Neno la Mungu—Ithibati la Kwamba Ni la Kweli
Kweli au si kweli?—Biblia imepokezanwa muda wa mihula iliyopita bila kufanyiwa badiliko.
Kweli au si kweli?—Maelfu ya mitofautiano iliyo katika hati-mkono za Biblia yanadhoofisha dai layo la kwamba ni Neno la Mungu.
KABLA hujajibu maswali hayo, fikiria habari fulani zilizotokezwa hivi majuzi kwenye Wonyesho wa “Neno la Mungu” uliofanywa katika Maktaba ya Chester Beatty katika Dublin, Ailandi.
Kurasa zile za mafunjo yaliyotatuka vipande-vipande zinachakaa kwa kukaa sana. Hata hivyo, mafunjo ya Chester Beatty ndizo hati-mkono zilizo za thamani kubwa zaidi katika maktaba hiyo. Ya lichimbuliwa katika uwanja wa makaburi ya Kikopti (Kimisri) karibu 1930. “[Huo ulikuwa] ugunduzi,” akasema Sir Frederic Kenyon, “ambao kifani chao ni ule tu wa Codex Sinaiticus.”
Kurasa hizo za mafunjo zilizoandikwa kwa mkono, kwa namna ya kodeksi, zilinakiliwa katika karne ya pili, ya tatu, na ya nne ya Wakati wa Kawaida wetu. “Baadhi yazo,” akasema Wilfrid Lockwood, aliye mtunza-maktaba, “huenda zikawa zilinakiliwa katika muda wa miaka mia moja baada ya kutungwa kwa zile za awali.” (Italiki ni zetu.) Kodeksi moja ina zile Gospeli (Injili) nne na kitabu cha Matendo. Nyingine ina nyingi za barua za mtume Paulo, kutia na barua yake kwa Waebrania.
Kunakili hati-mkono kama hizi kulikuwa kazi ya kunyong’onyeza na kuchosha, na ya kuweza kukosea. Ilikuwa rahisi kusoma vibaya herufi fulani au kuruka mstari fulani, hata kama mnakili angeweza kuwa mwangalifu kadiri gani. Nyakati fulani mnakili alipendezwa zaidi na kupata wazo kuu na maana ya ile habari ya awali kuliko vile alivyopendezwa na maneno yale yenyewe hasa. Nakala ziliponakiliwa-nakiliwa upya, makosa yaliendelezwa. Wanachuo wenye kuchunguza maandishi-awali walizipanga hati-mkono zenye mitofautiano inayofanana zikiwa jamii-jamii. Mafunjo hayo ya Chester Beatty, ambayo ndiyo hati-mkono zilizo za zamani zaidi za Biblia ya Kigiriki, yaliwapa wanachuo hao rai mpya wasiyokuwa wametarajia, kwa kuwa hayakufaa kuhesabiwa katika yoyote ya jamii zile.
Kabla ya wakati wa Yesu, na hasa kufuata uharibifu wa Yerusalemu (607 K.W.K.) na mtawanyo uliofuata wa Wayahudi, nakala nyi ngi zilizoandikwa kwa mkono za Maandiko ya Kiebrania yaliyo matakatifu zilifanyizwa. Karibu na 100 W.K., wenye mamlaka Wayahudi walitumia nakala hizo kuanzisha andishi-awali la Kiebrania lililokubaliwa na Wayahudi wa asili.
Pia waliweka wazi kanuni halisi za kujaribu kuhakikisha kwamba hilo andishi-awali lilinakiliwa sawasawa kabisa. Walieleza waziwazi ni vifaa gani vingeweza kutumiwa na hata ukubwa na mtenganisho wa nafasi kati ya herufi, maneno, mistari, na safu. “Ni lazima neno wala herufi, wala hata yod moja [ambayo ndiyo herufi ndogo zaidi katika alfabeti ya Kiebrania], isiandikwe kwa kutegemea kumbukumbu ya akilini,” wao wakasema. Hivyo wanakili walitokeza hati-kunjo kama Torah (fundisho), ikiwa na vitabu vitano vya kwanza vya Biblia, na kitabu cha Esta. Hizo hati-mkono za andishiawali la Kiebrania, ikasema orodha ile ya wonyesho, “zinaonyesha upatano wa kadiri ya kuvutia.”
Yalikuwa ya uzito gani makosa yaliyopenya katika hati-mkono za Kiebrania na za Kigiriki pia za wakati wa Kikristo? “Inapasa kukaziwa,” akasema Bw. Lockwood, “kwamba miachano iliyo kati ya hati-mkono za Biblia ni ya kijuu-juu tu ikilinganishwa na ile inayopatikana katika hati-mkono za fasihi ya kipagani . . . Hakuna mahali popote ambapo wazo lolote la fundisho la Kikristo limeathiriwa na ufisadi wa waandishi.”—Italiki ni zetu.
Vitabu vya Biblia vya kabla na baada ya wakati wa Yesu vilitafsiriwa kuingizwa katika lugha nyinginezo. Moja ya fasiri zilizo za zamani zaidi kati ya hizo ni Pentateuko ya Kisamaria. Wasamaria walikuwa watu waliolikaa eneo la ufalme wa Israeli wenye makabili kumi baada ya mfalme wa Ashuru kupeleka Waisraeli uhamishoni (740 K.W.K.) Walichagua kufuata sehemu fulani za ibada ya Kiyahudi na wakakubali vitabu vitano vya kwanza tu vya Biblia, ile Pentateuko. Andishi-awali la Kisamaria la vitabu hivyo, lililoandikwa kwa namna ya hati ya Kiebrania cha kale, ina mitofautiano 6,000 isiyo sawa na andishi-awali la Kiebrania. “Iliyo mingi,” ikasema ile orodha ya wonyesho, “si ya maana sana kwa hilo andishiawali ingawa inapendeza kwa sababu ya uyamkini wa kuwa inahifadhi sehemu za matamshi au sarufi ya kale.”
Katika karne ya tatu K.W.K., wanachuo Wayahudi katika Alexandria, Misri, walitokeza fasiri ya Kigiriki ya Septuagint ya Maandiko ya Kiebrania, nayo ikaja kutumiwa na Wayahudi wenye kunena Kigiriki katika sehemu zote za ulimwengu. Baada ya muda Wayahudi waliacha kuitumia, lakini ikawa ndiyo Biblia ya kundi la mapema la Kikristo. Wakati waandikaji wa Biblia walio Wakristo waliponukuu kutokana na Maandiko ya Kiebrania yaliyo matakatifu, walitumia Septuagint. Mafunjo ya Chester Beatty ya Maandiko ya Kiebrania ni kutia ndani kurasa 13 za kitabu cha Danieli zilizo katika Septuagint.
Fasiri za baadaye za Biblia zilitokezwa kati ka lugha kama vile Kilatini, Kikopti, Kisiria, na Kiarmeni. Kielelezo kimoja katika wonyesho kilikuwa kodeksi iliyoandikwa katika velamu (ngozi ya mbuzi) au ya fasiri ya Kikopti ya kisehemu kimoja cha Biblia cha kutoka karne ya sita au ya saba W.K. Fasiri kama hiyo zinasaidiaje wanachuo wa Biblia na wachambuzi wa maandishi? Kwa kawaida fasiri hizo huwa ni tafsiri zenye kufuatilia sana uhalisi wa maneno katika kufasiri hati-mkono za Kigiriki ambazo watafsiri walitumia. “Ikiwa andishi la Kigiriki lililofanyiwa kazi na mtafsiri lilikuwa la kadiri nzuri,” anaeleza Bw. Lockwood, “ni wazi kwamba fasiri ile itaandaa msaada wa maana katika kazi ya kurudisha yale maneno ya awali ya Kigiriki.”
Wonyesho ulio wa thamani kubwa sana na usio na kifani katika maktaba hiyo ni kitabu kimoja cha maelezo kilichotungwa na mwandikaji Msiria wa karne ya nne, Ephraem, kuhusu Diatessaron kilichotungwa na Tatian. Karibu 170 W.K., Tatian alikusanya usimulizi uliopatanishwa kuhusu maisha na huduma ya Yesu, akitumia madondoo kutokana na zile Gospeli nne (Diatessaron inamaanisha “kupitia [zilej nne”. Kwa sababu hakuna nakala zilizobakia, wachambuzi fulani katika karne iliyopita walitoa ubishi juu ya kama kweli kuna wakati Gospeli hizo zilipokuwa na upatano. Wachambuzi hao walikazania kwamba zile Gospeli nne zenyewe hazikuandikwa mpaka katikati ya karne ya pili.
Hata hivyo, katika miaka mia moja iliyopita, kugunduliwa kwa tafsiri za Diatessaron katika Kiarmeni na Kiarabu kulilazimisha wachambuzi wa juu zaidi warudi nyuma kwa kuiacha rai yao. Halafu, katika 1956, Sir Chester Beatty alipata kitabu hicho kisicho na kifani cha maelezo ya karne ya tano/sita kilicho na madondoo marefu kutokana na kazi ya awali ya Tatian. “Kwa uhakika kilikomesha wazo la kwamba zile Gospeli nne hazikuwa zikienezwa katika enzi hiyo,” akasema Bw. Lockwood.
Wonyesho wa “Neno la Mungu” ulikuwa kikumbusho cha wingi wa vifaa vilivyopatikana ili viangaliwe na wanachuo wa Biblia na wachambuzi wa maandishi-awali. Acha mmoja wa wanachuo hao, Sir Frederic Kenyon, aeleze umaana wa hizo hati-mkono za Kibiblia ambazo zimegunduliwa na wakati ule ule ajibu maswali yaliyotokezwa mwanzoni:
“Huenda watu fulani wakawa na mfadhaiko wa kutotaka kuacha dhana ya kwamba Biblia haiwezi kuwa ilipokezanwa muda wa mihula yote hiyo bila kufanyiwa badiliko . . . Uhakikishio unapatikana mwishowe kwa kukuta kwamba tokeo la ujumla la magunduzi yote haya na uchunguzi wote huu ni kuimarisha uthibitisho wa kwamba Maandiko ni ya kweli, na usadikisho wa kwamba kile tulicho nacho katika mikono yetu, kikiwa na ukamilifu mkubwa, ni Neno la Mungu lenye uhakiki.” (The Story of the Bible, ukurasa 113)—Zaburi 119:105; 1 Petro 1:25.
[Picha katika ukurasa wa 27]
funjo la karne ya tatu—2 Wakorintho 4:13–5:4
[Hisani]
llinakiliwa kwa ruhusa ya Chester Beatty Library
[Picha katika ukurasa wa 28]
Hati-kunjo za ngozi na velamu za karne ya 18 za Esta
[Hisani]
llinakiliwa kwa ruhusa ya Chester Beatty Library
[Picha katika ukurasa wa 29]
Kodeksi ya velamu ya karne ya sita au ya saba—Yohana 1:1-9, fasiri ya Kikopti
[Hisani]
llinakiliwa kwa ruhusa ya Chester Beatty Library
[Picha katika ukurasa wa 30]
Kodeksi ya velamu ya karne ya tano au ya sita—maelezo ya Ephraem yanayotia ndani madondoo kutoka Diatessaron cha Tatian, katika Kisiria
[Hisani]
llinakiliwa kwa ruhusa ya Chester Beatty Library