Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w89 2/1 kur. 22-27
  • Tukifanya Penzi la Mungu, Yeye Hatatuacha Sisi Kamwe

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tukifanya Penzi la Mungu, Yeye Hatatuacha Sisi Kamwe
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Uhusiano Pamoja na Baba
  • Siku za Mapema za Upainia
  • Kufanya Kazi Chini ya Vizuizi!
  • Nguvu ya Yehova ya Utegemezaji
  • Mungu Amenionyesha Rehema
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Mfano wa Wazazi Wangu Uliniimarisha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Nilifurahia Kufanya Mengi Zaidi
    Amkeni!—2005
  • ‘Nilipanda Juu kwa Mabawa Kama Tai’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
w89 2/1 kur. 22-27

Tukifanya Penzi la Mungu, Yeye Hatatuacha Sisi Kamwe

Kama ilivyosimuliwa na Grete Schmidt

MIMI nilizaliwa katika Budapest, Hangari, katika 1915. Vita ya ulimwengu ya kwanza ilikuwa ikiendelea, na baba yangu alikuwa katika mistari ya mbele pamoja na jeshi la Austria-Hangari. Alipokufa mwaka mmoja baadaye, Mama alirudi pamoja nami Yugoslavia, walikoishi watu wa ukoo wake.

Kwa kuwa Mama hakufunga ndoa tena, alilazimika kutafuta kazi, kwa hiyo akamkabidhi dada yake itibari ya kunilea mimi. Shangazi yangu alikuwa mwenye shamba moja karibu kilometa 5 kutoka kwenye jiji la Maribor kaskazini mwa Yugoslavia. Huko nikakaa miaka mingi yenye furaha, sikuzote nikitazamia Jumapili wakati ambapo Mama angekuja kutoka kule chini Maribor ili kunizuru. Wakati uo huo, nilisitawisha tamanio kubwa la kuwa na baba.

Uhusiano Pamoja na Baba

Watu wa ukoo wangu walikuwa Wakatoliki, na kwa kuwa mbingu na helo zinashiriki fungu la maana katika dini ya Katoliki, hitilafiano lilitokea katika akili yangu. Mimi sikuhisi nilikuwa mwema vya kutosha nistahili kuwa mbinguni, lakini nilihisi sikuwa mbaya vya kutosha nistahili kushutumiwa kwenda helo (moto wa mateso). Niliongea kuhusu tatizo hilo pamoja na kila mtu, tangu nyanya yangu mpaka padri wa kijiji.

Mama ndiye niliyesumbua zaidi. Kwa hiyo baada ya miezi fulani, yeye akanipa kijitabu cha Kislovenia, Where Are the Dead? (Wafu Wako Wapi?), alichokuwa amepata mjini. Mama hakuwa amekisoma yeye mwenyewe, lakini aliwaza kingeweza kujibu maswali yangu.

Katika maisha yangu yote sikuwa kamwe nimesoma kichapo chochote mara nyingi kama kijitabu hicho! Si kwamba tu kilijibu maswali yangu kuhusu uhai na kifo bali pia kilinionyesha jinsi ya kusitawisha uhusiano wenye usiri pamoja na Baba yangu wa kimbingu. Niliagiza vijitabu vitano kwa madhumuni ya kuvigawanya mbele ya kanisa.

Katika kijiji chetu jamia ya wanawake walihudhuria ibada za kanisani siku ya Jumapili, lakini wanaume walibaki nje wakizungumza habari zao zilizowapendeza zaidi, mifugo na ukulima. Hivyo, padri alipokuwa akihubiria wanawake ndani ya kanisa, mimi nilihubiria wanaume nje. Nilikuwa na miaka 15 tu, na ni wazi wao waliona shangwe juu ya idili yangu ya ujana, kwa maana walilipia vijitabu vyao, nami nikatumia michango ile kupata ugavi mpya.

Muda si muda padri alipata habari juu ya utendaji wangu na akaja kunena na shangazi yangu. Jumapili iliyofuata, padri alionya hivi akiwa kwenye mimbari: “Kwa uhakika, hakuna mmoja katika kijiji chetu atakayekuwa na akili haba sana hata aitikadi hadithi za kijana-tineja.” Tokeo ni kwamba, kila mtu katika kijiji aligeuka akawa dhidi yangu. Hata shangazi yangu aliaibika na kujulisha mama yangu kwamba hangeweza tena kukaa nami.

Mimi nikahisi nimeachwa kweli kweli, lakini katika sala kwa Yehova, nilifarijika na kupata upya imara. Nilihama nikaenda kukaa pamoja na mama yangu katika Maribor, nasi tukawa na wakati wa kufurahisha sana pamoja. Ingawa yeye hakushiriki mapendezi yangu ya kiroho, aliniruhusu nihudhurie mikutano ya kundi dogo la huko. Siku ya Agosti 15, 1931, nilionyesha ufananisho wa wakfu wangu kwa Mungu kwa kubatizwa katika maji.

Nilipata majonzi makuu Mama alipokuwa mgonjwa ghafula na kufa majuma machache baadaye. Maneno ya mwisho aliyoniambia yangali yamenakshiwa katika kumbukumbu yangu: “Gretel, mpendwa wangu, gandamana na imani yako. Mimi nina uhakika huo ndio ukweli.” Baada ya kifo chake, nilihisi maumivu mengi ya kujiona nimeachwa tena, hata hivyo uhusiano wangu pamoja na Baba yetu wa kimbingu ulinisaidia kuendelea.

Mume na mke wasio na watoto wao wenyewe walinichukua nikae nao, nami nikatumikia nikiwa mkurufunzi mwenye kuwafanyia kazi katika duka la ushonaji ambalo mke wake alisimamia. Nilikuwa katika hali nzuri sana kimwili, lakini tamaa ya moyo wangu ilikuwa kutumikia Mungu wakati wote. Katika kundi letu dogo katika Maribor, wote walisadiki kwamba wakati uliobaki kwa huu mfumo wa mambo ulikuwa mfupi. (1 Wakorintho 7:29) Kwa siri mimi nilimwomba Yehova katika sala zangu ili aahirishe kuchukua hatua mpaka niwe nimemaliza ukurufunzi wangu. Nilimaliza siku ya Juni 15, 1933, na ile ile kesho yake, nikaondoka kwenye maskani yangu ili kuanza kupainia! Kwa sababu ya ujana wangu​—nilikuwa na miaka 17 tu​—hata baadhi ya akina ndugu walijaribu kunizuia, lakini mimi nilikuwa nimepiga moyo konde.

Siku za Mapema za Upainia

Mgawo wangu wa kwanza ulikuwa Zagreb, jiji moja la karibu wakaaji 200,000 si mbali kutoka Maribor. Kundi lilikuwa na wahubiri sita tu. Mimi nilijifunza mengi sana kwa kufanya kazi pamoja na Ndugu Tucek, painia wa kwanza kabisa katika Yugoslavia. Baadaye, nilipainia nikiwa peke yangu kwa karibu mwaka mmoja. Hata hivyo, pole kwa pole mapainia wengi zaidi waliwasili kutoka Ujeremani, kwa kuwa hivi majuzi kazi ya kuhubiri ilikuwa imepigwa marufuku huko na serikali ya Nazi.

Mimi nilisaidia hesabu fulani ya waume na wake zao walio mapainia kwa kutumikia nikiwa mtafsiri wao. Kufanya kazi pamoja na Wakristo hao waliokomaa kulikuwa ono la thamani kubwa sana kwangu. Niliongezeka katika maarifa na uelewevu, na uthamini wangu kwa pendeleo la kuhubiri habari njema za Ufalme ukakua daima.

Baada ya muda, sisi tukawa kikundi cha kuvutia cha mapainia 20 wenye kutumikia katika Mikoa ya Balkan. Jitihada yetu ya ujumla ya kujulisha Neno la Mungu ilitufungamanisha, kila mmoja akiwa tayari kusaidia mwenzake katika uhitaji. Sisi sote tulisukumwa na riia ambayo hupatikana miongoni mwa watu wa Mungu peke yao. Hicho “kifungo cha muungano” kilicho cha pekee, upendo, kinaendelea miongoni mwa wale wa kikundi hicho walio hai bado leo.​—Wakolosai 3:14.

Maisha ya painia yana utajiri wa maono, nayo hutolea mtu unamna-namna wa mambo mengi sawasawa na vile kulivyo na mawingu ya namna-namna katika anga. Sisi tulihisi tumetajirishwa kupitia lile ono la thamani kubwa la kupata kujua mabara na vikundi vya watu tusiowajua hapo kwanza, kutia na desturi zao na njia yao ya maisha. Zaidi ya hilo, tuliona jinsi Yehova hutunza watumishi wake waaminifu, sawa na vile Paulo anavyotuhakikishia kwenye Waefeso 3:20, NW: ‘Kulingana na nguvu yake ambayo inafanya kazi ndani yetu, yeye anafanya mengi kwa wingi unaozidi kwa kupita sana mambo yote ambayo sisi tunaomba au kudhania.’

Utunzaji wenye upendo wa Yehova ulionyeshwa wakati Ndugu Honegger alipotuzuru sisi kutoka Switzerland na akaona kwamba tulilazimika kutembea hadi kilometa 40 ili kufikia vijiji vya kandokando ya Zagreb. Yeye aliona kwamba tulivua viatu vyetu na kuviangika juu ya mabega yetu mara tulipokwisha kuondoka jijini ili kuokoa nyayo zavyo za chini zisimalizike. Kwa hiyo akatununulia baiskeli 12, hata ingawa, kama alivyosema baadaye, hiyo ilimaliza pesa zote alizokuwa nazo! Kwa uhakika Yehova husukuma mioyo ya wenye mioyo minyoofu. Baiskeli hizo, zikiwa kama zawadi kutoka mbinguni, zilitutumikia sisi zikiwa waandamani waaminifu wakati wa miaka 25 ya utumishi wa painia.

Wakati mmoja, Willi na Elisabeth Wilke na mimi tuliwasili kwenye kijiji kimoja cha Kikroati chenye ukubwa wa kadiri, ambako kila mmoja wetu alifanya kazi peke yake​—kuanzia viungani kuelekea kitovu cha kijiji. Tulikuwa tukitoa kile kijitabu Righteous Ruler (Mtawala Mwadilifu), kilichoonyesha Yesu Kristo katika ukurasa wenye kichwa. Mwaka ule tu uliotangulia, katika 1934, mfalme wa Yugoslavia, Alexander, alikuwa ameuawa, na Peter mwanaye ndiye angekuwa mwandamizi wake katika kiti cha ufalme. Hata hivyo, wanakijiji walipendelea zaidi kuwa na serikali ya kujitawala wenyewe badala ya mmaliki wa kutoka Serbia (Yugoslavia ya kusini).

Baada ya saa kadhaa za kuhubiri, taharuki yenye makelele ingeweza kusikiwa kutoka njia kuu ya kijiji. Huko, Ndugu Wilke na mimi tulipata Dada Wilke akiwa amezungukwa na kikundi cha karibu wanaume na wanawake 20, baadhi yao wakiwa wameshika miundu, wengine wakiwa na kazi nyingi ya kuchoma vijitabu vyetu. Dada Wilke hangeweza kunena lugha ile kwa uzuri wa kutosha hata awaondolee wanakijiji hao ukosefu wao wa itibari.

“Mabibi na mabwana,” mimi nikapaaza sauti, “mnafanya nini?”

“Sisi hatumtaki Mfalme Peter!” wakajibu kama kwa sauti moja.

“Wala sisi hatumtaki,” mimi nikajibu.

Kwa kushangaa, watu hao wakaelekeza vidole kwenye picha iliyokuwa juu ya kijitabu kile na kuuliza, “Mbona basi mnamfanyia propaganda?” Walikuwa wamekosea kwa kumdhania Yesu Kristo kuwa ni Mfalme Peter!

Ukosefu huo wa kutoelewana ulimalizwa, na ushahidi kamili kuhusu Mfalme Yesu Kristo ukatolewa. Watu fulani waliokuwa wamechoma vijitabu vyao sasa wakataka vipya. Sisi tukaondoka katika kijiji hicho tukiwa na hali ya furaha, tukihisi kwamba mkono wa himaya ya Yehova ulikuwa umekuwa juu yetu.

Baadaye tulipanua kuhubiri kwetu kufika ndani ya Bosnia, kitovu cha Yugoslavia. Huko, karibu nusu ya wakaaji walikuwa Waislamu, nasi tulikabiliwa tena na desturi mpya na hali nyingi za woga wa kishirikina. Katika vijiji, watu walikuwa hawajaona kamwe mwanamke akiwa amepanda baiskeli, kwa hiyo kuwasili kwetu ni kama kulifadhaisha watu, kukichochea udadisi. Viongozi wa kidini walieneza uvumi wa kwamba mwanamke mmoja aliyepanda baiskeli alileta bahati mbaya kwenye kijiji fulani. Baada ya hapo sisi tukaacha baiskeli zetu nje ya vijiji na kuviingia kwa kutembea kwa miguu.

Kwa kuwa sasa fasihi yetu ilipigwa marufuku, mara nyingi polisi walitushika. Kwa kawaida, tuliagizwa tuondoke kwenye mkoa huo. Polisi wawili wangeandamana nasi hadi mpakani, umbali wa kuanzia kilometa 50 hadi 100. Walishangaa kwamba tulikuwa waendeshaji hodari sana wa baiskeli, wenye kuweza kupiga mwendo mmoja nao ijapokuwa tulibeba nguo zetu zote na fasihi na jiko dogo la mafuta-taa. Sikuzote wasindikizaji wetu walifurahia kutafuta mkahawa mdogo njiani, na mara nyingi walitualika tupate kinywaji au hata mlo. Sisi tuliona shangwe juu ya pindi hizo, kwa maana alawansi yetu ndogo haikuruhusu tuwe na ziada hizo. Bila shaka, tulibamba fursa hiyo kuwaambia juu ya tumaini letu, na mara nyingi wao walikuwa wakikubali baadhi ya vichapo hivyo “vilivyoharamishwa.” Mara nyingi, sisi tuliagana nao kwa masikilizano mazuri.

Ndipo ulipokuja mwaka 1936. Tulikuwa tukihubiri katika Serbia habari zilipotufikia kwamba mkusanyiko wa kimataifa ungefanywa katika Lucerne, Switzerland, katika Septemba. Basi moja ya pekee ingeondoka Maribor, lakini hiyo ilikuwa kilometa 700 kutoka tulipokuwa​—mwendo mrefu kwa baiskeli! Hata hivyo, tulianza kulimbika pesa zetu na, baadaye mwakani, tukafunga safari hiyo.

Tulikuwa tukiomba ruhusa kwa wakulima ili tukae usiku kucha katika chumba chao cha kuwekea nyasi za ng’ombe badala ya kulipia chumba kwenye nyumba ya wageni. Asubuhi, tuliuliza kama tungeweza kununua kiasi fulani cha maziwa kutoka kwao, lakini kwa kawaida walitupatia bure na nyakati fulani wakatupatia hata kiamsha-kinywa cha kutosha. Tulionyeshwa fadhili nyingi za kibinadamu, na hiyo ingali sehemu yenye furaha ya kumbukumbu zetu za kipainia.

Kabla ya kuondoka Maribor kwenda Lucerne, mapainia zaidi waliwasili kutoka Ujeremani. Miongoni mwao alikuwa Alfred Schmidt, aliyekuwa ametumikia miaka minane katika Betheli kule Magdeburg, Ujeremani. Mwaka mmoja baadaye mimi nikawa mke wake.

Karibu mapainia wote katika Yugoslavia waliweza kuhudhuria ule mkusanyiko katika Lucerne. Ulikuwa wangu wa kwanza, na hisia zangu zilivutwa sana na upendo na ujalifu ulioonyeshwa na ndugu wa Switzerland, zaidi ya kuvutiwa na upendezi wa jiji la Lucerne. Sikujua kwamba miaka 20 baadaye, ningekuwa nikipainia huko!

Kufanya Kazi Chini ya Vizuizi!

Tulipokuwa tukirudi kutoka Switzerland yenye sura nzuri kwenda Yugoslavia, muda si muda tulianza kupata mnyanyaso wa kweli kweli. Tulikamatwa na kufungiwa katika gereza kuu katika Belgrade. Ndugu mwenye daraka kwa ajili ya kazi katika Yugoslavia aliomba ruhusa atufanyie ziara, lakini akanyimwa. Hata hivyo, alinena na mlinzi mmoja wa gereza kwa sauti kubwa sana hata tukaweza kumsikia, na mvumo wenyewe wa sauti yake ulikuwa kitia-moyo kikubwa kwetu.

Baada ya siku chache, tulipelekwa kwenye mpaka wa Hangari tukiwa na pingu mikononi; tulikuwa tumenyang’anywa fasihi yetu na pesa zetu. Hivyo, tuliwasili katika Budapest bila peni, lakini tukiwa na chawa tele waliojishikiza kwetu wakiwa kionyesho cha kwamba tulitoka gerezani. Muda si muda tukakutana pamoja na mapainia wengine na kushiriki pamoja nao katika kazi ya kuhubiri huko.

Kila Jumatatu sisi mapainia katika Budapest tulikutana katika mahali pa kuoga kwa mvuke wenye joto, na tulipokuwa tukioga, akina dada na akina ndugu wakiwa mbali mbali waliona shangwe ya kufanya “mbadilishano wa kitia-moyo . . . kila mmoja kupitia imani ya yule mwingine.” (Warumi 1:12, NW) Kukutana pamoja kulikuwa njia ya kujua kama mtu fulani alikuwa mgonjwa au alitiwa gerezani.

Baada ya miezi sita, tulipokuwa ndiyo sasa tu tunazoea mazingira yetu mapya, kibali chetu cha kuturuhusu kukaa Hangari kilimalizika. Muda huo, Alfred na mimi tulikuwa tumekwisha kufunga ndoa. Sasa tulipokea maagizo tupate kibali cha kwenda Bulgaria. Mume na mke mapainia wa huko walikuwa wamefukuzwa nchini, na vijitabu elfu kumi walivyokuwa wameagiza vilikuwa tayari kwenye sehemu ndogo ya uchapaji katika Sofia. Fasihi yao ilikuwa imechomwa hadharani, kwa hiyo tulijua tulivyopaswa kutarajia kutendewa.

Hatimaye tulipata kibali cha kukaa Bulgaria miezi mitatu. Tulipitia Yugoslavia usiku, na ndugu mmoja mwenye daraka alitulaki kwenye kituo fulani kilichopangwa mapema akiwa na pesa za kununua vijitabu. Hatimaye, tuliwasili salama katika Sofia na kupata chumba chenye kufaa.

Sofia lilikuwa jiji la ki-siku-hizi lenye wakaaji karibu 300,000, lakini hakukuwa na Mashahidi wowote huko. Siku iliyofuata kuwasili kwetu, tulienda ile sehemu ya uchapaji. Mwenyewe alikuwa amesikia habari za kupigwa marufuku kwa fasihi yetu na kuondoshwa nchini kwa wale mume na mke waliokuwa wameagiza vijitabu vile, kwa hiyo alipojua kwamba sisi tulikuwa tumekuja kuvinunua, karibu atukumbatie. Sisi tuliingiza vijitabu hivyo ndani ya mifuko mitupu na kuendesha gari tukiwapita polisi kadhaa, ambao, mimi nafurahi kusema, hawakuweza kusikia jinsi mioyo yetu ilivyokuwa ikidunda-dunda kasi!

Tatizo letu lililofuata lilikuwa mahali pa kuweka vijitabu hivyo na jinsi ya kuangusha hesabu kubwa hivyo katika miezi mitatu tu. Kwa kweli mimi nililiogopa rundo hilo la vijitabu! Sikuwa nimepata kuona vijitabu vingi jinsi hiyo. Lakini hapo tena Yehova alikuwa Msaidiaji wetu. Tulipata mafanikio makubwa sana, tukiangusha kufikia 140 kwa siku, na katika muda wa majuma machache, Ndugu na Dada Wilke waliwasili kutusaidia.

Hata hivyo, siku moja karibu mambo yaende kombo. Mimi nilikuwa nikihubiri katika eneo moja la kikazi ambako kila mlango ulikuwa na kibamba cha shaba chenye jina la Dakt. Fulani-wa-Fulani. Baada ya muda wa karibu saa mbili, nilikuta bwana mmoja mzee-mzee aliyeniuliza maswali ya upekuzi mwingi kwa kutoniitibari. Aliniuliza kama nilijua hapo ni wapi.

“Sijui sawasawa hili ni jengo la aina gani, lakini nimeona kwamba wanasheria wote walio hodari wanaonekana ni kana kwamba wameunganisha ofisi zao hapa,” mimi nikajibu.

“Humu ulimo ni Wizara ya Mambo ya Ndani,” yeye akajibu.

Ingawa karibu moyo wangu usimame tuli, mimi nilijibu kwa utulivu hivi: “Oh, kumbe ndiyo sababu mabwana wote hawa wamenionyesha urafiki sana!” Neno hilo likalainisha mwelekeo wake, naye akanirudishia paspoti yangu baada ya kuichunguza kweli kweli. Niliondoka kwa kutusha pumzi, nikimshukuru Yehova kwa himaya yake.

Hatimaye, vijitabu vyote viliangushwa, na siku ikafika ya sisi kuliacha hilo “bara la mawaridi,” Bulgaria. Ilikuwa vigumu kuwaacha watu hao wenye urafiki mwingi, lakini kumbukumbu linalowahusu lilibaki likiwa limetia nanga ya kina kirefu katika mioyo yetu.

Kwa maana tulikuwa na paspoti za Kijeremani, tuliweza kurudi Yugoslavia, lakini tuliruhusiwa kukaa muda mfupi tu. Baadaye, ili tuepuke kukamatwa, tulilazimika kulala mahali tofauti kila usiku. Tuliishi hivyo kwa karibu miezi sita. Ndipo, katika nusu ya mwisho ya 1938, tukapokea barua kutoka ofisi ya Sosaiti katika Bern, Switzerland, ikituagiza tujaribu kuja Switzerland. Jeshi la Nazi lilikuwa tayari limeingia Austria kukaa, na mbano wa kisiasa ulikuwa ukiongezeka. Kwa uhakika, serikali ya Yugoslavia ilikuwa tayari imewatia baadhi ya mapainia Wajeremani mikononi mwa Wanazi.

Kwa hiyo mume wangu na mimi tukasafiri kwa mtengano kwenda Switzerland, huku Alfred akifuata njia ya Italia na mimi nikipitia Austria. Tuliungana tena kwa furaha na kupewa mgawo wa kazi kwenye shamba la Sosaiti, Chanelaz, halafu baadaye kwenye Betheli katika Bern. Hilo lilikuwa ono jipya kabisa kwangu. Sasa nililazimika kujifunza kutunza nyumba mtindo wa Switzerland, nami nikaja kuthamini sana tengenezo la Yehova zaidi ya wakati mwingine wowote.

Nguvu ya Yehova ya Utegemezaji

Baada ya kutumikia Betheli wakati wa Vita ya Ulimwengu 2 na baadaye, katika 1952 Alfred na mimi tuliingia tena kazi ya painia, utendaji uliokuwa umefanyiza umbo la maisha zetu. Sisi hatukuwa kamwe na watoto wetu wenyewe, lakini katika muda wa miaka hiyo iliyopita, tumepokea maneno mengi sana ya kuonyeshwa upendo kutoka kwa watoto wetu wa kiroho. Mathalani, katika Februari 1975 tulipokea kibarua kinachofuata:

“Mimi nakumbuka siku ile ambayo mwanamume mmoja mwenye hekima, aliye na mvi, alipozuru mshauri mmoja mwenye kichwa kigumu wa Kanisa Evanjeliko na kumtolea funzo la Biblia. Kwa mashaka-mashaka na kwa kuchambua-chambua mambo, jamaa yangu na mimi tulikubali halafu tukachunguza kila jambo sawasawa na walivyofanya Waberoya, mpaka tukalazimika kukiri kwamba nyinyi mlituletea ukweli. . . . Lo, Yehova Mungu ni Baba mwenye fadhili kama nini! Kwake yeye na kuwe sifa na heshima na shukrani kwa ajili ya fadhili na rehema zake zote. Lakini sisi tunataka kuwashukuru nyinyi pia, wapendwa Alfred na Gretel, kutoka kwenye kina cha mioyo yetu, kwa ajili ya saburi ya ujalifu mwingi sana mliyotuonyesha sisi. Yehova awabariki sana kwa kufanya hivyo. Sisi tunatumaini kwa moyo mweupe kwamba yeye atatupatia sisi pia imara ya kudumu tukiwa wavumilivu.”

Katika Novemba 1975 mume wangu Alfred alikufa ghafula kutokana na ugonjwa wa moyo. Kwa miaka 38 tulikuwa tumetumikia Yehova pamoja, tukivumilia mazuri na magumu ya upainia. Hiyo ilifanya uhusiano wetu uwe wa ukaribiano mkubwa. Hata hivyo, alipokufa ile hisia ya kujiona mtupu na kuwa katika hali ya kuachwa ilinipenya tena. Lakini kwa kutafuta kimbilio katika Yehova, nilifarijiwa tena.

Uhusiano wangu pamoja na Baba yetu wa kimbingu umenitegemeza kupita katika miaka zaidi ya 53 nikiwa katika utumishi wake wa wakati wote. Na maoni yangu ya ndani yanaendelea kuwa yale ya Yesu Kristo: “Mimi si peke yangu, kwa kuwa Baba yupo pamoja nami.”​—Yohana 16:32.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Alfred na Frieda Tucek wakipainia katika Yugoslavia wakiwa na vifaa kamili, katika 1937

[Picha katika ukurasa wa 25]

Alfred na Grete Schmidt wakipainia katika Mostar, kisehemu cha Kiislamu cha Yugoslavia, katika 1938

[Picha katika ukurasa wa 26]

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki