Ya Mwisho ya Zile Serikali Kubwa za Ulimwengu
Wakati kitabu cha Biblia cha Ufunuo kilipoandikwa, takriban miaka 1,900 iliyopita, kilisema kwamba “wafalme” watano, au serikali kubwa za ulimwengu, zilikuwa tayari zimekuja na kwisha. Hizo zilikuwa Misri, Ashuru, Babuloni, Umedi-Uajemi, na Ugiriki. Ile ya sita, Roma, ‘ilikuwako’ bado, lakini ya saba ilikuwa haijawasili. (Ufunuo 17:10, NW) Hiyo serikali kubwa ya saba ya ulimwengu ilikuwa nini? Ilikujaje kuwako? Na ni nini itakayoifuata? Majibu kwa maswali haya ya maana ndiyo habari ya makala hii.
MFUATANO mkubwa wa historia ya ulimwengu kwa muda wa miaka 2,500 iliyopita ulitolewa mapema katika kitabu kile chenye kuenezwa zaidi ya vyote ambacho ulimwengu umepata kujua. Hata hivyo, ni watu wachache kwa kulinganisha walio na nakala ya kitabu hicho, Biblia, ambao wanajua lo lote juu ya habari za kustaajabisha zilizomo.
Mathalani, zaidi ya miaka 500 kabla ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo, nabii Danieli aliandika njozi iliyovuviwa kwa njia ya kimungu ambamo zile serikali kubwa za ulimwengu za tangu wakati wake ziliwakilishwa na wanyama wenye nguvu nyingi. Kila mnyama alikuwa na tabia za serikali kubwa ya ulimwengu aliyowakilisha. Ile Milki ya Roma yenye uweza ilielezwa kuwa mnyama mkubwa sana ‘wa kuogopesha na wa kutisha sana na mwenye nguvu zisizo za kikawaida.’ Danieli alisema kwamba ‘huyo alikuwa kitu tofauti na wanyama wale wengine ambao walimtangulia, na alikuwa na pembe kumi.’—Danieli 7:2-7, NW.
Ile ‘Pembe Ndogo’
Baada ya muda, Milki ya Roma ilikua ikafunika eneo ambalo lilitandaa kutoka Visiwa vya Uingereza kushuka chini mpaka ng’ambo kwenye sehemu kubwa zaidi ya Ulaya, na kwenda umbali wote ule kuzunguka Mediterania na kuruka ng’ambo ya Babuloni mpaka kwenye Ghuba ya Ajemi. Milki hii yenye uweza ilivunjika-vunjika hatimaye ikawa mataifa mengi—ikawa zile “pembe kumi” ambazo Danieli aliona.a Ndipo Danieli alipoona “pembe nyingine, ndogo, ikaja miongoni mwa hizo, na kulikuwa na tatu za zile pembe za kwanza ambazo ziling’olewa kutoka mbele ya hiyo.” (Danieli 7:8, NW) Hiyo ilimaanisha nini?
Danieli aliambiwa: “Kwa habari ya zile pembe kumi, kutoka katika ufalme huo [wa Kiroma] kuna wafalme kumi ambao watainuka; na bado mwingine mmoja [ile ‘pembe ndogo’] atainuka baada ya hao, na yeye mwenyewe atakuwa tofauti na wale wa kwanza, na wafalme watatu yeye atanyenyekeza.” (Danieli 7; 24, NW) Ni nani aliyekuwa ile ‘pembe ndogo,’ na ni nani waliokuwa wale wafalme watatu ambao alinyenyekeza?
Kisiwa kimoja katika pembe ya kaskazini-magharibi ya Milki ya Roma kilikuwa kimebaki kando bila kuhusishwa sana katika mambo ya ulimwengu. Ni kama vile mwanahistoria mmoja alivyoeleza: “Katika karne ya kumi na sita Uingereza ilikuwa imekuwa serikali ya kikawaida tu. Utajiri wayo ulikuwa hafifu ukilinganishwa na ule wa Uholanzi. Idadi ya watu wayo ilikuwa kidogo sana kuliko ile ya Ufaransa. Kani zayo za kijeshi (kutia na jeshi la baharini) zilikuwa duni kwa zile za Hispania.” Hata hivyo, Uingereza ilisitawisha kikosi cha baharini chenye umashuhuri fulani, na maharamia wayo wa baharini, na meli za watu binafsi, wakaanza kuvamia makoloni ya Hispania na meli zao zilizojazwa hazina.
Zile Pembe Tatu
Katika 1588 Phillip 2 wa Hispania aliondokesha kile kikosi cha meli za Armada cha Hispania dhidi ya watesi wake Waingereza. Kikosi hiki cha meli 130 chenye kuchukua wanaume zaidi ya 24,000 kilisafiri polepole kikielekea juu katika ule Mfereji wa Uingereza, kumbe kikakabiliwa na pepo na dhoruba kali-kali za Atlantiki. Katika Modern Europe to 1870, mwanahistoria Carlton Hayes anaandika kwamba tukio hili “lilikuwa ndiyo hatua ya kukata maneno ambapo uhodari wa meli za kijeshi uliacha kuwa wa Hispania ukawa wa Uingereza.”
Katika karne ya 17, Waholanzi walisitawisha kikosi cha meli za ubiashara chenye ukubwa unaovizidi kwa mbali vikosi vinginevyo vyote ulimwenguni. Meli zao ndizo zilizozitawala bahari, nazo zilisaidia kufikisha faida zao kwenye serikali za kote kote. Lakini Uingereza ikawa ndiyo yenye nguvu zaidi katika jambo hili pia, kwa sababu ya kuongezeka kwa makoloni yake ya ng’ambo.
Ndipo, katika karne ya 18, Waingereza na Wafaransa walipigana wakiwa sehemu za mbali mbali sana kama Amerika ya Kaskazini na India, na hiyo ikaongoza kwenye ule Mkataba wa Paris katika 1763. Kuhusu mkataba huo, William B. Willcox aliandika katika kitabu chake Star of Empire—A Study of Britain as a World Power kwamba ingawa mkataba huo ulionekana kama kuacha msimamo wa kwanza, “kwa kweli ulitambua msimamo mpya wa Uingereza kuwa ndiyo serikali kubwa zaidi ya Ulaya katika ulimwengu uliokuwa ng’ambo ya Ulaya.”
Wanahistoria wengine wanaafikiana na jambo hilo, wakisema: “Kutokana na karne mbili za kufanya vita pamoja na Wahispania, Waholanzi, na Wafaransa, Uingereza Kuu iliibuka katika 1763 ikiwa ndiyo serikali ya mbele zaidi kibiashara na kikoloni katika ulimwengu.” (Modern Europe to 1870) “Katika 1763 Milki ya Uingereza ilitagaa kwa kukanyaga ulimwengu ikiwa kwa namna fulani kama Roma iliyohuishwa na kupanuliwa.” “Iliibuka katika vile vita vya katikati ya karne ile ikawa ndiyo milki iliyo kubwa na yenye imara kupita zote—tena ikiwa ndiyo serikali kubwa yenye kuchukiwa kabisa kuliko zote.” (Navy and Empire, kilichotungwa na James L. Stokesbury) Ndiyo, ‘pembe ndogo’ hii ilikuwa imekua ikawa ndiyo serikali kubwa ya saba ya ulimwengu katika historia ya Biblia.
Waingereza walisonga upande wa juu wa Mto Nailo na kuvuka ng’ambo ya Mto Zambezi. Walihamia ndani ya Burma ya Juu, Borneo ya Kaskazini, na visiwa vya Pasifiki. Waaidha, wao walifanya Kanada, Australia, New Zealand, na pwani ya mashariki ya Amerika ya Kaskazini ziwe koloni zao. “Milki ya Roma ilijishughulisha na mambo yayo yenyewe,” anaandika James Morris katika Pax Britannica. “Milki ya Uingereza ilieneza shughuli zayo pande zote za dunia. “Ikiwa ndiyo milki kubwa zaidi ya zote katika historia ya aina ya binadamu, ikizunguka karibu robo moja ya uso wa nchi-kavu ya dunia, na zaidi ya robo moja ya idadi ya watu wayo. Ilisemwa kwamba jua halikuchwea kamwe katika eneo la utawala wayo.
Serikali Yenye Sehemu Mbili
Katika kitabu cha Ufunuo, hii serikali kubwa ya saba ya ulimwengu ilikuwa pia imeelezwa kuwa yenye “pembe mbili kama mwana-kondoo.” (Ufunuo 13:11, NW) Kwa sababu gani pembe mbili? Kwa sababu Milki ya Uingereza na lile taifa jipya la Amerika, ambazo ziliunganishwa na lugha moja, kanuni za namna moja, na miongozo ya namna moja, zilianza ushirikiano baada ya muda mfupi. Katika mambo mengi zikawa serikali kubwa ya ulimwengu ya sehemu mbili, yenye kusema Kiingereza.
William B. Willcox anaonyesha katika Star of Empire kwamba katika karne ya 19 United States ‘ilikuwa imetenganishwa na Ulaya na kile kikosi cha Uingereza.’ Yeye anaongezea hivi: “Kwa karne moja United States ilikuwa huru kukua iwe serikali kubwa bila kupata kamwe sifa ya kuwa na jeshi au kikosi-bahari ambacho ndicho kilifanya kila serikali kubwa nyingine ijulikane, isipokuwa katika vita yayo ya wenyewe kwa wenyewe.” Amerika ‘ilikuwa imeweza kujimudu kukaa mbali peke yayo kwa sababu kile Kikosi cha Mfalme kilikuwa kimekuwa ndiyo kinga yayo dhidi ya serikali za Uingereza.” Baadaye, United States ikawa pia serikali kubwa kijeshi.
Kielelezo cha kutokeza juu ya utendaji ulioungana wa Uingereza na Amerika kilitukia siku ya Juni 6, 1944, wakati ambapo wimbi la Vita ya Ulimwengu ya Pili lilibadilika katika Ulaya ya kaskazini. Siku hiyo, askari 156,000 wa Uingereza, Amerika, na kani nyingine za vikosi marafiki zilishambulia kontinenti ya Ulaya. Kani hii ya muungano ilikuwa chini ya amri ya ujumla ya jemadari mmoja wa United States, na amri ya kupambana ilikuwa ya mwelekeza-vita-mkuu Mwingereza—Eisenhower akiwa ndiye wa ujumla na yule mwingine akiwa ni Montgomery. Zaidi ya hilo, makombora ya atomi yaliyomaliza ile vita pamoja na Japani yalitengenezwa kwa jitihada ya muungano wa wanasayansi Waingereza na Waamerika.
Kama vile Los Angeles Times la Mei 5, 1986, lilivyoonyesha, hata wakati wa amani, Uingereza na Amerika zimefanya ushirikiano “katika mambo yanayotaka uangalifu mwingi sana kama vile ujasusi na tekinolojia ya nyukilia.” Kanada, Australia, na New Zealand zilipojiunga nazo baadaye, hizo ‘zimegawanya tufe hili likawa maeneo ya kazi ya kukusanya taarifa za kijasusi na zikaafikiana kushirikiana hata habari zilizo za siri zaidi.’ Karatasi-habari hiyo ilisema kwamba ingawa ‘si sikuzote ambapo umekuwa laini’ uhusiano huo, ‘umeonekana wazi zaidi kwa sababu ya ukaribiano wao kuliko maudhiano yao.’
Yaliyo mengi ya makoloni ya Uingereza yamepata uhuru na kujiunga na Jumuiya ya Madola. Ingawa huenda milki yenyewe ikawa imeisha, ile Serikali Kubwa ya Ulimwengu ya Waingereza-Waamerika ingali ipo. Lakini itakuwako kwa “kitambo kidogo” tu, inapolinganishwa na zile karne nyingi ambazo serikali kubwa ya Kiroma iliyoitangulia ilidhibiti utawala.—Ufunuo 17:10, NW.
Utawala Mpya wa Ulimwenguni Pote
Unabii wa Danieli kuhusu zile serikali kubwa za ulimwengu umethibitika kuwa kweli muda wote wa miaka 2,500 ya kuwako kwa serikali ya ulimwengu—kutoka kabla ya 500 K.W.K. kuteremka mpaka ile serikali kubwa ya saba ya ulimwengu katika siku yetu. Hivyo, sisi tunaweza kuwa na uhakika katika sehemu yote nyingine ya unabii huo. Uhakika wa kustaajabisha ni kwamba unabii huo hauelezi juu ya nyingine zaidi za serikali kubwa za kibinadamu za ulimwengu! Ufunuo pia ulionyesha kwamba kungekuwa na saba tu.b Halafu ni jambo gani litakalotukia baada ya hapo?
Sura ya 7 ya Danieli, ambayo inasimulia juu ya hizi serikali kubwa za ulimwengu, inaendelea kueleza juu ya jambo fulani la kugutusha hata zaidi—badiliko kubwa katika njia ambayo dunia inatawalwa! Tawala za kibinadamu zenye kushindwa zitamalizika na mahali pazo pachukuliwe na serikali ya kimbingu iliyo ya uadilifu.
Njozi ya Danieli ilimruhusu akione kiti cha ufalme cha kimbingu kilicho adhimu, cha “yule Mkale wa Siku “Yehova Mungu. Aliyeletwa mbele ya Mmoja huyu alikuwa “mtu fulani kama mwana wa binadamu”—Yesu Kristo mfufuliwa.c Danieli anasimulia hivi: “Kwake yeye zilipewa utawala na fahari na ufalme, kwamba jamii za watu, vikundi vya kitaifa na lugha vipaswe kutumikia hata yeye. Utawala wake ni utawala unaodumu kwa wakati usio dhahiri ambao hautapitilia mbali, na ufalme wake [kwa utofauti na falme za kibinadamu zenye kushindwa] ni mmoja ambao hautaletwa kwenye angamizo.”—Danieli 7:9, 10 13, 14, NW.
Unabii mmoja wa mapema zaidi aliopewa Danieli kuhusu hizo hizo serikali kubwa za ulimwengu ulikuwa umesema: “Katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atasimamisha ufalme ambao hautaletwa kamwe kwenye angamizo... Utaponda-ponda na kuweka mwisho kwenye falme zote hizi [za kibinadamu], na huo wenyewe utasimama hadi nyakati zisizo dhahiri. . . . Na ile ndoto ni yenye kutegemeka, na ile fasiri yayo ni yenye kustahili itibari.”—Danieli 2:44, 45, NW.
Serikali hii ya Ufalme yenye kuendeshwa na Mungu ndiyo ile ile ambayo Yesu alitufundisha kusali tukiiomba. Yeye alisema: “Basi ninyi salini hivi; Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe, Ufalme wako uje, Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.”—Mathayo 6:9, 10.
Wakaaji wa dunia watakuwa wenye furaha kama nini chini ya serikali hiyo! Hilo litakuwa badiliko la kutoka kunyonywa na wanadamu kuja kwenye haki ya kimungu, kutoka kwenye njia ya mwanadamu isiyokamilika ya kufanyia mambo kuja kwenye viwango bora kabisa vya Mungu. Yanayosemwa na Biblia juu ya uendeshwaji wa Ufalme huo yatazungumziwa na makala ya wakati ujao katika mfululizo huu.
[Maelezo ya Chini]
a Pembe, ambayo ni silaha isiyoshindwa kwa urahisi, inatumiwa mara nyingi katika Biblia kuwakilisha watawala na nasaba zenye kutawala.—Kumbukumbu 33:17; Zekaria 1:18-21; Ufunuo 17:3, 12.
b Ufunuo 17:11 unataja “mnyama-mwitu” ambaye ni “mfalme wa nane, lakini anatokana na yule wa saba.” Hii serikali kubwa ya nane ambayo ingekuwako wakati wa maisha ya ile ya saba itazungumziwa katika makala moja ya baadaye.
c Usemi “Mwana wa binadamu” unapatikana karibu mara 80 katika yale masimulizi ya Injili, na katika kila kisa unarejeza kwa Yesu Kristo.—Ona Mathayo 26:63, 64, NW.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Mvamio wa Mataifa Marafiki juu ya Ulaya siku ya Juni 6, 1944, ulikuwa kielelezo cha kutokeza cha ushirikiano wa muungano wa Waingereza-Waamerika
[Hisani]
U.S. Coast Guard photo