Jinsi ya Kuimarisha Vifungo vya Kijamaa
Sababu ambazo zinafanya vijana waondoke nyumbani ni nyingi na mara nyingi zinahusu mambo mengi sana. Ingawa makala hii haiwezi kuzishughulikia kwa kina kirefu, inaonyesha kwamba kanuni za Biblia zikitumiwa zinaweza kufanya jamaa ibaki ikiwa imeungana.
NI VIGUMU kuthibitisha ni watoto wangapi hasa wanaotoroka nyumbani. Makadirio yaliyopigwa chapa yanaonyesha kuna watoto kuanzia 600,000 mpaka 3,000,000 wenye kukosekana kila mwaka katika United States tu. Mara nyingi makadirio hayo yanawajumlisha wote hao katika fungu moja kwa kuwataja kuwa wanaotoroka, wasukumwa-nje, watupiliwa-mbali, na watoto waliotoroshwa kwa haramu na wazazi ambao hawana haki ya utunzaji wa kisheria. Lazima hayo yawe ni makadirio tu, kwa maana watoto ambao wanaachiliwa mbali na wazazi wao hawasemwi kuwa wamekosekana, na watoto fulani wanatoroka nyumbani kwa ukawaida. “Mvulana wa miaka 16 ambaye hutoroka mara tano kwa mwaka na kukaa nje usiku kucha kila wakati anapotoroka alikuwa akihesabiwa katika . . . takwimu kuwa ni watoto watano wenye kukosekana,” inasema The New York Times.
Jambo lililo la maana kuliko hesabu zao ni sababu zinazofanya watoto waondoke nyumbani. “Wakati kijana anapotoroka, kwa kawaida hiyo ni dalili ya kuonyesha kuna kasoro ya utendaji wa mazingira ya nyumbani,” linataarifu gazeti Medical Aspects of Human Sexuality. Huenda ikawa ni kwa sababu ya matatizo ambayo tayari yapo, kama vile kutendwa vibaya kimwili, kutoonyeshwa ujalifu, ukosefu wa upendo, talaka, madai ya kupita kiasi, au sheria katili na ngumu. Au huenda ikawa ni kwa sababu ya kuogopa matokeo, kama vile katika visa vinavyohusu mimba au kukosana-kosana na wenye sheria. Wanapoulizwa sababu iliyowafanya waondoke nyumbani, walio wengi wa watoto wanaotoroka wanataja sababu zinazotia ndani uhusiano wao na wazazi wao. “Inaonekana uhusiano kati ya mzazi na mtoto ni kisababishi kikubwa mno cha ile tabia ya kutoroka,” linasema jarida Adolescence. Linaongezea hivi: “Watoto wanaotoroka wanaripoti kwamba visababishi vikubwa vinavyofanya watoroke nyumbani ni mahusiano mabaya kati ya mzazi na mtoto, mhitilafiano mkubwa mno wa kijamaa, kutenganishwa na urafiki wa wazazi, mivutano kati ya mtu na mtu, na kutowasiliana vizuri pamoja na wazazi.
Kuzielewa Sababu
Hizi ni nyakati zenye shida. “Huku ukosefu wa kazi ya kuajiriwa ukiongezeka, na jamaa nyingi zaidi na zaidi zikiwa katika magumu makubwa ya kipesa, mivutano na matatizo ya kinyumbani yanazidishwa,” linasema gazeti Ladies’ Home Journal. “Wakati baba anapoachishwa kazi kwa muda na kodi ya nyumba inakosa kulipwa, kila mmoja katika jamaa anahisi shida. Vijana, ambao hawajakuza zile stadi za kupambana na mifinyo hiyo, wanatumia kutoroka kuwa njia ya kuepukia jambo hilo.” Nyakati fulani wazazi wenyewe ndio wanaoondosha nje watoto wao bila kujua. Kwa hasira, huenda wao wakaambia wazaliwa wao wakubali maamuzi yao au sivyo waondoke. Kwa sababu ya kuchokorwa-chokorwa na kuchoshwa na pambano la matatizo yao ya kiuchumi kila siku, hawawi na nishati nyingi za kushughulika na watoto wao.
Wakati ule ule, ile hali yenyewe tu ya kuwa kijana-mbalehe inatokeza shida zayo yenyewe. Matineja wanatatizika kati ya kuhitaji ule usalama na utunzaji walioupokea wakiwa watoto na ule mnyeto wa kuhisi wanajitegemea wenyewe mbali na wazazi wao, huku wakijitahidi kuwa watu wazima. Hiyo inasababisha mvurugiko na wasiwasi kwao. Pia mabadiliko ya kimwili yanakuwa yakitukia. Maisha zao zimetatanika kwa ghafula, na huenda wao wakahisi kwamba wameshindwa kabisa. Wao wanahisi wakipatwa na mfinyo kutoka kwa marika wao. Pia wanapatwa na vipindi vya kujitilia mashaka na vya kushuka moyo. “Wakati wewe unapojaribu kujielewa u mtu wa namna gani, usishangae ikiwa nyakati fulani unahisi ukieleweka vibaya nyumbani,” linashauri gazeti ‘Teen. “Ingawaje, ikiwa wewe mwenyewe huwezi kujielewa, wazazi wako watawezaje kujua yaliyo akilini mwako?” Wazazi wengi hawana uhakika ni uhuru wa kadiri gani wanaopaswa kuwapa watoto wao, hasa wazaliwa wao wa kwanza-kwanza. Uzuizi unaopita kiasi na ukosefu wa uelewano umeongoza vijana wengi watoroke.
“Lakini kutoroka hakutatui tatizo lo lote,” anasema mtungaji Judy Blume katika kitabu chake Letters to Judy. “Kutoroka ni dalili tu, si utatuzi. Badala ya hivyo, jamaa nyingi zinalazimika kuketi pamoja na kukubali kuelekeana na mambo ya uhakika. Zinalazimika kushughulika na matatizo bila kujaribu kuyaepuka. Hapo tu ndipo wao wanapoweza kufanya mabadiliko ambayo yatawasaidia waishi pamoja kwa amani. Na mara nyingi wao wanahitaji msaada katika kufanya hivyo.”
Kupata Msaada Unaohitajiwa
Chanzo kilicho bora zaidi cha msaada huo ni Neno la Mungu, Biblia. Kwa sababu gani? Kwa sababu Mungu aliye Muumba wa mwanadamu, ndiye anayejua yaliyo bora zaidi kwa uumbaji wake. Na yeye ametupa sisi maagizo kwa kusudi hilo, “kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu apate kuwa na uwezo wa kutosha, aliye tayari kabisa kwa kila kazi njema.” (2 Timotheo 3:16, NW) Kanuni za Biblia zinaleta mafaa, nazo zinahusu kila upande wa maisha.
Ingawa hivyo, kama ilivyosemwa ni lazima washiriki wote katika jamaa wawe na nia ya kukubali kuelekeana na mambo ya uhakika na kufanya mabadiliko. Bila utambuzi na tamaa ya kukubali hivyo, maendeleo hayatafanywa, na ile kani yenye kusukuma watu kuepa itabaki. Ndivyo ilivyo hasa katika jamaa zilizo na matatizo ya utumizi wa kileo, dawa za kulevya, na utumizi mbaya wa ngono. Ni lazima mambo hayo yashindwe, kabla ya kuweza kushughulikia ile mifinyo ya kikawaida ya maisha. Imani katika Mungu na kutamani kwa moyo mweupe kumpendeza yeye, kwa kutegemea maarifa sahihi ya Neno lake, ni mambo ambayo yamesaidia jamaa nyingi kushinda hali zenye misiba ambazo katika jamaa fulani-fulani zimesukuma vijana kutoroka.—Linganisha 1 Wakorintho 6:9-11.
Kule tu kuishi katika huu ulimwengu wa ki-siku-hizi pamoja na ubinafsi wao unaoongezeka, ukosefu wa kuitibariana, na ongezeko kubwa sana la uhalifu kunaweza kutatiza sana vifungo vya kijamaa. Hiyo ndiyo sababu “yote yaliyotangulia kuandikwa [katika Biblia] yaliandikwa ili kutufundisha sisi; ili kwa saburi na faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini.”—Warumi 15:4.
Kutumia Kanuni za Biblia
Kwa kuwa na maarifa ya kujua visababishi vinavyofanya mtoto atoroke, kanuni za Biblia zinaweza kutumiwa. Biblia inashughulika na visababishi hivyo kwa kushauri wazazi watumie wakati bora unaohitaji kutumiwa wakiwa pamoja na watoto wao, watoe mazoezi yasiyo na ugeugeu, yenye upendo. Kule kupita kiasi katika pande zote mbili, kukosa kupendezwa na watoto na kuwatia nidhamu yenye sheria kali mno, kunapasa kuepukwe. Neno la Mungu linashauri hivi: “Akina baba, msiwe mkiwaudhi watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” —Waefeso 6:4; Mithali 22:6, NW.
Kama katika nyakati za Biblia, usimamizi unaofaa, uelekezeaji fikira, na maagizo, ni mambo ambayo ingefaa wazazi watoe daima—‘wakati wanapoketi katika nyumba yao, wakati wanapotembea barabarani, wakati wanapolala, na wakati wanapoamka.’ (Kumbukumbu 11:19, NW) Ingawa nidhamu inahitajiwa nyakati fulani, hiyo inapasa kutolewa kwa upendo. (Mithali 13:24) Bila shaka furaha ya kijamaa itaongezewa ikiwa shauri hilo linafuatwa!
Watoto wanapaswa pia kutimiza fungu lao: “Watoto, tiini wazazi wenu katika muungano na Bwana, kwa maana hili ni jambo la uadilifu: ‘Heshimu baba yako na mama yako.’ “(Waefeso 6:1, 2, NW) Sulemani mtu mwenye hekima wa kale, ambaye aliandika ili “kuwapa wasio na ujuzi akili chapuchapu, kumpa kijana mwanamume maarifa na uwezo wa kufikiri,” anashauri hivi pia: “Sikiliza, mwana wangu, nidhamu ya baba yako, na usiache sheria ya mama yako. . . . Ikiwa watenda dhambi wanajaribu kutongoza wewe, usitoe idhini.”—Mithali 1:1-10, NW.
Matatizo ya kijamaa yangeshughulikiwa jinsi gani? Kwa upendo, kwa maana Biblia inashauri hivi: “Acheni mambo yenu yote yatukie kwa upendo.” (1 Wakorintho 16:14, NW) Huo unapasa uwe upendo wenye mizizi ya kina kirefu, ambao una nia ya kuachilia makosa ya kutokamilika na vijitabia vya mtu mwingine ambavyo visipoachiliwa huenda vikachokora-chokora mtu na kumkwaruza-kwaruza. “Zaidi ya mambo yote, mwe na upendo mwingi sana kwa mmoja na mwenzake,” Biblia inasema, “kwa sababu upendo unafunika wingi wa dhambi.” —1 Petro 4:8, NW.
Upendo kama huo unapendezwa pia na kuona wengine wakiwa na furaha na hali njema na unavuta jamaa ikaribiane zaidi pamoja. Angalia kwamba ile inayoitwa kanuni bora ilikuwa ya mwelekeo chanya: “Fanya kwa ajili ya wengine lile ambalo wewe unataka hao wafanye kwa ajili ya wewe.” (Mathayo 7:12, Today’s English Version) Walio wengi kati ya vijana wanaotoroka waliohojiwa katika uchunguzi mmoja walisema kwamba hawakuwa wakihusishwa sana katika mambo ya jamaa yao kabla ya wao kuondoka nyumbani. “‘Mwondokano wa kijamaa’ ni kisababishi kikubwa cha ule mfuatano-fuatano wa hatua za kuamua kutoroka na kuendelea kukaa mbali na nyumbani,” inasema Adolescence. Lakini kwa kufuata onyo la upole la Biblia la ‘kuendelea kuangalia, si masilahi ya kibinafsi juu ya mambo yenu wenyewe tu, bali pia masilahi ya kibinafsi juu ya mambo yale ya wengine,’ wakati mwingi zaidi utatumiwa pamoja mkiwa jamaa, na matatizo ya mahusiano mabaya, kutenganishwa na urafiki wa wazazi, na mawasiliano haba yanaweza kushindwa. (Wafilipi 2:4, NW) Kwa kuwa na hisia ya kukaribiana, na mtu kupendezwa na mwenzake nyumbani, kule kuongozwa na mavutano ya marika ya mtu ambayo huenda yakamshawishi mtoto atoroke kutapungua sana.
Kwa kutumia kanuni za Biblia, kutoroka nyumbani hakuonekani sana kuwa ndio utatuzi wa matatizo yaliyomo maishani, ambayo ni lazima kila mtu aelekeane nayo. Kwa kupata tegemezo lenye upendo kutoka kwa washiriki mmoja mmoja wa jamaa, jamaa inakuwa mahali pa kujificha mifinyo ya ulimwengu wa nje. Uelewevu kamili zaidi wa kanuni za Biblia na utumizi wazo, pamoja na lile tumaini ambalo Mungu anatoa, utaongezea furaha hiyo. Kwa sababu gani usiache Mashahidi wa Yehova wazungumze jambo hilo pamoja nawe?
[Sanduku/Picture katika ukurasa wa 7]
MAMBO AMBAYO WAZAZI WANAWEZA KUFANYA
Tumieni wakati mkiwa pamoja na watoto wenu, mjue matatizo na mahitaji yao
Mwe wadumifu katika kuwaelekezea fikira na usimamizi
Toeni nidhamu na mazoezi kwa upendo
Fanyeni nyumbani pawe mahali penye furaha
MAMBO AMBAYO WATOTO WANAWEZA KUFANYA
Mwe watii, wenye upendo, na wenye staha kwa wazazi
Epukeni kujitenga kwa kukaa peke yenu; pendezweni sana na mambo ya kijamaa
Fikirieni jamaa kwa ujumla, si tamaa zenu wenyewe tu
Fungulieni fikira mlizo nazo moyoni na mfanye mawasiliano
[Picha katika ukurasa wa 5]
Mahusiano kati ya mzazi na mtoto ni ya maana sana