Sababu kwa Nini Watu Fulani Wamebadili Dini Yao
ILI MTU achukue hatua hiyo kubwa sana ya kubadili dini yake, hakika lazima yeye awe na sababu nzuri. Manufaa yangepaswa yashinde hasara yo yote.
Je! wewe ungefikiria kupata kujua Muumba wako na kukuza uhusiano mzuri pamoja naye kuwa sababu nzuri? Imekuwa hivyo kwa wengi. Ili kukuza uhusiano na mtu fulani, lazima tupate kujua mtu huyo vizuri. Mathalani, mtoto mdogo huenda akaogopa kushika mkono wa mgeni mpaka apate kumjua. Ndivyo na sisi, ni lazima tupate kujua Mungu kabla hatujaanza kuwa na itibari katika yeye. Kweli, dini zilizo nyingi zina kitu kikuu ambacho zinaabudu kama Mungu. Lakini je! si kweli pia kwamba kwa watu walio wengi Mungu hafahamiki vizuri na yu mbali sana na hana utu unaoelezwa wazi kabisa? Kwa hiyo sisi tunapata kumjua jinsi gani?
Tunapotazama vitu vinavyotuzunguka, tunastaajabishwa na yale tunayoona. Tunaona uzuri, elimu na uwezo. Ubuni wa vyote hivi unawatatanisha wengi, lakini kuna kitabu kinachoeleza haya kwa uwazi. Ni Biblia. Kupitia kurasa zayo, tunajifunza kwamba maajabu haya yalibuniwa na Muumba aliye na jina na utu. Tunapojifunza Biblia kwa umakini, utu wa Mungu unakuwa wazi kabisa kwetu. Tunamwona kama Mungu mwenye upendo na mwenye kujali. “Mungu ni upendo,” yasema Biblia. (1 Yohana 4:8) Tunavutwa kwenye utu huu wa ajabu, uliosawazika kikamilifu katika upendo, hekima, haki, na uwezo. Uhusiano wa karibu unafuata.
Misae alipatwa na jambo kama hilo la kuvutwa karibu na Yehova. Mwanamke huyo anaeleza hivi: ‘Nilipokuwa mtoto, nilifunzwa kwamba kuna miungu wengi. Kulikuwa na mungu wa maji, mungu wa miti, na mmoja wa nyumba. Ingawa mimi nilikuwa na mashaka kuhusu kuwapo kwao, mimi niliitikadi kwamba lazima kuwe na Mungu mmoja wa kweli. Malezi yangu ya Kibuddha-Shinto yenye kushurutisha utii yalisababisha nifikirie Mungu kuwa wa kuogopwa, mtu aliyetoa adhabu kwa makosa. Ijapokuwa nilikuwa na tamaa ya kwenda kanisani na kujifunza juu ya Mungu wa Wakristo, malezi yangu ya Kibuddha yalinizuia. Kisha mwanamke mmoja akaja kwenye nyumba yangu na akajitolea kujifunza Biblia nami. Kupitia funzo hilo, nilijifunza kwamba Mungu ana jina, Yehova. Nilisisimuka kujua kwamba yeye si Mungu mwenye kuogofya bali mwenye upendo, mwenye kutuangalia sikuzote, si ili atuadhibu, bali atusaidie. Nilitaka kumtumikia Mungu huyo, na kwa hiyo nikabadili dini yangu.’ Mwanamke huyo amekuwa akifurahia uhusiano wenye kuridhisha pamoja na Mungu kwa takriban miaka 29.
Uhusiano Unaotoa Uhuru na Tumaini
Kuna manufaa mengine ambayo wengi wamepokea kupitia kwa kukuza uhusiano pamoja na Mungu. Mahusiano mengine yanapoanza kutokuwa ya maana sana maishani mwao, wengi wamepata uhuru kutokana na woga wa mwanadamu wenye kutumikisha na desturi zenye kuenea zisizo na maana na thamani halisi. Kwa sababu hii, wamewekwa huru kutoka gharama zenye kulemea za kudumisha tendo la kujisingizia tu na mapokeo, ambazo zinaweka jamaa nyingi katika madeni daima. “Kuwaogopa wanadamu huleta mtego;” inaonya Biblia, ikiongezea uhakika huu, “Bali amtumainiye BWANA [Yehova, NW] atakuwa salama.”—Mithali 29:25.
Uhuru mwingine utakaopatikana ni uhuru kutoka woga wa kifo. Misae anayetajwa juu anasema: “Nilipokuwa na miaka 22, nilipatwa na homa ya matumbo. Nilipolala hapo nikiwa nimezimia, ningeweza kuwasikia marafiki na washiriki wa jamaa wakizungumza juu yangu kama kwamba walitazamia nife. Lakini niliogopa kifo. Wazo nililokuwa nalo tu ni kwamba nilitaka kuishi, na inafurahisha kwamba nilipata nafuu. Kupitia funzo langu la Biblia baadaye, niliwekwa huru kutoka woga huo wa kifo. Nilijifunza kwamba kifo ni kutokuwapo tu.” Biblia inasema hivi: “Wafu hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5, 10) Mtu akifa, kuna tumaini la ajabu la ufufuo kwa sababu wafu wanaendelea kuishi katika kumbukumbu la Mungu.—Yohana 5:28, 29.
Wengine wengi ambao wanajifunza Biblia wamepata vivyo hivyo kwamba mambo ambayo wamejifunza yameyapa maisha yao maana halisi na tumaini. Hii ndiyo sababu moja iliyofanya Biblia iandikwe, yaani, “tupate kuwa na tumaini.” (Warumi 15:4) Ubuddha haufundishi cho chote kuhusu Muumba au Mungu. Inasemekana kwamba uovu na kuteseka umekuwako sikuzote na utaendelea milele kupitia vipindi visivyokoma vya kuzaliwa tena. Dini nyingi za Magharibi zinafundisha kwamba wazuri wataenda mbinguni, mahali dhahiri lakini kwa habari ya watakachofanya huko, hawajui sana. Tofauti na falsafa hizi za kidini ambazo zinatoa tumaini au maana ndogo sana kwa maisha zao, Biblia inafundisha kwamba mwanadamu aliumbwa ili afurahie uhai milele duniani akiwa mtunzaji wayo. (Mwanzo 2:15-17; Isaya 45:18) Hivyo huenda sisi tukang’amua kwamba maisha yanapaswa yatumiwe si kupata miliki tu na kujitumikia mwenyewe bali kumtumikia Mungu na wengine katika njia isiyo ya ubinafsi.—Mhubiri 12:13; Mathayo 22:37-39.
Kupata Ukweli na Marafiki wa Kweli
Watu fulani wanasukumwa wabadili dini yao kwa sababu nyingine. Kati yazo ni tamaa ya kutafuta ukweli wa kidini. Bila shaka, watu wengi wanahisi kwamba hakuna kitu kama ukweli kamili na kama Biblia inavyosema, wao ‘hawafanyi uchunguzi.’—Zaburi 10:4, NW.
Lakini kuna wale ambao wanafanya uchunguzi huo. Sakae, anayeishi katika Japani ya kati, alitoka katika farakano moja la Kibuddha na kuingia katika lingine kwa miaka 25 ili apate ukweli. Mwanamke huyo hakuridhika kamwe. Alipopanda vyeo vyenye madaraka katika kila tengenezo, sikuzote yeye aliona mambo yenye kumkwaza, kama vile biashara, ukosefu wa adili, na kupunja. Yeye hata alisafiri kwenda India ili atafute chanzo cha dini ya Buddha katika mahali pa kihistoria ambapo Buddha aliishi na kufunza. Alitamaushwa sana alipopata upendezi mdogo sana katika dini ya Buddha katika nchi ya Wahindi. Halafu alipokuwa akiongea na Mashahidi wa Yehova, aliambiwa kwamba dini zote hazitoki kwa Mungu lakini zinatoka kwa adui yake, Shetani Ibilisi.—1 Wakorintho 10:20.
Jambo hili lilimgutusha Sakae, lakini lilimfanya afikiri na kuchunguza-chunguza. Alisoma kitabu What Has Religion Done for Mankind?a na vichapo vingine vya Biblia. Alianza kuona kwamba hali dini ya Buddha kama ilivyozoewa katika Japani ilifanya mabadiliko mengi katika muda wa miaka, Biblia haijabadilika kwa maelfu ya miaka. Hatimaye uchunguzi wake ulimfaidi. Alipata ukweli aliokuwa akitafuta. Shangwe yake ilikuwa kama shangwe ya yule mtu katika mfano wa maneno wa Yesu aliyepata hazina imefichwa katika shamba: “Kwa ile shangwe ambayo yeye anayo yeye anakwenda na kuuza vitu alivyo navyo na kununua lile shamba.”—Mathayo 13:44, NW.
Wale ambao wamepata ukweli wa kidini wanawaonyesha wengine wanaoutafuta “hisia mwenzi.” (1 Petro 3:8, NW) Kwa kweli, uchangamfu wao mwanzoni na upendo wa kweli kwa ya kwanza unawavutia wengi wajifunze Biblia. “Wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi,” akasema Yesu. (Yohana 13:35) Ni wapi tunapoweza kupata hali hiyo yenye kupendeza leo? Akiandika katika safu yake kwa ajili ya Daily Yomiuri ya Tokyo, Kazuhiko Nagoya alieleza jinsi alivyotendewa kwa uchangamfu alipozuru mahali pa mkutano pa Mashahidi wa Yehova. “Jinsi walivyotabasamu,” akasema Nagoya, “ilionekana kama kwamba wao walikuwa wamenifahamu toka mkutano uliotangulia na walikuwa na furaha kuniona tena.” Lakini haikuwa hivyo. “Niliangalia nyuso zao kwa kukaza macho nami nikapata kwamba wao walikuwa wageni kabisa.” Wakati watu wengine wawili walipotabasamu pia, “Nilihisi kuwa mwenye furaha sana,” akumbuka Nagoya. “Hivyo ndivyo watu hao wanavyotabasamu kwa wageni, wanapomwona katika yo yote ya mikutano yao.
Uchangamfu na upendo havitokani na watu kujuana vizuri sana mmoja na mwenzake kwa sababu ya kukusanyika mahali pamoja kwa ukawaida. Badala yake, hili linatokana na funzo la Biblia la kikawaida na kutumia kanuni zayo katika maisha yao. Watu wengi walioalikwa kuhudhuria “Washika Ukamilifu” Mikusanyiko ya Wilaya ya Mashahidi wa Yehova ya 1985-86 katika mabara ya kigeni waliguswa sana na upendo na ukarimu ulioonyeshwa na wakaribishaji wao. Watu wawili vijana waliooana kutoka Japani waliohudhuria mkusanyiko katika Ufilipino walieleza hivi: “Sisi sote tulipojiunga kuimba wimbo wa hatima, kila mmoja akiimba katika lugha yake mwenyewe, tulivutwa sana sana. Tulihisi kwa mara ya kwanza kinachomaanishwa kuwa katika udugu wa kweli kweli wa kimataifa.”
Kwa kumalizia, wengi watakuambia juu ya mabadiliko makubwa ambayo wamefanya maishani mwao kama tokeo la kujifunza Biblia na kuitumia. Watu ambao hapo mwanzoni walikuwa na nyutu zenye kutofautiana kama vile kondoo walivyo tofauti na mbwa mwitu sasa wanapatana kwa kuamanika katika kusanyiko la Kikristo. (Isaya 11:6) Watu fulani walikuwa wepesi wa kukasirika na wasio na urafiki, wasiozuia tabia-moyo yao na hata wenye kuogofya. Wengine walikuwa na tatizo la kushuka moyo. Bado wengine walikuwa wenye tabia ya kujipendeza wenyewe na wenye kujifikiria wenyewe. Wengi walikuwa na tabia mbaya sana za kushinda. Lakini kwa jitihada yenye bidii, pamoja na tamaa ya kupendeza Mungu, waliweza kufanya mabadiliko makubwa sana.
Namna gani wewe? Je! zo zote za sababu zilizo juu za kufanya mabadiliko zinakuvutia wewe? Ikiwa ndivyo, tunakutia moyo ufanye funzo la Biblia kwa uzito. Biblia inaonyesha kwamba dini zote za bandia zimo katika mwendo wa kugongana pamoja na Mungu wa Biblia. Kama rubani wa ndege aliyetajwa katika makala iliyotangulia, unahitaji kuchukua tendo kubwa sana ili uokoe uhai wako na uhai wa wapendwa wako. “Njia ni pana iendayo upotevuni,” akasema Yesu, “nao ni wengi waingiao kwa mlango huo. Bali mlango ni mwembamba, na njia imesonga iendayo uzimani.” (Mathayo 7:13, 14) Ndiyo, ikiwa wewe unatembea katika ile ‘njia pana,’ kuna sababu nzuri kwako wewe kubadili dini yako!
[Maelezo ya Chini]
a Kilitangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Malezi yangu ya Kibuddha-Shinto yenye kushurutisha utii yalisababisha nifikirie Mungu kuwa wa kuogopwa
[Picha katika ukurasa wa 7]
‘Njia ni nyembamba na imesonga iendayo uzimani’