Wapendwa Wetu Walio Wafu Wako Wapi Sasa?
“YUKO wapi jamaa huyo mdogo sasa?” Yule mama mwenye taabu nyingi akilini (aliyetajwa katika makala iliyotangulia) alifuliza kutaka kujua alikuwa ameenda wapi mtoto wake mfu. Je! alikuwa mbinguni au alikuwa katika mahali fulani pengine?
Mama ya Andrew alipewa jibu baada ya muda mfupi. Aliposikia juu ya tanzia hiyo, mtoto wake mwenye umri mkubwa zaidi, ambaye pia alikuwa Mkatoliki wa Kiroma, alijibu hivi: “Andrew yumo katika Limbo.” Lakini je! yeye alikuwa humo?
Limbo Ni Mahali Gani Au Ni Kitu Gani?
The Concise Oxford Dictionary inasema kwamba Limbo ni “jimbo lililo kwenye mpakano wa moto wa mateso, ambapo panadhaniwa kuwa ndiyo makao ya watu waadilifu wa nyakati zilizotangulia Ukristo na pa vitoto vichanga visivyobatizwa; . . . hali ya kuachiliwa mbali au kusahauliwa kabisa.” Kwa habari ya Limbo, New Catholic Encyclopedia inasema: “Leo neno hilo linatumiwa na wanatheolojia kumaanisha hali na mahali ama pa zile nafsi ambazo hazikustahili kuwa katika moto wa mateso na adhabu zao za milele lakini hazikuweza kuingia mbinguni kabla ya ile Fidia (Limbo ya akina baba) ama pa zile nafsi ambazo zinaepushwa milele zisiwe kwenye njozi ile ya raha nyingi ya ajabu kwa sababu ya ile dhambi ya awali tu (Limbo ya watoto).”
Hata hivyo, ensaiklopedia hiyo hiyo inasema hivi pia: “Ule msiba wa vitoto vichanga kufa kabla ya Ubatizo ni tatizo tata kweli kweli. . . . Suala la Limbo lingali miongoni mwa masuala ya theolojia ambayo hayajatatuliwa kikamili. Hakuna taarifa rasmi iliyotolewa na Kanisa juu ya kuwako kwa Limbo.” Katika kuhakikisha jambo hilo, The New Encyclopcedia Britannica inataarifu hivi: “Kwa sababu Kanisa Katoliki la Kiroma halijapata kamwe kuthibitisha kikamili fundisho la kwamba limbo ni hali au mahali fulani, ile dhana ya limbo inabaki ikiwa suala lisilotatuliwa kikamili.”
Ijapokuwa hivyo, Wakatoliki wengi wenye kujitoa sana wanakubali dhana hiyo ya Limbo. Lakini tafadhali fikiria wazo hili kwa uangalifu: Kwa nini watoto wachanga washutumiwe kwa umilele wote kuwa katika mahali pa kifumbo pasipofahamika, kwa sababu tu wao hawakubatizwa?
Je! Biblia inataja Limbo? Hapana, Neno la Mungu haliitaji kamwe. Hivyo jambo hilo linatokeza swali hili muhimu: Watu, kutia na watoto wachanga, huenda wapi wanapokufa?
Watu Huenda Wapi Wanapokufa?
Rai ya wengi miongoni mwa waenda-kanisani wa Jumuiya ya Wakristo ni kwamba watu wanapokufa huenda ama mbinguni ama kwenye moto wa mateso. Lakini Biblia inasema nini juu ya jambo hilo? Hiyo inataarifu hivi: “Kwa sababu walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5) Kwa hiyo wafu hawajui kitu. Wao hawaishi mahali fulani bali wao ni wafu kwa uhalisi na kwa ukamili. Hawana ufahamu wa kitu chochote.
Uhakika huo unahakikishwa na taarifa hizi katika kitabu cha Biblia cha Zaburi: “Sio wafu wamsifuo BWANA [Yehova, NW], wala wo wote washukao kwenye kimya.” (Zaburi 115:17) “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake. Pumzi [roho, NW] yake hutoka, huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.”—Zaburi 146:3, 4.
Lakini namna gani juu ya nafsi? Si hiyo ni kitu kisichoweza kufa? Hapana. Tofauti na vile watu walio wengi wanavyoitikadi, nafsi si kitu kisichoweza kufa. Uhakika huo unataarifiwa wazi katika Biblia, ambayo inasema hivi: “Nafsi inayofanya zambi, itakufa.” (Ezekieli 18:4, 20, ZSB) Uhakikisho zaidi wa jambo hilo unapatwa kwenye Matendo 3:23, NW, ambayo inasema: “Kweli kweli, nafsi yoyote ambayo haisikilizi Mnabii huyo [Yesu] itaharibiwa kikamili.”
Je! Kifo Ndio Mwisho wa Kila Kitu?
Kifo sio mwisho wa kila kitu kwa lazima. Ufufuo wa wafu unafundishwa wazi katika Maandiko. Yesu alisema: “Msistaajabie maneno hayo; kwa maana saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini [makaburi ya ukumbusho, AW] wataisikia sauti yake. Nao watatoka; wale waliofanya mema kwa ufufuo wa uzima, na wale waliotenda mabaya kwa ufufuo wa hukumu.” (Yohana 5:28, 29) Zaidi ya hilo, Yesu kwa kweli alifufua watu fulani wakati wa huduma yake duniani. Kisa chenye kustaajabisha zaidi ya vyote kilikuwa kile cha Lazaro rafiki ya Yesu. Yeye alikuwa amekuwa mfu kwa siku nne. Lakini Yesu alipopaaza sauti hivi: “Lazaro, njoo huku nje”! mwanamume yule mfu aliitikiza, akatoka ndani ya kaburi. Ulikuwa msisimuko ulioje kwa kutano la watu wenye kutazama! Tena lilikuwa tukio lenye shangwe kama nini kwa Mariamu na Martha, dada za Lazaro!—Yohana 11:38-45.
Lazaro alikuwa amekuwa wapi wakati wa siku nne hizo? Mbinguni? Katika moto wa mateso? Katika Limbo? Hapana. Biblia haisemi wala haionyeshi hivyo. Kama Lazaro angalikuwa amekuwa na fahamu akiwa mahali pengine, kwa uhakika yeye angaliambia wengine jambo hilo. Lakini kama vile Biblia inavyosema: “Wafu hawajui kitu.”—Mhubiri 9:5, Zaire Swahili Bible.
Kituko kingine cha kuchangamsha moyo kilitukia kwenye jiji la Naini. Yesu alipokuwa akikaribia lango la jiji, yeye alikutana na andamano la maziko. Mfu alikuwa ndiye “mwana pekee wa mamaye,” ambaye alikuwa mjane. Kama ambavyo ingetarajiwa, yeye alikuwa akilia machozi kwa uchungu. Jambo hilo liligusa moyo wa Yesu wenye fadhili na upendo. Yeye akakaribia, akasimamisha andamano lile, na kusema: “Kijana, nakuambia, Inuka”! Na yule mwanamume mfu akafanya hivyo! Je! unaweza kuwazia mzumbao mwingi wa mama yule na ustaajabu wa wasimama-kando?—Luka 7:11-17.
Je! mwanamume huyu kijana alikuwa na lolote la kusema kwamba alikuwa mbinguni au Limbo? Hapana. Angewezaje? “Wafu hawajui kitu.” Biblia inafananisha kifo na usingizi mzito pia. Daudi alisema: “Ee BWANA [Yehova, NW], Mungu wangu, uangalie, uniitikie; uyatie nuru macho yangu, nisije nikalala usingizi wa mauti.” (Zaburi 13:3) Waaidha, kabla tu ya yeye kufufua Lazaro, Yesu alifananisha kifo na usingizi.—Yohana 11:11-14.
Kufikia hapo, swali jingine linatokea.
Je! Kuna Watu Wowote Wema Ambao Huenda Mbinguni?
Ndiyo, watu fulani walio wema huenda mbinguni. Uhakika ulio wa kupendeza sana juu ya watu wema, au Wakristo wa kweli, ambao haujulikani na waenda-kanisani walio wengi ni kwamba kuna vikundi viwili. Wachache wenye hesabu ndogo huenda mbinguni wakatawale pamoja na Yesu Kristo, hali walio wengi watafurahia uhai wa milele duniani. Labda jambo hilo linakushangaza wewe. Kwa hiyo, acheni tufikirie mambo ambayo Biblia inasema juu ya habari hiyo ya kupendeza.
Ni nini lililokuwa kusudi la awali la Mungu kwa ajili ya aina ya binadamu? Wakati yeye alipoumba Adamu na Hawa, je! alikusudia kwamba wao wafurahie uhai kwa kitambo katika bustani ya Edeni halafu wafe na kwenda mbinguni? Hapana. Mungu aliwapa mgawo wa pekee kuhusu dunia, akisema: “Zaeni mkaongezeke, mkaijaze nchi [dunia, NW], na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi [dunia, NW].” (Mwanzo 1:28) Na Yehova habadili kusudi lake lililowekwa imara. Yeye anatangaza hivi, kwenye Zaburi 89:34, NW: “Mimi sitabadili usemi unaotoka kwenye midomo yangu.” Kwa hiyo ni lazima ile Paradiso ya Kiedeni irudishwe na kufurahiwa na watumishi waaminifu wa Yehova—kile kikundi cha walio wengi kilichotajwa juu.
Kikundi cha walio wachache kinapewa pendeleo la pekee sana, lile la kutawala pamoja na Kristo mbinguni. Ndiyo kusema, wao watashiriki pamoja na Yesu katika kuwasimamia wale wenye kuishi duniani. Hiyo ndiyo serikali ya Ufalme ambayo Wakristo wanasali kuiomba katika sala ya Bwana. Kwa kupendeza, katika sala hiyo hiyo, sisi husema: “Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.”—Mathayo 6:9, 10.
Je! Biblia inafunua ni wangapi wataenda kufurahia pendeleo hilo kubwa la kutawala pamoja na Kristo mbinguni? Ndiyo, inafanya hivyo. Unasema hivi Ufunuo sura ya 14, mstari wa 1: “Nikaona, na tazama, huyo Mwana-Kondoo amesimama juu ya mlima Sayuni, na watu mia na arobaini na nne elfu pamoja naye, wenye jina lake na jina la Baba yake limeandikwa katika vipaji vya nyuso zao.” Zingatia kwamba Ufunuo hutumia vifananishi, au “ishara,” kama inavyosemwa katika mstari ule wa ufunguzi, Ufunuo 1:1, NW. “Mwana-Kondoo” ni Yesu Kristo. (Linganisha Yohana 1:29.) Na Mlima Sayuni haurejezi kwenye ule mji mkuu wa kisiasa wa Israeli bali kwenye “Yerusalemu wa mbinguni.”—Waebrania 12:22.
Ufunuo sura ya 7 unatupa sisi habari juu ya vikundi vyote viwili, cha kimbingu na cha kidunia, ambavyo tumevitaja. Mistari 4-8 inataja wale 144,000 “waliotiwa muhuri katika kila kabila ya Waisraeli.” Hicho ni kisa kingine cha ufananishi na kinamaanisha Israeli wa kiroho, au “Israeli wa Mungu.” (Wagalatia 6:16) Warumi 2:29 inasema hivi: “Yeye ni Myahudi aliye Myahudi kwa ndani; na tohara ni ya moyo.” Ndipo Ufunuo 7:9 unaposimulia juu ya kile kikundi cha kidunia, ukisema: “Tazama, mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha.”
Watu Wema Wataishi Duniani
Mabilioni ya watu wema wataishi katika dunia-paradiso. (Luka 23:43, ZSB) Je! wewe ungependa kuwa miongoni mwao? Bila shaka ungependa. Litakuwa pendeleo lililoje kuishi katika dunia itakayokuwa imesafishilizwa ambayo itabaki bila uchafuzi, njaa, uhalifu, ugonjwa, mateso, na lile tazamio la kuogofisha sana kuhusu pigano la kinyukilia! Je! Biblia kweli inatabiri hivyo? Ndiyo, kweli kweli. Inasema hivi: “Watenda mabaya wataharibiwa, bali wamngojao BWANA [Yehova, AW] ndio watakaoirithi nchi [dunia, AW]... Wenye upole watairithi nchi [dunia, NW], watajifurahisha kwa wingi wa amani. Wenye haki watairithi nchi [dunia, NW], nao watakaa humo milele.”—Zaburi 37:9, 11, 29; linganisha Mathayo 5:5.
Basi, namna gani juu ya watoto wachanga ambao wamekufa? Je! wao pia watakuwa katika dunia Paradiso? Wao hawaendi Limbo, ambayo haipo. Lakini wachanga walio katika kumbukumbu ya Mungu watarudi katika ufufuo wa wafu—moja ya ahadi zilizo nzuri ajabu katika Neno la Mungu, kama vile tumeona tayari. (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Labda wewe umepoteza wapendwa katika kifo na mara nyingi unataka kujua wao wako wapi sasa. Kutokana na Maandiko ni wazi kwamba wao wamelala wakingojea ule ufufuo. Je! wewe ungependa kupata habari zaidi juu ya tumaini hilo lililo zuri ajabu la uhai katika dunia paradiso? Ikiwa ndivyo, kwa nini usizungumze mambo hayo pamoja na Mashahidi wa Yehova wakati watakapozuru kwenye maskani yako safari ile nyingine?
[Blabu katika ukurasa wa 6]
Watu fulani walio wema huenda mbinguni. Wao ni akina nani?
[Picha katika ukurasa wa 5]
Lazaro alikuwa wapi alipokuwa mfu?
[Picha Credit Line katika ukurasa wa 7]
Photo taken at Brooklyn Botanic Garden