Muono-Ndani Juu ya Habari
Elimu Isiyofaa
Kwa miaka kumi iliyopita, koleji moja katika Mkoa wa New York imekuwa ikitolea watu mtaala juu ya habari ya ujinsia wa kibinadamu ambayo inaweza kufanya wanafunzi wapate maksi za juu kiasi katika masomo matatu ya mtihani wa koleji. Wanafunzi hao “wanatakwa wafunge ‘visafari vya nje’ kwa kwenda kuongea na malaya, kuzuru nyumba za pombe zilizo na wagoni-jinsia moja au kwenda kuangalia jinsi mambo yalivyo katika fuo za bahari zilizo na watembea-uchi,” ndivyo anavyoripoti mwandikaji habari katika safu ya gazeti New York Post. Kitabu cha mafundisho ya darasa kinasemwa kuwa kinaandaa maagizo ya wazi kabisa juu ya kujihusisha katika ngono ya mdomoni na kutia moyo zoea la kupiga punyeto. Kulingana na Post, wanafunzi wanaonyeshwa filamu, iliyo sehemu ya mtaala wa darasani, iliyo na “watu wawili wawili wakifanya ngono,” na pia “migusano ya karibu-karibu ya miili ya kiume na kike.” Je! kunaweza kweli kuwako jambo lililo kinyume cha kawaida za usafi na wema kuliko hilo?—Wafilipi 4:8, 9.
Ingawa vijana wanahitaji kujua mambo ya uhakika juu ya maisha na kuwa na mwelekeo wenye afya kuyahusu, wazazi hasa ndio wenye daraka la msingi la kuandaa agizo hilo. (Mithali 22:6) Bila shaka, mtaala wowote wa shule unaotia moyo kufanya ngono nje ya ndoa na kuwataka wanafunzi waone filamu za mambo mabaya na kuchunguza ugoni-jinsia-moja na umalaya hazingekubalika kamwe kwa waabudu wa kweli wa Mungu. Biblia inawaeleza wazi wale wanaozoea uasherati (ngono kabla ya ndoa), uzinzi (ngono nje ya ndoa), na ugoni-jinsia-moja kuwa watu wenye “hamu zenye aibu za ngono,” wenye kujitia katika kilicho ‘kichafu kiadili.’ Kuhusu mambo hayo, Biblia inaamuru hivi: ‘Shikeni mwiko wa uasherati.’ Zaidi ya hilo, inaongeza hivi: “Acheni uasherati... hata usitajwe miongoni mwa nyinyi.”—Warumi 1:24-32; 1 Wathesalonike 4:3; Waefeso 5:3, 5; Wagalatia 5:19-21, NW.
Tumaini Bandia
Watu wanaotafuta “njia ya kibinafsi zaidi ya kupita” waingie katika kifo wanaepuka namna za kikawaida za maziko kwa kupendelea zoea la kikale la kuhifadhi maiti kwa kuigandisha, inaripoti The Wall Street Journal. Bei ya chini ya dola 7,500 “itawezesha mteja kuloweshwa kwa miezi miwili katika divai, miti-shamba na kemikali za hifadhi, kupakwa mafuta yenye manukato na kufungwa katika kizungushio cha kitambaa-kitani, kioo cha utembo, polithilini na plasta,” inaongezea Journal hiyo. Kwa wale wanaojifikiria kuwa watu wa maana sana kama Mafarao wa kale, machaguo wanayoweza kufanya ni pamoja na kuzungusha ganda la dhahabu au vito vya thamani juu ya majeneza ya shaba yaliyo na umbo kama la mwili kwa kulipa dola 100,000 na zaidi.
Hata hivyo, kile hasa kinachovutia wateja si jambo hilo la kwamba ni maiti za watu wachache sana zinazohifadhiwa kwa kugandishwa. Mtu mmoja mwenye kufikiria utaratibu huo alisema kwamba “ikiwa ni kweli kama Wakristo fulani wasemavyo kwamba katika Siku ya Hukumu Kristo atatuita tuinuke kutoka kaburini, basi mimi nataka kuwa katika umbo bora zaidi kadiri niwezavyo.”
Kama Wamisri wa kale walioitikadi kwamba mwili unapasa kuhifadhiwa kwa ajili ya kurudi kwa mwili katika uhai wa baadaye, kwa kawaida msingi wa matumaini hayo huwa ni fundisho la kwamba nafsi haiwezi kufa. Viongozi wa kidini wamefundisha kwamba katika Siku ya Hukumu, miili ya kila mtu mwadilifu na mwovu itaunganishwa upya na nafsi yake ili kushiriki raha mustarehe ya kimbingu au kushutumiwa adhabu ya milele katika moto wa mateso.
Hata hivyo, fundisho la uwezo wa kutokufa unaorithiwa ukiwa asili ya mtu halifundishwi katika Biblia. Badala ya hivyo, Biblia inafundisha kwamba nafsi hufa. Kwa usemi wa wazi Biblia inataarifu hivi: “Nafsi inayofanya [dh]ambi, itakufa.” (Ezekieli 18:4, ZSB) Hivyo, tumaini la Kibiblia kwa uhai wa wakati ujao linategemea, si juu ya kuokoka kifo kwa nafsi isiyoweza kufa, bali juu ya mtu kufufuliwa na Mungu akiwa na kiolezo chake mwenyewe cha uhai. Mtu atarudishwa akiwa na mwili wa kibinadamu unaofaa wenye utambulishi na kumbukumbu za utu wake peke yake sawasawa na zilivyokuwa alipokufa. Yesu angeweza kusema hivi kwa usahihi: “Saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini [makaburi ya ukumbusho, NW] wataisikia sauti yake. Nao watatoka.”—Yohana 5:28, 29.
“Si Sehemu ya Ulimwengu”
Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi Biblia na Trakti ilikutana pamoja na Baraza la Makadirio la Jiji la New York mwaka uliopita ili kuomba waruhusiwe kufanya badiliko fulani kuhusiana na ramani za ujenzi wa jengo la kukaa lenye ghorofa 19. Ingawa walio wengi wa wanabaraza (na wakaaji wa mtaa wa Brooklyn Heights) walipinga mradi huo wa ujenzi, kura mbili zilizopendelea badiliko hilo la ujenzi zilipigwa na meya wa Jiji la New York, Edward Koch. Katika taarifa ya maandishi yenye kueleza msingi wa uamuzi wake, Meya Koch alionelea kwamba “Mashahidi wa Yehova, ambao kihistoria wamenyanyaswa katika nchi nyingi kutia na Ujeremani ya Nazi, ... wamejionyesha kuwa watu tofauti sana katika United States na katika Brooklyn Heights. Kwa maoni yangu inafaa kuwaona kuwa majirani wema kabisa ... Mimi huwaheshimu kwa staha ya juu kabisa.” Halafu akaongeza hivi: “Mimi naambiwa kwamba kwa sababu za kidini wao hawapigi kura katika uchaguzi wowote unaogombewa kikura na huenda ikawa hilo ni moja la matatizo yanayohusiana na mradi huu, kwa sababu ni vigumu sana watu wasiopiga kura kupata ushindi katika ubishi ambamo maofisa waliochaguliwa wanakazwa-kazwa na idadi kubwa za watu ili wafuate maoni yao.”
Meya Koch anapongezwa kwa ushujaa wake na kutoonyesha upendeleo kwa kukabiliana na watu wengi hivyo wenye kupinga mradi huo. Ingawa huenda ikawa mambo yangalikuwa tofauti kama Mashahidi wa Yehova wangeshiriki katika machaguzi ya kisiasa, wao hawawezi kusadikishwa waache msimamo wao wa kutokuwamo katika mambo ya kisiasa—hata zawadi ya kufanya hivyo iwe kubwa kadiri gani. Mambo yako wazi kwa Wakristo wa kweli. Yesu alisema: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu.”—Yohana 17:16, NW.