirikiana na Yesu, Petro alikuwa na uhakika wa kwamba Yesu alikuwa ndiye Mesiya. Pindi moja Yesu aliwauliza wanafunzi wake hivi: “Watu wanasema kwamba mimi ni nani?” Akapata majibu tofauti-tofauti. Akawauliza: “Ingawa hivyo, nyinyi mwasema mimi ni nani?” Petro akajibu akiwa na uhakika: “Wewe ndiwe Kristo.” Unaweza kushangazwa na hatua ambayo Yesu alichukua. “Akawaagiza kwa mkazo wasimwambie yeyote” jambo hilo. (Marko 8:27-30; 9:30; Mathayo 12:16) Kwa nini alisema hivyo? Yesu mwenyewe alikuwapo kati yao, basi hakutaka watu wafikie maamuzi yaliyotegemea tu mambo yaliyosikiwa. Hilo lapatana na akili, sivyo? (Yohana 10:24-26) Jambo kuu ni kwamba, Muumba wetu vilevile anataka tujue mambo juu yake kupitia kujichunguzia wenyewe ushuhuda halisi. Anatutarajia tuwe na usadikisho unaotegemea mambo ya hakika.—Matendo 17:27.

Kama unavyojua, baadhi ya watu wa nchi ya Yesu hawakumkubali, japo uthibitisho wa kutosha wa kwamba alikuwa ameungwa mkono na Muumba. Wengi, wakishughulikia tu vyeo vyao au miradi yao ya kisiasa, hawakumpenda huyo Mesiya mnyenyekevu na mwenye kufuatia haki. Huduma yake ilipokaribia mwisho, Yesu alisema: “Yerusalemu, muuaji wa manabii na mpigaji kwa mawe wale waliotumwa kwake,—ni mara nyingi kadiri gani nilitaka kuwakusanya watoto wako pamoja . . . Lakini nyinyi watu hamkutaka hilo. Tazameni! Nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mathayo 23:37, 38) Badiliko hilo kwa taifa hilo likawa hatua muhimu katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu la kubariki mataifa yote.

Punde tu baadaye Petro na mitume wengine watatu walisikia Yesu akitoa unabii wenye mambo mengi kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo.”d Mambo ambayo Yesu alitabiri yalitimizwa kwanza wakati wa shambulio la Waroma dhidi ya Yerusalemu na kuharibiwa kwake mnamo 66-70 W.K. Historia yathibitisha kwamba yale aliyoyatabiri Yesu kwa kweli yalitukia. Petro alishuhudia mambo yaleyale ambayo Yesu alitabiri, na hilo laonyeshwa katika Petro wa 1 na wa 2, vile vitabu viwili ambavyo Petro aliviandika.—1 Petro 1:13; 4:7; 5:7, 8; 2 Petro 3:1-3, 11, 12.

Katika huduma yake, kwa subira Yesu alikuwa amewaonyesha fadhili Wayahudi waliokuwa naye. Lakini hakusita kushutumu uovu wao. Jambo hilo lilimsaidia Petro, nalo laweza kutusaidia kumwelewa Muumba wetu vizuri zaidi. Petro alipoona mambo mengine yakitimiza unabii wa Yesu, aliandika kwamba Wakristo wadumishe “kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.” Petro pia alisema: “Yehova si wa polepole kwa habari ya ahadi yake, kama watu fulani waonavyo kuwa ni upolepole, bali yeye ni mwenye subira kwenu kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” Kisha Petro akatoa maneno yenye kutia moyo kuhusu ‘mbingu mpya na dunia mpya ambazo katika hizo uadilifu utakaa.’ (2 Petro 3:3-13) Je, sisi kama Petro, tunathamini sifa za Mungu zinazoonyeshwa katika Yesu, na je tunadhihirisha kwamba tunatumaini ahadi zake za wakati ujao?

Kwa Nini Yesu Alikufa?

Usiku wake wa mwisho akiwa na mitume, Yesu alishiriki mlo wa kipekee pamoja nao. Kwenye mlo kama huo, mkaribishaji Myahudi angeonyesha ukaribishaji wake kwa kuwaosha miguu wageni wake, ambao huenda walikuwa wametembea kwenye barabara zenye vumbi kwa makubazi. Lakini, hakuna mtu aliyejitolea kumwosha Yesu miguu. Basi, kwa unyenyekevu aliinuka, akachukua taulo na beseni, na kuanza kuosha miguu ya mitume wake. Zamu ya Petro ilipofika, aliona aibu kukubali kutumikiwa na Yesu. Petro akasema: “Hakika wewe hutaosha kamwe miguu yangu.” Yesu akajibu, “Isipokuwa nikuoshe, wewe huna sehemu pamoja na mimi.” Yesu alijua ya kwamba karibuni atakufa, kwa hiyo akaongezea: “Ikiwa mimi, nijapokuwa Bwana na Mwalimu, niliosha miguu yenu, nyinyi pia mwapaswa kuoshana miguu. Kwa maana mimi niliweka kiolezo kwa ajili yenu, ili, kama vile nilivyowafanyia nyinyi, nyinyi mpaswe kufanya pia.”—Yohana 13:5-17.

Miongo kadhaa baadaye Petro aliwahimiza Wakristo wamwige Yesu, si kwa kufuata desturi ya kuosha miguu, bali kwa kuwatumikia wengine kwa unyenyekevu badala ya ‘kupiga ubwana.’ Petro pia alitambua kwamba kielelezo cha Yesu kilithibitisha kwamba “Mungu hupinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili isiyostahiliwa.” Hilo ni somo lililoje kuhusu Muumba! (1 Petro 5:1-5; Zaburi 18:35) Lakini, Petro alijifunza hata mengi zaidi.

Baada ya mlo huo wa mwisho, Yudasi Iskariote, ambaye alikuwa mtume lakini akawa mwizi, aliongoza kikosi cha watu waliojihami wamkamate Yesu. Walipokuwa wakimkamata, Petro alichukua hatua. Alichomoa upanga wake na kumjeruhi mtu mmoja aliyekuwa katika umati huo. Yesu akamrekebisha Petro: “Rudisha upanga wako mahali pao, kwa maana wale wote wauchukuao upanga wataangamia kwa upanga.” Kisha, Petro akitazama, Yesu alimgusa mtu yule, akamponya. (Mathayo 26:47-52; Luka 22:49-51) Kwa wazi, Yesu alitenda kwa kupatana na fundisho lake la “endeleeni kupenda maadui wenu” kwa kuiga Baba yake, ambaye “hufanya jua lake lichomoze juu ya watu waovu na wema na kufanya mvua inyeshe juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.”—Mathayo 5:44, 45.

Katika usiku huo wenye mikazo sana, Yesu alisikilizwa kijuu-juu tu na mahakama kuu ya Kiyahudi. Alishtakiwa kwa uwongo kwa kukufuru, akapelekwa kwa Gavana Mroma, kisha akapelekwa kuuawa isivyo haki. Wayahudi na Waroma walimdhihaki. Alitendwa kikatili sana na hatimaye kutundikwa mtini. Kutendwa vibaya huko kwingi kulitimiza unabii mbalimbali ulioandikwa karne nyingi awali. Hata askari waliokuwa wakimtazama Yesu akiwa kwenye mti wa mateso walikiri hivi: “Hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu.”—Mathayo 26:57–27:54; Yohana 18:12–19:37.

Ni lazima matukio hayo yalifanya Petro na wengine waulize, ‘Kwa nini Kristo alilazimika kufa?’ Ni baadaye tu ndipo walipoelewa. Kwanza, matukio hayo yalitimiza unabii ulio katika Isaya sura ya 53, ambao ulionyesha kwamba Kristo angefanya wokovu upatikane si kwa Wayahudi tu bali pia kwa wanadamu wote. Petro aliandika hivi: “Yeye mwenyewe alichukua dhambi zetu katika mwili wake mwenyewe juu ya mti, ili tupate kuachana kabisa na dhambi na kuishi kuelekea uadilifu. Na ‘kwa mapigo yake mliponywa.’” (1 Petro 2:21-25) Petro alipata umaana wa kweli ambayo Yesu alikuwa ametaja: ‘Mwana wa binadamu alikuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu na kutoa nafsi yake kuwa fidia katika kubadilishana kwa ajili ya wengi.’ (Mathayo 20:28) Ndiyo, ilikuwa lazima Yesu aache haki yake ya kuishi akiwa mwanadamu mkamilifu ili awakomboe wanadamu kutokana na dhambi ambayo walirithi kutoka kwa Adamu. Hilo ni fundisho la msingi la Biblia—fidia.

Fidia inahusisha nini? Unaweza kufikiria jambo hilo kwa njia hii: Tuseme una kompyuta lakini mojawapo ya faili zake imevurugwa na kasoro fulani ambayo mtu mwingine alitia katika programu hiyo iliyokuwa kamilifu. Hilo latoa mfano wa athari ya kitendo cha Adamu alipokosa kumtii Mungu kimakusudi, au kutenda dhambi. Ebu tuendelee na ule mfano. Nakala zozote utakazofanyiza na ile faili yenye kasoro ya kompyuta zitaathiriwa. Lakini, hiyo haimaanishi kwamba hakuna namna ya kurekebisha hali. Kwa programu ya kipekee, unaweza kugundua na kuondoa ile kasoro yenye kuvuruga kwenye faili zako na kompyuta yako. Kwa kulinganisha, wanadamu walipokea kasoro, dhambi, kutoka kwa Adamu na Hawa, nasi twahitaji msaada wa nje ili kuiondoa. (Waroma 5:12) Kulingana na Biblia, Mungu aliandaa utakaso huo kupitia kifo cha Yesu. Ni uandalizi wenye upendo ambao tunaweza kunufaika nao.—1 Wakorintho 15:22.

Kuthamini kile alichofanya Yesu kulimsukuma Petro “kuishi wakati wake uliobaki katika mwili, si tena kwa ajili ya tamaa za wanadamu, bali kwa ajili ya mapenzi ya Mungu.” Kwa Petro na kwetu sisi, hiyo yamaanisha kuepuka tabia zenye kufisidi na mitindo-maisha isiyo ya adili. Wengine wanaweza kujaribu kutaabisha mtu anayejaribu kufanya “mapenzi ya Mungu.” Hata hivyo, yeye atapata kwamba maisha yake ni yenye kuthawabisha zaidi, na yenye umaana zaidi. (1 Petro 4:1-3, 7-10, 15, 16) Ndivyo ilivyokuwa na Petro, na inaweza kuwa hivyo kwetu ‘tukabidhipo nafsi zetu, au uhai wetu, kwa Muumba mwaminifu tunapotenda mema.’—1 Petro 4:19.

Mwanafunzi Aliyetambua Upendo

Mtume Yohana alikuwa mwanafunzi mwingine ambaye alishirikiana kwa ukaribu na Yesu na ambaye basi, aweza kutusaidia kumwelewa Muumba vizuri zaidi. Yohana aliandika Gospeli moja na pia barua tatu (Yohana ya 1, ya 2 na ya 3). Katika mojawapo ya barua hizo, yeye alitufahamisha hivi: “Twajua kwamba Mwana wa Mungu amekuja, na yeye ametupa sisi uwezo wa akili ili tupate ujuzi juu ya aliye wa kweli [Muumba]. Na sisi tumo katika muungano na aliye wa kweli, kwa njia ya Mwana wake Yesu Kristo. Huyu ndiye Mungu wa kweli na uhai udumuo milele.”—1 Yohana 5:20.

Yohana alipata ujuzi wa yule “aliye wa kweli” kwa kutumia “uwezo wa akili.” Yohana alitambua nini kuhusu sifa za Muumba? “Mungu ni upendo,” Yohana akaandika, “na yeye ambaye hukaa katika upendo hukaa katika muungano na Mungu.” Kwa nini Yohana alikuwa na uhakika juu ya jambo hilo? “Upendo uko hivi, si kwamba sisi tumempenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda akamtuma Mwana wake” atoe dhabihu ya fidia kwa ajili yetu. (1 Yohana 4:10, 16) Kama Petro, Yohana pia aliguswa na upendo ambao Mungu alionyesha kwa kumtuma Mwana wake afe kwa niaba yetu.

Kwa kuwa Yohana alikuwa karibu sana naye, angeweza kufahamu hisia za Yesu. Tukio moja katika Bethania, karibu na Yerusalemu, lilivutia sana Yohana. Baada ya Yesu kupokea ripoti ya kwamba rafikiye Lazaro alikuwa mgonjwa mahututi, alisafiri kwenda Bethania. Yeye na mitume walipofika, Lazaro alikuwa amekufa kwa angalau siku nne. Yohana alijua kwamba Muumba, aliye Chanzo cha uhai wa kibinadamu, alikuwa akimpa Yesu nguvu. Basi, je, Yesu angeweza kumfufua Lazaro? (Luka 7:11-17; 8:41, 42, 49-56) Yesu alimwambia dada ya Lazaro aitwaye Martha: “Ndugu yako atainuka.”—Yohana 11:1-23.

Kisha Yohana akamwona dada mwingine wa Lazaro, Maria, akija kumlaki Yesu. Yesu aliitikiaje? Yeye “akapiga kite katika roho na kuwa mwenye kutaabika.” Ili kufafanua itikio la Yesu, Yohana alitumia neno la Kigiriki (lililotafsiriwa ‘kupiga kite’ katika Kiswahili) ambalo lilimaanisha hisia za ndani zitokazo moyoni bila kukusudia. Yohana aliona kwamba Yesu ‘alikuwa akitaabika,’ au alikuwa na hisia nyingi za ndani, huzuni nyingi. Yesu alijali na hakujitenga. “Akatokwa na machozi.” (Yohana 11:30-37) Kwa wazi, Yesu alikuwa na hisia nyororo za ndani, jambo ambalo lilimsaidia Yohana afahamu hisia za Muumba, nalo lapasa kutusaidia sisi vilevile.

Yohana alijua kwamba hisia za Yesu zilifuatana na matendo mazuri kwa sababu alimsikia Yesu akipaaza sauti akisema: “Lazaro, njoo huku nje!” Na ikafanyika hivyo. Lazaro akapata uhai akatoka kaburini. Ni lazima dada zake na watazamaji wengine walipata shangwe iliyoje! Kisha wengi wakawa na imani kwa Yesu. Maadui wake hawangeweza kukana kwamba alikuwa amefanya ufufuo, lakini habari hiyo ilipoenea, wao “wakafanya shauri kumuua Lazaro” na Yesu pia.—Yohana 11:43; 12:9-11.

Biblia inafafanua Yesu kuwa ‘mwakilisho sawasawa wa utu wa Muumba mwenyewe.’ (Waebrania 1:3) Basi, huduma ya Yesu iliandaa uthibitisho wa kutosha wa tamaa yake kubwa na ya Baba yake ya kuondoa madhara ya ugonjwa na kifo. Na hiyo inahusu mengi kuliko idadi ndogo tu ya ufufuo mbalimbali uliorekodiwa katika Biblia. Kwa hakika, Yohana alikuwapo na kusikia Yesu akisema: “Saa inakuja ambayo katika hiyo wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti [ya Mwana] na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Ona kwamba badala ya neno la kawaida la kaburi, hapo Yohana alitumia neno lililotafsiriwa “makaburi ya ukumbusho.” Kwa nini?

Kumbukumbu ya Mungu yahusika. Kwa hakika Muumba wa ulimwengu huu mkubwa aweza kukumbuka kila kijambo kidogo cha kila mmoja wa wapendwa wetu waliokufa, kutia ndani tabia zilizorithiwa na alizositawisha. (Linganisha Isaya 40:26.) Na si kwamba aweza tu kukumbuka. Wote wawili yeye na Mwana wake wanataka kukumbuka. Kuhusu tarajio tukufu la ufufuo, Ayubu mwaminifu aliuliza Mungu hivi: “Mtu akifa, je! atakuwa hai tena? . . . Wewe [Yehova] ungeita, nami ningekujibu; ungekuwa na tamaa ya kazi ya mikono yako.” (Ayubu 14:14, 15, italiki ni zetu; Marko 1:40-42) Tuna Muumba mzuri ajabu kama nini, astahiliye ibada yetu!

Yesu Aliyefufuliwa—Ufunguo wa Maisha Yenye Umaana

Mwanafunzi mpendwa Yohana alimtazama Yesu kwa makini hadi kifo Chake. Isitoshe, Yohana alirekodi ufufuo mkubwa zaidi uliowahi kutokea, tukio ambalo linaweka msingi thabiti wa kuwa na uhai wa milele na wenye umaana.

Maadui wa Yesu walimfanya auawe, akiwa amepigiliwa misumari kwenye mti kama mhalifu tu. Watazamaji—kutia ndani viongozi wa kidini—walimdhihaki alipokuwa akiteseka kwa saa kadhaa. Ajapokuwa na maumivu makali kwenye mti, Yesu alimwona mama yake mwenyewe na kumwambia mamake hivi kumhusu Yohana: “Mwanamke, ona! Mwana wako!” Kufikia wakati huo ni lazima Maria alikuwa mjane, na wale watoto wake wengine bado hawakuwa wanafunzi.e Kwa hiyo, Yesu alikabidhi utunzi wa mamake aliyekuwa akizeeka kwa mwanafunzi Yohana. Jambo hilo pia lilionyesha kufikiri kwa Muumba, ambaye alitia moyo kuwatunza wajane na mayatima.—Yohana 7:5; 19:12-30; Marko 15:16-39; Yakobo 1:27.

Lakini alipokufa, Yesu angetekelezaje fungu lake, akiwa “mbegu” ambaye kupitia kwake ‘mataifa yote yangejibarikia’? (Mwanzo 22:18) Kwa kifo chake, katika alasiri hiyo ya Aprili mnamo 33 W.K., Yesu alitoa uhai wake kuwa msingi wa fidia. Baba yake mwenye kufahamu aliyokuwa akipitia ni lazima alihisi uchungu kwa maumivu makali ya Mwana wake asiye na hatia. Lakini kwa njia hiyo, uandalizi ulifanywa wa kulipa thamani ya fidia iliyohitajiwa ili kuwaondolea wanadamu dhambi na kifo. (Yohana 3:16; 1 Yohana 1:7) Basi msingi ulikuwa umewekwa kwa ajili ya tukio tukufu.

Kwa sababu Yesu Kristo anatimiza fungu kuu katika kutimizwa kwa makusudi ya Mungu, ilikuwa lazima arudie uhai. Ikatokea hivyo, Yohana akashuhudia. Mapema katika siku ya tatu baada ya kifo na kuzikwa kwa Yesu, baadhi ya wanafunzi walienda kwenye kaburi. Lilikuwa tupu. Walishangaa hadi Yesu alipowatokea kadhaa kati yao. Maria Magdalena akaripoti, “Nimemwona Bwana!” Wanafunzi hawakukubali ushahidi wake. Baadaye wanafunzi walikusanyika katika chumba kilichokuwa kimefungwa na Yesu akawatokea tena, hata akazungumza nao. Kwa siku chache, zaidi ya wanaume na wanawake 500 wakajionea ya kwamba kwa kweli Yesu alikuwa hai. Watu wa wakati huo ambao huenda walikuwa wenye kutilia shaka wangeweza kuwahoji mashahidi hao wenye kuaminika na kuthibitisha ushuhuda wao. Wakristo waliweza kuwa na uhakika wa kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa na alikuwa hai akiwa kiumbe wa roho kama Muumba. Uthibitisho wa jambo hilo ulikuwa mwingi na wenye kutegemeka hivi kwamba wengi walikabili kifo badala ya kukana kufufuliwa kwa Yesu.—Yohana 20:1-29; Luka 24:46-48; 1 Wakorintho 15:3-8.f

Mtume Yohana pia alinyanyaswa kwa kutoa ushuhuda kuhusu ufufuo wa Yesu. (Ufunuo 1:9) Lakini alipokuwa uhamishoni kwa sababu ya adhabu, alipokea zawadi isiyo ya kawaida. Yesu alimpa mfululizo wa njozi ambazo zinatuonyesha Muumba kwa udhahiri zaidi na kufunua mambo ambayo yatakuja wakati ujao. Utapata hayo katika kitabu cha Ufunuo, ambacho kinatumia ishara nyingi. Katika kitabu hicho, Yesu Kristo anaonyeshwa akiwa Mfalme mshindi ambaye karibuni atamaliza ushindi wake dhidi ya maadui wake. Maadui hao wanatia ndani kifo (adui wetu sote) na kiumbe wa roho aliyefisidika aitwaye Shetani.—Ufunuo 6:1, 2; 12:7-9; 19:19–20:3, 13, 14.

Karibu na mwisho wa ujumbe wa ufunuo, Yohana alikuwa na njozi ya wakati ambapo dunia itakuwa paradiso. Sauti moja ikataja hali ambazo zitaenea wakati huo: “Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao [wanadamu]. Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:3, 4) Katika utimizo wa kusudi la Mungu, ahadi ambayo Mungu alimpa Abrahamu itatimizwa.—Mwanzo 12:3; 18:18.

Wakati huo uhai utakuwa “uhai ulio halisi,” unaolingana na yale yaliyokuwa mbele ya Adamu alipoumbwa. (1 Timotheo 6:19) Mwanadamu hatatafuta-tafuta tena Muumba wao na kuelewa uhusiano wao naye. Lakini, huenda ukauliza, ‘Hayo yatatokea lini? Na kwa nini Muumba mwenye kujali anaruhusu uovu na kuteseka kuwepo hadi wakati wetu?’ Ebu tufuatie kuzungumzia maswali hayo.

[Maelezo ya Chini]

a Mathayo, Marko, na Yohana walikuwa mashahidi waliojionea. Luka alichunguza kitaaluma hati na ushuhuda wa watu waliojionea mambo hayo. Hizo Gospeli zadhihirisha ishara ya kwamba rekodi hizo ni sahihi, zenye kufuatia haki, na zenye kutumainika.—Ona kichapo Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote, ukurasa wa 16-17, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

b Qurani yasema: “Jina lake ni Masih, Isa [Kristo Yesu], mwana wa Maryamu, mwenye hishima katika dunia na Akhera.” (Sura 3:45) Akiwa binadamu, Yesu alikuwa mwana wa Maria. Lakini ni baba yupi aliyemzaa? Qurani yasema: “Hali ya Isa [Yesu] kwa Mwenyezi Mungu ni kama hali ya Adam.” (Sura 3:59) Maandiko Matakatifu yasema juu ya Adamu kuwa “mwana wa Mungu.” (Luka 3:23, 38) Wala Adamu wala Yesu hakuwa na baba wa kibinadamu; hakuna mmoja wao aliyezaliwa kutokana na ngono iliyofanywa na mwanamke fulani. Kwa hiyo, Adamu alikuwa mwana wa Mungu, na ndivyo ilivyo na Yesu.

c Mtazamo wa Yesu unalingana na wa Yehova, kama unavyoonyesha katika Zaburi ya 103 na Isaya 1:18-20.

d Twaweza kusoma unabii huo katika Mathayo sura ya 24, Marko sura ya 13, na Luka sura ya 21.

e Angalau wawili kati yao baadaye wakawa wanafunzi na wakaandika barua za kitia-moyo zinazopatikana katika Biblia, Yakobo na Yuda.

f Ofisa mmoja Mroma mwenye cheo alisikia ushuhuda wa Petro wa mambo aliyojionea: “Nyinyi mwaijua habari iliyoongewa kotekote katika Yudea . . . Mungu alimfufua Huyu katika siku ya tatu na kumruhusu awe dhahiri . . . Alituagiza sisi tuwahubiri watu na kutoa ushahidi kamili kwamba Huyu ndiye aliyeagizwa na Mungu kuwa hakimu wa walio hai na wafu.”—Matendo 2:32; 3:15; 10:34-42.

[Sanduku katika ukurasa wa 150]

Huenda ukafurahia kulinganisha masimulizi yanayolingana ya jinsi Yesu alivyomponya mama-mkwe wa Petro. (Mathayo 8:14-17; Marko 1:29-31; Luka 4:38, 39) Tabibu Luka alitia ndani jambo la kitiba la kwamba huyo mama-mkwe alikuwa na “homa kali.” Ni nini kilichomwezesha Yesu amponye na kuponya wengine? Luka alikiri kwamba “nguvu ya Yehova ilikuwa hapo ili [Yesu] afanye uponyaji.”—Luka 5:17; 6:19; 9:43.

[Sanduku katika ukurasa wa 152]

Mahubiri Makuu Zaidi

Kiongozi wa Kihindu Mohandas Gandhi alinukuliwa akisema kwamba kwa kufuata mafundisho hayo, “tutakuwa tumetatua matatizo . . . ya ulimwengu wote.” Mtaalamu mashuhuri wa asili ya binadamu Ashley Montagu aliandika kwamba ugunduzi wa kisasa kuhusu umuhimu wa upendo kisaikolojia ni “uthibitisho” tu wa mahubiri hayo.

Watu hao walikuwa wakirejezea Mahubiri ya Mlimani ya Yesu. Gandhi alisema pia kwamba “mafundisho ya Mahubiri hayo yalikusudiwa kila mmoja wetu.” Hivi majuzi Profesa Hans Dieter Betz alisema hivi: “Mavutano ya yale Mahubiri ya Mlimani kwa ujumla yapita mipaka ya Dini ya Kiyahudi na Ukristo, au hata utamaduni wa Magharibi.” Aliongezea kusema ya kwamba mahubiri hayo “yana uvutio wa kipekee ulimwenguni pote.”

Mbona usisome hotuba hii fupi lakini yenye kuvutia? Utaipata katika Mathayo sura ya 5 hadi 7 na katika Luka 6:20-49. Hapa pana mambo makuu ambayo tunapata katika mahubiri hayo makuu zaidi:

Jinsi ya kuwa mwenye furaha—Mathayo 5:3-12; Luka 6:20-23.

Jinsi ya kudumisha kujistahi—Mathayo 5:14-16, 37; 6:2-4, 16-18; Luka 6:43-45.

Jinsi ya kuboresha uhusiano na wengine—Mathayo 5:22-26, 38-48; 7:1-5, 12; Luka 6:27-38, 41, 42.

Jinsi ya kupunguza matatizo ya familia—Mathayo 5:27-32.

Jinsi ya kukabiliana na mahangaiko—Mathayo 6:25-34.

Jinsi ya kutambua ubandia wa dini—Mathayo 6:5-8, 16-18; 7:15-23.

Jinsi ya kupata umaana wa maisha—Mathayo 6:9-13, 19-24, 33; 7:7-11, 13, 14, 24-27; Luka 6:46-49.

[Sanduku katika ukurasa wa 159]

Mtu wa Matendo

Yesu Kristo hakuwa mtu ajitengaye asiyetenda. Yeye alikuwa mtu mwenye kauli moja na mwenye matendo. Alisafiri “vijijini katika mzunguko, akifundisha,” akiwasaidia watu ambao walikuwa ‘wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.’ (Marko 6:6; Mathayo 9:36; Luka 8:1) Tofauti na viongozi wengi wa kidini wa sasa walio matajiri, Yesu hakujirundikia mali, hakuwa na “mahali popote pa kulaza kichwa chake.”—Mathayo 8:20.

Ingawa Yesu alikazia jitihada zake kwenye uponyaji na ulishaji wa kiroho, hakupuuza mahitaji ya kimwili ya watu. Aliwaponya wagonjwa, walemavu, na waliopagawa na roho waovu. (Marko 1:32-34) Mara mbili alilisha maelfu ya wasikilizaji wenye hamu kwa sababu aliwahurumia. (Marko 6:35-44; 8:1-8) Alifanya miujiza kwa sababu aliwahangaikia watu.—Marko 1:40-42.

Yesu alitenda kwa kauli moja alipowaondosha wafanya-biashara wenye pupa kutoka hekaluni. Wale waliomtazama walikumbuka maneno ya mtunga-zaburi: “Bidii kwa ajili ya nyumba yako itanila mimi kabisa.” (Yohana 2:14-17) Aliwashutumu waziwazi viongozi wa kidini wenye unafiki. (Mathayo 23:1-39) Wala hakushindwa na mkazo wa watu maarufu kisiasa.—Mathayo 26:59-64; Yohana 18:33-37.

Utasisimuka sana kusoma huduma yenye nguvu ya Yesu. Wengi ambao huisoma kwa mara ya kwanza huanza na masimulizi mafupi lakini yenye kusisimua ya Marko juu ya mtu huyo wa matendo.

[Sanduku katika ukurasa wa 164]

Yesu Aliwachochea Watende

Katika kitabu cha Matendo, tunaweza kupata rekodi ya kihistoria ya jinsi Petro, Yohana, na wengine walivyotoa ushahidi kuhusu ufufuo wa Yesu. Sehemu kubwa ya kitabu hicho inasimulia matukio yanayohusu mwanafunzi mmoja wa sheria mwerevu aliyeitwa Sauli, au Paulo, ambaye aliupinga Ukristo kijeuri sana. Yesu aliyefufuliwa alimtokea. (Matendo 9:1-16) Akiwa na uthibitisho usioweza kukanushwa kwamba Yesu alikuwa hai mbinguni, baadaye Paulo alitoa ushahidi kwa bidii kuhusu jambo hilo kwa Wayahudi na kwa wasio-Wayahudi, kutia ndani wanafalsafa na watawala. Inavutia kusoma kile alichowaambia watu mashuhuri na wenye elimu kama hao.—Matendo 17:1-3, 16-34; 26:1-29.

Katika kipindi cha miongo kadhaa, Paulo aliandika vitabu vingi vya lile liitwalo Agano Jipya, au Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Biblia nyingi zina orodha ya yaliyomo, au orodha ya vitabu. Paulo aliandika vitabu 14 kati ya hivyo, tokea Waroma hadi Waebrania. Vitabu hivyo viliandaa kweli za ndani na mwongozo wenye hekima kwa Wakristo wa wakati huo. Na vitabu hivyo ni muhimu hata zaidi kwetu, sisi ambao hatukupata kuwaona moja kwa moja mitume na mashahidi wengine wa mafundisho, matendo, na ufufuo wa Yesu. Utapata kwamba maandiko ya Paulo yanaweza kukusaidia katika maisha yako ya familia, katika shughuli zako na wafanyakazi wenzako na majirani, na katika kuongoza maisha yako ili yawe na maana halisi na yenye kukuletea uradhi.

[Picha katika ukurasa wa 146]

Wanasayansi hutungisha mimba nje ya mwili. Muumba alihamisha uhai wa Mwana wake awe binadamu

[Picha katika ukurasa wa 148]

Wengi waliomsikia Yesu na kuona jinsi alivyowatendea wanadamu walipata kumjua Baba vizuri zaidi

[Picha katika ukurasa wa 154]

Yesu aliosha miguu ya mitume, akiweka kiolezo cha unyenyekevu ambacho Muumba huthamini

[Picha katika ukurasa wa 157]

Kasoro ya kompyuta yaweza kuondolewa kabisa kutoka kwenye mfumo; wanadamu wanahitaji fidia ya Yesu ili kuondolea mbali kutokamilika kulikorithiwa

[Picha katika ukurasa wa 163]

Mashahidi waliona Yesu akiwa amewekwa ndani ya kaburi (kama hili), akafufuliwa siku ya tatu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki