‘Kikombe Changu Kimekuwa Kimejaa’
Kama ilivyosimuliwa na Tarissa P. Gott
“KWA SABABU gani jambo hili likapasa kutukia?” Mume wangu na mimi tulijiuliza ulizo hili tukiwa tumeketi katika kikokoteni cha farasi na kushika jeneza dogo mikononi mwetu. Kivulana changu kichanga kilikuwa kimepatwa na msokoto mkali wa tumbo nacho kikafa katika majuma machache. Huko nyuma katika 1914, haikufahamiwa sana jambo la kuufanya ugonjwa huo. Lilikuwa jambo baya sana kupenda kitoto kichanga kwa miezi sita, kukiona kikikupa tabasamu, kisha kifo kikunyang’anye kutoka mikononi mwako. Moyo wangu ulivunjika.
Mama yangu alitutembelea wakati huo wenye huzuni na kuanza kutufariji kwa ujumbe wa Biblia kuhusu ufufuo. Ujumbe huo ulitusaidia sana. Kilikuwa kitulizo kilichoje kwa mume wangu Walter na mimi kujifunza kwamba ingewezekana sisi kumwona tena Stanley wetu mdogo.
Huo haukuwa wakati wangu wa kwanza kukutana na ukweli wa Biblia. Muda fulani kabla, babu yangu alikuwa amepata mabuku matatu ya kwanza ya Studies in the Scriptures, ya Charles Taze Russell. Yale ambayo Babu alikuwa ameyasoma katika vitabu hivyo, pamoja na funzo lake la Biblia, yalimsukuma kwenda nje na kuhubiri. Jambo hili liliwaghadhibisha sana viongozi wa kidini wa mahali hapo, ambao walimfukuza kutoka makanisani katika Providence, Rhode Island. Mama hakupata tena kwenda kanisani baada ya hapo. Sasa yeye pamoja na babu walihudhuria mikutano ya Wanafunzi wa Biblia, lakini mimi sikufanya mengi sana na ukweli wakati huo.
Nikiwa na miaka 16, niliolewa na kijana mmoja, Walter Skillings, nasi tukatulia katika Providence. Sisi sote tulitamani sana kushirikiana na watu ambao walilipenda Neno la Mungu. Ijapokuwa kufikia 1914 tulikuwa na binti mwenye umri wa miaka sita, Lillian, haikuwa mpaka kivulana wetu mchanga alipokufa ndipo yale ambayo mama alikuwa ametuambia juu ya ukweli yakaingia moyoni. Mwaka uliofuata, 1915, mume wangu pamoja nami tulibatizwa na Wanafunzi wa Biblia. Ubatizo wetu ulifanyika wakati wa kiangazi kwenye ufuo mmoja wa karibu. Mimi nilivalia kanzu nyeusi yenye shingo ndefu na mikono mirefu, tofauti sana na mavazi ya kuogelea yanayovaliwa sasa. Bila shaka, hilo halikuwa vazi la kawaida la kuvaa ufuoni siku hizo lakini lilitolewa kama vazi la pekee kwa ajili ya ubatizo.
Baada ya ubatizo wetu, maisha yetu yalibadilika. Walter alifanyia kazi Kampuni ya Lynn ya Gesi na Umeme, na wakati wa majira ya baridi, nyakati nyingine yeye alipelekwa kwenye makanisa mbalimbali ili aiyeyushe mifumo yao ya maji iliyogandamana barafu. Yeye alikuwa akiitumia kwa faida nafasi hii kuandika Maandiko katika ubao wa kanisa, maandiko ambayo yalionyesha mambo ambayo Biblia inasema juu ya kutokufa, Utatu, moto wa mateso, na kadhalika.—Ezekieli 18:4; Yohana 14:28; Mhubiri 9:5, 10.
Tungeenda Wapi?
Katika 1916 Ndugu Russell, msimamizi wa kwanza wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi Biblia na Trakti, alikufa, na ilionekana kwamba kila kitu kilibomoka-bomoka. Sasa wengi wa wale waliokuwa wameonekana kama wenye nguvu sana, waliojitolea sana Bwana, walianza kugeukia kwingine. Ilionekana wazi kwamba wengine walikuwa wamekuwa wakifuata mwanadamu badala ya Yehova na Kristo Yesu.
Wazee wawili ambao walisimamia kundi letu walifuatana na kikundi chenye kupinga na hivyo wakawa washiriki wa jamii ya ‘mtumwa mwovu.’ (Mathayo 24:48) Yote haya hayakuonekana kuwa sawa hata kidogo, lakini yalikuwa yakitukia, nayo yalituudhi. Lakini mimi nilijiambia: ‘Je! si tengenezo hili ambalo Yehova alitumia kutuweka huru kutoka katika vifungo vya dini ya uwongo? Je! sisi hatukuonja wema wake? Kama tungeondoka sasa, tungeenda wapi? Je! hatungejikuta mwishowe tukifuata mwanadamu fulani?’ Hatukuweza kuona sababu ya kwenda pamoja na wapinga-Kristo, hivyo tukabaki.—Yohana 6:68; Waebrania 6:4-6.
Msiba Watokea Tena
Mume wangu alishikwa na homa ya Kihispania, na tarehe 9 ya Januari 9, 1919, akafa huku mimi nikiwa nimezuiliwa kitandani na ugonjwa huo. Mimi nilipona ugonjwa wangu, lakini nilimkosa Walter sana.
Walter akiwa amekwenda, ilinilazimu niende kazini, hivyo niliiuza nyumba yangu nikahama ili niishi na dada wa kiroho. Niliiweka fanicha yangu katika nyumba ya dada mwingine katika Saugus, Massachusetts. Mwanaye, Fred A. Gott, akawa mume wangu wa pili baadaye. Tulioana katika 1921, na katika muda wa miaka mitatu iliyofuata, tukawa wazazi wa Fred na Shirley.
Suala la Kusalimu Bendera
Baadaye, Fred na Shirley walipoenda kwenye shule ya watu wote, suala la kuisalimu bendera lilitokea. Suala hilo lilikazia fundisho la Biblia kwamba “ikimbieni ibada ya sanamu.” (1 Wakorintho 10:14) Ndugu mmoja kijana katika Kundi la Lynn alikuwa amekataa kuisalimu na kuahidi kuitii bendera. Katika muda wa mwezi mmoja baada ya hapo, watoto saba kundini walifukuzwa shuleni, Fred na Shirley wakiwa miongoni mwao.
Lazima nikiri kwamba ulikuwa mshangao kidogo kwetu kwamba watoto wetu walichukua msimamo huo shuleni. Bila shaka, tulikuwa tumewafundisha heshima kwa nchi na bendera, na pia tulikuwa tumewafundisha juu ya amri za Mungu za kutoinamia mifano na sanamu. Kama wazazi, hatukutaka watoto wetu wafukuzwe shuleni. Lakini kwa kuwa sasa suala hilo lilikuwa limelazimishwa, ilionekana kuwa inafaa kabisa wachukue msimamo kwa ajili ya Ufalme wa Mungu. Hivyo kwa kupima uzito wa mambo, tulithamini kwamba watoto wetu walikuwa wakifanya jambo linalofaa na ikiwa tungemtumaini Yehova yote yangetokeza ushuhuda kwa jina lake.
Shule ya Ufalme Yapangwa
Sasa swali lilikuwa, Watoto watapataje elimu yao? Kwa muda fulani tulijaribu kuwafundisha nyumbani kwa vitabu vyo vyote vya mafundisho ambavyo tuliweza kukusanya. Lakini mume wangu nami tulikuwa na wakati mgumu sana mwaka huo wa kwanza wa shule tulipokuwa tukijaribu kuwaelimisha watoto wetu wawili. Mume wangu alikuwa akifanya kazi ya wakati wote, nami nilikuwa nikifulia watu nguo na kuzipiga pasi ili kuongezea malipo ya kila juma. Kwa kuongezea hilo, nilikuwa na mwana wa kutunza mwenye umri wa miaka mitano, Robert.
Karibu tu na wakati huo, wakati wa majira ya 1936, Cora Foster, dada mmoja katika kundi aliyekuwa mwalimu katika shule za watu wote za Lynn kwa miaka 40, alifukuzwa kazini kwa sababu ya kutoisalimu bendera na kutokubali kiapo cha walimu ambacho kilikuwa desturi wakati huo. Kwa sababu hii ikapangwa kwamba Cora angewafundisha watoto ambao walikuwa wamefukuzwa shuleni na kwamba nyumba yetu ingetumiwa kama Shule ya Ufalme. Cora alipanga piano yake ikahamishwa kuletwa kwenye nyumba yetu pamoja na vitabu vingine vya mafundisho ambavyo watoto wangetumia, na wengine wa wavulana wenye umri mkubwa wakatengeneza madawati kutoka masanduku ya machungwa na tabaka za mbao. Tulianza shule mwishoni mwa mwaka huku watoto kumi wakihudhuria.
Mwana wangu mdogo, Robert, alianza elimu yake kwa kuhudhuria darasa la kwanza la Shule ya Ufalme. “Kabla ya kuanza somo letu la kawaida darasani,” Robert anakumbuka, “Shule ya Ufalme ilifunguliwa kwa wimbo wa Ufalme kila siku, kisha kwa nusu saa tungejifunza somo la Mnara wa Mlinzi la juma lililofuata.” Siku hizo Sosaiti haikuchapisha maulizo kwa mafungu ya makala ya kujifunza, hivyo likawa daraka la watoto kutokeza maulizo kwa mafungu ambayo yangetumiwa kwenye mkutano wa kundi.
Cora alikuwa mwalimu mwenye kujitoa. “Niliposhikwa na kifaduro,” anakumbuka Robert, na shule ikawa imefungwa mpaka ugonjwa huo wenye kuambukia ukapungua, “Dada Foster alitembelea nyumba ya kila mwanafunzi na kumpa mgawo wa shuleni wa kufanyia nyumbani.” Ajapokuwa mwenye kujitoa, lazima awe alihisi kuvurugika mawazo nyakati nyingine, kwa sababu ilimlazimu kuwafundisha wanafunzi katika madarasa yote 12 katika chumba kimoja. Mwishoni mwa kipindi cha miaka mitano ambacho tulikuwa na Shule ya Ufalme katika nyumba yetu, walikuwako watoto 22 waliokuwa wakihudhuria shule hiyo.
Ubaguzi na Fadhili
Suala la kuisalimu bendera halikutokeza tu wakati wa jaribu na mikazo bali pia lilitangazwa sana magazetini na katika redio. Lilikuwa jambo la kawaida sana kuwaona wapigaji picha mbele ya nyumba yetu wakipiga picha za watoto wakiwasili kwenye Shule ya Ufalme. Wengi wa jirani zetu ambao mwanzoni walikuwa wenye urafiki sana, sasa wakawa wenye uadui. Waliliona kuwa jambo baya sana watoto wetu kukataa kuisalimu bendera ya Amerika. ‘Ingawaje,’ wangesema, ‘je! si nchi hii inayowapa ninyi mkate na siagi?’ Wao hawakuthamini kwamba bila utunzaji wa Yehova hakungekuwa na mkate wala siagi.
Kwa upande mwingine, kulikuwa wengine ambao waliyaelewa masuala yaliyohusika nao wakatupa tegemezo. Wakati watu wa ujirani walipokataa kununua bidhaa kutoka duka ambalo mwangalizi-msimamizi wa kundi letu alikuwa meneja, mtu mwema aliyependezwa na uhuru wa kiraia alinunua nyingi za bidhaa hizo katika duka hilo na kuwagawia bure akina ndugu kundini.
Haikuwa mpaka 1943, wakati Mahakama Kuu ya United States ilipogeuza msimamo wayo kuhusu suala la kuisalimu bendera, ndipo mwanangu Robert aliporuhusiwa kuingia katika shule ya watu wote,
‘Kikombe Changu Kimekuwa Kimejaa’
Nilikuwa mwenye furaha namna gani kumwona Robert akiyaweka maisha yake wakfu kwa Yehova na kubatizwa kwenye mkusanyiko katika St. Louis katika 1941. Pia, kwenye mkusanyiko huo ndiko watoto wangu wote watatu walipendelewa kuwa miongoni mwa wale wengi waliopokea bure nakala yao binafsi ya kitabu Children kutoka kwa Ndugu Rutherford, aliyekuwa msimamizi wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi wakati huo.
Katika 1943 mwana wangu mkubwa, Fred, aliichukua huduma ya painia wa wakati wote. Hata hivyo, hiyo iliendelea kwa miezi michache tu kwa kuwa Vita ya Ulimwengu ya Pili ilikuwa ikipiganwa, na yeye alikuwa wa umri wa kuandikishwa awe mpigaji-vita. Wakati baraza la mahali petu la kuchagua wapigaji-vita lilipokataa kutambua madai yake ya kutoandikishwa kwa sababu ni mhudumu, baada ya hapo alihukumiwa miaka mitatu katika gereza kuu la serikali Danbury, Connecticut. Katika 1946 alifunguliwa, na kufikia mwishoni mwa mwaka huo, alikuwa mfanya kazi wa wakati wote katika makao makuu ya ulimwengu ya Sosaiti ya Mnara ya Mlinzi katika Brooklyn, New York, ambako alifurahia miaka kadha ya utumishi. Sasa yeye ni mwangalizi, akitumikia pamoja na jamaa yake katika Providence, Rhode Island.
Katika 1951, Robert pia alialikwa Betheli, naye angali huko mpaka leo hii pamoja na mkeye Alice. Yeye, pia, ni mwangalizi, katika kundi moja la Mji wa New York.
Kisha kuna binti yangu mpendwa Shirley, ambaye amebaki nyumbani. Alitunza mume wangu na mimi mpaka mume wangu alipokufa katika 1972; tangu wakati huo yeye amekuwa faraja kubwa kwangu mimi. Sijui sana vile mambo yangekuwa bila yeye, lakini namshukuru Yehova kwa upendo wa Shirley na bidii ya kujitoa kwake.
Mimi nina umri wa miaka 95 sasa, na hata hivyo tumaini la mfumo mpya wa Yehova lingali linang’aa zaidi na zaidi. Nyakati nyingine ninajikuta nikisema, “Kama tu ningalikuwa na nguvu nilizokuwa nazo wakati uliopita.” Siwezi tena kwenda nyumba kwa nyumba, lakini kwa muda ambao nina ulimi, nitaendelea kumsifu Yehova. Nathamini pendeleo hili zaidi leo kuliko nilivyowahi kufanya katika maisha yangu yote. Ndiyo, ‘kikombe changu kimekuwa kimejaa.’—Zaburi 23:5, NW.
[Picha katika ukurasa wa 21]
Shule ya Ufalme ikiongozwa katika kao letu wakati wa miaka ya 1930
[Picha katika ukurasa wa 23]
Tarissa Gott pamoja na Robert, Shirley, na Fred