Maisha na Huduma ya Yesu
Kunufaika Kutokana na Mifano ya Yesu
WANAFUNZI wanapomjia Yesu baada ya hotuba yake kwa umati wa watu ufuoni mwa bahari, wanataka kujua juu ya njia yake mpya ya kufundisha. Oh, wamemsikia akitumia mifano mbeleni lakini si kwa wingi sana hivyo. Basi wanataka kujua: “Ni kwa sababu gani wewe unasema nao kwa matumizi ya mifano?”
Sababu moja ya yeye kufanya hivyo ni kwa kutimiza maneno ya manabii: “Mimi nitafumbua kinywa changu kwa mifano, nitatangaza mambo yaliyofichwa tangu kuwekwa misingi [ya dunia].” Lakini kuna mengi zaidi ya hilo katika jambo hili. Matumizi yake ya mifano hutumikia kusudi la kusaidia kufichua mwelekeo wa moyoni wa watu.
Kwa kweli, watu wengi wanapendezwa katika Yesu akiwa tu msimuliaji hadithi mstadi na mfanya miujiza, si akiwa mmoja anayepasa kutumikiwa akiwa Bwana na kufuatwa bila ubinafsi. Wao hawataki kusumbuliwa katika maoni yao juu ya mambo au njia yao ya maisha. Wao hawataki ujumbe upenye kwa kadiri hiyo. Basi Yesu anasema hivi:
“Hii ndiyo sababu mimi nasema nao kwa matumizi ya mifano, kwa sababu, kutazama, watazama bure, na kusikia, wasikia bure, wala hawapati maana yalo; na kuwaelekea unabii wa Isaya unapata utimizo, usemao, ‘... Kwa kuwa moyo wa watu hawa umekuwa usioitikia.’”
“Hata hivyo,” Yesu anaendelea, “yenye furaha ni macho yenu kwa sababu yanaona, na masikio yenu kwa sababu yanasikia. Kwa kuwa kweli kweli mimi nawaambia ninyi, Manabii wengi na watu waadilifu walitamani kuona mambo mnayoyaona ninyi na hawakuyaona, na kusikia mambo mnayoyasikia ninyi na hawakuyasikia.”
Ndiyo, wale mitume kumi na wawili na wale waliokuwa pamoja nao wana mioyo yenye kuitikia. Kwa hiyo Yesu anasema hivi: “Kwa ninyi imejaliwa kufahamu zile siri takatifu za ufalme wa mbinguni, lakini kwa watu hawa haikujaliwa.” Kwa sababu ya tamaa yao ya kufahamu, Yesu anaandalia wanafunzi wake elezo la mfano wa mpanzi.
“Ile mbegu ni neno la Mungu,” Yesu asema, na ule udongo ni moyo. Kwa habari ya ile mbegu iliyopandwa juu ya kando ya barabara ngumu, yeye anaeleza: “Yule mwovu huja na kunyakua neno kutoka mioyo yao ili kwamba wasiamini na kuokolewa.”
Kwa upande mwingine, mbegu iliyopandwa katika udongo ulio juu ya mwamba inaelekeza kwenye mioyo ya watu wanaolipokea lile neno kwa furaha. Hata hivyo, kwa sababu neno haliwezi kutia mizizi yenye kina katika mioyo kama hiyo, watu hao wanaanguka kando wakati muda wa kujaribiwa au mateso ufikapo.
Kwa habari ya mbegu iliyoanguka miongoni mwa miiba, Yesu anaendelea, hiyo inaelekeza kwa watu waliolisikia lile neno. Hata hivyo, hawa, wanachukuliwa na mahangaikio na utajiri na anasa za maisha haya, hivyo wanasongwa kabisa wasilete cho chote katika ukamilifu.
Mwishowe, kwa habari ya ile mbegu iliyopandwa katika udongo mzuri, Yesu anasema, hao ndio wale ambao , baada ya kulisikia lile neno kwa moyo mzuri na mwema, wanabaki nalo na kuzaa tunda kwa uvumilivu.
Jinsi walivyobarikiwa wanafunzi hao waliomtafuta Yesu wapate elezo la mafundisho yake! Yesu anakusudia kwamba mifano yake ifahamiwe, ili iwape wengine ukweli. “Taa hailetwi ikawekwe chini ya kikapo cha kupimia au chini ya kitanda, sivyo?” yeye auliza. Hapana, “inaletwa ikawekwe juu ya kinara cha taa.” Hivyo Yesu anaongeza: “Kwa hiyo, angalieni jinsi mnavyosikiliza ninyi.” Mathayo 13:10-23, 34-36, NW; Marko 4:10-25, 33, 34, NW; Luka 8:9-18, NW; Zaburi 78:2, NW; Isaya 6:9, 10, NW.
◆ Ni kwa sababu gani Yesu alisema katika mifano?
◆ Wanafunzi wa Yesu walijionyeshaje wenyewe kuwa tofauti na umati wa watu?
◆ Yesu anaandaa elezo gani la mfano wa mpanzi?