Maisha na Huduma ya Yesu
Fundisho Zaidi Siku ya Saba
SIKU ya mwisho ya Sikukuu ya Mahema (Vibanda), ile siku ya saba, ingali inaendelea. Yesu anafundisha katika kisehemu cha hekalu kinachotajwa kuwa “chumba cha hazina.” Inaonekana hapa ni katika eneo linaloitwa Ua wa Wanawake ambapo pana masanduku ambamo watu wanatumbukiza michango yao.
Kila usiku wakati wa sikukuu, kuna wonyesho wa mmuliko wa pekee katika eneo hili la hekalu. Majiti makubwa manne ya mishumaa yamesimamishwa hapa, kila moja likiwa na mabakuli makubwa manne yaliyojazwa mafuta. Nuru inayotoka katika mabakuli haya 16 yenye mafuta yanayowaka inatosha kumulika sehemu zinazozunguka, mpaka kufikia umbali mkubwa wakati wa usiku. Jambo ambalo sasa Yesu anasema huenda likakumbusha wasikilizaji wake juu ya wonyesho huu. “Mimi ndiyo nuru ya ulimwengu,” Yesu anapaaza sauti. “Yeye ambaye ananifuata mimi hatatembea kwa vyo vyote katika giza, bali atakuwa na nuru ya uhai.”
Mafarisayo wanakataa: “Wewe unatoa ushuhuda juu yako mwenyewe; ushuhuda wako si kweli.”
Kwa kujibu Yesu anarudisha hivi: “Hata ikiwa mimi natoa ushuhuda juu yangu mwenyewe, ushuhuda wangu ni kweli, kwa sababu mimi najua ambako mimi nilitoka na ambako mimi ninaenda. Lakini ninyi hamjui ambako mimi nilitoka na ambako mimi ninaenda.” Yeye anaongezea hivi: “Mimi ni mmoja ambaye natoa ushuhuda juu yangu mwenyewe, na Baba ambaye alinituma mimi anatoa ushuhuda juu yangu.”
“Yuko wapi Baba yako?” Mafarisayo wanataka kujua.
“Ninyi hamjui wala mimi wala Baba yangu,” Yesu anajibu. “Kama mngalinijua, ninyi mngalijua Baba yangu pia.” Hata ingawa Mafarisayo bado wanataka Yesu akamatwe, hakuna mmoja anayemgusa.
“Mimi ninaenda zangu,” Yesu anasema tena. “Mahali ambako mimi ninaenda ninyi hamwezi kuja.”
Kwa sababu ya hilo Wayahudi wanaanza kushangaa hivi: “Yeye hatajiua mwenyewe, sivyo? Kwa sababu yeye anasema, ‘Mahali ambako mimi ninaenda ninyi hamwezi kuja.’”
“Ninyi ni wa kutoka yale makao ya chini,” Yesu anaeleza. “Mimi ni wa kutoka yale makao yaliyo juujuu. Ninyi ni wa kutoka kwenye ulimwengu huu; mimi si wa kutoka kwenye ulimwengu huu.” Ndipo yeye anapoongezea hivi: “Ikiwa ninyi hamwitikadi kwamba mimi ndiye, ninyi mtakufa katika dhambi zenu.”
Bila shaka, Yesu anarejeza kwenye kuwako kwake kabla ya kuwa mwanadamu, na kwenye uhakika wa kwamba yeye ndiye Mesiya aliyeahidiwa, au Kristo. Hata hivyo, wao wanauliza hivi, bila shaka kwa madharau makubwa: “Wewe ni nani?”
Kwa kuelekeana moja kwa moja na katao lao, Yesu anajibu: “Ni kwa nini hata ninasema na ninyi katu?” Na bado yeye anaendelea kusema: “Yeye aliyenituma mimi ni wa kweli na mambo yale yale yenyewe ambayo mimi nilisikia kutoka kwake mimi ninanena katika ulimwengu.” Yesu anaendelea hivi: “Mara ninyi mkiisha kuwa mmenyanyua Mwana wa mwanadamu, hapo ndipo ninyi mtajua kwamba mimi ndiye, na kwamba mimi sifanyi jambo la uanzilishi wangu mwenyewe; bali sawa na vile Baba alinifundisha ndivyo mimi nanena mambo haya. Na yeye ambaye alinituma mimi yuko pamoja nami; yeye hakuniacha nibaki mimi mwenyewe tu, kwa sababu sikuzote mimi nafanya mambo yanayomfurahisha.”
Wakati Yesu anaposema mambo haya, wengi wanatia imani katika yeye. Kwa hao yeye anasema: “Ninyi mkibaki katika neno langu, ninyi ni wanafunzi wangu kweli kweli, na ninyi mtajua ule ukweli, na ule ukweli utawaweka ninyi huru.”
“Sisi ni wazaliwa wa Abrahamu,” wapinzani wake wanafoka, “na sisi hatujawa kamwe watumwa kwa mtu ye yote. Ni jinsi gani wewe unasema, ‘Ninyi mtakuwa huru’?”
Ingawa mara nyingi Wayahudi wamekuwa chini ya utumikisho wa kigeni, wao hawakiri mwonevu ye yote kuwa bwana-mkubwa. Wao wanakataa kuitwa watumwa. Lakini Yesu anaonyesha wazi kwamba wao ni watumwa kweli kweli. Kwa njia gani? “Kweli kweli kabisa mimi nawaambia ninyi,” Yesu anasema, “kila mtendaji wa dhambi ni mtumwa wa dhambi.”
Kukataa kukubali utumwa wao kwa dhambi kunatia Wayahudi katika msimamo hatari. “Mtumwa habaki kati ya watu wa nyumbani milele,” Yesu anaeleza. “Mwana anabaki milele.” Kwa kuwa mtumwa hana haki za urithi, huenda akawa katika hatari ya kuondoshwa kazini wakati wo wote. Mwana ambaye kwa kweli alizaliwa au alichukuliwa alelewe kati ya watu wa nyumba ile ndiye peke yake anayebaki “milele,” yaani, maadamu yeye yuko hai.
“Basi ikiwa yule Mwana anawaweka ninyi huru,” Yesu anaendelea, “ninyi kwa kweli mtakuwa huru.” Hivyo, ukweli ambao unaweka watu huru ni ule ukweli kuhusu yule Mwana, Yesu Kristo. Ni kwa njia ya dhabihu tu ya uhai wake mkamilifu wa kibinadamu kwamba mtu ye yote anaweza kuwekwa huru kutoka kwenye dhambi inayoleta kifo. Yohana 8:12-36, NW.
◆ Yesu anafundisha wapi siku ya saba? Ni jambo gani linalotukia huko wakati wa usiku, nalo linahusiana jinsi gani na fundisho la Yesu?
◆ Yesu anasema nini juu ya chanzo chake, na hilo linapasa kufunua nini juu ya utambulishi wake?
◆ Ni kwa njia gani Wayahudi ni watumwa, lakini ni ukweli gani utakaowaweka huru?