Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w88 7/1 kur. 23-28
  • “Yehova Ni Mchungaji Wangu”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Yehova Ni Mchungaji Wangu”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Yehova, Mchungaji Mwenye Upendo
  • Yehova Anahami Kondoo Zake
  • Karamu Nono Katikati ya Maadui
  • Yehova Ni Mchungaji Wetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • “Yehova Ni Mchungaji Wangu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Zaburi 23:4—“Nijapopita Kati ya Bonde la Uvuli wa Mauti”
    Mistari ya Biblia Yafafanuliwa
  • Mchungaji Mwenye Upendo
    Kumsikiliza Mwalimu Mkuu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
w88 7/1 kur. 23-28

“Yehova Ni Mchungaji Wangu”

Yehova ni Mchungaji wangu, mimi sitakosa kitu cho chote.”​—ZABURI 23:1, NW

1, 2. Ni nini baadhi ya mambo yaliyotimizwa na Daudi, na yeye alitunga zaburi ngapi?

WAZIA tamasha hii: Vikosi vya Kifilisti vinaelekeana na jeshi la Israeli. Goliathi, jitu Mfilisti, ni mkaidi. Mwanamume mmoja kijana, ambaye silaha yake ni kombeo na mawe tu, anapiga mbio kukutana naye. Jiwe moja lililolengwa shabaha vizuri linatoboa fuvu la kichwa cha jitu huyo na kumwua. Huyu kijana mwanamume alikuwa nani? Daudi, mchungaji aliyepata ushindi huu wa kushangaza sana kwa msaada wa Yehova Mungu.​—1 Samweli, sura ya 17.

2 Baada ya muda, huyu mwanamume kijana akawa mfalme wa Israeli, akitawala kwa miaka 40. Yeye alikuwa mpiga-kinubi stadi na alitunga mashairi mengi chini ya uvuvio wa kimungu. Daudi aliandika pia zaidi ya zaburi nzuri 70 ambazo ni chanzo cha kitia-moyo kingi na mwongozo kwa watu wa Yehova leo. Inayojulikana vizuri zaidi kati ya hizi ni Zaburi 23. Kwa nini usifungue Biblia yako ufuatishe wakati sisi tunapoanza funzo la mstari kwa mstari la zaburi hii?

Yehova, Mchungaji Mwenye Upendo

3. (a) Ni katika pindi zipi Daudi alijasirisha uhai wake ili ahami kondoo zake? (b) Ni katika maana gani Yehova ni Mchungaji wetu?

3 “Yehova ni Mchungaji wangu.” (Zaburi 23:1, NW) Akiwa mchungaji mwenye kujionea mengi, Daudi alijua jinsi ya kuongoza, kulisha, na kuhami kondoo. Mathalani, yeye alihami kondoo zake kwa ushujaa kutokana na simba katika pindi moja na dubu katika pindi nyingine. (1 Samweli 17:34-36) Kondoo za Daudi waliitibari mchungaji wao kabisa kabisa. Lakini kwa kuhusiana na Yehova, yeye mwenyewe alikuwa kondoo. Kwa kuwa Daudi alihisi akiwa salama salimini katika utunzaji wenye upendo wa Mungu, yeye angeweza kusema: “Yehova ni Mchungaji wangu.” Je! wewe unafurahia hisia hii ya usalama-salimini chini ya yule Mchungaji Mkuu, Yehova Mungu? Kwa uhakika yeye anaongoza, analisha, na kuhami waabudu wake walio kama kondoo leo. Waaidha, wakiwa wazee wawekwa rasmi katika makundi ya Mashahidi wa Yehova, wachungaji wadogo waaminifu walio wenye upendo wanatunza kondoo kwa juhudi.​—1 Petro 5:1-4.

4. Ni jinsi gani hali yetu leo ilivyo kama ile ya Waisraeli katika jangwa?

4 “Mimi sitakosa kitu cho chote.” Fikiria kwa uangalifu taarifa hii. Kwa sababu ya utunzaji wenye upendo wa Yehova, je! wewe huna hisia yenye kutuliza moyo ya utulivu na uhakika wa kutumainia? Je! wewe unakumbuka yaliyopata Waisraeli wakati walipotanga-tanga katika jangwa kwa miaka 40? Naam, Mungu aliwaandalia mahitaji yote ya msingi! Hivyo ndivyo ilivyo leo. Watumishi waaminifu wa Yehova hawakosi kitu cho chote. Wengi wanaweza kusema sawasawa na maneno haya ya Daudi yenye uvuvio: “Mimi nilikuwa mwanamume kijana, mimi nimekua nikawa mzee pia, na bado mimi sijaona mtu ye yote mwadilifu ameachwa kabisa kabisa, wala mzao wake akiwa anatafuta mkate.” (Zaburi 37:25, NW) Leo, wingi wa chakula cha kiroho unaandaliwa kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye uangalifu.” (Mathayo 4:4; 24:45-47, NW) Zaidi ya kuwako mikutano kadhaa kwa juma, tuna Biblia, magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, na vichapo vingine vingi. Hata katika nchi nyingi ambako kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova imepigwa marufuku, ugavi wa chakula cha kiroho unapokewa kwa ukawaida. Kondoo za Yehova hawakosi kitu cho chote!

5. Kwa nini kondoo za Yehova leo ni wenye amani na wamestareheka, na tokeo ni nini?

5 “Katika malisho yenye nyasi-nyasi yeye ananifanya mimi nilale chini.” (Zaburi 23:2, NW) Kulikuwa na maeneo makubwa ya malisho yenye nyasi-nyasi kuzunguka majiji mengi katika Israeli ya kale. Kama vile mchungaji mwenye upendo alivyoongoza kondoo zake wakati huo kwenye maeneo mazuri yaliyo salama malishoni, ndivyo Yehova anavyotunza kondoo zake leo. Anasema hivi mtunga zaburi: “Sisi ndio watu wa malisho yake.” (Zaburi 79:13; 95:7, NW) Kondoo halisi wanaendelea vizuri wakati wanapokuwa wameridhika na wanaweza kupumzika katika joto la mchana. Leo kondoo za Yehova ni wenye amani na wamestareheka kwa sababu wao wana uhakika wa kutumaini katika wachungaji waliokomaa—waangalizi wenye mazoezi walio katika makundi na mizunguko. Kama matokeo, makundi ya kondoo za kiroho yanaongezeka. Watu wengi ambao hapo kwanza walitendwa vibaya na wachungaji bandia wa Babuloni Mkuu ni wenye furaha sana sasa na wameridhika wakiwa kondoo za Yehova.

6. Ni jinsi gani Yehova ‘anatuongoza sisi karibu-karibu na mahali pa pumziko palipo na maji ya kutosha’?

6 “Karibu-karibu na mahali pa pumziko palipo na maji ya kutosha yeye ananielekeza mimi.” Katika Israeli mchungaji alilazimika kuongoza kundi lake la kondoo kwenye kidimbwi au kijito cha maji. Lakini mara nyingi ilikuwa vigumu kupata maji katika majira ya ukavu. Leo, Yehova ‘anatuelekeza kwenye mahali pa pumziko penye maji ya kutosha’ kwa kuandaa maji ya ukweli yakiwa mengi sana. (Linganisha Ezekieli 34:13, 14.) Na nabii Isaya anatoa mwaliko huu wenye kuamsha: “Hei, ninyi nyote wenye kiu! Njoni kwenye maji.” (Isaya 55:1, NW) Kwa kutwaa maji haya ya kiroho, kondoo wanapata himaya wasipatwe na hukumu moto-moto zitakazokuja juu ya wale “ambao hawajui Mungu na wale ambao hawatii habari njema.” —2 Wathesalonike 1:8; Ufunuo 7:16, 17, NW.

7. Ni wakati gani burudisho la kiroho kutoka kwa Yehova linapokuwa lenye msaada hasa, na ni chini ya hali gani maandiko ya Biblia yaliyotiwa katika kumbukumbu ya akili yanaweza kuthibitika kuwa yenye manufaa sana?

7 “Nafsi yangu yeye anaburudisha.” (Zaburi 23:3, NW) Wakati sisi tunapokuwa wachovu katika matata, wenye kuvunjika moyo, au tunapoelekeana na upinzani mzito, Yehova anatuburudisha kwa njia ya Neno lake. Kwa sababu hiyo, ni vema Wakristo wafanye liwe zoea kusoma kisehemu fulani cha Biblia kila siku. Je! wewe hufanya hivi? Watu fulani wanaona ni jambo lenye msaada kutia maandiko fulani katika kumbukumbu ya akili yao, kama vile Kutoka 34:6, 7 au Mithali 3:5, 6. Kwa nini hili ni jambo lenye manufaa? Mgogoro fulani mkubwa ukitukia na wewe uwe huna Biblia mkononi, fikira za Kimaandiko zenye kufariji zinaweza kukuimarisha mara hiyo. Ndugu wengi waliohukumiwa kwenda jela au kwenye kambi za gereza kwa sababu ya kusimamia kwa uthabiti kanuni za uadilifu wameburudishwa sana na kuimarishwa kwa kukumbuka maandiko waliyotia katika kumbukumbu ya akili yao. Ndiyo, Neno la Mungu linaweza kusababisha “moyo ushangilie” na kufanya “macho yang’ae”!—Zaburi 19:7-10, NW.

8. Je! ni rahisi kufuata “vipito vya uadilifu,” lakini kufanya hivyo kunaongoza kwenye nini?

8 “Yeye ananiongoza katika vipito vya uadilifu.” Ni vigumu kufuata vipito vya uadilifu, lakini vinaongoza kwenye uhai. Ni kama vile Yesu alivyosema: “Mlango ni mwembamba, na njia imesonga iendayo uzimani.” (Mathayo 7:14) Mtume Paulo alitaja fikira inayohusiana na hiyo kwa kuambia wanafunzi katika Listra, Ikonio, na Antiokia hivi: “Ni lazima sisi tuingie ndani ya ufalme wa Mungu kupitia dhiki nyingi.” Na kwa uhakika Paulo alijua alilokuwa akisema. Muda mfupi tu kabla ya hapo, yeye alikuwa amepigwa kwa mawe kule Listra na kuachwa akidhaniwa amekufa!—Matendo 14:19-22, NW.

9. (a) Ni jinsi gani Mungu ‘anatuongoza katika vipito vya uadilifu’? (b) Ni katika njia gani Zaburi 19:14 inaweza kuwa yenye msaada? (c) Ni maandiko gani yanaweza kutusaidia tuepuke mitego ya ngono haramu?

9 Yehova ‘anatuongoza katika vipito vya uadilifu’ kwa kutuongoza na kutuagiza kupitia Neno na tengenezo lake. Lakini watu walio wengi wanafuata barabara ile pana iliyo na nafasi kubwa “iendayo upotevuni.” (Mathayo 7:13) Ukosefu ulioenea sana wa usafi katika ngono na lile pigo linalosambaa haraka-haraka la UKIMWI ni mambo yanayokazia uhitaji wa Wakristo kuepuka mashirika mabaya. (1 Wakorintho 15:33) Ni lazima sisi tujiangalie pia ili fikira zetu zenyewe zisitange-tange kuingia katika njia zisizo safi. (Zaburi 19:14) Kwa kusudi hilo, acheni sikuzote tutumie mashauri mazuri ambayo Neno la Mungu linatupa kuhusu ngono na jinsi ya kuepuka ile mitego mingi ya ukosefu wa adili.​—1 Wakorintho 7:2-5; Waefeso 5:5; 1 Wathesalonike 4:3-8.

10. (a) Ni daraka gani ambalo Mashahidi wa Yehova wanalo kuhusiana na jina la kimungu? (b) Kwa nini mara nyingi watu wa kilimwengu wanatuchambua? (c) Ni chini ya hali gani Yehova atatusaidia?

10 “Kwa ajili ya jina lake.” Mashahidi wa Yehova wana daraka zito la kutukuza jina la Mungu na kutoleta suto lo lote juu yalo. (Mathayo 6:9; Kutoka 6:3; Ezekieli 38:23) Watu wengi wa kilimwengu wanafanya haraka kuelekeza kidole chenye mashtaka kwa watu wa Yehova. Ikiwa hilo linafanywa kwa sababu ya msimamo wetu kwa ajili ya kanuni za Biblia kama vile kutokuwamo au utakatifu wa damu, dhamiri yetu ni safi. Lakini kama jambo hilo lingetukia kwa sababu ya kutenda kwetu makosa, tungekuwa tukivunjia Yehova heshima. (Isaya 2:4; Matendo 15:28, 29; 1 Petro 4:15, 16) Kwa hiyo sisi na tuchukie yaliyo mabaya. (Zaburi 97:10) Sisi tukilazimika kunyanyaswa, sikuzote Yehova atatusaidia na kutuhami kwa ajili ya jina lake.

Yehova Anahami Kondoo Zake

11. Ni nini linalomaanishwa na “bonde la uvuli wenye kina kirefu,” na huenda hili likatukumbusha nini kwa habari ya Yesu?

11 “Hata ingawa mimi natembea katika bonde la uvuli wenye kina kirefu, mimi siogopi ubaya wo wote.” (Zaburi 23:4, NW) Tafsiri ya Isaac Leeser inasomwa hivi: “Naam, ingawa mimi natembea kupitia bonde la uvuli wa kifo, mimi sitaogopa ovu.” Huenda hii ikaleta akilini fikira ya vile vibonde, au mabonde, vyenye vina virefu ambavyo viliteremka chini kutoka kwenye milima ya Yudea upande wa magharibi wa Bahari Nyekundu. Bonde, au genge ambako hayawani-wala-nyama wanajibanza katika vivuli ni mahali hatari kwa kondoo. Daudi alipitia mabonde mengi yenye hatari katika muda wa maisha yake, akielekeana na kifo uso kwa uso. Lakini kwa kuwa Mungu alikuwa akimwongoza, yeye alikuwa na uhakika na hakujiacha aingiwe na hofu isiyozuiliwa. Inatupasa sisi tuwe na uhakika kama huo katika Yehova. Rejezeo hili linalohusu “uvuli wa kifo” huenda pia likatukumbusha juu ya unabii wa Isaya: “Wale wanaokaa katika bara la uvuli wenye kina kirefu, nuru yenyewe imeangaza juu yao.” Mathayo alirejeza kwenye unabii huu na akautumia kwa Yesu Kristo, akisema: “Watu wanaoketi katika giza waliona nuru kubwa, na kwa habari ya wale wanaoketi katika jimbo la uvuli wenye kifo, nuru iliinuka juu yao.” Jinsi gani? Kwa ile kampeni kubwa ya kuhubiri ambayo Yesu aliendesha.​—Isaya 9:2; Mathayo 4:13-16.

12. (a) Ni jinsi gani watumishi wa Yehova wamejirekebisha wajipatanishe na hali za mnyanyaso katika nchi nyingi, na tokeo likawa nini? (b) Ni jinsi gani Petro aliwatia moyo Wakristo wa mapema wenye kunyanyaswa?

12 Daudi ‘hakuogopa ubaya wo wote.’ Ndivyo ilivyo kuhusu watumishi wa Yehova leo, hata ingawa wao hawapendwi na watu wengi katika ulimwengu huu mwovu unaotawalwa na Shetani. (1 Yohana 5:19) Watu wengi wanawachukia wao kikweli, nao wananyanyaswa vikali katika nchi fulani fulani. Lakini katika mabara haya wao wanaendeleza kuhubiri habari njema za Ufalme, ingawa si katika mahali peupe kama vile ambavyo wangefanya kwa kawaida. Wao wanajua kwamba Yehova yupo pamoja nao na atawahami. (Zaburi 27:1) Maendeleo mazuri yanafanywa katika nchi nyingi ambako ni lazima kazi ya Ufalme ifanywe kichini-chini. Katika nchi kama hizo, Mashahidi wa Yehova wanasema sawasawa na maneno ya zaburi: “Yehova yuko upande wangu; mimi sitahofu. Ni nini ambalo mwanadamu wa duniani anaweza kunitenda mimi?” (Zaburi 118:6, NW) Mashahidi hawa wamo katika msimamo kama ule wa Wakristo wa mapema ambao mtume Petro aliandikia maneno haya ya kutia moyo: “Hata ninyi mkipaswa kuteseka kwa ajili ya uadilifu, ninyi ni wenye furaha. Hata hivyo, ninyi msihofu kitu kile kilicho hofu yao, wala msitaharuki.”​—1 Petro 3:14, NW.

13. (a) Ni badiliko gani la kupendeza linalotukia kwenye Zaburi 23:4, na kwa nini? (b) Ni jinsi gani Wakristo wanaweza kushinda hofu zao?

13 “Kwa maana wewe upo pamoja na mimi.” Tafadhali angalia jambo la kupendeza sana katika kifungu hiki. Mtunga zaburi aliyevuviwa amegeuka akaacha kutaja nafsi ya mtu wa tatu kuja kwenye mtu wa pili. Badala ya kunena juu ya Yehova kuwa “yeye,” sasa Daudi anatumia kiwakilishi “wewe.” Kwa nini? Kwa sababu kinaonyesha kuwa na uhusiano wa ndani zaidi. Hatari inatuleta karibu zaidi na Baba yetu mwenye upendo, Yehova. Ndipo sisi tunapofurahia uhusiano wa ndani zaidi pamoja naye. Kwa njia ya sala na dua, sisi tunaweza kuitia jina lake ili tupate himaya, na hivyo tushinde hofu zetu.​—Linganisha Sefania 3:12.

14. (a) Ni vifaa gani ambavyo wachungaji walikuwa navyo katika wakati wa Daudi, na wao walivitumia jinsi gani? (b) Ni jinsi gani wachungaji Wakristo wanahami kundi la kondoo leo?

14 “Ufito wako na fimbo yako ndivyo vitu ambavyo vinanifariji mimi.” Neno la Kiebrania she’vet, linalofasiriwa “ufito,” linaweza kumaanisha bakora ya mchungaji. Vyote viwili, ufito na fimbo, vinaweza kutumiwa kwa kujikinga na kuwakilisha au kuonyesha mamlaka. Kwa uhakika, vifaa hivi vingekuwa vyenye mafaa sana katika kupiga na kufukuza wanyama wanyemelezi kama majibwa-mwitu na nyoka. Bakora ya mchungaji ingeweza kutumiwa pia kudukua kondoo waelekee upande unaofaa au hata kuvuta kondoo arudi nyuma ili asiende kando karibu mno na kisehemu ambapo huenda akaanguka na kuumia. Leo, Yehova anaandaa wachungaji waaminifu, wazee katika makundi, ambao wanakinga kundi la kondoo lisipatwe na wanyemelezi wa kiroho kama waasi-imani. Au huenda ikawa lazima wazee washauri wale wanaokuwa wazembe katika kuhudhuria mikutano au wanaopotoka kutoka kwenye mwenendo wa Kikristo.

Karamu Nono Katikati ya Maadui

15. (a) Ni badiliko gani lenye umaana mkubwa katika kielezi linalotukia kwenye Zaburi 23:5? (b) Ni mambo gani ya uhakika yanaonyesha kwamba watu wa Yehova wanalishwa vizuri kiroho, kwa utofautiano na watu gani?

15 “Wewe unapanga meza mbele yangu mimi katika mahali panapoelekeana na wale wanaoonyesha mimi uhasama.” (Zaburi 23:5, NW) Hapa tuna badiliko lenye kujaa maana katika kielezi, kutoka kwa mchungaji kuja kwa mkaribisha-wageni. Akiwa mkaribisha-wageni aliye mkarimu sana, Yehova anaandaa wingi wa chakula cha kiroho kupitia jamii ya “mtumwa” mpakwa-mafuta. (Mathayo 24:45) Ingawa sisi tunaishi katika ulimwengu wenye uhasama sisi tunalishwa vya kutosha. Mnara wa Mlinzi unatangazwa katika lugha zaidi ya mia moja ili watu wanaoishi katika mahali mbalimbali kama Afrika Kusini, Greenland, Solomon Islands, na India waweze kulishwa kiroho. Tena, yale makundi karibu 55,000 ulimwenguni pote yana wasemaji na walimu waliozoezwa vizuri kuhutubu mbele ya watu wote, na mahali pazuri pa mikutano, kutia na mamia ya Majumba ya Ufalme mapya. Zaidi ya mafunzo ya nyumbani ya Biblia 3,000,000 yanaongozwa ili yasaidie wenye mfano wa kondoo. Tofauti na hilo, wale walio katika Babuloni Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini bandia, wanashinda na njaa.​—Isaya 65:13.

16. (a) Tofauti na mwanamke mmoja mwenye dhambi, ni jambo gani ambalo Farisayo fulani alipungukiwa kufanyia Yesu? (b) Ni mafuta ya aina gani ambayo Yehova anaandaa kwa ajili ya watumishi wake washikamanifu leo?

16 “Wewe umepaka kichwa changu kwa mafuta.” Katika Israeli ya kale mkaribisha-wageni aliye na nia ya kutoa aliandaa mafuta ya kupaka vichwa vya wageni wake. Kwa kupendeza, katika pindi fulani Yesu alikuwa mgeni wa Farisayo mmoja ambaye hakupaka kichwa cha Yesu kwa mafuta wala hakumwandalia maji ya kuosha nyayo zake. Wakati huo, mwanamke mmoja mwenye dhambi aliosha nyayo zake wa machozi yake na kuzipaka mafuta ya pekee yenye marashi. (Luka 7:36-38, 44-46) Lakini Yehova ni mkaribishaji-wageni aliye mkarimu sana! Kwa ajili ya watumishi wake washikamanifu, yeye anaandaa “mafuta ya mchachawo.” (Isaya 61:1-3, NW) Ndiyo, kwa uhakika watu wa Yehova leo wana furaha ya kuchachawa.

17. (a) ‘Kikombe kilichojazwa vizuri’ kinamaanisha nini? (b) Ni jinsi gani Yehova anaandaa ‘kikombe kilichojazwa vizuri’ kwa ajili ya watumishi wake leo?

17 “Kikombe changu kimejazwa vizuri.” Fasiri nyingine ni hii: “Kikombe changu kinajaa furufuru na kumwagika.” (Moffatt) Hii inamaanisha wingi wa kiroho. Ingawa linalomaanishwa si kunywa kupita kiasi, maneno haya yanadokeza kikombe cha divai nzuri sana. Kinywaji hiki kimefanyizwa kikiwa na vitu vya kuponya, kama inavyoonyeshwa na shauri la Paulo kwa Timotheo: “Usinywe maji tena, bali tumia divai kidogo kwa ajili ya tumbo lako na visa vyako vya mara kwa mara vya ugonjwa.” (1 Timotheo 5:23, NW) Katika maana ya kiroho, divai inafanya mioyo yetu ishangilie pia. (Zaburi 104:15) Yehova, Baba yetu mwenye upendo anaandaa kwa ukarimu karamu ya kiroho ya vitu vyema kwa ajili ya watumishi wake washikamanifu, kutia na ‘kikombe kilichojazwa vizuri’ cha shangwe.

18. (a) Wema wa Yehova na fadhili za upendo zinafurahiwa na nani, na Zaburi 103:17, 18 inaonyesha hilo jinsi gani? (b) Ni tazamio gani tukufu lililoko mbele kwa ajili ya wale walio waaminifu kwa Yehova?

18 “Kwa uhakika wema na fadhili za upendo zenyewe zitanifuatia mimi siku zote za maisha yangu.” (Zaburi 23:6, NW) Wema ni sehemu ya tunda la roho takatifu ya Yehova. (Wagalatia 5:22, 23, NW) Wema na fadhili za upendo za Mungu zinafurahiwa na wale wanaotembea katika njia yake. (Zaburi 103:17, 18, NW) Wakiwa na imani imara katika Yehova, watu wake wanaweza kuelekeana na jaribu lo lote wanalokabili. Sikuzote wao ndio wa kupewa baraka yake na utunzaji wenye upendo. Na kuwa na uaminifu kwa kusudi hilo kutamaanisha uhai wa milele katika ulimwengu mpya. Ni tazamio zuri kama nini!

19. (a) Inamaanisha nini ‘kukaa katika nyumba ya Yehova’? (b) Tengenezo la Yehova limesimamisha nini imara ili liendeleze ibada ya kweli leo, na kwa nini maelfu ya watu waliojiweka wakfu wanaliona kuwa pendeleo kutumikia huko? (c) Ni akina nani wengine ambao wamepiga moyo konde kutumikia Mungu milele?

19 “Na mimi nitakaa katika nyumba ya Yehova mpaka kwenye urefu wa masiku.” Katika siku ya Daudi patakatifu pa Mungu palikuwa lile hema takatifu, kwa maana hekalu lilikuwa halijajengwa bado. Kwa kuwa mtunga zaburi alikuwa akifikiria mkaribisha-wageni aliye na neema, ‘kukaa katika nyumba ya Yehova’ kulimaanisha kuwa na uhusiano mwema pamoja na Mungu akiwa mgeni Wake. (Zaburi 15:1-5) Leo, nyumba hiyo inaweza kutambulishwa kuwa hekalu takatifu la Yehova, mpango wake kwa ajili ya ibada yenye kutakata. Mfalme Sulemani alipewa pendeleo la kujenga hekalu la kwanza la vitu vya kimwili, lenye kupambwa sana kwa dhadhabu na kujengwa kwa heshima ya Yehova. Lilikuwa pendeleo kama nini kutumikia huko! Ingawa hekalu hilo halipo tena, Mungu ana tengenezo takatifu la kumheshimu yeye na kuendeleza ibada yenye kutakata. Kama njia moja ya kufanyia hivyo, tengenezo la Yehova limesimamisha imara Maskani za Betheli katika nchi nyingi. “Betheli” inamaanisha “Nyumba ya Mungu,” na maelfu ya watu waliojiweka wakfu wanatumikia katika vitovu hivi vya kitheokrasi. Baadhi ya wanaume na wanawake hawa wametumikia kwa njia hii “mpaka kwenye urefu wa masiku,” wakiwa wametumia sehemu kubwa ya maisha zao katika utumishi wa Betheli. Mamilioni ya wengine, wasio washiriki wa jamaa ya Betheli, wamepiga moyo konde kwa njia iyo hiyo watumikie Yehova milele.

20. (a) Kwa nini Zaburi 23 ni sehemu iliyo ya kutokeza ya Maandiko, na inatusaidia kusitawisha nini? (b) Ni mapendeleo gani ambayo yanangojea watumishi waaminifu wa Yehova?

20 Zaburi ya 23 ni kama kito chenye nyuso nyingi zinazong’aa-ng’aa nuru. Hiyo inakweza jina tukufu la Baba yetu mwenye upendo wa kimbingu, Yehova, na kufunua jinsi yeye anavyoongoza, kuhami, na kuandalia kondoo zake. Kama matokeo, watu wake ni wenye furaha, wanalishwa vizuri kiroho, na wanaongezeka hesabu haraka-haraka, hata katika nchi ambamo mna upinzani mkali. Zaburi 23 inatusaidia pia kusitawisha kifungo kichangamfu cha uhusiano wa ndani pamoja na Muumba wetu. Na wakati sisi tunapotazama mbingu zenye nyota kama vile Daudi alivyofanya mara nyingi alipokuwa akitazama kundi la kondoo zake, sisi tunaweza kuwa na shukrani kwamba Muumba wa huu ulimwengu wote mzima anatutunza sisi kama Mchungaji mwenye upendo. Kwa upendo, yeye anatutolea uhai wa milele pia katika ulimwengu mpya ikiwa sisi tunadumisha ukamilifu wetu kwake. Litakuwa jambo adhimu kama nini kukutana na watumishi wa Mungu watakaofufuliwa walio waaminifu kama Daudi! Na ni pendeleo kama nini kutumikia Yehova, yule Mchungaji Mkuu, mpaka umilele wote!

Wewe Ungejibu Jinsi Gani?

◻ Ni jinsi gani Yehova anathibitika kuwa Mchungaji wetu mwenye upendo?

◻ Ni kwa njia gani Mungu‘anatuongoza katika vipito vya uadilifu’?

◻ Ni jinsi gani Yehova anahami kondoo zake?

◻ Ni katika jambo gani Mungu ameandaa meza kwa ajili yetu katikati ya maadui wetu?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki