Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w87 11/15 kur. 15-20
  • Useja—Njia ya Maisha Yenye Kuthawabisha

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Useja—Njia ya Maisha Yenye Kuthawabisha
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Miaka ya Useja Yenye Kuthawabisha
  • Thawabu za Useja Msafi
  • Vielelezo vya Wakati Uliopita
  • Vielelezo vya Ki-Siku-Hizi
  • Kudumisha Useja Msafi
  • Wakati Ujao Wenye Kuthawabisha
  • Asiyefunga Ndoa Lakini Kamili kwa Utumishi wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Tumia Vizuri Kabisa Useja Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • ‘Ifanyie Nafasi’
    Huduma Yetu ya Ufalme—2003
  • Waseja Ambao Hupata Uradhi Katika Utumishi wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
w87 11/15 kur. 15-20

Useja—Njia ya Maisha Yenye Kuthawabisha

“Yeye ni huru kuolewa na mutu anayetaka; katika Bwana tu. Lakini ninazania ya kuwa ana furaha zaidi kama akikaa hivi.”​—1 WAKORINTHO 7:39, 40, ZSB.

1. Tuwe waseja au tumefunga ndoa, tunamwia Yehova nini?

YEHOVA anastahili ibada ya nafsi yote ya wote wale ambao wamejitoa wakfu kwake. Tuwe tumefunga ndoa au tu waseja, inatupasa kumpenda Mungu kwa moyo wetu wote, nafsi, akili, na nguvu. (Marko 12:30) Kweli, Mkristo mseja ana vivuta fikira vichache kuliko wale ambao wameunganishwa katika ndoa. Lakini je! mtumishi wa Yehova asiyefunga ndoa anaweza kuwa mwenye furaha kweli?

2, 3. (a) Katika maana halisi, Paulo alisema nini kwenye 1 Wakorintho 7:39, 40? (b) Ni maulizo gani yanayostahili kufikiriwa?

2 Mtume Paulo anajibu ndiyo. Kuhusu wale ambao wakati fulani walikuwa wamefunga ndoa lakini hali zao zimebadilika, yeye anaandika hivi: “Mwanamuke amefungwa kwa wakati mume wake ni hai; lakini kama mume wake amekufa, yeye ni huru kuolewa na mutu anayetaka; katika Bwana tu. Lakini ninazania ya kuwa ana furaha zaidi kama akikaa hivi: na ninazania ya kuwa nina Roho ya Mungu.”—1 Wakorintho 7:39, 40, ZSB.

3 Kwa kuwa Paulo anaonyesha kwamba watu wasiofunga ndoa wanaweza kuwa na furaha, ni nani ambaye kwa kufaa anaweza kufikiria kubaki mseja angalau kwa wakati fulani? Ni kitu gani kinachochangia furaha ya Wakristo wasiofunga ndoa? Kwa kweli, useja unaweza kuwaje njia ya maisha yenye kuthawabisha?

Miaka ya Useja Yenye Kuthawabisha

4. Ukweli ni nini kwa habari ya miaka ya mwanamume na mwanamke kijana?

4 Mfalme Sulemani mwenye hekima alisihi hivi: “Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako, kabla hazijaja siku zilizo mbaya [za uzeeni], wala haijakaribia miaka utakaposema, Mimi sina furaha katika hiyo.” (Mhubiri 12:1) Miaka ya mwanamume na mwanamke vijana kwa kawaida ni wakati wa angalau uzima usiolinganika na afya nzuri. Ni jambo lenye kufaa jinsi gani, basi, kwamba mali hizi zitumiwe katika utumishi wa Yehova bila kuvutwa na mambo mengine! Tena, miaka hii ya mapema ni wakati wa kupata ujuzi maishani, kukuza uthabiti. Lakini hiki pia ndicho kipindi ambacho vijana wa ulimwengu wanalewa mahaba. Kwa mfano, ebu yafikirie matokeo ya uchunguzi unaohusu watu 1,079 kati ya umri wa miaka 18 na 24. Wao walikuwa wamepata wastani wa “maono ya kimahaba” mara saba nao kwa upatani walisema kwamba wanalopata sasa ni upendo wa kweli, si ulevi wa mahaba.

5. Kuhusu ndoa, ni maulizo gani ya kibinafsi ambayo kijana anafaa kufikiria?

5 Takwimu za kutengana, kutalikiana, na jamaa zilizovunjika kwa njia nyinginezo zinaoonya dhidi ya ndoa za mapema. Badala ya kujiingiza haraka-haraka katika matembezi ya wavulana pamoja na wasichana, uchumba, na kufunga ndoa, vijana Wakristo watakuwa wenye hekima wakifikiria kwa njia inayofaa kuhusu jinsi wanavyoweza kutumia angalau miaka yao ya mapema katika utumishi kwa Yehova bila kuvutwa na mambo mengine. Kwa kupima hali zako kama kijana, utafanya vema kujiuliza mwenyewe maulizo kama haya: Je! sasa mimi nimekomaa kimoyoni na niko tayari kufikiria kwa uzito kufunga ndoa? Je! mimi nina ujuzi wa kutosha maishani utakaoniwezesha niwe mwenzi mzuri wa ndoa? Je! mimi naweza kutwaa madaraka ya ndoa na labda jamaa pamoja na watoto? Kwa sababu ya kujitoa wakfu kwangu kwa Yehova, je! hainipasi mimi nimpe yeye nishati na nguvu za ujana bila kuvutwa na mambo yanayohusiana na ndoa?

Thawabu za Useja Msafi

6, 7. (a) Ni faida gani ambazo kwa kawaida zinafurahiwa na Wakristo wasiofunga ndoa? (b) Kwa habari hii, ni nini ambacho kimesemwa na mmisionari mmoja katika Afrika ambaye hajaoa?

6 Wakristo ambao hawajafunga ndoa wanafurahia uhuru wa kutovutwa na mambo mengine na wanaweza kupata “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.” (1 Wakorintho 7:32-34; 15:58, NW) Badala ya kumkazia fikira mtu mmoja wa ile jinsia tofauti, mseja ana nafasi zaidi za kuupanua upendo wake wa Kikristo kwa wengi kundini, kutia na walio wazee-wazee na wengine ambao wanahitaji msaada wenye upendo. (Zaburi 41:1) Kwa kawaida, waseja wana wakati zaidi wa kujifunza na kutafakari juu ya Neno la Mungu. (Mithali 15:28) Wao wana nafasi kubwa zaidi ya kukuza uhusiano wa karibu pamoja na Yehova, wakijifunza kumtegemea sana na kuutafuta mwelekezo wake. (Zaburi 37:5; Wafilipi 4:6, 7; Yakobo 4:8) Mwanamume mmoja mseja ambaye ametumikia Yehova kwa miaka mingi katika Afrika amesema hivi:

7 “Maisha katika vijiji vya Afrika yamekuwa rahisi sana katika miaka hii iliyopita, bila mambo mengi ya kuvuta fikira kando ya mweruvuko wa kisasa. Nimekuwa na nafasi ya kutosha kujifunza na kutafakari juu ya Neno la Mungu, bila kuvutwa na mambo haya. Jambo hilo limenifanya niwe mwenye nguvu. Ndiyo, maisha ya umisionari yamekuwa baraka kweli kweli na ulinzi dhidi ya kutafuta vitu vya kimwili. Wakati wa jioni zenye kupendeza za kitropiki kumekuwa na wakati wa kutosha kutafakari na kufikiria sana uumbaji wa Yehova na kumkaribia yeye. Furaha yangu kubwa zaidi huja kila jioni akili zangu zikiwa zingali zinafanya kazi, na nikiwa peke yangu ninatumia wakati fulani chini ya mbingu zenye mng’aro wa nyota nikitembea na kuzungumza pamoja na Yehova. Hili limenifanya mimi nimkaribie Yehova zaidi.”

8. Kuhusu useja, ni nini kilichosemwa na dada mmoja asiyeolewa ambaye alikuwa ametumikia katika makao makuu ya Sosaiti kwa miaka mingi?

8 Jambo linalostahili kuangaliwa pia, ni elezo hili lililotolewa na dada mmoja mseja ambaye ametumikia kwa miaka mingi katika makao makuu ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi: “Mimi nimechagua kuwa mseja katika utumishi wangu kwa Yehova. Je! kuna wakati wo wote mimi huhisi nikiwa na upweke? Sivyo hata kidogo. Kwa kweli, muda ninapokuwa peke yangu ni miongoni mwa ule ambao unakuwa wenye thamani zaidi sana. Mimi ninaweza kuongea na Yehova katika sala. Mimi ninaweza kufurahia kutafakari na kujifunza kibinafsi bila kuvutwa na mambo mengine. . . . Useja umechangia mengi kwa furaha yangu.”

9. Ni baadhi ya mapendeleo gani ya utumishi ambayo Mkristo mseja huenda akafurahia?

9 Pia mseja anaweza kukubali mapendeleo ya utumishi ambayo huenda yasiwe wazi kwa watu waliofunga ndoa wenye madaraka ya jamaa. Kwa mfano, huenda kukawa na nafasi za kuwa katika huduma ya wakati wote kama painia katika sehemu ambazo watangazaji wa Ufalme wanahitajiwa sana. Au kijana mwanamume mseja huenda akawa na pendeleo la kutumika kama mshiriki wa jamaa ya Betheli katika makao makuu ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi au afisi ya tawi. Mwanamke kijana asiyeolewa huenda akaweza kujiunga na dada mseja mwenye umri mkubwa kidogo katika utumishi wa painia katika kundi la kwao au jingine ambalo lina eneo linalohitaji kuenezwa. Mbona usizungumze uwezekano huo pamoja na mwangalizi wa mzunguko? Ukiwa Mkristo asiyefunga ndoa, jifanye wewe mwenyewe upatikane kwa utumishi ulioongezeka kwa sifa ya Yehova naye atakubariki wewe kwa wingi.—Malaki 3:10.

Vielelezo vya Wakati Uliopita

10. Ni nani aliyetoa kielelezo kikuu cha mtumishi wa Yehova asiyeoa, na kwa sababu gani wewe unafikiri kwamba useja wake ulikuwa wenye faida?

10 Kielelezo kikuu cha mtumishi wa Yehova asiyeoa ni Yesu Kristo. Yeye alijishughulisha kabisa katika kufanya mapenzi ya Mungu. “Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake,” akasema Yesu. (Yohana 4:34) Jinsi alivyokuwa mwenye shughuli sana—akihubiri, akiwaponya wagonjwa, na kadhalika! (Mathayo 14:14) Yeye alipendezwa kikweli na watu naye alistarehe katika kuwapo kwa wanaume, wanawake, na watoto. Kwa kweli, alisafiri-safiri katika huduma yake, wengine wakiandamana naye katika pindi fulani. (Luka 8:1-3) Lakini jinsi utendaji huo ungekuwa mgumu kama angeambatana na mke na watoto wadogo! Pasipo shaka, useja ulikuwa wenye faida kwa habari ya Yesu. Leo, Mkristo mseja huenda akafurahia faida zinazolingana na hizi, hasa akilazimika kutangaza ujumbe wa Ufalme katika sehemu za mbali au zenye hatari.

11, 12. Ni vielelezo gani gani ambavyo vimetajwa kwa wanawake waseja wanaotumikia Yehova leo?

11 Lakini wengine pia walipata useja kuwa wenye mafaa na wenye kuthawabisha. Binti ya Yeftha alijitoa kwa hiari kutimiza nadhiri ya baba yake kwa kubaki mseja katika jamii iliyokazia sana ndoa na kuwa na watoto. Yeye alipata furaha katika utumishi wake kwa Yehova, na ni jambo linalostahili kuangaliwa kwamba wengine kwa ukawaida walitia yeye moyo. Kwani, ‘binti za Israeli walienda mwaka baada ya mwaka ili kumkumbuka huyo mwana wa Yeftha, Mgileadi, siku nne katika mwaka’! (Waamuzi 11:34-40) Vivyo hivyo, Wakristo waliofunga ndoa na wengineo wapaswa kuwasifu na kuwatia moyo wanawake waseja wanaotumikia Yehova leo kwa ushujaa.

12 Binti wanne mabikira wa Filipo ‘walitabiri.’ (Matendo 21:8, 9) Lazima wanawake hawa wasioolewa wawe walitosheka na utumishi wao kwa sifa ya Yehova. Kwa kulinganisha, wanawake wengi vijana walio waseja leo wana pendeleo lenye kuthawabisha la kutumikia kama mapainia, au watangazaji wa Ufalme wa wakati wote. Kwa hakika, wanastahili kusifiwa kama sehemu ya ‘jeshi kubwa la wanawake wanaotangaza habari njema.’—Zaburi 68:11, NW.

13. Hali ya Paulo inaonyeshaje kwamba useja unaweza kuwa njia ya maisha yenye kuthawabisha?

13 Mtume Paulo alipata kuona kwamba useja ni wenye faida. Yeye alisafiri maelfu ya maili katika huduma yake naye alikabiliana na magumu mengi sana, hatari nyingi, mausiku ya kukosa usingizi, njaa yenye kuumiza. (2 Wakorintho 11:23-27) Pasipo shaka, yote haya yangekuwa magumu zaidi na yenye kutaabisha sana ikiwa Paulo angekuwa ameoa. Zaidi ya hilo, haielekei kwamba yeye angepata kuwa na mapendeleo yake ya kuwa “mtume wa watu wa Mataifa” kama angekuwa akitunza jamaa. (Warumi 11:13) Yajapokuwa majaribu aliyokabili, Paulo alikuwa na ushuhuda wa kujionea mwenyewe kwamba useja unaweza kuwa njia ya maisha yenye kuthawabisha.

Vielelezo vya Ki-Siku-Hizi

14. Ni mambo gani yaliyoonwa yaliyofurahiwa na makolpota, wengi wao wakiwa hawajafunga ndoa?

14 Kama Paulo na Wakristo wengine wa mapema wasiofunga ndoa, hesabu kubwa ya watu wa Mungu walioshiriki katika kazi ya Kolpota (kuanzia 1881 na kuendelea) walikuwa waseja wasio na jamaa zenye kuwategemea. Wao kwa hiari yao wenyewe walienda kwenye majiji, miji wasiyofahamu, na sehemu za mashambani wakitafuta wale wenye mioyo mizuri na kuwaangushia vichapo vya Biblia. Huenda walisafiri kwa gari-moshi, baiskeli, kigari kilichokokotwa na farasi, au gari. Sana sana, wao walitembea nyumba kwa nyumba kwa furaha. (Matendo 20:20, 21) “Nyakati nyingine wangebadilisha [vichapo vya Biblia] na mazao ya shambani, kuku, sabuni na vitu kama hivyo, ambavyo wangetumia au kuwauzia wengine,” akakumbuka Shahidi mmoja wa Yehova, akiongeza hivi: “Nyakati nyingine, katika sehemu ambazo watu wachache waliishi, wao walikaa na wakulima na wenye mashamba ya mifugo usiku huo, na hata nyakati nyingine walilala juu ya majani yaliyokaushwa . . . waaminifu hawa [walio wengi wao wakiwa wasiofunga ndoa] waliendelea kwa miaka na miaka mpaka uzee ulipowafikilia.” Kwa hakika, mwanamke aliyekuwa mmoja wao alizungumza kwa niaba ya makolpota hao wa wakati wa zamani kwa ujumla alipoandika hivi: “Tulikuwa vijana na wenye furaha katika utumishi huo, tukifurahia kutumia nguvu zetu kwa kumtumikia Yah.”

15. Kwa mapainia wengi wasiofunga ndoa, ni mlango gani unaoongoza kwenye utendaji mkubwa zaidi uliofunguka miaka kama 45 iliyopita?

15 Mapainia wengi wa baadaye, au watangazaji wa Ufalme wa wakati wote, walikuwa pia wasiofunga ndoa. Mara nyingi wao walitoa ushuhuda katika sehemu zisizogawiwa mtu, walisaidia kuanza makundi mapya, nao walifurahia mibaraka mingi katika utumishi wa Yehova. Kwa wengine wao, mlango wenye kusisimua wenye kuongoza kwenye utendaji mkubwa zaidi ulifunguka wazi wakati shule ya Gileadi ya Biblia ya Mnara wa Mlinzi ilipoanza kufanya kazi katika 1943 huku Vita ya Ulimwengu ya Pili ikipiganwa vikali sana. (1 Wakorintho 16:9) Ndiyo, wengi wa mapainia hao wasiofunga ndoa walipokea mazoezi ya umisionari katika shule ya Gileadi na upesi wakawa wakieneza ujumbe wa Ufalme katika maeneo mapya. Wakiwa hawalemewi na madaraka ya ndoa, walijifanya wapatikane kwa ajili ya utumishi wa Yehova, na baadhi ya wahitimu hao wa mapema wangali waseja na watendaji katika kazi ya umisionari au utumishi fulani wa wakati wote.

16. Kuna ithibati gani ya kwamba washiriki wa jamaa ya Betheli wasiofunga ndoa wamepata kuona kwamba useja ni njia ya maisha yenye kuthawabisha?

16 Wakristo wengi wasiofunga ndoa wametumikia kwa miaka mingi wakiwa washiriki wa jamaa ya Betheli katika makao makuu ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi au katika matawi yayo sehemu nyingine ulimwenguni. Je! wao wamepata useja kuwa njia ya maisha yenye kuthawabisha? Ndivyo, kweli kweli. Kwa mfano, ndugu mmoja mseja ambaye alikuwa ametumikia katika Betheli ya Brooklyn kwa miaka mingi alisema hivi: “Ile furaha ya kuona mamilioni ya magazeti na vichapo vingine vikiwa na ujumbe wa Neno la Mungu vikienezwa kwenye miisho ya dunia yenyewe imekuwa thawabu ya ajabu.” Baada ya miaka kama 45 ya utumishi wa Betheli, ndugu mwingine asiyeoa alisema hivi: “Kila siku mimi ninamwomba Baba yetu mpenzi wa kimbingu katika sala anipe msaada na hekima ya kujitunza kiroho na kuwa mwenye afya kimwili na mwenye nguvu ili mimi niweze kuendelea kufanya mapenzi yake matakatifu. . . . Kweli kweli mimi nimefurahia njia ya maisha yenye furaha, yenye kuthawabisha na yenye baraka.”

Kudumisha Useja Msafi

17. Ni misaada gani miwili ya kudumisha useja msafi?

17 Uhakika wa kwamba useja unaweza kuwa wenye kuthawabisha unaonekana wazi kutokana na vielelezo vya Kibiblia na vya ki-siku-hizi. Bila shaka, wakati wa kipindi cho chote cha maisha yako kinachotumiwa katika hali ya useja, unahitaji kuwa ‘umesimama ukiwa umetulia katika moyo wako.’ (1 Wakorintho 7:37, NW) Lakini ni nini kinachoweza kukusaidia udumishe usafi huku ukiwa hujafunga ndoa. Chanzo kikubwa zaidi cha msaada ni Yehova, yule “msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2, NW) Hivyo lifanye liwe zoea lako kumsihi yeye mara kwa mara. ‘Dumu katika sala,’ ukiomba roho ya Mungu na msaada wake katika kuonyesha tunda layo, linalotia ndani amani na kujiweza. (Warumi 12:12, NW; Luka 11:13; Wagalatia 5:22, 23, NW) Ndipo, pia, kwa mwelekeo wa sala, tafakari kwa ukawaida na sikuzote utumie shauri la Neno la Mungu.

18. 1 Wakorintho 14:20 inahusianaje na kubaki kwa mmoja kuwa safi akiwa mtu asiyefunga ndoa?

18 Njia nyingine ya kudumisha useja msafi ni kwa kuepuka kitu cho chote kinachoweza kuamsha harara ya ngono. Kwa wazi, hii inatia ndani pornografia na vitumbuizo visivyo vya adili. Paulo alisema: “Katika uovu mgeuzwe watoto wachanga, bali katika akili zenu mkawe watu wazima.” (1 Wakorintho 14:20) Usitafute maarifa au ujuzi kuhusu mabaya, lakini kwa msaada wa Mungu kwa hekima endelea kuwa asiye na ujuzi na bila hatia kama kitoto kidogo kwa habari hii. Wakati uo huo, kumbuka kwamba ukosefu wa adili kingono na kutenda mabaya hakufai machoni pa Yehova.

19. Ni maandiko gani yanayoelekeza kwenye njia nyingine za kubaki ukiwa safi ukiwa mtu mseja?

19 Utasaidiwa pia kubaki ukiwa safi ukiwa mtu asiyefunga ndoa kwa kulinda mashirika yako. (1 Wakorintho 15:33) Epuka kushirikiana na wale ambao wanafanya ngono na ndoa ziwe sehemu kubwa ya maisha zao na mazungumzo. Kwa vyo vyote epuka mzaha wa mambo machafu! Paulo alishauri hivi: “Acheni uasherati na ukosefu wa usafi wa kila namna au pupa hata usitajwe miongoni mwa ninyi, sawasawa na vile inavyolaiki watu watakatifu; wala mwenendo wenye aibu wala maongezi ya kipumbavu wala mzaha wa mambo machafu, mambo ambayo hayafai, bali kuwe ni kule kutoa kwa shukrani.”—Waefeso 5:3, 4, NW.

Wakati Ujao Wenye Kuthawabisha

20. Kutumia kwa mtu miaka ya useja kwa njia iliyo bora zaidi katika utumishi wa Yehova kutatokeza nini?

20 Kutumia miaka yako ukiwa Mkristo asiyefunga ndoa katika njia nzuri iwezekanayo kwa utumishi wa Yehova kutakutosheleza sasa na kukupa amani ya akili. Kufanya hivyo pia kutachangia uthabiti na ukomavu wako wa kiroho. Ukiendelea kuwa mseja kwa ajili ya Ufalme mpaka mwisho wa mfumo huu mbovu wa mambo, Yehova hatasahau jitihada zako za kujidhabihu katika utumishi wake mtakatifu.

21. Ikikupasa kufunga ndoa baada ya kipindi cha useja msafi na wenye kuthawabisha, yaelekea utaingia katika kifungo cha ndoa ukiwa na nini?

21 Ukifuatia masilahi za Ufalme kwa bidii ukiwa mwanamume asiyeoa au mwanamke asiyeolewa, wewe utafurahia mibaraka mingi. (Mithali 10:22) Halafu ikikupasa kufunga ndoa miaka ya baadaye maishani, utaingia katika ndoa ukiwa na ujuzi mkubwa zaidi na malezi mazuri ya kiroho. Zaidi ya hayo, kwa kufuata shauri la Maandiko, wewe utachagua mwenzi mshika-ukamilifu aliyejitoa wakfu atakayekusaidia wewe utumikie Yehova kwa uaminifu. Wakati huu, wewe unaweza kupata kuona useja kuwa njia ya maisha yenye kuthawabisha katika utumishi wa Mungu wetu mwenye upendo, Yehova.

Wewe ungeitikiaje?

◻ Miongoni mwa watumishi wa Yehova, ni nini baadhi ya thawabu za useja msafi?

◻ Kuna vielelezo vipi vya Kimaandiko vinavyoonyesha kwamba useja unaweza kuthawabisha?

◻ Katika nyakati za ki-siku-hizi, ni vielelezo gani vya useja wenye kuthawabisha tulivyo navyo?

◻ Ni nini kinachoweza kumsaidia Mkristo abaki akiwa msafi huku akiwa hajafunga ndoa?

[Sanduku katika ukurasa wa 19]

Misaada ya Kudumisha Useja Msafi

◆ Sali kwa ukawaida kwa ajili ya roho ya Mungu na msaada wake katika kuonyesha tunda layo

◆ Sikuzote tafakari na kutumia shauri la Neno la Mungu

◆ Epuka pornografia na vitumbuizo visivyo vya adili

◆ Linda mashirika yako

◆ Epuka maongezi ya kipumbavu na mzaha wa mambo machafu

[Picha katika ukurasa wa 19]

Binti ya Yeftha, mtume Paulo, na watumishi wengine wa Yehova walipata kuona kwamba useja ni njia ya maisha yenye kuthawabisha. Je! wewe unaweza kupata kuona hivyo?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki