Je! Msalaba Ni kwa Ajili ya Wakristo?
“MAMA yangu alinipatia huo.” “Ni kiume.” “Mimi nauvaa kama pambo.” “Ningekosa utulivu nisipouvaa.” “Unanilinda mimi na mabaya.” “Ni kitu cha kuning’inia kwenye mkufu tu.”
Ndivyo walivyojibu watu mbalimbali walioulizwa kwa nini wanauvaa msalaba. Ingawa ni wazi kwamba si watu wote wanauovaa kwa sababu ya ibada ya kidini, kuuvaa msalaba ni jambo la kawaida katika sehemu fulani za ulimwengu. Hata vijana kutoka Urusi wameonwa wakiwa wameuvaa. Watu wengi wanaupa msalaba umaana mzito sana wa kidini, kwa kuwa, kama anavyosema kijana mmoja kwa urahisi, “ni mtakatifu.”
Lakini je! ni sawa kweli kwa Mkristo kuvaa msalaba? Je! unaonyesha kwa usahihi alivyokufa Kristo? Na je! kuna makatazo halali ya kutouvaa hata kama pambo tu? Ili tufahamu, ebu tuchunguze kwanza chanzo cha msalaba.
Je! Ni Mfano wa Kikristo?
Huenda ukadhani kwamba Wakristo ndio waliokuwa wa kwanza kutumia msalaba. Hata hivyo, The Encyclopedia Americana, kinazungumza juu ya “kutumiwa kwao kwa kikale na Wahindi na Wabudha katika India na China na Waajemi, Waashuri, na Wababuloni.” Vivyo hivyo, Chambers’s Encyclopaedia, (chapa ya 1969) kinasema kwamba msalaba “ulikuwa mfano ambao kwao maana ya kidini na kifumbo ilifungamanishwa muda mrefu kabla ya wakati wa Kikristo.”
Kwa kweli, hakuna ushuhuda wa kwamba Wakristo wa kwanza waliutumia msalaba katika ibada yao. Wakati wa siku za kwanza-kwanza za Ukristo, Waroma wapagani ndio waliotumia msalaba! The Companion Bible inasema: “Misalaba hiyo ilitumiwa kama mifano ya mungujua wa Kibabuloni, +, na inaonekana mara ya kwanza katika sarafu ya Julius Caesar, 100-44 B.C., halafu kwenye sarafu iliyopigwa chapa na mrithi wa Caesar (Augusto), 20 B.C.” Nyakati nyingine mungu-asili wa Kiroma Bacchus aliwakilishwa akiwa na kilemba cha kichwani chenye misalaba mingi.
Basi, msalaba ulipata kuwaje mfano wa Jumuiya ya Wakristo?
Konstantino na Msalaba
Katika 312 W.K., Konstantino, akitawala ile sehemu inayojulikana sasa kama Ufaransa na Uingereza, alielekea kupigana vita dhidi ya shemeji yake, Maxentius, wa Italia. Akiwa safarini imeripotiwa kwamba yeye aliona njozi—msalaba ambao ulikuwa na maneno “Hoc vince,” yanayomaanisha, “Kwa huu ushinde.” Baada ya ushindi wake, Konstantino akaufanya msalaba bendera ya majeshi yake. Baadaye Ukristo ulipokuwa dini ya serikali ya Milki ya Kiroma, msalaba ukawa mfano wa kanisa.
Lakini je! njozi hiyo ilitukia kweli? Kwa vyo vyote, masimulizi ya hekaya hii, yanasimuliwa na watu wanosemekana waliyasikia na yanahitilafiana sana. Kusema kweli, ingekuwa vigumu sana kupata mtu mwingine asiyefaa kupewa ufunuo wa kimungu kuliko Konstantino. Wakati wa tukio hilo linalokisiwa, yeye alikuwa mwabudu mwenye bidii wa mungu-jua. Hata Konstantino aliiweka wakfu Jumapili iwe siku ya kuabudu jua. Mwenendo wake baada ya ati kuongoka kwake pia ulitoa ushuhuda mdogo wa kujiweka kwake wakfu kabisa kwa kanuni zinazofaa. Maisha yake yaliongozwa na mauaji, hila, na kutaka cheo cha kisiasa. Inaonekana kwamba, kwa Konstantino, Ukristo ulikuwa chombo tu cha kisiasa cha kuunganisha milki iliyovunjika vipande-vipande.
Pia kuna ushuhuda mdogo sana kwamba aina ya msalaba ‘aliouona’ Konstantino uliwakilisha kweli chombo kilichotumiwa kumwua Kristo. Misalaba yenye umbo la X ikiwa na “P” juu yayo imechorwa kwenye sarafu nyingi alizozifanyiza Konstantino baadaye. (Ona picha.) An Expository Dictionary of New Testament Words, cha W. E. Vine, kinasema: “Kwa habari ya Chi, au X, ambayo Konstantino alitangaza kwamba alikuwa ameona katika njozi iliyomwelekeza kuishindania imani ya Kikristo, herufi hiyo ilikuwa herufi ya kwanza ya neno ‘Kristo’ [katika lugha ya Kigiriki] na haikuhusiana kwa njia yo yote na ‘ule Msalaba,’” yaani, kama chombo cha kufishia. Kwa kweli, msalaba wa aina hii unakaribia sana kufanana na mfano wa kipagani wa jua.
Kwa sababu gani, basi, msalaba ulikubaliwa kwa urahisi sana na “Wakristo”? Dictionary ya Vine inaendelea kusema: “Kufikia katikati ya [karne] ya 3 A.D. ama makanisa yalikuwa yameondoka, ama yalikuwa yamefanya mwigo uliopotoshwa, wa mafundisho fulani ya dini ya imani ya Kikristo. Ili kuongeza sifa ya mfumo wa makanisa wenye kuasi-imani wapagani walipokewa katika makanisa bila wongofu kwa njia ya imani, na hata waliruhusiwa sana kutunza ishara zao za kipagani na mifano. Kwa hiyo Tau au T, katika namna yayo ya kawaida sana ikiwa na kipande kilichokingama kimeshushwa, ilikubaliwa iwakilishe msalaba wa Kristo.”
Mageuzi ya Msalaba
Je! upendo kwa ajili ya Kristo ndio uliosababisha ule msalaba, wakati huu wa nyumaye, uwe kitu chenye kuheshimiwa? Encyclopaedia of Religion and Ethics kinasema: “[Kuanzia] na karne ya nne imani ya kiuchawi ilianza kushika kwa uthabiti zaidi ndani ya Kanisa.” Kama vile ilivyo kwa habari ya hirizi ya kiuchawi, kufanya tu ile ishara ya msalaba kulifikiriwa kuwa “ulinzi ulio hakika zaidi sana dhidi ya mashetani, na ponyo la magonjwa yote.” Matumizi ya msalaba ya ushirikina yanaendelea mpaka leo hii.
Wakati wa kupita kwa miaka, karibu mitindo 400 tofauti-tofauti ya misalaba imesitawi. Mwanzoni Kristo mwenyewe hakuonyeshwa. Bali, kijana mmoja mwenye kushika msalaba uliofanyizwa kwa kito angeonyeshwa. Baadaye, mwana-kondoo alitiwa ndani. Katika 691 W.K., baraza la Trullo lilifanya msalaba wenye kuonyesha kifua cha mwanamume kijana, badala ya kondoo, juu ya msalaba ule iwe “rasmi.” Baada ya kupita wakati uliendelea ukawa msalaba wenye sanamu ya Yesu akiwa amepigiliwa msalabani—msalaba wenye mfano wa mwili wa Kristo.
Je! Kristo Alikufa Msalabani?
Huenda mmoja akauliza hivi: ‘Lakini je! Biblia haifundishi kwamba Kristo kweli alikufa msalabani?’ Ili kujibu ulizo hili, ni lazima sisi tuchunguze maana ya maneno mawili ya kigiriki ambayo waandikaji wa Biblia walitumia ili kueleza chombo ambacho Kristo alikufa juu yacho: stauros’ na xy’lon.
The International Standard Bible Encyclopedia (1979) inasema hivi chini ya kichwa “Msalaba”: “Mwanzoni stauros’ ya Kigiriki ilimaanisha mti uliochongoka, ulio wima ukiwa umewekwa imara ardhini. . . . Uliwekwa upande kwa upande katika mistari-mistari ili kufanyiza ua au boma la kujilinda kuzunguka mji mdogo, au miti mmoja-mmoja iliwekwa kama vyombo vya mateso ambavyo juu yavyo wahalifu wabaya wa sheria wangetundikwa hadharani ili wafe (au, ikiwa walikuwa wameuawa tayari, maiti yao ingewekwa juu yao ili heshima yao ishushwe kabisa).”
Kweli, Waroma walitumia chombo cha kuua kinachojulikana katika Kilatini kama crux. Na katika kuitafsiri Biblia katika Kilatini neno hili crux lilitumiwa kwa kutafsiri stauros’. Kwa sababu neno la Kilatini crux na neno la Kiingereza cross yanafanana, watu wengi wanadhani kwa makosa kwamba crux kwa lazima ulikuwa mti wenye kisehemu kinachokingama. Hata hivyo, The Imperial Bible-Dictionary inasema: “Hata miongoni mwa Waroma crux (ambao kutoka kwao msalaba wetu ulipatikana) unaonekana kwamba mwanzoni ulikuwa mti ulio wima, na sikuzote hii iliendelea kuwa ndiyo sehemu yenye kutokeza sana.”
Kitabu kinachoitwa The Non-Christian Cross kinaongezea hivi: “Hakuna sentensi hata moja katika yo yote ya maandishi mengi yanayofanyiza Agano Jipya, ambamo, katika Kigiriki cha awali, yanatoa hata ushuhuda usio wa moja kwa moja kwa maana ya kwamba stauros iliyotumiwa kwa habari ya Yesu ilikuwa jambo jingine zaidi ya stauros ya kawaida [boriti au mti]; achia mbali maana ya kwamba ilifanyizwa kwa, si kipande kimoja cha mbao, bali vipande viwili vikiwa vimepigiliwa misumari pamoja kwa namna ya msalaba.” Kristo angaliweza kuwa alitundikwa kwa kufaa kwenye aina fulani ya crux (stauros’) unaojulikana kama crux simplex. Hivyo ndivyo mti wa aina hiyo ulivyoelezwa na mwanachuo wa Roma Katoliki Justus Lipsius wa karne ya 16.
Namna gani lile neno lingine la Kigiriki, xy’lon? Lilitumiwa katika tafsiri ya kigiriki ya Septuagint ya Biblia katika Ezra 6:11 katika tafsiri ya Biblia ya New World (Kingereza) mstari huo unasomwa hivi: “Na kupitia kwangu mimi amri imetolewa kwamba, mtu ye yote atakayevunja agizo hili, ubao utavutwa kutoka nyumba yake na yeye atatundikwa juu yao, na nyumba yake itageuzwa iwe msala wa watu wote kwa habari hii.” Kwa wazi, mti mmoja, au “ubao,” ndio uliohusika hapa.
Basi watafsiri wengi wa Maandiko ya Kikristo ya Kigiriki (Agano Jipya) wanayatafsiri maneno ya Petro katika Matendo 5:30 kusoma hivi: “Mungu wa babu zetu alimfufua Yesu, ambaye ninyi mlimwua mkimtundika katika mti [au “mutini,” Zaire Swahili Bible, The Jerusalem Bible, na Revised Standard Version].” Huenda pia ukataka kuchunguza jinsi Biblia yako inavyotafsiri xy’lon kwenye: Matendo 10:39; 13:29; Wagalatia 3:13; na 1 Petro 2:24.
Kutembea kwa Imani, Si kwa Kuona
Hata baada ya kuzungumzia ushuhuda huu wa kwamba kwa kweli Kristo alikufa mtini, huenda wengine wasione kosa lo lote katika kuuvaa msalaba. Huenda wakasema hivi: ‘Ni pambo tu.’
Ingawaje, kumbuka jinsi msalaba umetumiwa wakati wote wa historia—kama chombo cha ibada ya kipagani na cha ushirikina wenye kutisha. Je! kuuvaa msalaba, hata kama pambo tu, kunaweza kupatanishwa na onyo la upole la mtume Paulo kwenye 1 Wakorintho 10:14: “Kwa ajili ya hayo, wapenzi wangu, ikimbieni ibada ya sanamu”?
Namna gani Wakristo wa kweli leo? Yawapasa, wao pia, wadhamirie uhitaji wa ‘kujilinda na sanamu,’ kama inavyoshauri Biblia. (1 Yohana 5:21) Kwa hiyo wao hawauoni msalaba kuwa pambo linalofaa. Wao wanayakumbuka maneno ya Paulo, “amelaaniwa kila mtu aangikwaye juu ya mti,” na hivyo wanapendelea kumfikiria Kristo kuwa Mfalme mtukufu aliyetawazwa!—Wagalatia 3:13; Ufunuo 6:2.
Ijapokuwa Wakristo hawa hawavai misalaba, wao wanathamini kwa kina kirefu uhakika wa kwamba Kristo alikufa kwa ajili yao. Wao wanajua kwamba dhabihu ya Kristo ni wonyesho wa ajabu wa “nguvu ya Mungu” na upendo wa umilele. (1 Wakorintho 1:18; Yohana 3:16) Lakini wao hawahitaji kitu chenye kuonekana kama vile msalaba ili kiwasaidie wao kuabudu huyu Mungu wa upendo. Kwa kuwa, kama anavyosihi Paulo ‘wanaenenda kwa imani, si kwa kuona.’—2 Wakorintho 5:7.
[Picha katika ukurasa wa 22]
Msalaba umegeuka-geuka katika mitindo na umbo mbalimbali kwa muda wa karne zilizopita
[Picha katika ukurasa wa 23]
Sanamu ya mungu wa Kigiriki Marsyas iliyochunuliwa ikiwa hai kwenye kisiki cha mti—The Louvre, Paris