Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w89 5/1 kur. 23-28
  • Maana ya Kumpenda Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maana ya Kumpenda Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Utumizi wa Msalaba Katika Dini
  • Msalaba wa Konstantino
  • Je! Chombo Kilichotumiwa Kuua Kiheshimiwe Mno?
  • Kulishika Neno Lililovuviwa
  • “Huku Ndiko Kumpenda Mungu”
  • Je, Kweli Yesu Alikufa Juu ya Msalaba?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Je! Msalaba Ni kwa Ajili ya Wakristo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Kwa Nini Wakristo wa Kweli Hawatumii Msalaba Katika Ibada?
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Msalaba
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
w89 5/1 kur. 23-28

Maana ya Kumpenda Mungu

“Huku ndiko kumpenda Mungu, kwamba tuzishike amri zake.”​—1 YOHANA 5:3.

1. Tunapaswa kuonyeshaje upendo kwa Mungu, na tokeo litakuwa nini?

KUHUSU wajibu ambao wanadamu wanao kuabudu Mungu, Yesu alisema: “Ni lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili zako zote.” (Mathayo 22:37, NW) Tunapaswa kuonyeshaje upendo huu? Biblia inajibu hivi: “Huku ndiko kumpenda Mungu, kwamba tuzishike amri zake.” (1 Yohana 5:3) Tokeo likiwa nini kwa wanaofanya hivyo? Yohana alisema: “Yeye ambaye anabaki katika upendo anabaki katika muungano pamoja na Mungu.”​—⁠ 1 Yohana 4:16b, NW.

2. Nani peke yake anapaswa kupokea ibada yetu?

2 Tukipenda Mungu, hatutakipa kiumbe chochote ibada yetu, kilicho hai au kilichokufa, bali tutampa Mungu tu. (Luka 4:7, 8) Mtume Petro, na hata malaika, alikataa kukubali ibada kutoka kwa wanadamu. (Matendo 10:25, 26; Ufunuo 22:8, 9) Pia, Yesu alionyesha kwamba mama yake, Mariamu, hapasi kupewa heshima yoyote ya ibada, kwa maana ni ya Mungu peke yake. (Luka 11:27, 28; Yohana 2:3, 4; Ufunuo 4:11) Mtu akielekeza ibada yake mahali pasipofaa tokeo litakuwa kupingana na amri za Mungu, kwa maana “hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili.”​—⁠Mathayo 6:24.

Utumizi wa Msalaba Katika Dini

3. Jumuiya ya Wakristo ina maoni gani juu ya utumizi wa msalaba?

3 Pia kuna vitu fulani visivyo hai ambavyo vikiheshimiwa mno vinaweza kuongoza kwenye uvunjaji wa amri za Mungu. Miongoni mwa vile vikubwa zaidi ni msalaba. Kwa karne kadhaa umetumiwa na watu katika Jumuiya ya Wakristo ukiwa sehemu ya ibada yao. The New Encyclopcedia Britannica inaita msalaba “kifananishi kikuu cha dini ya Kikristo.” Katika kesi moja ya mahakamani katika Ugiriki, Kanisa Orthodoksi la Ugiriki hata lilishikilia kwamba wale wanaoukataa ‘Msalaba Mtakatifu’ si Wakristo. Lakini je! kweli msalaba ni kifananishi cha Kikristo? Ulianzia wapi?

4, 5. (a) Kamusi moja inasema nini juu ya neno stau·rosʹ, linalotafsiriwa “msalaba” katika Biblia fulani? (b) Utumizi wa msalaba ulianzia wapi?

4 Chombo kilichotumiwa kwa kifo cha Yesu kinaonwa katika vifungu vya Biblia, kama vile kwenye Mathayo 27:32 na 40. Humo neno la Kigiriki stau·rosʹ limetafsiriwa “msalaba” katika Biblia mbalimbali. Lakini staurosʹ lilimaanisha nini katika karne ya kwanza wakati Maandiko ya Kigiriki yalipoandikwa? An Expository Dictionary of New Testament Words, iliyotungwa na W. E. Vine, inasema: “stauros . . . huonyesha hasa mti uliochongoka au kiguzo chenye kusimama wima. Wahalifu walipigiliwa misumari kwa kuuawa juu ya miti ya jinsi hiyo. Jina lenyewe [stau·rosʹ] na pia kitenzi stauroō, kufungilia kwenye mti uliochongoka au kiguzo, hapo kwanza lilitofautiana na ile namna ya msalaba wenye maboriti mawili utumiwao na wanadini. Asili ya umbo la huu wa pili ilikuwa Kaldayo ya kale, nalo lilitumiwa kuwa ufananisho wa mungu Tammuzi (akiwa kwa umbo la Tau ya kifumbo, ambayo ndiyo herufi ya kwanza ya jina lake) katika nchi hiyo na mabara ya kando-kando, kutia na Misri.”

5 Vine anaendelea kusema: “Kufikia karne ya 3 A.D. makanisa yalikuwa ama yameondoka kwenye kanuni fulani zilizopokewa za imani ya Kikristo, ama yalikuwa yameziiga kwa ubandia. Ili kuongezea fahari ya mfumo wa uanadini wa kuasi imani, wapagani walipokewa ndani ya makanisa bila kuzaliwa upya kwa imani, na kwa kadiri kubwa waliruhusiwa kubaki na ishara na vifananishi vyao vya kipagani. Kwa sababu hiyo ile Tau au T ilichaguliwa isimamie msalaba wa Kristo, ikiwa kwa namna ile ya kawaida, kwa kushusha chini kidogo kile kipande chenye kukingama katikati.”

6, 7. (a) Neno “cross” (msalaba) limetoka wapi, na kwa nini halina haki ya kutumiwa? (b) Utumizi wa Biblia wa neno xyʹlon unashuhudizaje kwamba stau·rosʹ kilikuwa kiguzo kilichosimama wima?

6 Chini ya kichwa “The Cross and Crucifixion” (Msalaba na Usulubisho), The Companion Bible inataarifu hivi: “Neno letu la Kiingereza ‘cross’ [msalaba] ni tafsiri ya crux ya Kilatini; lakini stauros ya Kigiriki haimaanishi crux kama vile neno ‘kijiti’ lisivyomaanisha ‘mkongojo wa kuegemea.’ Homer anatumia neno stauros kuhusu ufito au kiguzo cha kawaida, au kipande kimoja tu cha mti. Na hiyo ndiyo maana na utumizi wa neno hilo katika maandishi yote ya Kigiriki sanifu. Halimaanishi kamwe vipande viwili vya mti vilivyokingamanishwa. . . . Katika Kigiriki cha A[gano] J[ipya] hamna jambo lolote hata la kugusia maana ya vipande viwili vya mti.”

7 Neno jingine la Kigiriki, xyʹlon, hutumiwa katika Biblia kutaja chombo ambacho Yesu aliuawa juu yacho. Neno hili linasaidia kuonyesha kwamba stau-rosʹ ulikuwa ufito wima usio na boriti la kukingama. Kama vile The Companion Bible inavyotaarifu: “Neno hilo [xyʹlon,] . . . kwa ujumla huonyesha kipande cha gogo kavu la ukuni, au mti, la kuwashia moto au la kusudi jingine lolote. . . . Kwa kuwa neno hili la pili [xyʹlon,] limetumiwa badala ya lile la kwanza stauros’ hiyo inatuonyesha kwamba kila moja lina maana ile ile kabisa. . . . Ndiyo sababu neno hilo [xyʹlon,] linatumiwa . . . kuhusiana na namna ya kifo cha Bwana wetu, na kutafsiriwa ‘mti’ katika Matendo 5:30; 10:39; 13:29; Wagalatia 3:13; 1 Petro 2:24 [King James Version].”

8. Vyanzo vingine vinasema nini kuhusu msalaba na asili yao?

8 Dictionnaire Encyclopedique Universel ya Kifaransa (Kamusi Inayohusisha Mambo Yote ya Kiensaiklopedia) inasema: “Kwa muda mrefu tuliamini kwamba msalaba, unaoonwa kuwa kifananishi cha kidini, ulikuwa kwa ajili ya Wakristo hasa. Sivyo ilivyo.” Kitabu Dual Heritage​—⁠The Bible and the British Museum kinataarifu hivi: “Huenda likawa jambo la kushtusha kujua kwamba katika Kigiriki cha Agano Jipya hamna neno kama ‘msalaba.’ Neno lililotafsiriwa ‘msalaba’ sikuzote huwa ni lile neno la Kigiriki [stau-rosʹ] linalomaanisha ‘kiguzo’ au ‘mti wima uliochongoka.’ Hapo kwanza msalaba haukuwa kifananishi cha Kikristo; chanzo chao ni kutoka Misri na kwa Konstantino.” New Catholic Encyclopedia inasema: “Sanaa ya kuchora vitu vya ufananishi katika karne za kwanza za Kikristo haikionyeshi kifo cha ukombozi wa Kristo kikitukia juu ya Golgotha. Kwa kuongozwa na katazo la Agano la Kale kuhusu mifano ya kuchongwa, Wakristo wa mapema hawakutaka kukichora hata chombo chenyewe kilichotumiwa kwa [kifo] cha Bwana. . . . Msalaba unakuja kuchorwa wakati wa Konstantino.”

Msalaba wa Konstantino

9. Mmaliki Konstantino anahusianishwaje na msalaba?

9 Konstantino ndiye mmaliki wa Kiroma aliyeitisha mkutano wa Baraza la Nikaya katika 325 W.K. na kulishawishi lichague kufuata kanuni hiyo iliyopokewa ambayo si ya Kimaandiko, kwamba Kristo alikuwa Mungu. Alifanya hivyo kuimarisha milki yake ya wapagani na Wakristo waasiimani. The Encyclopcedia Britannica inasema hivi juu yake: “Jioni iliyotangulia ushindi wa Konstantino juu ya Maxentius katika 312, yeye aliona njozi ya ‘ishara ya kimbingu’ ya msalaba, naye akaamini kwamba hiyo ilikuwa ishara ya kimungu kwamba yeye atapata shangwe ya ushindi.” Pia inasema kwamba baada ya hapo Konstantino alifanya msalaba uendelee kupewa heshima nyingi mno.

10. Kwa nini si jambo la kiakili wala la Kimaandiko kuamini kwamba Mungu au Kristo alimpa Konstantino “ishara” inayohusu msalaba?

10 Hata hivyo, je! Mungu angempa ishara kiongozi mpagani asiyekuwa akifanya penzi la Mungu, tena ishara ya kipagani? Yesu aliwakemea watu wa nchi yake mwenyewe kwa kutaka ishara. (Mathayo 12:38-40) Zaidi ya hilo, mtawala huyo mpagani alikuwa akimwaga damu isiyo na hatia kwa silaha za kimwili ili awazidi wengine wote kisiasa, na alifanya mipango ili watu wa ukoo na washirika wengine wauawe katika hila za kisiasa. Kinyume cha hilo, Yesu alisema: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungalikuwa sehemu ya ulimwengu huu, wahudumu wangu wangalikuwa wamepiga vita.” (Yohana 18:36, NW) Ndiyo sababu alimwamuru Petro hivi: “Rudisha upanga wako mahali pake; maana wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga.”​—⁠Mathayo 26:52.

11. Ni nini kilichosukuma Konstantino kuendeleza utumizi wa msalaba?

11 Kitabu Strange Survivals kinasema hivi juu ya Konstantino na msalaba wake: “Hatuwezi kutia shaka kwamba yeye alitumia mbinu ya ujanja; kifananishi alichoanzisha kiliridhisha Wakristo katika jeshi lake upande mmoja, na Wagauli [wapagani] upande ule mwingine. . . . Kwa hawa wa pili kilikuwa dalili ya kupendelewa na mungu-jua wao,” yule mungu-jua ambaye wao walimwabudu. Hapana, ‘ishara ya kimbingu’ ya Konstantino haikuhusiana kamwe na Mungu wala Kristo bali ni ya kipagani kabisa.

Je! Chombo Kilichotumiwa Kuua Kiheshimiwe Mno?

12, 13. Msalaba haupasi kuheshimiwa mno kwa sababu gani nyinginezo?

12 Hata tukipuuza ithibati na kuchukulia kwamba Yesu aliuawa juu ya msalaba, je! unapasa kuheshimiwa mno? Hapana, kwa maana Yesu aliuawa kama mhalifu, kama wanaume waliotundikwa kando yake, na njia iliyotumiwa kumuua ilimsingizia vibaya kabisa. Wakristo wa karne ya kwanza hawangekuwa walikiona kuwa kitakatifu chombo kilichotumiwa kumuua. Kukiheshimu mno kungalimaanisha kutukuza kosa lililofanywa juu yao, kuuawa kwa Yesu.

13 Ikiwa rafiki yako umpendaye zaidi angeuawa kwa mashtaka bandia, je! wewe ungefanyiza mfano wa chombo kilichotumiwa kumuua (tuseme kamba ya mnyongaji au kiti chenye nguvu za umeme au bunduki ya askari wanaofyatua watu waliojipanga mstari) halafu ubusu nakala hiyo, uchome mishumaa mbele yayo, au uivae shingoni kama pambo takatifu? Lingekuwa jambo lisilofikirika. Ndivyo ilivyo pia kuhusu kuwa na kicho kingi mno kwa msalaba. Uhakika wa kwamba msalaba una asili ya kipagani unaongezea tu ubaya wenyewe.

14. Ni lazima tukate shauri gani kuhusu msalaba kwa sababu ya ushuhuda wa habari za kilimwengu na wa Kibiblia?

14 Kuuheshimu mno msalaba si jambo la Kikristo. Hakuonyeshi upendo kwa Mungu wala Kristo bali kunapuuza mambo wanayopendelea. Kunavunja amri za Mungu dhidi ya ibada ya sanamu. Kunastahi mno kifananishi cha kipagani kinachosingiziwa kuwa cha Kikristo. (Kutoka 20:4, 5; Zaburi 115:4-8; 1 Wakorintho 10:14) Kufikiria kifananishi cha kipagani kuwa kitakatifu kunavunja amri ya Mungu: “Msifungiwe nira pamoja na wasioamini, kwa jinsi isivyo sawasawa; kwa maana pana urafiki gani kati ya haki [uadilifu, NW] na uasi? . . . Msiguse kitu kilicho kichafu.”​—⁠2 Wakorintho 6:14, 17.

Kulishika Neno Lililovuviwa

15. Kwa nini tunapaswa kukataa mapokeo yanayohitilafiana na Neno la Mungu?

15 Makanisa yanasema kwamba mazoea kama kuuheshimu mno msalaba ni sehemu ya “pokeo takatifu.” Lakini pokeo linapopingana na Neno la Mungu, wale wanaopenda Mungu wanakataa pokeo hilo. Mambo tunayohitaji kabisa kwa ibada ya kweli yametiwa tayari katika Neno la Mungu. Kama vile Paulo alivyoandikia Timotheo: “Kutoka utoto mchanga wewe umejua miandiko mitakatifu, ambayo inaweza kufanya wewe uwe mwenye hekima kwa ajili ya wokovu kupitia ile imani kuhusiana na Kristo Yesu. Andiko lote limevuviwa na Mungu na lina manufaa kwa kufundisha, kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu apate kuwa anaweza mambo kikamili, akiwa kabisa na vifaa kwa ajili ya kila kazi njema.” (2 Timotheo 3:15-17, NW) Biblia haisemi mahali popote kwamba mtu hawezi kupata wokovu akiondolea mbali mapokeo yanayopingana na Neno la Mungu.

16. Yesu alisema nini kwa viongozi wa kidini Wayahudi kuhusu mapokeo yao?

16 Hitilafiano kati ya Maandiko na pokeo la kibinadamu si jipya. Katika kipindi cha tangu kukamilishwa kwa Maandiko ya Kiebrania hadi kuja kwa Yesu, viongozi wa kidini Wayahudi waliongeza mapokeo mengi ya mdomo, ambayo baadaye waliyaingiza katika miandiko isiyovuviwa na Mungu. Mara nyingi mapokeo hayo yalihitilafiana na Maandiko. Basi Yesu aliwaambia hivi viongozi wa kidini: “Mbona ninyi nanyi huihalifu amri ya Mungu kwa ajili ya mapokeo yenu? . . . Mkalitangua neno la Mungu kwa ajili ya mapokeo yenu.” Yeye alitumia Neno la Mungu kuwahusu wao aliposema: “Nao waniabudu bure, wakifundisha mafundisho yaliyo maagizo ya wanadamu.” (Mathayo 15:1-6, 9) Yesu hakutaja kamwe mapokeo hayo katika mafundisho yake. Yeye alivuta fikira kwenye Neno la Mungu lililoandikwa.​—⁠Mathayo 4:4-10; Marko 12:10; Luka 10:26.

17. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Biblia ni nanga imara kwa tumaini letu?

17 Mungu hakukabidhi uhifadhi wa “neno la uhai” katika mikono isiyoaminika ya wanamapokeo wa kidini. (Wafilipi 2:16, NW) Bali, kwa roho takatifu yake iliyo na nguvu nyingi, alivuvia uandikaji wa Biblia ili kwa “faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini.” (Warumi 15:4) Kusema kwamba Biblia si kamili na kwamba pia tunahitaji kutegemea fikira za wanadamu wasiokamilika, wasiovuviwa, ni kukana nguvu za Mungu. Kwa uhakika, Muumba wa ulimwengu wote mzima ambaye ni mweza yote na wa kutisha, angeweza kuandika kitabu! Naye alifanya hivyo ili tuweze kuwa na nanga imara kwa tumaini letu na tusilazimike kutegemea mapokeo ya kibinadamu yanayoongoza watu kuvunja amri za Mungu. Kwa sababu hiyo, Neno la Mungu linasema: “Mpate kujifunza kutopita yale yaliyoandikwa.” (1 Wakorintho 4:6) Wale wanaopenda Mungu kikweli watafuata shauri hilo.​—⁠Ona pia Mithali 30:5, 6.

“Huku Ndiko Kumpenda Mungu”

18. Ikiwa tunapenda Mungu kikweli, ni lazima tutii amri gani?

18 “Huku ndiko kumpenda Mungu, kwamba tuzishike amri zake,” inataarifu 1 Yohana 5:3. Wakati viongozi wa kidini wanapopunguza uzito wa amri hizo, au kuzipuuza, au kuzibadili kwa mapokeo yenye kuhitilafiana ya wanadamu, hapo wanaongoza wafuasi wao kinyume cha penzi la Mungu. Kwa kielelezo, fikiria kanuni ya Ukristo iliyo ya msingi: upendo. Ilikuwa sehemu muhimu ya fundisho la Yesu. Yeye alisema: “Ni lazima wewe upende jirani yako kama wewe mwenyewe.”​—⁠Mathayo 22:39, NW.

19. (a) Ni jambo muhimu jinsi gani Wakristo wa kweli wapendane? (b) “Amri mpya” ambayo Yesu alitoa kuhusu upendo ilitofautianaje na ile ya zamani?

19 Upendo huu wa jirani ni wa maana jinsi gani? Yesu alifundisha kwamba Wakristo wa kweli wanaweza kutambulishwa na upendo walio nao miongoni mwao wenyewe. Yeye alisema: “Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo. Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:34, 35) Ni kweli, Sheria waliyopewa Israeli wa kale ilihusisha ndani amri ya ‘kumpenda jirani yako kama nafsi yako.’ (Walawi 19:18) Lakini jambo lililokuwa jipya kuhusiana na amri ya Yesu lilikuwa usemi wake, “kama vile nilivyowapenda ninyi.” Usemi huo uliutilia nguvu upendo wa Kikristo, kwa maana ni lazima Mkristo awe hata na nia ya kutoa uhai wake kwa ajili ya waamini wenzake, sawasawa na vile Yesu alivyofanya.

20. Kumbukumbu la historia ya karne hii inatambulisha nani kuwa wakitii amri ya ‘kupendana’?

20 Hivyo, watumishi wa kweli wa Mungu leo wanaweza kutambulishwa na kifungo kisichovunjika cha upendo wenye kuwaungamanisha katika mataifa yote. Ni akina nani katika wakati wetu wameonyesha utii huo kwa amri za Mungu kuhusu upendo? Ni akina nani wamenyanyaswa, wakatiwa gerezani, wakatupwa ndani ya kambi za mateso, au wakauawa kwa sababu walikataa kubeba silaha dhidi ya waamini wenzao​—⁠au hata dhidi ya wasio waamini​—⁠wa mataifa mengine? Kumbukumbu la historia ya karne hii linajibu: ni Mashahidi wa Yehova tu.

21. Makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yamefanyiza kumbukumbu la matendo gani kuhusu amri ya kupenda waamini wenzao?

21 Kwa upande ule mwingine, dini za Jumuiya ya Wakristo zimevunja kwa ukawaida amri za Mungu kuhusu upendo. Katika vita vyote vya karne hii, makasisi wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo wameongoza watu wao wakutane katika nyanja za vita wakiwa kwenye pande zinazopingana na kuuana kwa mamilioni. Waprotestanti waliua Waprotestanti wenzao, Wakatoliki wakaua Wakatoliki wenzao, na bado wote walidai kuwa ni Wakristo. Lakini Neno la Mungu linajulisha wazi hivi: “Mtu akisema, Nampenda Mungu, naye anamchukia ndugu yake, ni mwongo; kwa maana asiyempenda ndugu yake ambaye amemwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hakumwona. Na amri hii tumepewa na yeye, ya kwamba yeye ampendaye Mungu, ampende na ndugu yake.”​—⁠1 Yohana 4:20, 21.

22. Kulingana na ufafanuzi ulio kwenye 1 Yohana 3:10-12, makanisa ya Jumuiya ya Wakristo ni watoto wa nani, na kwa nini?

22 Neno la Mungu linasema hivi pia: “Katika hili watoto wa Mungu ni dhahiri, na watoto wa Ibilisi nao. Mtu ye yote asiyetenda haki hatokani na Mungu, wala yeye asiyempenda ndugu yake. . . tupendane sisi kwa sisi; si kama Kaini alivyokuwa wa yule mwovu, akamwua [akamchinja, NW] ndugu yake.” (1 Yohana 3:10-12) Makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yanadai kuwa watoto wa Mungu, lakini hayawezi kuwa, kwa maana yanakosa vibaya sana kutii amri za Mungu juu ya upendo na ‘kuchinja ndugu yao.’ Yanaweza kuwa watoto wa “yule mwovu” tu. Kwa sababu hiyo, Neno la Mungu linawahimiza hivi walio na mioyo myeupe katika dini hizo: “Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake.” (Ufunuo 18:4) Karibuni Mungu atafikiliza hukumu zake dhidi ya dini bandia zote. Wale wanaozishikilia sana watapata kitakachozipata. (Ufunuo 17:16) Kwa upande ule mwingine, “yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele.”​—⁠1 Yohana 2:17.

Wewe Ungejibuje?

◻ Kwa nini neno la Kiingereza kwenye 1 ni tafsiri ya kimakosa kuhusu neno la Kigiriki stau·rosʹ?

◻ Kuuheshimu sana msalaba kulianzia wapi, na kwa nini tunapaswa kuukataa?

◻ Yesu aliweka kielelezo gani kuhusu mapokeo ya kidini?

◻ Ni ushuhuda gani unaotambulisha wale wanaotii amri zinazohusu upendo wa kidugu?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 25]

ASILI ZA MSALABA

Muda mrefu kabla ya enzi ya Ukristo, namna za msalaba zilitumiwa karibu kila sehemu ya dunia zikiwa vifananishi vya kidini

Crux Ansata ulitumiwa na Wamisri wa kale kama kifananishi cha uhai wa wakati ujao

Crux Ouadrata ulifananisha zile elementi nne ambazo iliaminiwa kwamba vitu vyote viliumbwa kutokana nazo

Crux Gammata unafikiriwa kuwa ulikuwa kifananishi cha moto au jua; kwa hiyo, cha uhai

Msalaba wa Kilatini unaopendwa sana katika Jumuiya ya Wakristo

Msalaba huu ni muunganisho wa herufi mbili za kwanza za Kigiriki katika neno “Kristo”

[Picha katika ukurasa wa 24]

Kristo alikufa juu ya kiguzo kilichosimama wima, si juu ya msalaba

[Picha katika ukurasa wa 26, 27]

Wanakiri ya kwamba wanamjua Mungu, bali kwa matendo yao wanamkana.”​—Tito 1:16

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki