Je! Wewe Unafanya Wasiwasi Juu ya Watoto Wako?
BILA shaka unafanya hivyo! Magonjwa, matumizi mabaya ya dawa za kulevya na kutokutii kwa watoto ni matatu tu kati ya matatizo ambayo wewe unajua yanahatirisha watoto wako. Ni jambo la kawaida wazazi kuhangaikia watoto wao—hata kufanya wasiwasi juu yao.
Hivyo ndivyo wazazi walio wengi wamehisi muda wote wa historia, kama Biblia inavyoonyesha. Kumbuka kwamba Yakobo alituma Yusufu akaangalie hali ya ndugu zake kwa sababu Yakobo aliwahangaikia. (Mwanzo 37:13, 14) Ayubu, pia, alifanya wasiwasi, hata ingawa wanaye walikuwa watu wazima wenye jamaa zao wenyewe. Yeye alifikiri hivi: “Labda wana wangu wametenda dhambi na wamelaani Mungu katika moyo wao.”—Ayubu 1:4, 5, NW.
Ndiyo, hata Yusufu na Mariamu walihangaikia Yesu mwana wao mkamilifu! Kwa kweli, katika pindi moja Yesu alipokuwa na umri wa miaka 12, wao walifanya wasiwasi juu yake kwa njia ya pekee, kwa maana walikuta kwamba alikuwa amekosekana. Hata hivyo, Yesu mtoto wao alikuwa akiwaletea sifa nzuri, na hawakuwa na jambo lote la kufanya wajiletee suto. Ebu tuone jambo hasa lililotukia katika pindi hiyo inayokumbukika na tufikirie ni masomo gani ambayo wazazi wa kisasa wanaweza kupata kutokana nalo.
Mwana Aliyepotea
Ikiwa wewe ni mzazi, labda unaweza kumhurumia Mariamu kwa hisia zake wakati yeye alipogombeza Yesu kwa kusema: “Mwana, mbona wewe umetutenda sisi jambo hili? Baba yako na mimi tumekuwa na wasiwasi mwingi mno tukijaribu kukupata wewe.” Yusufu na Mariamu walikuwa wametenganishwa na Yesu kwa muda wa siku tatu. Unaweza kuthamini sababu iliyowafanya wafadhaike wakifikiria mahali aliko mvulana wao wa miaka 12.—Luka 2:48, Today’s English Version.
Kwa sababu gani Yusufu na Mariamu walimpoteza Yesu? Mwelezaji anayejulikana sana aliwachambua wao kwa kufanya hivyo, akiandika hivi: “Kwa kujua kwamba yeye alikuwa hazina kubwa sana kwao, wangewezaje kukawia sana hivyo kuitafuta hazina hiyo? Zilikuwa wapi huruma na hangaiko jororo la mama yule?” Lakini kwa kweli, kama vile tutakavyoona, uchanganuzi wa karibu juu ya usimulizi huo unawaondelea Yusufu na Mariamu lawama nzito.
Uhakika ni kwamba Biblia inaonyesha kwamba Mariamu alikuwa mwanamke mzuri sana na mama mwema. Wakati malaika Gabrieli alipokuja kutangaza kuzaliwa kwa Yesu, yeye alisema kwamba Mariamu alikuwa “amepata upendeleo kwa Mungu.” (Luka 1:28, 30, NW) Yeye alikubali kwa nia mgawo wa kuzaa mtoto-mwanamume huyo wa pekee, pamoja na lile daraka zito la kumlea na kumpa mazoezi. Yeye alikuwa mwanamke wa unyenyekevu na imani yenye nguvu katika Mungu. Baada ya kuzaliwa kwa Yesu yeye alifanya kila jambo lililotakwa na Sheria ya Yehova, “sawasawa na ilivyoandikwa.”—Luka 1:38, 45-48; 2:21-23, 39.
Yusufu, mwanamume yule aliyemwoa Mariamu na akawa baba mlezi wa Yesu, alikuwa pia mwanamume mzuri sana mwenye uadilifu aliyekuwa amekuwa na upashani habari pamoja na malaika wa Yehova katika pindi nne. (Mathayo 1:19, 20; 2:13, 19, 22) Kumbuka, Yehova aliwachagua Yusufu na Mariamu walee Mwana Wake mzaliwa-pekee, mwenye thamani kubwa. Je! Mungu angalifanya punde kuliko kuchagua mwanamume na mwanamke ambao wangefanya vizuri katika kusaidia mwana huyo akue katika hekima ya kimungu?
Bila shaka, inaelekea wazazi leo wanafanya wasiwasi juu ya watoto wao kwa sababu ya kuwa na mazingira hatari na yenye ukosefu wa kutokutii. Nao wanajua kwamba watoto wao si wakamilifu, kama alivyokuwa Yesu. Na bado, sisi tunaweza kufaidika na mfano wa Yusufu, Mariamu, na Yesu.