Wale Mamajusi Watatu ni Uhakika au ni Hadithi Tu?
“C + M + B”
Je! herufi hizo zinamaanisha lolote kwako? Ikiwa unaishi ndani ya eneo la Katoliki ya Kiroma la Jamhuri ya Muungano ya Ujeremani, huenda zikamaanisha jambo fulani. Ukiwa huko utaona mara nyingi herufi hizo zikiwa zimeandikwa kwa chokaa katika mihimili ya milango. Kwa nini?
Hadithi maarufu ya kimapokeo husema kwamba hizo ni herufi za maneno ya kwanza katika Kijeremani ya wale waitwao Mamajusi watatu, au “wanaume wenye hekima,” Gaspar (Kijeremani, Caspar), Melchior, na Balthasar.a Inasemekana kwamba mifupa ya Mamajusi hao ilihamishwa ikapelekwa Cologne katika mwaka 1164 na baadaye ikawekwa akiba katika kathedro ya jiji hilo, hiyo ikifanya jiji la Cologne liwe kitovu cha maombi yao. Kila mwaka, siku Januari 6—ambayo inajulikana kuwa Karamu ya wale Watakatifu Watatu—vikundi vya vijana waliovalia kama wafalme wa kale huenda mlango kwa mlango wakiandika herufi hizo kwa chokaa katika mihimili ya milango. Kulingana na desturi, hiyo inatolea wenye nyumba himaya ya kutopatwa na mambo mabaya.
Sanaa na mapokeo ya kidini hudokeza maana ya kwamba wale Mamajusi watatu, au “wafalme,” waliongozwa na “nyota” mpaka mahali alipozaliwa Yesu. Kwa sababu ya heshima, hata maombi, wanayopewa “wafalme” hao, swali linatokea juu ya kama msingi wa itikadi hiyo ni Maandiko.
Mathayo ndiyo Injili moja tu inayorejezea wafanya-ziara hao. (2:1-12) Lakini je! Mathayo anataja kwamba kulikuwa na watatu na kwamba wao walikuwa wafalme, na je! anaandika majina yao katika kumbukumbu? Karatasi-habari ya Kikatoliki Kirchenzeitung für das Bistum Aachen inakiri hivi: “Wale Wafalme Watakatifu Watatu hawarejezewi kuwa hivyo katika Biblia. Kuanzia karne ya sita, hao wanaume wenye hekima walieleweka kuwa walikuwa . . . wafalme watatu. . . . Kwa habari ya hesabu ya wanajimu, . . . Mathayo hatoi maelezo ya kirefu. . . . Katika karne ya tisa wao walionekana kwa mara ya kwanza wakitajwa kwa majina Gaspar, Melchior, na Balthasar.” Zaidi ya hilo, kamusi ya marejezo ya Kikatoliki Lexikon für Theologie und Kirche kinasema kwamba neno la Kigiriki ma’goi halimaanishi wafalme, bali “walio na maarifa ya siri juu ya unajimu.” Justin Martyr, Origen, na Tertullian walielewa kila mmoja kwamba neno hilo lilimaanisha “mnajimu.” Watafsiri wa Biblia wa ki-siku-hizi wanatumia pia “wanajimu” kwenye Mathayo 2:1, 7.—The Living Bible; An American Translation.
Ingawa tamasha za Kuzaliwa kwa Yesu akiwa mtoto mchanga huwatia ndani nyakati zote wale “wafalme watatu,” je! wao walikuwa kwenye uzaliwa wake? Kamusi hiyo inaongeza hivi: “Mathayo 2:16 inaonyesha kwamba ziara hiyo ilitukia labda mwaka mmoja au zaidi baada ya kuzaliwa kwa Yesu.” Kweli kweli, mstari wa 11 unanena juu ya “nyumba,” wala si boma la ng’ombe, ambapo wao “walimwona yule mtoto mchanga.”—King James Version.b
Namna gani juu ya mtajo “Wafalme Watakatifu”? Je! inaweza kufaa wafanya-ziara hao waitwe watakatifu? Andiko haliwaelezi kamwe kuwa hivyo. Kwa uhakika, wao walikuwa wavunjaji wa kanuni ya kimungu. Kwenye Isaya 47:13, 14, NW, Mungu anashutumu “waabudu [“wanajimu,” kulingana na Septuagint] wa mbingu, watazama nyota.” (Linganisha Kumbukumbu 18:10.) Wanajimu hao walikuja “kutoka sehemu za mashariki,” ambazo inaelekea sana zilikuwa ndicho kitovu cha ibada ya siri za kimafumbo wakati huo, Babuloni isiyo takatifu, ambako wao waliabudu miungu bandia. Hivyo, wao waliongozwa na kile walichokifikiria kuwa “nyota” yenye kujongea, ambayo hakuna mtu mwingine yeyote anayeripotiwa kuwa aliiona. Pia, Mathayo anaonyesha kwamba “nyota” hiyo iliwaongoza kwanza kwa Mfalme Herode, na ndipo yeye akajaribu kufanya Yesu auawe.—Mathayo 2:1, 2.
Sivyo, Mungu hakupeleka “nyota” ya kuwaonyesha njia ya mahali alipokuwa Yesu. Je! haielekei zaidi kuwa “nyota” hiyo ilipelekwa na mtu fulani mwenye kutaka kuharibu Yesu kabla hajaweza kutimiza mgawo wake aliopewa na Mungu?—Linganisha Mwanzo 3:15.
Yesu alionya kwamba Neno la Mungu lingeweza ‘kutanguliwa’ kwa kuchanganywa na “mapokeo.” (Mathayo 15:6) Mapokeo yanayohusu watu hao si ya kimaandiko. Kwa hiyo, je! wewe hukubali kwamba lingekuwa kosa kuwaheshimu mno wanajimu hao au kuwaona kuwa watakatifu?
[Maelezo ya Chini]
a Makasisi huonyesha pia kifungu cha maneno ya Kilatini Christus mansionem benedicat, “Kristo na abariki nyumba hii,” kuwa njia ya kueleza jambo hilo.
b Ili upate habari zaidi kuhusu kuwasili kwa wanajimu hao, ona toleo la Desemba 15, 1979 (Kiingereza) la Mnara wa Mlinzi, ukurasa 30.