Je! Maoni Yako Binafsi Ndiyo Hutawala Yote?
“KANISA Jipya Lagawanyika Kuhusu Mapadri Wagoni-Jinsia-Moja,” kikasema kichwa kikuu cha habari. Ripoti hiyo ya habari iliendelea kufichua migawanyiko ya kina kirefu katika Kanisa la Uingereza kuhusu suala la mapadri wagoni-jinsia-moja.
“Kanisani mna nafasi ya wagoni-jinsia-moja,” akadai mhudumu mwenye daraka la kuingiza makasisi wapya kanisani. Kwa oni lake, mgoni-jinsia-moja aliye ‘mfuataji haki na mwenye kujali madaraka’ katika uhusiano wake pamoja na mwanamume mwingine ana haki ya kuagizwa rasmi.
Itikadi pinzani ya kasisi mmoja wa parokia ya kanisa ilikuwa kwamba “makasisi wanaofanya kazi wakiwa wagoni-jinsia-moja ni watenda dhambi na lazima wajiuzulu.” Yeye alihisi kwamba makasisi wanapaswa kuwa vielelezo katika mwenendo wao wote wa kiadili.—The Sunday Times, London, Novemba 8, 1987.
Bila shaka kila mmoja wa wanaume hao alisadiki kwamba oni lake lilikuwa sawa. Lakini je! oni la kibinafsi ndilo linalopasa kuwa mamlaka ya mwisho katika mambo muhimu? Labda wewe utasema ndiyo, ukishikilia kwamba “kila mtu ana haki ya kufuata maoni yake mwenyewe.”
Hata hivyo, fikiria maelezo haya mawili yaliyovuviwa yaliyo katika Biblia: “Basi kama ni hivyo, na tufuate mambo ya amani na mambo yafaayo kwa kujengana.” “Basi ndugu, nawasihi . . . kwamba nyote mnene mamoja; wala pasiwe kwenu faraka, bali mhitimu katika nia moja na shauri moja.”—Warumi 14:19; 1 Wakorintho 1:10.
Kwa hiyo, namna gani ikiwa wewe, uliye Mkristo, unaona ni vigumu kukubaliana na kundi la Kikristo juu ya jambo fulani la maana? Ungeshughulikaje na jambo hilo ili amani na umoja muhimu wa kundi uweze kudumishwa?—Mathayo 5:9; 1 Petro 3:11.
Fikiria hali moja iliyositawi katika kundi la Kikristo la karne ya kwanza wakati watu fulani walipofanya kauli yao ya kibinafsi ikawa ndiyo yenye kutawala nyingine zote. Ona jambo hilo liliongoza kwenye nini hatimaye na ujiulize hivi: ‘Mimi ningalifanya nini kama ningalikuwako?’
Masuala Kuhusu Tohara
Katika 36 W.K. ndipo kwa mara ya kwanza watu wasiotahiriwa wasio Wayahudi walikubaliwa kuingia katika kundi la Kikristo. Ingawa Mungu alikuwa amemtayarisha mtume Petro kwa ajili ya tukio hili la kutazamisha, Petro na wale waliokuwa pamoja naye walistaajabu kuona roho takatifu ikimiminwa juu ya watu wasiotahiriwa. (Matendo 10:1-16, 34-48) Wakristo wengine wengi Wayahudi waliona hilo likiwa jambo gumu kukubali. Kwa uhakika, Wakristo fulani Wayahudi, “walio [wategemezaji, NW] wa tohara,” walichambua Petro kwa kufanya ushirika pamoja na watu wasiotahiriwa.—Matendo 11:2, 3.
Kwa nini wachambuzi hao walifadhaika? Kwa sababu kwa karibu miaka 2,000, tohara ilikuwa imekuwa ishara ya kuwa na uhusiano maalumu pamoja na Mungu. Wakati Yehova Mungu alipomwamuru Abrahamu atahirishe watu wote wa kiume katika nyumba yake, Yeye alisema hivi: “Hili ndilo agano langu utakalolishika, kati ya mimi na wewe . . . milele [kwa wakati usio dhahiri, NW]” (Mwanzo 17:10-13) Karne nyingi baadaye, bado tohara ilikuwa ya maana sana kwa Wayahudi. Wengi wao walihisi kwamba kutotahiriwa kulimaanisha kutokuwa safi. (Isaya 52:1) Walihisi kwamba watu watakatifu wa Mungu hawakupaswa kufanya mishughuliko yoyote pamoja na watu wasio Wayahudi ambao hawakuwa safi wala hawakutahiriwa.
Katika 49 W.K. mtume Paulo alikabiliwa katika Antiokia ya Shamu na baadhi ya hawa ‘walio wategemezaji wa tohara.’ Mwishoni mwa safari yake ya kwanza ya umisionari, aliripotia kundi la huko jinsi Mungu alivyokuwa “amewafungulia Mataifa [wasiotahiriwa, NW] mlango wa imani.” Kwake yeye ilionekana wazi kwamba hakukuwa na uhitaji watu wa mataifa watahiriwe. Hata hivyo, watu fulani kutoka Yudea walikuwa na kauli tofauti. “Msipotahiriwa kama desturi ya Musa,” wao wakakazania, “hamwezi kuokoka.” Walihisi kwamba tohara ilihitajiwa sana kwa ajili ya wokovu na kwamba ilikuwa lazima watu wote wasio Wayahudi, ambao waliongolewa kuja kwenye Ukristo, watahiriwe.—Matendo 14:26-15:1.
Hisia kali-kali zilihusishwa ndani. Bila shaka kila mmoja angeweza kujikusanyia hoja za kuvuta wengine kwa usadikisho ili kuunga mkono oni lake. Amani na umoja wa kundi vingedumishwaje? Baada ya mazungumzo mengi juu ya habari hiyo, kundi katika Antiokia likapanga “kwamba Paulo na Barnaba na wengine miongoni mwao wapande kwenda Yerusalemu kwa mitume na wazee kwa habari ya swali [bishano, NW] hilo.” (Matendo 15:2) Hakukuwa na dokezo lolote kwamba katika jambo zito jinsi hiyo, kila mmoja alikuwa na haki ya kufuata oni lake mwenyewe. Wakristo hao walikuwa na unyenyekevu na ushikamanifu wa kutosha kuelekea utaratibu wa kitheokrasi hata watafute uamuzi wenye mamlaka kutoka baraza lao kuu la kufundishia.—1 Wakorintho 14:33, 40; Yakobo 3:17, 18; 1 Petro 5:5,6
Uamuzi Wafanywa
Mitume na wanaume wazee katika Yerusalemu (ambao kwa uwazi walitambuliwa kuwa baraza lenye kuongoza katika kundi la mapema la Kikristo) walichunguza kwa uangalifu Maandiko yaliyovuviwa kwa roho na kufanya mapitio ya kuangalia jinsi roho takatifu ilivyokuwa imeelekeza mambo kwa muda wa miaka zaidi ya 13 iliyotangulia. Uamuzi wao ukawa nini? Kwa waongofu wasio Wayahudi, tohara haikuwa takwa la lazima kwa ajili ya wokovu. (Matendo 15:6-29) Hilo sasa lilikuwa amrisho la uwazi la kuchukua mahali pa oni la kibinafsi.
Makundi yaliyotii mwongozo huu “yakatiwa nguvu katika ile Imani, hesabu yao ikaongezeka kila siku.” (Matendo 16:4, 5) Ingawa hivyo, watu fulani hawakukubali uamuzi wa baraza lenye kuongoza. Bado wao walisadiki kwamba oni lao lilikuwa sahihi na kwamba ilihitajiwa sana kufuata Sheria ya Musa kwa ajili ya wokovu. Wewe ungalifanya nini? Wao wakawa uvutano hatari wenye mgawanyiko miongoni mwa Wakristo. Angalia shauri lililotolewa na mtume Paulo muda wa miaka 15 iliyofuata akijaribu kuwapa himaya Wakristo waaminifu kutoka kwenye uvutano wa washupavu hao wenye kushikilia oni lao.
Galatia, Esia Ndogo, karibu 50-52 W.K. Uhuru uliopatwa na Wakristo kupitia dhabihu ya Yesu Kristo ulihatarishwa. Kuhofu kunyanyaswa na adui Wayahudi kulifanya Wakristo fulani watake kulazimisha maagizo yaliyotokana na Sheria ya Musa juu ya Wakristo wenzao. (Wagalatia 6:12, 13) Mtume Paulo aliwakumbusha wanafunzi kwamba kuanza kufuata mazoea ya Kiyahudi kama tohara kungekuwa kujiacha ‘wanaswe [wazuilike, NW] tena chini ya kongwa la utumwa.’ Kwa maana walikuwa watenda dhambi, hakuna wowote kati yao wangeweza kuishika Sheria kikamilifu, kwa hiyo wangeshutumiwa na Sheria, sawa na vile Wayahudi walivyoshutumiwa. Dhabihu ya Yesu tu ndiyo ingeweza kuwasafisha na kuwaokoa. “Mkitahiriwa [na hivyo mwe na wajibu wa kufanya yote yaliyo katika Sheria],” Paulo anasema, “Kristo hatawafaidia neno.”—Wagalatia 5:1-4; Matendo 15:8-11.
Korintho, Ugiriki, karibu 55 W.K. Hoja zilizohusu tohara zilikuwa zikigawanya kundi. Paulo alijua kwamba tohara yenyewe tu haikuwa dhambi. Ilikuwa imekuwa sehemu ya Sheria kamilifu ya Mungu. (Zaburi 19:7; Warumi 7:12) Paulo mwenyewe alikuwa hata amepangia Timotheo mwandamani wake kijana (ambaye mama yake alikuwa wa asili ya Kiyahudi) atahiriwe. Paulo alifanya hivyo, si kwa sababu ulikuwa wajibu, bali kwa sababu hakutaka kuwapa Wayahudi kisababishi chochote cha kujikwaa juu ya habari njema. (Matendo 16:3) Aliwatia moyo Wakristo wasijihusishe katika mzozano wenye hoja za kuvuruga amani. “Je! mtu fulani ameitwa hali amekwisha kutahiriwa?” yeye akauliza. “Asijifanye kana kwamba hakutahiriwa. Mtu fulani ameitwa hali hajatahiriwa bado? basi asitahiriwe [akifikiri kwamba hilo ni jambo muhimu kwa ajili ya wokovu].” Jambo la maana lilikuwa kutii amri za Mungu zilizo wazi, kutia na zile zinazokuja kupitia kundi la Kikristo.—1 Wakorintho 7:18-20; Waebrania 13:17.
Filipi, Ugiriki, karibu 60-61 W.K. Wale waliohisi kwamba Wakristo walikuwa wangali wamefungwa na sheria ya Kiyahudi waliendelea kupuuza ithibati hiyo ya wazi kwamba Yehova alikuwa akibariki kundi la Kikristo, ambalo sasa lilitia ndani waitikadi wengi wasiotahiriwa. Wale wenye kutetea tohara walikuwa wakisababishia wengine umizo kwa kusukumiza maoni yao ya kibinafsi ili yafuatwe. Kwa hiyo, sasa uneni ambao mtume Paulo anatumia ni thabiti zaidi: “Jihadharini na mbwa [walioonwa na Wayahudi kuwa si safi kisherehe], jihadharini na watendao mabaya, jihadharini na wajikatao [mnofu, NW].”—Wafilipi 3:2.
Krete, karibu 61-64 W.K. Mtume Paulo alikuwa amemwacha Tito awe na uangalizi wa kazi ya Wakristo katika Krete. Kwa kupendeza, Tito asiye Myahudi hakuwa ameshurutishwa kutahiriwa. (Wagalatia 2:3) Sasa Paulo alimwelekeza Tito ashughulike kwa imara na adui za ukweli, na hivyo ndivyo waendelezaji hawa wa tohara walikuwa wamekuwa. Wanapaswa hata kuondoshwa katika kundi wakizidi kutangaza peupe maoni yao ya kibinafsi yenye kuleta mgawanyiko. Yeye alinena juu ya watu “wasiotii, wenye maneno yasiyo na maana, wadanganyaji [wa akili, NW], na hasa wale wa tohara,” na akaendelea kusema: “Yawapasa wazibwe vinywa vyao. Hao wanapindua watu wa nyumba nzima, wakifundisha yasiyowapasa.”—Tito 1:10, 11; 3:10, 11; 1 Timotheo 1:3, 7.
Ni matokeo ya kuhuzunisha kama nini! Watu hao walikuwa na kiburi sana juu ya maoni yao ya kibinafsi hata wakakataa mwelekezo wa kundi la Kikristo, wakapindua imani ya wengine, na kuharibu uhusiano wao mwema pamoja na Mungu.—Linganisha Hesabu 16:1-3, 12-14, 31-35.
Wewe Utafanya Nini?
Je! sisi tunaweza kuepuka kufanya kosa hilo hilo leo? Ndiyo, ikiwa kwanza tutahakikisha kwamba oni letu la kibinafsi halipingani na fundisho lililo wazi la Biblia. Kielelezo, kuhusu ugoni-jinsia-moja Biblia inasema hivi: “Wala wasio na adili kingono . . . wala wakosaji kingono-jinsia-moja . . . hawatarithi ufalme wa Mungu.” (1 Wakorintho 6:9, 10, New International Version) Wakati ambapo huenda mwelekezo wa Kimaandiko ukaonekana na sisi kuwa uko wazi kufanyiwa maoni tofauti-tofauti, tunahitaji kuonyesha itikio la unyenyekevu lililoonyeshwa na Wakristo wa mapema na kukubali maamuzi na mielekezo kutoka kundi la Mungu. Mwisho kabisa, katika maeneo ambamo jambo si sawa wala si kosa Kimaandiko bali limeachiwa uamuzi wa kibinafsi, inatupasa tuheshimu sana kuwa na amani pamoja na wengine, hivyo tukiwa tayari kukubalia maoni mengine mara nyingi.
Je! wewe una nia ya kudhihirisha roho hiyo? Ikiwa ndivyo, unaonyesha usawaziko wa kadiri nzuri, ukitambua kwamba amani na umoja ni mambo ya thamani kubwa kuliko maoni yako ya kibinafsi.