Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w89 2/15 kur. 10-15
  • Haki kwa Wote Kupitia Hakimu Mwekwa wa Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Haki kwa Wote Kupitia Hakimu Mwekwa wa Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ni Hukumu na Haki ya Namna Gani?
  • “Siku” ya Kuhukumu​—Lini?
  • Matatizo ya Zamani ya Ukosefu wa Haki Yatatuliwa
  • “Njia Zake Zote Ni Haki”
    Mkaribie Yehova
  • Mwige Yehova—Dhihirisha Haki na Uadilifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Yehova—Chanzo cha Haki na Uadilifu wa Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Yehova—Mpenda Uadilifu na Haki
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
w89 2/15 kur. 10-15

Haki kwa Wote Kupitia Hakimu Mwekwa wa Mungu

“Kwa kuwa Baba ampenda Mwana, naye . . . amempa Mwana hukumu yote.”​—YOHANA 5:20, 22.

1. Wewe unakabilianaje na maswali yanayofanana na yale yaliyokabiliwa na watu fulani katika karne ya kwanza?

HAKI ina umaana gani kwako? Wewe ungefanya jitihada ya kadiri gani ili uwe na uhakikisho wa kupokea haki ya kweli na hata kuishi wakati itakapokuwapo kwa wingi duniani pote? Ni juu yako kufikiria maswali hayo, kama walivyofanya wanaume na wanawake fulani mashuhuri katika Athene, Ugiriki.

2, 3. (a) Ni nini kilichoongoza Paulo kutolea wasikilizaji wake Waathene wito wa kutubu? (b) Kwa nini toba ingesikika kuwa jambo geni kwa wasikilizaji hao?

2 Wao walisikia hotuba yenye kukumbukika ambayo mtume Mkristo Paulo aliitolea mahakama yenye sifa kubwa ya Areopago. Kwanza yeye alisababu juu ya kuwako kwa Mungu mmoja, Muumba, ambaye kwake sisi sote tuna deni la uhai wetu. Hiyo ikaongoza kwenye kukata shauri la kiakili kwamba sisi tuna wajibu wa kutolea Mungu hesabu. Kufikia hapo Paulo alitangaza hivi: “Zamani zile za ujinga [wa kuwa watu wanaoabudu sanamu], Mungu alijifanya kama hazioni; bali sasa anawaagiza watu wote wa kila mahali watubu.”​—Matendo 17:30.

3 Kwa kusema wazi, toba ingekuwa dhana ya kugutusha wasikilizaji hao. Kwa nini? Wagiriki wa kale waliijua toba katika maana ya kuhisi majuto kwa sababu ya tendo au taarifa fulani. Hata hivyo, kama vile kamusi moja inavyoonyesha wazi, neno hilo “ha[liku]dokeza kamwe mgeuzo wa mwelekeo wa kiadili kwa ujumla, badiliko lenye kina kirefu katika mwelekezo wa maisha, uongofu ambao unaathiri mwenendo mzima.”

4. Elezo la Paulo juu ya toba liliungwa mkono na sababu gani ya kiakili?

4 Hata hivyo, bila shaka wewe unaweza kuona ni kwa nini toba hiyo ya kina kirefu inafaa. Fuata sababu ya kiakili inayotolewa na Paulo. Wanadamu wote wana deni la Mungu kwa uhai wao, kwa hiyo wote wana wajibu wa kumtolea hesabu. Basi, ni sawa na haki kabisa kwamba Mungu awatarajie wao kumtafuta yeye, kupata maarifa juu yake. Ikiwa Waathene hao hawakujua kanuni na penzi lake, walihitaji kujifunza mambo hayo kisha watubu ili kupatanisha maisha zao na kanuni hizo. Hiyo haingetegemea kadiri ambavyo ingekuwa rahisi kufanya hivyo. Tunaweza kuona sababu kutokana na upeo wa Paulo wenye kani nyingi: “Kwa maana ameweka siku atakayowahukumu walimwengu kwa haki [uadilifu,NW], kwa mtu yule aliyemchagua [aliyemweka, NW]; naye amewapa watu wote uthabiti wa mambo haya kwa kumfufua katika wafu.”​—Matendo 17:31.

5. Wasikilizaji waliitikiaje hotuba ya Paulo, na kwa nini?

5 Mstari huo, uliojaa sana maana, ulio wa kusadikisha sana, unastahili ukaguzi wetu wa uangalifu, kwa maana unachochea kutumainia haki kamilifu katika wakati wetu. Angalia vile vifungu vya maneno: ‘weka siku,’ ‘hukumu walimwengu,’ ‘kwa uadilifu,’ ‘kwa mtu ambaye amemweka,’ ‘kawapa watu wote uthabiti,’ ‘kamfufua.’ Neno hilo ‘kamfufua’ lilileta tendo-mwitikio la dhati kutokana na wasikilizaji wa Paulo. Kama mistari 32-34 inavyoonyesha, baadhi yao walifanya mzaha. Wengine walienda zao tu wakaliacha zungumzo hilo. Na bado, wachache wakawa waitikadi wenye toba. Hata hivyo, acheni sisi tuwe wenye hekima kuliko walio wengi wa wasikilizaji Waathene, kwa kuwa hili ni jambo la maana kabisa ikiwa tunataka sana haki ya kweli. Ili upate maana iliyo kubwa zaidi kutokana na mstari 31, kwanza tazama kifungu cha maneno yanayosema: “Atakayowahukumu walimwengu kwa haki [“yeye anakusudia kuhukumu dunia inayokaliwa, NW].” Ni nani huyo “yeye,” na ana viwango gani, hasa kuhusu haki?

6. Sisi tunaweza kujifunzaje juu ya Mmoja ambaye ameweka siku ya kuhukumu dunia?

6 Basi, Matendo 17:30 inaonyesha Paulo alikuwa akirejezea nani​—Mungu yule yule anayeambia wote watubu, Mpaji-Uhai wetu, Muumba. Ni wazi kwamba tunaweza kujua mengi juu ya Mungu kutokana na kazi zake za uumbaji. Lakini kiwango chake cha haki kinaonekana wazi zaidi kutokana na chanzo kingine, Biblia, kilicho na kumbukumbu za maandishi yanayohusu shughuli zake na watu kama Musa na sheria za Mungu kwa Israeli.

Ni Hukumu na Haki ya Namna Gani?

7. Musa anaandaa ushuhuda gani juu ya Yehova na haki?

7 Huenda ikawa una habari kwamba kwa miongo kadhaa Musa alikuwa na shughuli za ukaribu pamoja na Yehova Mungu, za ukaribu sana hivi kwamba Mungu alisema alinena na Musa “mdomo kwa mdomo.” (Hesabu 12:8) Musa alijua jinsi Yehova alivyokuwa amemtendea, na pia jinsi Mungu alivyokuwa ameshughulika na wanadamu wengine na mataifa mazima-mazima. Karibu na mwisho wa maisha yake, Musa alitoa uelezaji huu wenye uhakikishio: “Yule Mwamba, ulio mkamilifu ni utendaji wake, kwa maana njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, ambaye kwake hakuna ukosefu wa haki; mwadilifu na mnyoofu ni yeye.”​—Kumbukumbu 32:4, NW.

8. Kwa nini tunapaswa kuangalia aliyoyasema Elihu juu ya haki?

8 Fikiria, pia, ushuhuda kutoka kwa Elihu, mwanamume aliyejulikana sana kwa hekima na ufahamivu wake. Yeye hakuwa mtu wa haraka-haraka kukata mashauri. Bali, katika kisa kimoja aliketi kwa zaidi ya juma moja akisikiliza hoja ndefu-ndefu kutoka pande zote mbili za mbishano. Sasa, kutokana na aliyojionea Elihu mwenyewe na uchunguzi wake wa njia za Mungu, yeye alikata shauri gani juu ya Mungu? Alitangaza hivi: “Nisikilizeni, enyi wenye fahamu; Mungu asidhaniwe kutenda udhalimu; wala Mwenyezi kufanya uovu. Kwani atamlipa binadamu kwa kazi yake, naye atamfanya kila mtu kuona sawasawa na njia zake. Naam, hakika, Mungu hatatenda mabaya, wala Mwenyezi hatapotosha hukumu.”​—Ayubu 34:10-12.

9, 10. Kwa nini viwango vya Mungu kwa mahakimu wanadamu vinapasa kututia moyo? (Walawi 19:15)

9 Jiulize hivi: “Je! hiyo haisimulii kikamilifu jambo ambalo sisi tungetaka kutokana na hakimu, kwamba amtendee kila mtu kulingana na vitendo au matendo yake, bila upendeleo wala kupotosha haki? Kama wewe ungelazimika kukabiliana na hakimu wa kibinadamu, je! hungehisi umetusha moyo kama angekuwa hivyo?

10 Biblia inarejezea Yehova kuwa “Hakimu wa dunia yote.” (Mwanzo 18:25, NW) Hata hivyo, nyakati fulani alitumia mahakimu wanadamu. Alitarajia nini kwa mahakimu waliomwakilisha? Katika Kumbukumbu 16:19, 20, NW, tunasoma mielekezo ya Mungu ambayo ni kama tu usimulizi kuhusu kazi ya mahakimu: “Ni lazima wewe usipotoshe hukumu. Ni lazima wewe usipendelee wala kukubali hongo, kwa maana hongo hupofusha macho ya wenye hekima na kugeuza vibaya maneno ya waadilifu. Haki​—haki ndiyo wewe unapaswa kufuatia, ili kwamba wewe upate kufuliza kuwa hai.” Huenda sanamu-umbo za ki-siku-hizi zinazofananisha Haki zikataka kujidhania zinaionyesha kuwa bila upendeleo kwa kuifunika kitambaa machoni, lakini wewe unaweza kuona kwamba Mungu alichukua hatua inayozidi hiyo. Kwa kweli alidai kimasharti kwamba mahakimu wanadamu wenye kumwakilisha wawe bila upendeleo na wafikilize sheria zake.

11. Tunaweza kukata shauri gani kwa kuzipitia habari hizi za Kibiblia juu ya haki?

11 Hayo maelezo marefu ya oni la Mungu juu ya haki yanahusu moja kwa moja upeo wa hotuba ya Paulo. Kwenye Matendo 17:31 Paulo alitangaza kwamba Mungu “ameweka siku atakayowahukumu walimwengu kwa haki [uadilifu, NW].” Hilo hasa ndilo tunaweza kutarajia kwa Mungu​—haki, uadilifu, kutopendelea. Na bado, huenda watu fulani wakahangaishwa na jambo la kwamba Mungu atatumia “mtu” ili kuhukumu wanadamu. “Mtu” huyo ni nani, nasi tuna uhakikishio gani kwamba atashika viwango bora vya Mungu vya haki?

12, 13. Tunajuaje ni “mtu” gani ambaye Mungu atamtumia kuhukumu?

12 Matendo 17:18 inatuambia kwamba Paulo alikuwa amekuwa “akihubiri habari [njema] za Yesu na ufufuo.” Kwa hiyo, mwishoni mwa hotuba yake, wasikilizaji walijua Paulo alimmaanisha Yesu Kristo aliposema Mungu ‘angehukumu walimwengu kwa haki, kwa mtu aliyemchagua na ambaye alimfufua katika wafu.’

13 Yesu alikiri kwamba Mungu alikuwa amemweka awe hakimu mwenye kutimiza kile kiwango cha kimungu. Kwenye Yohana 5:22 alisema hivi: “Tena Baba hamhukumu mtu ye yote, bali amempa Mwana hukumu yote.” Baada ya kutaja ufufuo wenye kuja wa wale walio katika makaburi ya ukumbusho, Yesu aliongeza hivi: “Mimi siwezi kufanya hata jambo moja kwa uanzilishi wangu mwenyewe; sawa na vile mimi nasikia, mimi nahukumu; na hukumu ambayo mimi natoa ni adilifu, kwa sababu mimi natafuta, si mapenzi yangu mwenyewe, bali mapenzi ya yeye ambaye alinituma mimi.”​—Yohana 5:30, NW; Zaburi 72:2-7.

14. Tunaweza kutarajia kutendewaje na Yesu?

14 Uhakikishio huo unapatana vizuri kama nini na yale tunayosoma kwenye Matendo 17:31! Hapo Paulo pia alitoa uhakikisho wa kwamba Mwana ‘angehukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa.’ Kwa uhakika hiyo haidokezi haki yoyote ya kushikilia mambo kwa ushupavu mno, bila kupindikana, na bila hisia, sivyo? Badala ya hivyo, hukumu ya haki inahusisha ndani kuchanganya haki pamoja na rehema na uelewevu. Tusisahau jambo hili: Ingawa sasa Yesu yuko mbinguni, yeye amewahi kuwa mwanadamu. Kwa hiyo anaweza kuwa na hisia-mwenzi. Kwenye Waebrania 4:15, 16 Paulo anagusia hilo anapoeleza kwamba Yesu ni kuhani mkuu.

15. Yesu anatofautianaje na mahakimu wanadamu?

15 Unaposoma Waebrania 4:15, 16, NW, fikiria kitulizo tunachopaswa kuhisi kuwa na Yesu akiwa Hakimu: “Kwa maana sisi tunaye akiwa kuhani mkuu [na hakimu], si mmoja ambaye hawezi kusikitikia udhaifu wetu, bali mmoja ambaye ametahiniwa katika mambo yote kama sisi wenyewe, lakini bila dhambi. Kwa hiyo, acheni tukaribie tukiwa na uhuru wa uneni kwenye kiti cha ufalme cha fadhili zisizostahiliwa, ili tupate rehema na kupata fadhili zisizostahiliwa kwa msaada katika wakati unaofaa.” Katika vyumba vya mahakama leo, mara nyingi inaogofya kuitwa mbele ya dawati ya hakimu. Lakini Kristo akiwa Hakimu, sisi tunaweza ‘kukaribia tukiwa na uhuru wa uneni ili tupate rehema, fadhili zisizostahiliwa, na msaada katika wakati unaofaa.’ Hata hivyo, una sababu nzuri ya kuuliza hivi kuhusiana na wakati, ‘Ni lini Yesu atakapohukumu aina ya binadamu kwa uadilifu?’

“Siku” ya Kuhukumu​—Lini?

16, 17. Tunajuaje kwamba kuhukumu kunaendelea sasa kutoka mbinguni?

16 Kumbuka Paulo alisema kwamba Mungu “ameweka siku” ya kuhukumu ulimwengu kwa Hakimu Wake mwekwa. Kwa kutazamia hiyo “siku” ya hukumu, Yesu anafanya kazi muhimu ya hukumu leo, ndiyo, sasa hivi. Kwa nini tunaweza kusema hivyo? Si muda mrefu kabla ya yeye kukamatwa na kushutumiwa kifo kwa ubandia, Yesu alitoa unabii wa kihistoria unaohusisha ndani siku yetu. Tunaupata katika Mathayo sura 24. Yesu alieleza matukio ambayo yangekitia alama kipindi kinachoitwa “umalizio wa mfumo wa mambo.” Vile vita, upungufu wa chakula, matetemeko ya dunia, na taabu kubwa nyinginezo ambazo zimetukia duniani pote tangu Vita ya Ulimwengu 1 vinashuhudiza kwamba sasa unabii wa Yesu unatimizwa na kwamba karibuni “mwisho utakuja.” (Mathayo 24:3-14, NW) Kwa miongo kadhaa Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakieleza hilo kutokana na Biblia. Ikiwa wewe ungependa ithibati zaidi ni kwa nini sisi tunajua tumo katika siku za mwisho za mfumo huu usio wa haki, Mashahidi wa Yehova wanaweza kukupa.

17 Ingawa hivyo, chunguza ile nusu ya pili ya Mathayo sura 25, iliyo sehemu ya unabii wa Yesu kuhusu siku za mwisho. Mathayo 25:31, 32 inatumika katika wakati wetu: “Wakati Mwana wa binadamu atakapowasili katika utukufu wake, na malaika wote pamoja naye, ndipo yeye ataketi juu ya kiti cha ufalme chake kitukufu [mbinguni]. Na mataifa yote yatakusanywa mbele yake, na yeye atatenganisha watu mmoja kutoka kwa mwingine, sawa na vile mchungaji hutenganisha kondoo kutoka kwenye mbuzi.” Sasa tazama pale chini ambapo Yesu anaeleza tokeo la kazi yake ya kutenganisha, au kuhukumu. Mstari 46: “Na hawa [watu ambao yeye anahukumu kuwa kama mbuzi] wataondoka wakaingie ndani ya kukatiliwa mbali kwa milele, lakini waadilifu [wale kondoo] ndani ya uhai wa milele.”

18. Kuhukumu katika wakati wetu kutaongoza kwenye nini?

18 Hivyo sisi tunaishi katika wakati muhimu sana wa hukumu. Wale ‘wanaotafuta Mungu na kumpata kikweli’ leo watahukumiwa kuwa “kondoo” ili wakaokoke mwisho wa mfumo uliopo na kuingia ndani ya ulimwengu mpya utakaofuata. Ndipo 2 Petro 3:13, NW, itakapotimizwa: “Ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo sisi tunangojea kulingana na ahadi yake, na katika hizo uadilifu utakaa.” Hiyo ndiyo “siku” yatakapotumika kikamili maneno ya Paulo kwenye Matendo 17:31, wakati wa dunia kuhukumiwa kwa uadilifu.

19, 20. Ni nani wataathiriwa na Siku ya Hukumu inayokuja?

19 Hiyo Siku ya Hukumu itahusisha ndani wengi sana kuliko hao waokokaji “kondoo,” watakaokuwa wamekwisha kuhukumiwa kuwa wanastahili kuuingia ulimwengu mpya. Kumbuka kwamba baada ya kusema Baba yake alikuwa amemkabidhi hukumu, Yesu alinena juu ya ufufuo wenye kuja. Pia, kwenye Matendo 10:42, mtume Petro alisema kwamba Yesu Kristo “ndiye aliyeamriwa na Mungu awe Mhukumu wa wahai na wafu.”

20 Hivyo basi, ‘siku iliyowekwa’ iliyotajwa kwenye Matendo 17:31 ambapo Mungu kupitia Yesu Kristo ‘atahukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa’ itakuwa wakati wa wafu kuinuliwa. Itakuwa shangwe kama nini kuona nguvu ya kimungu ikitendeshwa kazi kushinda kifo, ambacho ndicho kimekuwa mara nyingi ukosefu wa haki ulio mkubwa zaidi. Watu fulani, kama Yesu mwenyewe, wameuawa isivyo haki na serikali mbalimbali au majeshi yenye kuvamia. Wengine wamepotezewa uhai wao na matukio yasiyotazamiwa kama tufani, matetemeko ya dunia, mioto ya kiaksidenti, na maafa ya namna hiyo.​—Mhubiri 9:11.

Matatizo ya Zamani ya Ukosefu wa Haki Yatatuliwa

21. Matendo ya zamani ya ukosefu wa haki yatashindwaje katika ulimwengu mpya?

21 Wazia kuweza kuwaona wapendwa wetu wakirudishwa kwenye uhai! Hivyo wengi watapata fursa yao ya kwanza ‘kutafuta Mungu na kumpata kikweli’ kisha mbele yao wawe na “uhai wa milele” unaoweza kuwa thawabu ya walio “kondoo.” Wafufuliwa fulani, na pia waokokaji wa huu mfumo usio na haki, wamekuwa majeruhi wa mambo yanayoonekana kama kutendwa isivyo haki: kuzaliwa na kasoro za kuumbuka mwili, upofu, uziwi, au vizuizi vya uneni. Je! mambo hayo yatafaa kuwa katika ‘dunia mpya ambamo uadilifu utakaa’? Yehova alimtumia Isaya kutokeza manabii mbalimbali yatakayokuwa na utimizo mkubwa halisi wakati wa Siku ya Hukumu inayokuja. Angalia tunayoweza kutarajia: “Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.”​—Isaya 35:5, 6.

22. Kwa nini Isaya sura 65 inatia moyo sana kuhusu haki?

22 Namna gani matendo mengineyo ya ukosefu wa haki yanayosababisha huzuni nyingi sana sasa? Isaya sura 65 ina majibu fulani yanayotia moyo kwa upendezo mwingi. Ulinganisho wa Isaya 65:17 pamoja na 2 Petro 3:13, NW, unaonyesha kwamba sura hiyo inaelekeza pia kwenye wakati wa “mbingu mpya na dunia mpya,” mfumo mpya wenye uadilifu. Hata hivyo, ni nini kitazuia waovu wachache wasiharibu amani na haki? Mbele kidogo, Isaya 65 inajibu vizuri jambo hilo ambalo lingeweza kuonekana kuwa tatizo.

23. Inawezekana kwamba Siku ya Hukumu itakuwa na matokeo gani kwa watu fulani mmoja mmoja?

23 Wakati wa hii Siku ya Hukumu inayoendelea, Yesu ataendelea na kazi yake ya kuhukumu watu mmoja mmoja, kama wanastahili au hawastahili uhai wa milele. Watu fulani hawatastahili. Baada ya kupewa muda wa kutosha, labda hata “miaka mia,” ili wamtafute Mungu, watu fulani wataonyesha kwamba wanakataa kuzoea uadilifu. Kwa haki watapoteza uhai katika huo ulimwengu mpya, kama tunavyoweza kuona kutokana na Isaya 65:20: “Mtenda dhambi mwenye umri wa miaka mia atalaaniwa.” Hao wenye kuhukumiwa kuwa wasiostahili uhai watakuwa wachache. Tuna kila sababu ya kutarajia kwamba sisi​—na wengine walio wengi ​—watakuwa na upendezo wa kujifunza uadilifu na kuuzoea.​—Isaya 26:9.

24. Kutakuwako hali gani kuhusu ukosefu wa haki kiuchumi?

24 Je! hiyo inamaanisha hakuna matendo yoyote ya ukosefu wa haki yatakayokuwa yakiendelea, wala hata ya kukosa haki kiuchumi? Ndivyo hasa! Isaya 65:21-23 inaelekezea uhakika huu: “Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine; maana kama siku za mti ndivyo zitakavyokuwa siku za watu wangu, na wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi. Hawatajitaabisha kwa kazi bure, wala hawatazaa kwa taabu; kwa sababu wao ni wazazo wa hao waliobarikiwa na BWANA [Yehova, NW], na watoto wao pamoja nao.” Lo, ni tofauti kama nini na leo! We, ni baraka kama nini!

25. Wewe unatumainia nini na unapiga moyo konde kufanya nini kuhusu haki itokayo kwa Hakimu mwekwa wa Mungu?

25 Kwa sababu hiyo, wote wanaotamani sana haki ya kudumu wanaweza kujipa moyo. Itakuja pasipo shaka​—karibuni. Katika wakati mfupi uliobaki katika huu muda wa hukumu, sasa ndio wakati wa kujiunga na Mashahidi wa Yehova kumtafuta Mungu na kumpata kikweli, kwa manufaa za milele.

Maswali kwa Kupitia

◻ Tuna ithibati gani juu ya kiwango cha Mungu juu ya haki?

◻ Yesu atahusikaje katika Siku ya Hukumu inayokuja?

◻ Kwa nini wakati wetu ni wa hatari kuhusiana na hukumu ya kimungu?

◻ Ukosefu wa haki wa wakati uliopita utasahihishwaje katika ulimwengu mpya?

[Hisani katika ukurasa wa 15]

Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki