Kujua Yaliyo Katika Habari
Wanastahiki Kuigwa
Barua moja ya hivi majuzi iliyotangazwa katika New Haven Register, iliyo karatasi-habari moja ya Connecticut, ilitoa rai fulani zisizo na upendeleo kuhusu mikusanyiko iliyofanywa na Mashahidi wa Yehova. Ikiwa imeelekezwa kwa mhariri, barua hiyo ilitaarifu hivi: “Mashahidi wa Yehova wametoka sasa tu kufanya makongamano yao ya kila mwaka kwenye Kolisiamu. Kati ya vikundi vyote vyenye kuja, hakuna kinachokaribishwa au kutafutwa sana kuliko wao. Kabla ya wao kukutana, hakuna wakati wowote ambapo Kolisiamu huwa safi kwa kadiri ambavyo inakuwa wakati wanapokutana, wala haitakati sana baadaye kama vile ilivyotakata walipokuwapo ziara ile iliyopita.”
Akirejeza kwenye mkusanyiko mmoja uliofanywa na Mashahidi miaka kadhaa iliyopita, mwandikaji wa barua hiyo aliongeza kwamba “Mashahidi 75,000 walikusanyika katika Yankee Stadium, wengine 20,000 wakiwa nje wakisikiliza vipaaza-sauti katika sherehe ya ibada iliyogutusha New York. Polisi mia mbili walipelekwa huko siku ya kwanza, hiyo ikiwa ndiyo hesabu ya kawaida ambayo hugawiwa kwenda kwenye umati mkubwa kadiri hiyo. Ni wawili tu waliopelekwa siku zilizofuata ili kutoa mielekezo. Jiji la New York lilipeleka watunza-usafi, wagawa-chakula, polisi na wenye mamlaka ya kuzima moto ili wakachunguze shughuli hiyo yenye kuendeshwa vizuri ajabu na kujifunza kutokana nayo. Hakuna hata kitonge kimoja cha chakula au takataka kilichoonekana walipoondoka, ijapokuwa walilisha washiriki wao. Hata kama wewe ni mwitikadi wa namna fulani nyingineyo ya mawazo ya fumbo la kitheolojia au hata kama wewe huyakataa yote, . . . lazima uvutiwe na kujitoa kwao, ufaaji wao, kielelezo chao cha kutokeza wazi cha mwenendo wa kibinadamu na maisha ya kiafya. Ingefaa sisi sote tufuate na kuzoea sifa nzuri sana ambazo watu hawa wanyenyekevu na wenye bidii ya kujitoa huonyesha.”
Ingawa wengi wana rai ya kwamba mwenendo wa Mashahidi wa Yehova ni bora isivyo kawaida, Mashahidi wenyewe wanajua kwamba ni lazima Wakristo wa kweli ‘waishi kulingana na roho’ na ni lazima ‘waendelee kutembea kwa utaratibu pia kulingana na roho.’ Roho ya Mungu ndiyo hutokeza ndani yao tunda la “upendo, shangwe, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti.” Sifa hizo zinastahiki kuigwa kweli kweli.—Wagalatia 5:22, 23, 25, NW.
Taji la Kukwaza
Mamia ya raia za Malaga, Hispania, wameunga mkono mchango wa watu wote ili kupata pesa za taji la dhahabu lenye madoido mengi lililo la yule bikira maarufu wa huko, “Bibi Yetu wa Tumaini.” “Gramu moja ya dhahabu kwa ajili ya [bikira]” ndiyo shime iliyotungwa miaka miwili iliyopita ili kutangaza mwito wa kuleta michango.” Tangu wakati huo, vipuli, medali, pete za arusi, na hata meno ya dhahabu vimechangwa. Vitu hivyo vimeyeyushwa vikawa kilogramu 1.5 za dhahabu safi, na hicho ni kiasi cha kutosha kufanyiza taji imara la dhahabu kwa ajili ya mfano huo.
Katika sherehe yenye kuadhimishwa kwa mawazo mazito, iliyosimamiwa na nansio mwakilisha-papa na maaskofu kadhaa walio mashuhuri katika Hispania, “Bibi Yetu wa Tumaini” alivikwa taji katika Juni 1988. Hata hivyo, si Wakatoliki wachache waliokuwa na mashaka-mashaka juu ya uvishaji huo wa taji. Karatasi-habari El País ya Hispania inaripoti kwamba katika barua moja ya maoni-wazi, wanaseminari wapatao 20 walikuwa wakiuliza: “Je! sisi bado si jiwe la kukwaza waitikadi na wasio waitikadi kwa desturi zetu zisizofaa kitu?” Vikundi vingine vya Kikatoliki vilirejeza kwenye barua ya papa ya hivi majuzi iliyopendekeza kwamba waaminifu “watoe hazina zao kuwapa maskini.” Kulingana na hilo, Wakatoliki hao walionyesha “ukinzani wa kidhamiri usioondoleka kuhusu hiyo sherehe ya anasa iliyotangazwa” na hilo “taji la gharama kubwa.”
Haishangazi kwamba watu wenye moyo mweupe wanakinza kuremba-remba mfano usio na uhai. Mungu mwenyewe anahisi hivyo hivyo Karne kadhaa zilizopita, yeye aliadhibu vikali Waisraeli kwa ajili ya zoea hilo hilo. Yehova alisema hivi kupitia Ezekieli mnabii wake: “Wao walikuwa wakijionea fahari kuhusu uzuri wa johari zao, ambazo kutokana nazo walifanyiza mifano na sanamu zao za kukirihisha.” (Ezekieli 7:20, The Jerusalem Bible) Kwa sababu hiyo, wapenda-ukweli wanatii kwa hekima shauri la Biblia lililo la wakati unaofaa ‘kukimbia ibada ya sanamu.’—1 Wakorintho 10:14.