Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w89 4/15 kur. 20-23
  • Babuloni Mkubwa Ashtakiwa Hatia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Babuloni Mkubwa Ashtakiwa Hatia
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Babuloni wa Ki-Siku-Hizi Analidharau Jina
  • Kwa Nini Sisi Tunakirihi Mafundisho ya Kibabuloni
  • Kwa Nini Sisi Tunakataa Falsafa Zinazopinga Mungu
  • Kwa Nini Sisi Tunakirihi Tunda la Babuloni Mkubwa
  • Kwa Nini Sisi Tunashutumu Ukosefu wa Adili wa Babuloni
  • Kwa Nini Sisi Tunakirihi Umalaya wa Kiroho wa Babuloni
  • Kwa Nini Sisi Tunachukizwa Sana na Hatia ya Damu ya Babuloni
  • Babuloni Mkubwa—Kaanguka na Kuhukumiwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Kuhukumu Kahaba Mwenye Sifa Mbaya
    Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
  • Kahaba Mwenye Sifa Mbaya Sana—Anguko Lake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Babiloni Mkubwa Ni Nani?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
w89 4/15 kur. 20-23

Babuloni Mkubwa Ashtakiwa Hatia

KATIKA mfululizo wa mikusanyiko kuzunguka ulimwengu katika 1988-89, mamilioni ya Mashahidi wa Yehova walikubali azimio lenye kuonyesha karaha yao juu ya mwenendo wa Babuloni Mkubwa, ile milki ya ulimwengu ya dini bandia​—⁠hasa kama inavyowakilishwa na Jumuiya ya Wakristo. Huenda watu fulani wenye moyo mweupe wakauliza, Je! huo si msimamo mkali mno? Sivyo, hata kidogo! Tunapoona jinsi wanabii wa Israeli ya kale walivyotoa kijasiri lawama la wazi juu ya ibada ya sanamu ya siku yao, na maneno makali ambayo Yesu alitumia kufichua unafiki wa kidini wa nyakati zake, sisi Mashahidi wa Yehova tunaitikadi kwamba msimamo huu ni wa haki kabisa. Hata unaamriwa na Mungu.​—⁠Isaya 24:​1-6; Yeremia 7:​16-20; Mathayo 23:​9-13, 27, 28, 37-39.

Kwa hiyo ni juu ya msingi gani sisi tunakirihi mwenendo wa Babuloni Mkubwa? Sisi tuna ithibati gani ya kihistoria juu ya kushindwa kwa dini kuheshimu Bwana wa kweli aliye Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote mzima, Yehova?

Babuloni wa Ki-Siku-Hizi Analidharau Jina

Bwana Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote mzima hakosi kuwa na jina. Amejitambulisha kama mara 7,000 katika Biblia kuwa yeye ni Yehova. Yeye analihesabia jina lake umuhimu mkubwa. Ya tatu ya zile Amri Kumi inataarifu hivi: “Usilitaje bure jina la Bwana [Yehova, AW], Mungu wako, maana Bwana [Yehova, AW] hatamhesabia kuwa hana hatia mtu alitajaye jina lake bure.” Na Yesu alikazia jina la Baba yake katika Sala ya Bwana, akisema, “Jina lako litukuzwe [litakaswe, AW].” ​—⁠Kutoka 20:7; Mathayo 6:9.

Kumbukumbu la matendo ya Jumuiya ya Wakristo katika kuheshimu jina la Mungu ni la kuhuzunisha. Hata Biblia ya King James ya 1611 inatumia jina Yehova, likiwa peke yalo na kwa muunganisho, mara saba tu.a Tafsiri nyingine zimeliondoa kabisa jina hilo. Dini zilizo nyingi haziliheshimu. Badala ya hivyo, wametukuza Utatu wao “mtakatifu” na, katika visa fulani, wakamtukuza Mariamu aitwaye eti Mama ya Mungu awe juu ya Mungu wa Biblia. Jina la Yehova lililo na thamani kubwa limeruhusiwa lizame liwe lisilotumiwa sana.b

Pongezi ni kwamba Uislamu hutambua Mungu mmoja, wanayemwita Allah, kwa kupatana na kitabu chao kitakatifu, Korani. Hata hivyo, wao hawatumii jina lake, Yehova, kama lilivyofunuliwa kwanza katika Biblia angalau miaka elfu mbili kabla Korani haijakuwako. Wahindu wanaabudu mamilioni ya miungu na miungu ya kike, lakini Yehova hayumo miongoni mwayo.

Inayotokeza wazi zaidi kuwa mkosaji wa kutotumia jina la Mungu ni dini ya Kiyahudi. Kwa maelfu ya miaka, Wayahudi wamedai kuwa ndio watu wa jina la Mungu, na hata hivyo kwa sababu ya pokeo lao wamesababisha jina la kweli la Mungu liache kabisa kutumiwa.

Kwa hiyo, sisi tulio mashahidi wa Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu, ni lazima tuonyeshe unyarafu wetu juu ya kupuuzwa kwa jina takatifu la Mungu kwa upande wa Babuloni Mkubwa.

Kwa Nini Sisi Tunakirihi Mafundisho ya Kibabuloni

Mamilioni ya watu wametumiwa kwa udanganyifu na kudumishwa katika hofu kwa msingi wa lile fundisho la Kibabuloni kwamba mwanadamu ana nafsi isiyokufa. Kuanzia nyakati za kale, dini bandia imetumia kwa udanganyifu hofu ya kwamba nafsi inaweza kuteswa milele katika moto wa mateso baada ya kifo. Namna iliyorekebishwa kwa ujanja zaidi ya fundisho hilo ni ule mteseko wa muda katika mioto ya pargatori. Watu wenye moyo mweupe wanatoa malipo ili Misa zisemwe kwa ajili ya wafu lakini hawapati kamwe kujua ni wakati gani malipo hayo yanapoacha kuhitajiwa kabisa! Doktrina hizo zenye makufuru hazina msingi katika Biblia.​—⁠Linganisha Yeremia 7:31.

Kwa uhakika, Biblia inafundisha kwamba mwanadamu ni nafsi inayoishi, inayoweza kufa. Kwa kutotii kwake, Adamu hakuhukumiwa kwenda kwenye moto wa mateso wala pargatori bali kwenye kifo. Kwa urahisi, “mshahara wa dhambi ni mauti.” (Warumi 6:23; Mwanzo 2:​7, 17; 3:19) Tumaini la Kimaandiko kwa wafu halitegemei juu ya msingi wa nafsi isiyokufa, bali juu ya ahadi ya Mungu ya ufufuo kwenye uhai mkamilifu katika dunia-paradiso.​—⁠Yohana 5:​28, 29; Ufunuo 21:​1-4.

Hata hivyo fundisho jingine la Kibabuloni ni ule Utatu “mtakatifu.” Fundisho hili la watu watatu katika Mungu mmoja halikupata kamwe kuwa sehemu ya imani ya Waebrania wa kale. (Kumbukumbu 5:​6, 7; 6:4) Yeye mwenyewe akiwa Myahudi, kwa uhakika Yesu hakuitikadi wala kufundisha kamwe kwamba alikuwa ndiye Mungu mweza yote. Hakudai alikuwa sehemu yoyote katika utatu fulani kama unavyofundishwa katika doktrina au fundisho la Kibabuloni lenye kushikiliwa sana.​—⁠Marko 12:29; 13:32; Yohana 5:​19, 30; 14:28; 20:17.

Kwa hiyo, sisi tunakataa doktrina za Babuloni zenye makufuru kama zinavyofundishwa katika dini bandia za ulimwengu. Sisi tunamtolea ibada Mungu mmoja wa kweli, Yehova, kupitia Mwana wake, ambaye akawa “dhabihu ya upatanishi” kwa ajili ya dhambi si za Wakristo wapakwa-mafuta tu bali pia za ulimwengu mzima wa aina ya binadamu.​—⁠1 Yohana 2:​2, NW.

Kwa Nini Sisi Tunakataa Falsafa Zinazopinga Mungu

Mapapa na makasisi wa Jumuiya ya Wakristo wanapiga mayowe kuhusu ongezeko kubwa la watu wasioamini kuna Mungu, na wengi wanalitumia kuunga mkono siasa za upande wa kulia. Hata hivyo, ni lazima swali hili liulizwe: Ni nani walioachilia kufanyika kwa matendo ya kukosa haki na usawa ambayo yalichochea mwinuko wa kuamini hakuna Mungu, hasa katika karne iliyopita? Hiyo ilitukia kwa njia ya kutokeza wazi katika makao ya Jumuiya ya Wakristo. Kwa kielelezo, Kanisa Orthodoksi la Kirusi lilikuwa limeandamana kirafiki na watawala Warusi, waliokuwa wameonea watu kikatili. Ukosefu wa thamani za kweli za Kikristo upande wa waliojionyesha kama wawakilishi wa Mungu ulichangia hali zilizositawisha sana imani ya kwamba hakuna Mungu.

Dini za Jumuiya ya Wakristo pia zimekubali kwa moyo lile fundisho la mageuzi linalomvunjia Muumba heshima. Wao wanasema kwamba kani za asili zisizo na macho ndizo zenye sifa ya kufanyiza namna zaidi ya milioni moja za uhai wa kustaajabisha sana ulio wa namna tofauti-tofauti. Kwa kweli, wanasema kwamba namna hizo tofauti-tofauti zilitokea kwa nasibu zenye manufaa. Falsafa hiyo inafanya Mungu awe asiyehitajiwa, na mwanadamu awe bila daraka la wajibu kwa mtu yeyote. Inakuwa juu ya mtu binafsi kujichagulia maadili yake. (Zaburi 14:1) Tokeo moja ni kwamba sasa visa vya kutoa mimba ni makumi ya mamilioni kila mwaka​—⁠katika nchi zinazodai kuwa za kidini!

Sisi tunakataa falsafa na mazoea haya yenye kupinga Mungu. Tunaabudu Yehova, “yule Mmoja ambaye huishi milele na milele, ambaye aliumba mbingu na vitu vilivyo ndani yayo na dunia na vitu vilivyo ndani yayo na bahari na vitu vilivyo ndani yayo.”​—⁠Ufunuo 10:6; 19:6, NW.

Kwa Nini Sisi Tunakirihi Tunda la Babuloni Mkubwa

Jumuiya ya Wakristo haikutii jumbe za kuonya yalizopewa makundi saba yaliyopangwa katika Ufunuo sura ya 2 na ya 3. Jumbe hizi zinashauri dhidi ya zoea la udhehebu-dhehebu, ibada ya sanamu, na uasherati, na dhidi ya uvuguvugu na kupuuza mambo.

Kuzuru karibu mahali popote pa ibada kutafunua ni wanadini wangapi wametukuza kiumbe juu ya Muumba. Jinsi gani? Kwa kustahi mno mifano na aikoni zao na kuabudu “watakatifu,” Madonna, na misalaba.​—⁠Linganisha Zaburi 115:​2-8; 2 Wakorintho 5:7; 1 Yohana 5:21.

Kwa habari yao, maneno ya Paulo yanapata utimizo: “Kwa sababu, walipomjua Mungu hawakumtukuza kama ndiye Mungu . . . walipumbazika; wakaubadili utukufu wa Mungu asiye na uharibifu kwa mfano wa sura ya binadamu aliye na uharibifu, na ya ndege, na ya wanyama, na ya vitambaavyo.”​—⁠Warumi 1:21-23.

Kwa Nini Sisi Tunashutumu Ukosefu wa Adili wa Babuloni

Katika miaka 20 iliyopita ugoni-jinsia-moja umekubaliwa au ukaachiliwa kuendelea ukiwa namna nyingine ya mtindo wa maisha. Mamilioni ya wagoni-jinsia-moja wamejitokeza peupe na sasa wanajipanga katika magwaride barabarani, wakionyesha wazi “Fahari ya Kujivunia Ugoni-Jinsia-Moja.” Mungu anauonaje ugoni-jinsia-moja wao?

Biblia ilitaarifu wazi hivi yapata miaka 3,500 iliyopita: “Usilale na mwanamume mfano wa kulala na mwanamke; ni machukizo.” (Walawi 18:22) Na karibu miaka 2,000 iliyopita Paulo alionyesha kwamba viwango vya Mungu havikuwa vimebadilika alipoandika hivi: “Hivyo Mungu aliwaacha wafuate tamaa zao za aibu, hata wanawake wakabadili matumizi ya asili kwa matumizi yasiyo ya asili; wanaume nao vivyo hivyo waliyaacha matumizi ya mke, ya asili, wakawakiana tamaa, wanaume wakiyatenda yasiyopasa, wakapata nafsini mwao malipo ya upotevu wao yaliyo haki yao.”​—⁠Warumi 1:​26, 27; 1 Wakorintho 6:​9, 10; 1 Timotheo 1:10.

Hata hivyo, makasisi wengi sana wa Jumuiya ya Wakristo ni wazoevu wa ugoni-jinsia-moja hivi kwamba wameweza kuimarisha kikundi cha wenye maoni ya kutetea sana ugoni-jinsia-moja katika nyingi za dini zile kubwa-kubwa. Wanadai kwamba mtindo wao wa maisha utambuliwe na kwamba wapewe cheo cha kuwa mhudumu. Kielelezo kimoja ni kile cha dhehebu la Kiprotestanti lililo kubwa zaidi Kanada, United Church of Canada, ambalo viongozi walo walipiga kura ya 205 kwa 160 siku ya Agosti 24, 1988, kwa kupendelea kuruhusu wagoni-jinsia-moja wawe wahudumu.

Kwa Nini Sisi Tunakirihi Umalaya wa Kiroho wa Babuloni

Ufunuo unalaumu wazi uasherati wa Babuloni pamoja na “wafalme wa dunia,” watawala wayo wa kisiasa. Kahaba huyu anaonyeshwa kuwa ameketi “juu ya maji mengi,” yanayomaanisha “vikundi vya watu na umati wa watu na mataifa na ndimi.” (Ufunuo 17:​1, 2, 15, NW) Kwa kuwa na uhusiano mchangamfu pamoja na watawala wa kisiasa, kwa muda wa karne zilizopita dini bandia imetumia uvutano wayo waziwazi au kwa kujificha ili kukandamiza na kuwatumia vibaya watu wa kawaida.

Vielelezo vya kutawala watu hivyo ni yale mapatano, au miafaka, ambayo Vatikani ilitia sahihi pamoja na watawala Wanazi na Wafashisti katika karne hii ya 20. Tokeo ni kwamba, uvutano wa kanisa juu ya makundi ya kondoo uliyaongoza yajitiishe kabisa kwa watawala wakatili. Katika 1929 Vatikani ilimaliza kufanya mapatano na mtawala Mfashisti aliye mtumia mabavu, Benito Mussolini. Halafu ikawaje katika Ujeremani? Kardinali Mjeremani Faulhaber anatoa muono-ndani juu ya vile papa alivyomfikiria Hitler, kwa kusema kwamba maneno yanayofuata yalinenwa na Pius wa 11: “Mimi nimefurahi; yeye ndiye kiongozi wa kwanza wa taifa kunena wazi dhidi ya Ubolshevisti [Ukomunisti].” Baadaye Faulhaber alisema hivi: “Safari yangu kwenda Roma ilithibitisha jambo ambalo labda nilishuku kwa muda mrefu. Katika Roma, Usoshalisti wa Kitaifa na Ufashisti unafikiriwa kuwa ndiyo njia pekee ya kukombolewa katika Ukomunisti na Ubolshevisti.”

Maaskofu Wakatoliki wa Ujeremani walikuwa wamepinga falsafa ya Nazi kabla ya 1933. Lakini kama anavyotaarifu mtungaji Mjeremani Klaus Scholder katika kitabu chake The Churches and the Third Reich, maaskofu waliamriwa na balozi wa Vatikani katika Ujeremani, Kardinali Pacelli, warekebishe mwelekeo wao kuhusu Usoshalisti wa Kitaifa. Jambo gani lilileta badiliko hili? Ni tazamio la kufanywa mapatano kati ya Milki ya Tatu (utawala wa Kijeremani) na Vatikani, yaliyomaliziwa Julai 20, 1933.

Klaus Scholder anaripoti hivi: “Kwenye uchaguzi na upigaji kura wa Novemba 12 [1933] Hitler alivuna matunda ya mapatano ya Milki kwa kupigiwa kura nyingi ajabu za ‘ndiyo,’ tena kati ya wachaguzi walio Wakatoliki hasa.”

Ingawa viongozi kadhaa Waprotestanti walisema maneno ya kupinga kutwaa mamlaka kwa Nazi katika 1933, muda si muda sauti zao zilipotelea katikati ya makelele ya umati wenye kutukuza taifa. Scholder anaeleza hivi: “Ilionekana wazi kwamba kanisa la Kiprotestanti lilizidi kuwa na nia ya kuacha tahadhari liliyokuwa nayo zamani na hatimaye hilo pia likawa sasa linataka kunaswa katika shauku ya kutukuza taifa. . . . Taarifa rasmi za kanisa zilitokea kwa mara ya kwanza zikiunga mkono ile Milki mpya bila kusita-sita.” Kwa uhakika, Uprotestanti ulijiuza kwenye utukuzaji taifa wa Kinazi na kuwa mtumishi wao, sawa na vile Kanisa Katoliki lilivyokuwa limefanya.

Kumbukumbu la matendo ya kihistoria linaonyesha kwamba, muda wa karne zote hizo dini bandia imeandamana kirafiki pamoja na vikundi vilivyo mashuhuri zaidi vya watawala na kuimarisha fahari yao kwa madhara ya watu wa kawaida. ‘Mwelekeo wa akili ya Kristo’ haukuonyeshwa na viongozi wa kidini walimwengu, ambao wamekuwa na njaa ya kutafuta mamlaka, mali, na utajiri. Sisi tulio Mashahidi wa Yehova, tunakirihi umalaya huo wa kiroho.​—⁠Yohana 17:16; Warumi 15:5; Ufunuo 18:3.

Kwa Nini Sisi Tunachukizwa Sana na Hatia ya Damu ya Babuloni

Katika kitabu cha Ufunuo, Babuloni Mkubwa anashtakiwa hatia kubwa sana ya damu: “Na mimi nikaona kwamba mwanamke alikuwa amelewa damu ya watakatifu na damu ya mashahidi wa Yesu. Ndiyo, katika yeye ilipatikana damu ya wanabii na ya watakatifu na ya wale wote ambao wamechinjwa juu ya dunia.”​—⁠Ufunuo 17:6; 18:​24, NW.

Historia ya dini bandia ni ya chuki na umwagaji damu, aliye na hatia kubwa zaidi ya damu akiwa ni Jumuiya ya Wakristo. Vita vya ulimwengu viwili vilianza katika makao ya yanayoitwa eti mataifa ya Kikristo. Viongozi wa kisiasa walio “Wakristo” waligeukia utumizi wa silaha katika 1914 na 1939, na makasisi katika mataifa yote yenye kushindana wakatoa baraka yao. The Columbia History of the World kinataarifu hivi kuhusu Vita ya Ulimwengu 1: “Thamani ya ukweli iliondolewa pamoja na thamani ya uhai, na hakuna hata sauti iliyopaazwa ili kuteta juu ya jambo hilo. Wale wanaopaswa kutetea neno la Mungu ndio walioongoza shime ya vita. Vita ya jumla ikaja kumaanisha chuki ya jumla.” (Italiki ni zetu.) Makasisi wa jeshini walihimiza askari wao wasonge mbele kwa juhudi kali ya kizalendo huku vijana wa pande zote mbili wakifyekwa-fyekwa na mizinga. Kitabu icho hicho cha historia kinataarifu hivi: “Kuharibu-haribu akili za wanadamu kwa shime za utukuzo wa taifa . . . kulizidi kuzuia utafutaji wa amani.”

Dini bandia ulimwenguni pote inaendelea kusababisha chuki huku mapigano yakiwaka moto kati ya Myahudi na Mwislamu, Mhindu na Mkalasinga, Mkatoliki na Mprotestanti, Mwislamu na Mhindu, Mbuddha na Mhindu. Ndiyo, dini bandia inaendelea kuchangia kumwagwa kwa damu “ya wale wote ambao wamechinjwa juu ya dunia.”​—⁠Ufunuo 18:24, NW.

Kwa sababu ya uthibitisho wote ulioonyeshwa juu, Mashahidi wa Yehova wanahisi kwamba azimio la mkusanyiko wa 1988 linafaa na ni la wakati wake. Kwa kufaa, sisi tunalaumu wazi dini bandia kuwa kahaba mwenye hatia ya damu, Babuloni Mkubwa. Tunatangazia ulimwengu njia pekee iliyo ya kweli ya kupata amani na ibada ya kweli​—⁠kugeukia Bwana Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote mzima, Yehova Mungu, kupitia Mmoja ambaye yeye alituma duniani, Kristo, au Mesiya, Yesu. Hiyo inamaanisha kukubali Ufalme wa Mungu tu kuwa ndiyo serikali adilifu na ya milele inayoweza kutosheleza mahitaji ya aina ya binadamu. Na pia inamaanisha sasa ndio wakati wa kutii amri hii: “Ondokeni katika yeye [Babuloni Mkubwa], watu wangu, ikiwa nyinyi hamtaki kushiriki pamoja na yeye katika madhambi yake, na ikiwa nyinyi hamtaki kupokea sehemu ya tauni zake.”​—⁠Ufunuo 18:4; Danieli 2:44; Yohana 17:3.

[Maelezo Chini]

a Mwanzo 22:14; Kutoka 6:3; 17:15; Waamuzi 6:24; Zaburi 83:18; Isaya 12:2; 26:4.

b Ili upate zungumzio refu juu ya umaana na umuhimu wa jina la Mungu, ona ile broshua yenye kurasa 32 Jina la Mungu Litakaloendelea Milele, iliyotangazwa kwa chapa na Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi Biblia na Trakti ya New York.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki