Tunaweza Kujifunza Nini Kutokana na Uumbaji wa Mungu?
NJIWA wanapata njia za nyendo zao kwa kutumia vibumba vya vioo vyangavu vyenye sumaku katika vichwa na shingo zao. Samaki fulani wanatokeza nguvu za umeme. Namna kadha za ndege wanaondoa chumvi ya kupita kiasi katika maji-bahari ambayo wanakunywa. Magegereka fulani (jamii za akina pweza) wana mianya ambayo inaweza ama kujazwa maji ili wapige mbizi majini ama inayoweza kujazwa gesi ili warudi juu ya maji.
Ndiyo, kama mwanadamu anang’amua au hang’amui jambo hilo, wakati yeye anapotumia dira, anapotokeza nguvu za umeme, anapobuni umbo la sabmarini, au anapoondoa chumvi katika maji-bahari ili yanyweke, kwa kweli yeye anakuwa akiiga tu uumbaji wa Mungu.
Kweli kweli, uumbaji wa Mungu una masomo mengi sana kwa mwanadamu hivi kwamba, nyakati fulani uumbaji huo unaitwa “kile kitabu cha asili.” Mathalani, somo la bioniki ni tawi moja la sayansi linalojihusisha na utumizi wenye mafaa wa mifumo ambayo inapatikana katika uumbaji. Hiyo ni kutia ndani mabawa ya ndege-abiria yaliyo na sehemu kama zile za nyuni, sabmarini zilizo na maumbo yanayofanana na dolfini, na miundo migumu iliyobuniwa umbo kama la mifupa ya kibinadamu. Lakini je! kile “kitabu cha asili” kina maarifa ya kiufundi tu?
Sivyo, nyakati fulani kinaandaa masomo yenye mafaa ya kiadili pia. Mathalani, kikirejeza kwenye bidii ya kikazi ambayo chungu anayo kwa njia ya silika, kitabu cha Biblia cha Mithali kinaonya kwa upole hivi: “Enda kwa chungu, wewe mvivu; ona njia zake na uwe mwenye hekima. Ingawa yeye hana amiri, afisa wala mtawala, yeye anatayarisha chakula chake hata katika kiangazi; yeye amekusanya akiba zake za chakula hata katika mavuno.”—Mithali 6: 6-8, NW.
Hata hivyo, somo la etholojia, sayansi ambayo inadai kutoa-toa masomo kutokana na tabia za wanyama, lina mapungukiwa fulani. Tabia ya kibinadamu haiwezi kulinganishwa iwe sawa-sawa kabisa na ile ya wanyama. Tofauti kubwa-kubwa lazima zifikiriwe, kama lugha na utaratibu wa kufikiria mambo yasiyo na kikomo ambao umo katika mwanadamu. Kama mwana-sayansi mmoja anavyosema: “Sisi si nyani wenye akili zaidi tu.” Akili zetu “zinatufanya sisi tutofautiane kwa ubora na namna nyingine zote za uhai.”
Waaidha, kuna maswali fulani ambayo kuchunguza tu uumbaji kwa ukaribu hakuwezi kuyajibu. Yanatia ndani maswali haya: Je! uhai una kusudi? Je! Mungu yuko, na ikiwa ndivyo, je! yeye anatujali sisi? Acheni sasa tuone kama maswali hayo yanaweza kujibiwa.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 3]
Uumbaji Ndio Uliokuwa wa Kwanza Kupata: Sona
Popo wana mfumo ambao kidogo unafanana na sona (kifaa cha mwilini ambacho kinasaidia viumbe fulani kugundua umbali wa kitu kilicho mbele yao). Mfumo huo unawawezesha popo kujua mahali windo lao lilipo na kufuata miendo yalo kwa kupeleka-peleka mivumo na kuchanganua miangwi inayorudishwa na mivumo hiyo. Lakini nondo fulani (yule dogbane tiger) ana kiashirio chenye kutatanisha mivumo, ambacho kinapeleka mawimbi yanayofanana na yale ya mpinzani wake. Wakati yule popo anapopokea kiashirio hicho, yeye anaepa yule nondo kwa kutegemea mfumo wake, kwa maana hana wakati wa kutosha kuchanganua kama nondo huyo ni kitu kilichomfungia au sivyo.
Profesa James Fullard, wa Chuo Kikuu cha Toronto, Kanada, alieleza mshangao wake, akisema. “Jambo la kustaajabisha ni ule wingi tu wa upelekaji wa habari na maamuzi makubwa ya ubongoni ambayo yanafanywa na akina popo na akina nondo, wakitumia hesabu ndogo sana ya chembe za neva. Wao wanatumia vifaa hivyo kwa uangalifu na kwa hali ya juu ya kadiri ambayo ingeweza kuonewa kijicho na wanadamu walio wataalamu wa kuvumbua maarifa ya vita vya angani.”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 4]
Uumbaji Ndio Uiiokuwa wa Kwanza Kupata: lie Kengele ya Kupigia Mbizi
Karibu-karibu na mwanzo wa karne ya 16, Leonardo da Vinci anasemwa kuwa alivumbua kifaa fulani cha kupigia mbizi. Lakini buibui fulani jina lake Argyroneta aquatica alikuwa tayari ana mfumo mkamilifu wa kupumulia chini ya maji. Kama vile bibi Andree Tetry anavyoeleza katika kitabu chake Les outils chez les etres vivants (Vyombo Vinavyotumiwa na Wenye Uhai), buibui huyo “anatulia katika vijito vyenye kutiririka polepole akiwa miongoni mwa mimea ya ndani ya maji, naye anafuma miongoni mwa mimea hiyo utando wa neti nzuri unaokingama, ukiwa umeshikamanishwa katika mahali hapo na nyuzi nyingi sana. Anaporudi juu ya uso wa maji, . . . buibui yule anajitupa ghafula kudaka povu la hewa katika nywele za tumboni mwake ambazo huzuia maji kupenya. . . . Halafu buibui huyo anashuka chini tena, naye analiachilia huru lile povu la hewa chinichini ya ule utando wa neti wa nyuzi za hariri. Ndipo povu lile linapoinuka na kufanyiza mfuro mdogo katika neti ile.” Kwa kuenda-enda mara nyingi, buibui huyo anakusanya hewa ya kumtosha ashinde mchana ule akiwa chini ya kengele yake, ambapo yeye anakula windo lililokamatwa wakati wa usiku. Kwa habari hiyo, Tetry anaongeza hivi: “Kwa hiyo, vifaa vya mwanadamu vya kupigia mbizi vinalingana na namna zile za utaalamu zaidi zinazoonwa katika asili.”