Tai Ndege-Wanofua-Mizoga
Ile Ishara
“PO POTE ulipo mzoga, ndipo watakapokusanyika tai [pamoja, NW].’ (Mathayo 24:28) Badala ya kujifunza somo kutokana na kielezi hicho, watu fulani wanatafuta-tafuta makosa ndani yacho. Wao wanasema kwamba tai ni wawindaji ambao hujiendea wakiwa peke yao na kujilisha mawindo yaliyo hai, si mizoga. Hivyo, Biblia fulani zinatumia neno “ndege-wanofua-mizoga.” Lakini neno la Kigiriki linalohusika, a·e·tosʹ, limetafsiriwa “tai” kama ifaavyo.
Jamii moja inayopatikana katika Israeli ni yule tai mwenye rangi ya kihudhurungi. “Kama ndege wengi wa mawindo,” wanaonelea John Sinclair na John Mendelsohn, “tai wa hudhurungi si asiyependa kula mizoga na mara nyingi sana anakuwa miongoni mwa walio wa kwanza kuwasili kwenye windo lililouawa hivi sasa tu.” Mwoneleaji mwingine anaripoti kikusanyiko cha tai 60 wa mikia mifupi na tai wa hudhurungi katika jangwa Kalahari la Afrika. Yeye aliongezea hivi: “Yule Tai Hudhurungi ndiye hutawala wengine wanapokutana penye mzoga. Katika visa kadhaa ndege wawili, wenye kudhaniwa kuwa mume na mkeye, wameonekana wakishirikiana kula windo lililouawa.”
Tai wa baharini wanapatikana sana pia katika mabara ya Mediterania. Katika karne zilizopita, tai wa baharini na tai wa bara walijilisha mizoga ya farasi waliochinjwa katika pigano. “Inajulikana vizuri . . . kwamba wao hufuata majeshi kwa kusudi hilo,” inataarifu Cyclopædia ya McClintock na Strong.
Kwa kuwa wana mwendo mwepesi sana na huona mbali, nyakati fulani tai huwa ndio ndege wa kwanza kuwasili kwenye mzoga uliouawa sasa hivi. Yesu aliifahamu sana ile fasili ambamo Yehova Mungu aliuliza Ayubu swali hili la kunyenyekeza: “Je! tai hupaa juu kwa amri yako, na kufanya kioto chake mahali pa juu . . . ya genge la jabali, na [mahali pasipoingilika, NW] ngomeni. Toka huko yeye huchungulia mawindo; macho yake huyaangalia toka mbali . . . Na kwenye maiti ndiko aliko.”—Ayubu 39:27-30.
Hivyo, Yesu alitoa vizuri kielezi cha kwamba ni wale tu wenye jicho la kitamathali lililo kama la tai ambao wangenufaika kutokana na ile ishara.