Yesu Yeye Ni Nani?
KUMBUKUMBU za kilimwengu ambazo zinazungumza juu ya Yesu ni chache. Hata hivyo, nyingine zipo, na kati yazo The Encyclopoedia Britannica inasema: “Masimulizi haya yasiyotegemea mengine yanathibitisha kwamba katika nyakati za kale hata wapinzani wa Ukristo hawakutilia mashaka kamwe masimulizi ya historia kuhusu Yesu, ambayo yalibishaniwa na waandikaji kadhaa kwa mara ya kwanza na kwa misingi isiyofaa mwishoni mwa karne ya 18, wakati wa karne ya 19, na mwanzoni mwa karne ya 20.”
Sasa jiulize mwenyewe, Ikiwa masimulizi ya kuwapo kwa Yesu ni hadithi tu, je! inaelekea kwamba ingefika karne ya 18 ndipo yagunduliwe? Pia fikiria uhakika wa kwamba zaidi ya watu bilioni moja sasa wanadai kuwa wafuasi wa Yesu. Uvutano ambao mafundisho yake yamekuwa nao juu ya utamaduni, elimu, na serikali—juu ya mwendo mzima wa historia ya ulimwengu—hauwezi kukanika. Je! inaonekana kuwa jambo lenye akili kwamba yote haya yamekuwa matokeo ya jambo fulani lisilo la maana zaidi kuliko hadithi tu?
Ikiwa mwanzilishi wa Uislamu, mnabii Mwarabu Muhamadi, alikuwa mtu halisi, tuna sababu ipi ya maana kuitikadi kwamba Yesu Kristo, mwanzilishi wa Ukristo, hakuwa mtu halisi? Huenda akawa aliishi miaka 600 hivi kabla ya Muhamadi, lakini angalia kwamba mwanzilishi wa Ubuddha, Siddhartha Gautama—Mbuddha, au “Mwenye Nuru ya Elimu”—aliishi mapema zaidi, zaidi ya miaka 500 kabla ya Yesu. Hata hivyo, ikiwa Buddha alikuwa mtu halisi, tuna sababu ipi ya maana sana kuitikadi kwamba Yesu hakuwa mtu halisi?
Mwanahistoria Mjeremani na mchimbuzi wa vitu vya kale Hans Einsle anaandika kwamba mwanahistoria Myahudi Flavio Yosefu, waandikaji Waroma Suetonius na Pliny, na hasa mwanahistoria Mroma Tacitus “wote wanategemeza masimulizi ya kihistoria ya Yesu na mambo makuu ya uhakika juu ya maisha yake.”
Ni Zaidi ya Mtu wa Kawaida Tu?
Yesu alikuwapo—lakini akiwa nani? Watu fulani wanabisha kwamba alikuwa mwanadamu wa kawaida tu, ingawa wanakubali kwamba lazima awe alikuwa mtu mwenye hekima sana, mwenye kusema ukweli. Hata maadui zake wa karne ya kwanza walikiri hivyo, wakisema: “Mwalimu, twajua . . . hutazami sura za watu; lakini katika kweli waifundisha njia ya Mungu.”—Marko 12:13, 14.
Hata hivyo, wengine wanasababu kwamba lazima Yesu awe alikuwa zaidi ya mwanadamu wa kawaida tu. Kwa nini? Kwa sababu, kwanza, yeye angefanya vitu ambavyo wanadamu wa kawaida hawawezi kufanya. Mathalani, Je! wewe umewahi kukutana na mtu ambaye anaweza kutembea juu ya maji, kugeuza maji yawe divai, kulisha watu takriban 5,000 kwa samaki wawili wadogo na mikate mitano ya shayiri, kuponya vipofu, au kufufua wafu?—Mathayo 14:25, 26; Marko 8:22-25; Yohana 2:1-11; 6:1-13; 11:30-44.
Pia Yesu angeweza kuona vitu ambavyo wanadamu wa kawaida hawawezi kuona. Mwanamke mmoja alipomwambia kwamba hana mume, Yesu alijibu: “Umesema vema, Sina mume; kwa maana umekuwa na waume watano, naye uliye naye sasa siye mume wako.” Akiwa ameshangaa, mwanamke huyo akamalizia hivi: “Bwana, naona ya kuwa u nabii!” (Yohana 4:16-19) Kwa kielelezo cha kuona mambo kimbele kwenye kustaajabisha kwa Yesu juu ya vile Petro angemkana, ona Luka 22:31-34, 54-62.
Yesu alikuwa na mamlaka isiyo ya kawaida. Watu ‘walishangaa mno kwa njia yake ya kufundisha; kwa maana hapo yeye alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye mamlaka, wala si kama waandishi.’ (Marko 1:22, NW) Waaidha, Yesu aliweza kuwapa “wanafunzi wake kumi na wawili... mamlaka juu ya roho wachafu, ili wao wawafukuze hao na kuponya kila aina ya magonjwa na kila aina ya udhaifu.”—Mathayo 10:1, NW.
Je! Tunaweza Kuitikadi Ripoti Hizo?
‘Lakini ngoja kidogo,’ huenda ukasema. ‘Je! si inaweza kuwa kwamba habari zinazohusu yale aliyofanya Yesu zilitiwa chumvi kidogo?’ Si kulingana na F. F. Bruce, Profesa aliyestaafu wa Uchambuzi wa Biblia na Mafafanusi katika Chuo Kikuu cha Manchester, ambaye anaandika: “Kwa kawaida haiwezekani kuonyesha kupitia hoja za kihistoria ukweli wa kila jambo katika andishi la kikale, iwe ni ndani au nje ya Biblia. Inatosha kuwa na utumainifu wenye maana katika kuitibarika kwa kawaida kwa mwandikaji; ikiwa huo umefanyizwa, kuna uwezekano zaidi wa kwamba maelezo yake ni ya kweli. . . . Agano Jipya haielekei kutokuwa yenye kutegemeka kihistoria kwa sababu Wakristo wanaipokea ikiwa kichapo ‘kitakatifu.’ “
Kila kitu kinaunga mkono kuitibarika kwa waandikaji wa Gospeli. Ingawa nyakati nyingine wanatofautiana katika njia yao ya kutoa maelezo, hawapingani mmoja na mwenzake, kama vile mashahidi wawili wenye kujionea aksidenti ya barabarani hawapingani mmoja na mwenzake wakati mmoja anaposema kwamba motokaa nyekundu iliyotoka upande wa kushoto iligonga motokaa ya kijani kibichi iliyokuwa ikitoka upande wa kulia, hali mwingine anasema kwamba Mercedes iliyokuwa ikiendeshwa kuelekea kusini iligonga Renault iliyoikuwa ikielekea kaskazini. Uhakika wa kwamba Gospeli zinatofautiana katika maelezo machache linaonyesha kwa nguvu kwamba hizo ni za kweli. Ikiwa waandikaji wazo wangalitaka kuwadaganya watu waitikadi hadithi tu, bila shaka wangalilinganisha masimulizi yao kwa ukaribu sana.
Hata maadui wa Yesu waliunga mkono ripoti zilizomhusu kuwa za kweli. Tunasoma hivi: “Walimletea mtu bubu mwenye pepo. Na pepo alipotolewa, yule bubu alinena... Lakini Mafarisayo wakasema, Kwa nguvu za mkuu wa pepo atoa pepo.” (Mathayo 9:32-34) Angalia kwamba Mafarisayo hawakukana kwamba Yesu alikuwa amefanya muujiza. Walikataa tu kuuona uwezo wake wa kufanya hivyo kuwa unatokana na roho takatifu ya Mungu.
Ithibati nyingine inayoonyesha kwamba maandishi ya kumbukumbu yanayohusu Yesu yalikuwa ya kweli ni uhakika wa kwamba ikiwa kanuni zilizounganishwa katika mafundisho yake zinafuatwa, zinatenda kazi kweli kweli. Zinatokeza maisha yenye mafanikio na yenye kufurahisha. Kwa kuongezea, manabii mengi ya muda mrefu yaliyotamkwa na Yesu, kama yale yaliyoandikwa katika Mathayo sura 24, Marko sura 13, na Luka sura 21, yametimizwa katika siku yetu.
Yesu—Ni Yehova wa “Agano la Kale”?
Kwa wazi, Yesu hakuwa mtu wa kawaida. Yeye alikuwa asiye na kifani kwa sababu, kama Biblia inavyotuambia, yeye alifurahia maisha mbinguni kabla hajaja duniani. (Yohana 6:38, 62) Hivyo alikuwa na maarifa na uwezo unaopita ule wa wanadamu wa kawaida. Jambo hilo linasaidia kueleza miujiza yake na hekima yake yenye kutokeza.
Lakini je! kuwapo kwa Yesu kabla ya kuwa mwanadamu kunamaanisha kwamba yeye alikuwa Mungu? Kitabu kimoja kidogo cha mafundisho cha mwalimu wa kidini kinadai hivyo, kikisema: “Wakati wo wote Yesu alipojirejezea Mwenyewe ‘Mimi Nipo’ . . . , Yeye alijitambulisha kuwa Yehova wa Agano la Kale.” Je! hilo ni kweli?
Kulingana na King James Version ikitumia Kutoka 3:13, 14, Musa aliuliza: “Nitakapokuja kwa watoto wa Israeli, nami nitawaambia wao, Mungu wa baba zenu amenipeleka mimi kwenu; na wao wataniambia mimi, Jina lake ni nani? mimi nitawaambia nini? Na Mungu akamwambia Musa, MIMI NIPO KILE AMBACHO MIMI NIPO: na yeye akasema, Hivyo ndivyo wewe utakavyowaambia watoto wa Israeli, MIMI NIPO amenipeleka mimi kwenu.” Kuhusu andiko hili, The Pentateuch and Haftorahs (Andiko la Kiebrania likiwa na tafsiri ya Kiingereza na fasiri, lililohaririwa na Dakt. J. H. Hertz) inasema kwamba katika usemi “Mimi nipo kile ambacho mimi nipo . . . mkazo unatiwa kwenye udhihirisho wenye kutenda wa kuwapo kwa Kimungu.” Basi, matumizi yayo kama cheo au jina la Mungu yalifaa kwa sababu kwa kuwatoa katika utumwa wa Misri, Mungu alikuwa karibu kudhihirisha kuwapo kwake kwa ajili ya watu wake katika njia yenye kutokeza. Hertz anasema kwamba “walio wengi wa ki-siku-hizi wanafuata Rashni [mwelezaji Mfaransa wa Biblia na Talmud mwenye sifa wa miaka ya katikati] kwa kutumia ‘Mimi nitakuwa kile ambacho mimi nitakuwa.”’ Hii inakubaliana na matumizi ya New World Translation, ambayo inasomeka hivi: “MIMI NITATHIBITIKA KUWA KILE AMBACHO NITATHIBITIKA KUWA.”
Kwenye Yohana 8:58, kwa mara nyingine katika King James Version Yesu anatumia usemi “Mimi nipo” kwa habari yake mwenyewe, akisema, “Kabla Abrahamu hajakuwapo, mimi nipo.” Lakini hapa usemi unatofautiana sana na ule unaotumiwa kwenye Kutoka 3:14. Yesu hakuutumia kama jina au cheo bali kama tu njia ya kueleza kuwapo kwake kabla ya kuwa mwanadamu. Hivyo, kulingana na New World Translation, matumizi yaliyo sawa ya Yohana 8:58 ni: “Kabla Abrahamu hajaja kuwapo, mimi nimekuwapo.”
Kwa wazi, hakuna msingi wa Kimaandiko uliopo wa dai la kwamba Yesu ni sawa na Yehova wa Maandiko ya Kiebrania. Hata kitabu kidogo cha kidini cha mwalimu kilichonukuliwa hapo mwanzo kinakubali hivi: “Kwamba Kristo alikuwapo kabla ya uzawa Wake katika Bethlehemu hakuthibitishi kwamba Yeye ni Mungu (Angalikuwapo kama malaika). Kwa kweli, hili ndilo Biblia inafundisha. Katika kuwapo kwake kabla ya kuwa mwanadamu, Yesu alikuwa “kamungu,” au wa kimungu, bali si yule Mungu, Mungu Mweza Yote Yehova.—Yohana 1:1-3; 2 Wathesalonike 4:16.
Hivyo ikiwa yeye si Mungu, Yesu ni nani hasa?
[Picha katika ukurasa wa 5]
Miujiza ya Yesu ilithibitisha kwamba yeye alikuwa zaidi ya mwanadamu wa kawaida tu