Maswali Kutoka kwa Wasomaji
◼ Yesu alisema, “Kama ninyi mngalikuwa vipofu, ninyi msingalikuwa na dhambi.” (Yohana 9:41, NW) Je! yeye alimaanisha kwamba wanadamu fulani hawana dhambi?
Sivyo, wanadamu wote leo ni watenda dhambi, kama vile wote walivyokuwa katika karne ya kwanza, isipokuwa Yesu mwenyewe. Katika maneno haya kutokana na Yohana 9:41, Yesu alikuwa anarejeza kwenye namna fulani hususa ya dhambi.
Adamu babu yetu wa kale kwa ujumla alilemeza wazao wake wote kwa dhambi. Adamu alikuwa ameumbwa akiwa mkamilifu, asiye na dhambi. (Kumbukumbu 32:4; 2 Samweli 22:31) Wakati yeye alipokosa kutii maagizo ya msingi ya Yehova, Adamu akawa asiyekamilika. Kufanya dhambi kwa msingi kunamaanisha “kuikosa alama.” Kwa kweli Adamu alifanya hivyo. Kwa hiyo kwa kuvunja amri ya Mungu, Adamu akawa mtenda dhambi.
Sisi sote tumeathiriwa kwa sababu sisi sote tulitokana na Adamu. Ungeweza kutolea jambo hili kielezi hivi: Mtu aliyezaliwa akiwa na kasoro fulani kubwa iliyotokana na chembe za urithi angeipitisha kwa wazaliwa wake wote; wao wangerithi kasoro hiyo hiyo. Wanasayansi wa ki-siku-hizi wanaweza kupambanua kama kasoro fulani zinazotokana na chembeuzi zimo katika kiini-tete au kitoto kilichozaliwa hivi karibuni, lakini Yehova anazidi hapo. Yeye anafunua kwamba kasoro mbaya zaidi ilikuja kuwa katika Adamu na kwamba hiyo imepitishwa kwa sisi sote. Kasoro hii ni dhambi. “Kupitia binadamu mmoja [Adamu] dhambi iliingia ndani ya ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kilienea kwa wanadamu wote kwa sababu wao wote walikuwa wametenda dhambi.” (Warumi 5:12, NW) Hali hii ya kuwa na dhambi iliondoa wanadamu katika upatani pamoja na Muumba, kwa kuongezea kuwaletea ugonjwa na kifo. Hakuna binadamu mbali na Yesu ambaye amekuwa mkamilifu na bila shutumu la kifo.—Warumi 5 18-21, 6:23; 2 Nyakati 6:36.
Hata hivyo, nyakati fulani katika Biblia watu mmoja mmoja wanaitwa “watenda dhambi” kwa sababu ya kuonwa kuwa wazoeaji wa kutokeza wa dhambi au wa namna ya dhambi yenye kufanywa kwa uovu wa wazi-wazi. (Luka 19:2-7; Marko 2:16, 17; 14:41, NW) Hiyo, bila shaka, haimaanishi kwamba watu wale wengine wote walikuwa wakamilifu, wasio na dhambi. Kama wangalikuwa, wao wasingalikuwa wazee na mwishowe wafe.
Usimulizi ulio katika Yohana sura ya 9 ulihusisha ndani mwanamume ambaye alizaliwa akiwa kipofu lakini ambaye mwono wake uliponywa na Yesu Mwanamume huyo hakuwa ameweza kibinafsi kusoma Maandiko, hata hivyo alikuwa na maarifa kidogo. Yeye alijua kwamba Mungu hasikii matakwa yenye kuombwa na watenda dhambi wa makusudi. Uhakika wa kwamba Yehova alimpa Yesu nguvu za kufanya ule mwujiza wa kuandaa mwono ulithibitisha kwamba Yesu alikuwa nabii. Ingawa hivyo, Mafarisayo wenye kiburi walikataa kukubali ushuhuda wa kimantiki wa binadamu huyu, nao wakamtupa nje.—Yohana 9:13-17, 26-34.
Baada ya jambo hili, Yesu alisema: “Kwa hukumu hii mimi nilikuja ndani ya ulimwengu huu: kwamba wale ambao hawawi wanaona wapate kuona na wale ambao wanaona wapate kuwa vipofu.” (Yohana 9.39, NW) Ndiyo, juu ya msingi wa kuhubiri kwake, utendaji mwingine, na fungu lake katika makusudi ya Mungu, watu mmoja mmoja ama wangepata mwono wa kiroho na kutembea katika nuru au wangekuwa katika giza la kiroho. (Isaya 9:1, 2; 42:6, 7; Mathayo 4:13-17; 6:23, 2 Petro 1:9, 2 Wakorintho 4:4) Kama wale viongozi wa kidini wangalikuwa ni Wayahudi tu wasio na habari, wenye lemezo la kikawaida la dhambi ya kibinadamu, kutokubali kwao Mesiya kungaliweza kutolewa udhuru. Lakini wao, ambao walidai “kuona,” au kuelewa, walikuwa wenye kulaumika hasa kwa sababu walikuwa na maarifa makubwa zaidi juu ya ile Sheria na juu ya Neno la kiunabii la Mungu. Kwa hiyo kukataa kwao Yesu kulikuwa dhambi nzito iliyowashutumu wao zaidi ya vile kutokamilika kwao kwa kikawaida na dhambi yao ya kibinadamu kulivyowashutumu. Hivyo, Yesu aliwaambia Mafarisayo hivi: “Kama ninyi mngalikuwa vipofu, ninyi msingalikuwa na dhambi. Lakini sasa ninyi mnasema, ‘Sisi tunaona.’ Dhambi yenu inabaki.”—Yohana 9 :41, NW.