Maisha na Huduma ya Yesu
Kutafuta Waliopotea
YESU ana hamu nyingi ya kutafuta na kupata wale watakaotumikia Mungu kwa unyenyekevu. Kwa hiyo anatafuta-tafuta na kuongea na kila mmoja juu ya Ufalme, kutia na watenda dhambi wenye sifa mbaya. Watu hao sasa wanakuja karibu wamsikilize.
Kwa kuona hilo, Mafarisayo na waandishi wanachambua Yesu kwa kufanya uandamani pamoja na watu ambao wao wanawafikiria kuwa wasiostahiki. Wananung’unika hivi: “Mtu huyu huwakaribisha wenye dhambi, tena hula nao.” Hilo ni jambo la hali ya chini lisilopatana na fahari yao! Mafarisayo na waandishi hutendea watu wa kikawaida kama mavumbi yaliyo chini ya nyayo zao. Kwa uhakika, wao walitumia usemi wa Kiebrania ‛am ha·’aʹrets, “watu wa dunia [bara],” kuonyesha madharau yao kwa watu hao.
Kwa upande ule mwingine, Yesu hutendea kila mmoja kwa fahari, fadhili, na huruma. Tokeo ni kwamba, wengi wa watu hao dhalili, kutia na watu wanaojulikana kwa kuzoea makosa, wana hamu nyingi ya kumsikiliza. Lakini namna gani juu ya ku chambuliwa kwa Yesu na Mafarisayo kwa sababu ya jitihada zake kwa niaba ya wale ambao wao wanawaona kuwa wasiostahiki?
Yesu anajibu upinzani wao kwa kutumia kielezi. Ananena kulingana na rai ya Mafarisayo wenyewe, kwamba wao ni waadilifu na wako salama katika zizi la Mungu, hali wale akina ‛am ha·’aʹrets, wenye kudharaulika wameacha njia na wamo katika hali ya kupotea. Msikilize anapouliza hivi:
“Ni nani kwenu, mwenye kondoo mia, akipotewa na mmojawapo, asiyewaacha wale tisini na kenda nyikani, aende akamtafute yule aliyepotea hata amwone? Naye akiisha kumwona, humweka mabegani pake akifurahi. Na afikapo nyumbani kwake, huwaita rafiki zake na jirani zake, akawaambia, Furahini pamoja nami, kwa kuwa nimekwisha kumpata kondoo wangu aliyepotea.”
Halafu Yesu anaonyesha utumizi wa hadithi yake, akieleza hivi: “Nawaambia, Vivyo hivyo kutakuwa na furaha mbinguni kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye, kuliko kwa ajili ya wenye haki [waadilifu, NW] tisini na kenda ambao hawana haja ya kutubu.”
Mafarisayo wanajiona wenyewe kuwa waadilifu na hivyo hawana uhitaji wa kutubu. Baadhi yao walipomchambua Yesu miaka kadhaa mapema kidogo kwa sababu ya kula pamoja na wakusanya kodi na watenda dhambi, yeye aliwaambia hivi: “Sikuja kuwaita wenye haki [waadilifu, NW], bali wenye dhambi.” Mafarisayo wenye kujitakia uadilifu wao wenyewe, wasioona uhitaji wa kutubu, hawaleti shangwe yoyote mbinguni. Lakini watenda dhambi wenye kutubu kikweli wanaileta.
Ili kurudufisha mkazo kwenye wazo la kwamba kurudishwa kwa watenda dhambi waliopotea ni kisababishi cha ushangilio mkuu, Yesu anasimulia kielezi kingine. Anasema: “Kuna mwanamke gani mwenye shilingi kumi [sarafu kumi za drakma, NW], akipotewa na moja, asiyewasha taa na kufagia nyumba, na kutafuta kwa bidii hata aione? Na akiisha kuiona, huwaita rafiki zake na jirani zake, akawaambia, Furahini pamoja nami, kwa kuwa nimeipata tena shilingi [drakma, NW] ile iliyonipotea.”
Halafu Yesu anaonyesha utumizi unaofanana na ule mwingine, akisema: “Nawaambia, Vivyo hivyo kuna furaha mbele ya malaika wa Mungu kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye.”
Ni jambo la kusifika kama nini kwamba malaika za Mungu wanahangaikia kwa upendo kurudishwa kwa watenda dhambi waliopotea! Hivyo ndivyo ilivyo hasa kwa maana akina ‛am ha·’aʹrets, hao waliokuwa dhalili na wenye kudharaulika huja mwishowe kuingia katika mstari wa kuwa washiriki katika Ufalme wa Mungu wa kimbingu. Tokeo ni kwamba, wao wanafikia kule mbinguni cheo cha juu kuliko kile cha malaika wenyewe! Lakini badala ya malaika kuhisi wivu au ya kwamba wameshushiwa heshima, wanathamini kwa unyenye kevu uhakika wa kwamba wanadamu hao wenye dhambi wamekabili na kushinda maishani hali zitakazowapa utayari wa kutumikia wakiwa wafalme na makuhani wa kimbingu walio na masikitikio na rehema. Luka 15:1-10; Mathayo 9:13; 1 Wakorintho 6:2, 3; Ufunuo 20:6, NW.
◆ Kwa nini Yesu anashirikiana pamoja na watenda dhambi wanaojulikana, hiyo ikitokeza uchambuzi gani kutoka kwa Mafarisayo?
◆ Mafarisayo wana rai gani juu ya watu wa kikawaida?
◆ Yesu anatumia vielezi gani, na sisi tunaweza kujifunza nini kutokana navyo?
◆ Kwa nini ushangilio wa malaika ni jambo la kusifika?