Wazee Litendeeni Kundi la Mungu kwa Wororo!
“Tulikuwa wapole katikati yenu, kama vile mlezi awatunzavyo watoto wake mwenyewe.”—1 WATHESALONIKE 2:7.
1. Kwa nini kila Shahidi mwaminifu-mshikamanifu wa Yehova anaweza kuhisi akiwa salama?
YEHOVA ndiye Mchungaji Mkubwa. Yeye anafanya uandalizi mwingi kwa watumishi wake walio kama kondoo naye anawaongoza “katika vipito vya uadilifu,” kwa ajili ya jina lake takatifu. Kwa sababu hiyo, wale wanaofanya penzi lake hawahitaji kuogopa kitu chochote kibaya na wanaweza kumtegemea Mungu wao mwenye huruma ili awape faraja. Kweli kweli, kila Shahidi mwaminifu-mshikamanifu wa Yehova ana sababu timamu ya kuhisi akiwa salama katika utunzaji wenye upendo wa Mungu.—Zaburi 23:1-4, NW.
2. Kwa kuonyesha utukufu wa Mungu, Yesu anaonyesha sifa gani?
2 Yesu Kristo ni “mng’ao wa utukufu [wa Mungu] na chapa ya nafsi yake.” (Waebrania 1:1-4) Kwa hiyo Yesu, Mchungaji Mwema, anaonyesha upendo na huruma pia. (Yohana 10:14, 15) Kwa kielelezo, katika pindi moja ‘aliona mkutano mkuu, akawahurumia; kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji; akaanza kuwafundisha mambo mengi.’—Marko 6:34.
3. (a) Kama Yehova Mungu na Yesu Kristo, wachungaji-wa-chini walio Wakristo wanapaswa waonyeshe sifa gani? (b) Mtume Paulo aliwapa waangalizi shauri na onyo gani?
3 Wakristo wote wanapaswa ‘kumwiga Mungu na kuendelea kutembea katika upendo sawa na Kristo alivyowapenda.’ (Waefeso 5:1, 2, JW) Kwa hiyo wanapaswa kuwa wenye upendo na huruma. Hasa inapaswa kuwa hivyo kuhusu wachungaji-wa-chini wa kundi la Mungu. Mtume Paulo alisema: “Toeni uangalifu kwa nyinyi wenyewe na kundi lote la kondoo, ambalo miongoni mwalo roho takatifu imeweka nyinyi kuwa waangalizi, kuchunga kutano la Mungu, ambalo yeye alinunua kwa damu ya Mwanaye mwenyewe. Mimi ninajua kwamba baada ya kuondoka kwangu mbwa-mwitu wenye kuonea wataingia miongoni mwenu nao hawatalitendea kundi la kondoo kwa wororo, na kutoka miongoni mwenu nyinyi watu watainuka na kusema mambo yaliyopotoshwa na kuvuta mbali wanafunzi baada yao wenyewe.”—Matendo 20:28-30, NW.
4. (a) Muda si muda, ni nini kilichotukia kulingana na onyo la Paulo kwenye Matendo 20:29, 30? (b) Ni maswali gani ambayo sasa yanastahili kufikiriwa?
4 Muda si muda, “mbwa-mwitu wenye kuonea” kwa uasi-imani wakatokea nao ‘hawakulitendea kundi kwa wororo.’ Lakini tuna nderemo iliyoje kwamba wazee walio miongoni mwa Mashahidi wa Yehova hawazoei ukatili wa aina hiyo! Hata hivyo, waamini wenzi wanaweza kutazamia kutendewaje na waangalizi hawa waliowekwa rasmi na roho? Na wawekwa hawa wanaweza kuonyeshaje ndoo za Yehova ufikirio mwororo?
Si Kupiga Ubwana Juu ya Kundi
5. (a) Mara nyingi viongozi wa kilimwengu huwatendeaje raia zao? (b) Yesu alionyeshaje kwamba ukatili hauna nafasi miongoni mwa wafuasi wake?
5 Kwa kufaa tunaweza kutazamia wazee Wakristo watutendee kwa njia yenye huruma Nao si kama watawala wa kilimwengu, ambao mara nyingi hupiga ubwana juu ya raia zao Kwa kielelezo, imeripotiwa kwamba mfalme Mfaransa Charlemagne (aliyetawala 768-814 W.K.) “aliwashurutisha Wasaksoni, wapokee ubatizo au sivyo wafe, aliwahukumu kwa adhabu kali sana walioivunja Kwaresima, na alianza kutumia nguvu kila mahali badala ya ushawishi.” (The History of the Christian Church, cha William Jones) Ukatili hauna nafasi miongoni mwa wafuasi wa Yesu, kwa kuwa yeye alisema: “Nyinyi mnajua kwamba watawala wa watu wa mataifa hupiga ubwana juu yao, na watu wao wakubwa hutawala kwa ukatili juu yao. Haipasi kuwa hivyo miongoni mwenu, bali yeyote anayetaka kuwa mkubwa miongoni mwenu ni lazima awe mtumishi wenu, na yeyote anayetaka kushika mahali pa kwanza miongoni mwenu lazima awe mtumwa wenu, sawa na Mwana wa Mtu asivyokuja kufanyiwa ungojezi, bali kuwafanyia watu wengine ungojezi, na kutoa uhai wake ili awakomboe wengine wengi.”—Mathayo 20:25-28, An American Translation.
6. (a) Kwa habari ya wazee, ni mambo gani ya msingi yanayotokeza wazi? (b) Kundi lina sababu ya kutazamia nini kutoka kwa wazee, na wanaume hawa wanapaswa kujionaje?
6 Mwanamume Mkristo ‘anayejitahidi kufikia cheo cha mwangalizi anatamani kazi nzuri.’ (1 Timotheo 3:1, NW) Tunapofikiria jambo hili na shauri la Yesu ambalo limetajwa sasa hivi, mambo haya ya msingi yanaonekana wazi: (1) Wazee Wakristo hawapaswi kutawala kwa ukatili juu ya wengine; (2) wale wanaochukua madaraka miongoni mwa wafuasi wa Yesu lazima wawe watumwa wao, si mabwana-wakubwa wao; na (3) wanaume wanaojitahidi kufikia cheo cha mwangalizi wanapaswa kuiona kuwa “kazi nzuri,” si cheo kilichokwezwa. (Mithali 25:27; 1 Wakorintho 1:31) Neno “mzee” halimkwezi mwanamume yeyote juu ya waabudu wengine wa Yehova. Bali, kundi lina sababu ya kutazamia wazee wote wawe wanaume waliokomaa kiroho, wenye ujuzi na unyenyekevu, ambao wanaongoza katika utumishi mtakatifu. Kweli kweli, wazee wapaswa wajione wenyewe kuwa watumwa wanyenyekevu wa Yehova Mungu, Yesu Kristo, na Wakristo wenzao.—Warumi 12:11; Wagalatia 5:13; Wakolosai 3:24.
7. (a) Wazee wanapaswa kutumiaje 2 Wakorintho 1:24 katika kushughulika na wengine? (b) Wazee wanapaswa wafanye nini kuhusu maagizo wanayopokea kutoka kwa Baraza Linaloongoza?
7 Kuwatumikia wengine kwa unyenyekevu kwa asili kunazuia mzee asijaribu “kupiga ubwana juu yao.” Na ni jambo zuri kama nini kwamba waangalizi wetu wanaonyesha mtazamo unaofanana na ule wa Paulo! Yeye aliwaambia Wakristo katika Korintho: ‘si sisi tulio mabwana-wakubwa wa imani yenu, bali sisi ni wafanya kazi wenzi kwa ajili ya shangwe yenu.’ (2 Wakorintho 1:24, NW) Kulingana na hayo, wale wanaotoa uangalizi wenye upendo hawalemei waamini wenzi kwa masharti ya kibinadamu yasiyohitajiwa. Bali, waangalizi walio miongoni mwa Mashahidi wa Yehova wanaongozwa na kanuni za Kimaandiko na wanatoa utumishi wenye fadhili, wenye msaada. Pia wanaonyesha kundi la kondoo za Mungu ufikirio wa kina kirefu kwa kutumia upesi maagizo yanayopokewa kutoka Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova.—Matendo sura 15.
8. Ni mtazamo gani ambao Paulo alikuwa nao kuelekea waamini wenzi, nao unapasa kuathirije wazee wa karne ya 20?
8 Kwa kuwa Paulo alikuwa na ufikirio mwororo kwa kundi la kondoo za Mungu, yeye angeweza kuwaambia hivi Wakristo katika Thesalonike: “Bali tulikuwa wapole katikati yenu, kama vile mlezi awatunzavyo watoto wake mwenyewe. Vivyo hivyo nasi tukiwatumaini kwa upendo mwingi [shauku nyororo, NW], tuliona furaha kuwapa, si Injili ya Mungu tu, bali na roho zetu pia, kwa sababu mmekuwa wapendwa wetu.” (1 Wathesalonike 2:7, 8) Paulo alitenda kama mama mlezi, anayependa watoto wake kwa kina kirefu hivi kwamba yeye anatanguliza masilahi yao mbele ya yaliyo yake mwenyewe na ana ufikirio mwororo kwao. Jinsi jambo hili linavyopaswa kuwasukuma wazee wa karne ya 20 kulitendea kundi la Mungu kwa wororo!
Vyanzo vya Msaada na Burudisho
9. Ni hali gani za watu wa kisasa wa Yehova zilizotabiriwa kwenye Isaya 32:1, 2?
9 Akielekeza kwenye siku hii ya utawala wa Ufalme unaofanywa kupitia Yesu Kristo, nabii Isaya alitabiri kwamba mfalme ‘angetawala kwa uadilifu wenyewe’ na “wana-wafalme” wangetawala “kwa haki yenyewe.” Kwa sababu hiyo, wazee walio katika tengenezo la kisasa la kitheokrasi wanashughulikia masilahi ya Ufalme wa kimbingu uliosimamishwa —utumishi ulio wa kifalme kweli kweli! Maneno zaidi ya unabii wa Isaya yanatumika kwa wanaume hawa wenye daraka: “Ni lazima kila mmoja awe kama mahali pa kujificha na upepo na mahali pa ficho kutokana na tufani ya mvua, kama vijito vya maji katika nchi isiyo na maji, kama kivuli cha jabali zito katika bara lenye kumalizwa nguvu kabisa.”—Isaya 32:1, 2, NW.
10. Kila mzee miongoni mwa Mashahidi wa Yehova anapaswa awe chanzo cha nini?
10 Tofauti na viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wenye kuonea watu, wazee walio miongoni mwa Mashahidi wa Yehova ni vyanzo vya kitulizo na burudisho. Wakiwa mabaraza ya wanaume wazee, wao wanaendeleza amani, utulivu, na usalama miongoni mwa watu wa Yehova. Kila mzee mmoja mmoja anaweza kuchangia hali hii nzuri kwa kulitendea kundi la kondoo za Mungu kwa wororo.
Kwa Haki na Uadilifu
11. (a) Ni hali gani ya ujumla iliyokuwa miongoni mwa Wakristo wa karne ya kwanza imo sana katika makundi yaliyo mengi ya Mashahidi wa Yehova leo? (b) Waangalizi wana daraka gani kuelekea kundi, na kwa nini?
11 Ijapokuwa matatizo yalizuka katika makundi fulani ya karne ya kwanza ya Kikristo, hali yayo ya ujumla ilikuwa ile ya amani, umoja, na shangwe. (1 Wakorintho 1:10-12; 3:5-9; Waefeso 1:2; Yakobo 2:1-9; 3:2-12; 4:11, 12; 1 Yohana 1:3, 4) Hali nzuri ya kiroho imo katika makundi yaliyo mengi ya Mashahidi wa Yehova leo pia kwa sababu ya baraka ya Mungu, uongozi wa Kristo, na kazi yenye uaminifu ya waangalizi waliowekwa rasmi. Ili kuhakikisha kuna amani, umoja, na shangwe ya kundi, wanaume hawa wanatafuta msaada wa kimungu nao wanajitahidi kwa bidii ya uendelevu kuliweka tengenezo la Mungu likiwa safi kiadili na kiroho. (Isaya 52:11) Tengenezo lisilo safi haliwezi kamwe kuwa na amani na shangwe, na kwa uhakika halingekuwa na upendeleo na baraka ya Mungu. Yeye ‘ni mwenye kutakata mno asiweze kuona lililo baya,’ kuvumilia utendaji makosa. (Habakuki 1:13) Miongoni mwa mambo mengine, basi, wazee wanatazamiwa kushughulikia mambo ya hukumu kwa njia nyoofu, ya Kimaandiko. Lakini ni mambo gani yanayopasa kukumbukwa wanaposhughulikia kesi hizi?
12. Ijapokuwa wazee hawatakiwi kujiingiza katika shughuli za kibinafsi ambazo hazivunji sheria au kanuni za Biblia, ni jambo gani linalopasa kufanywa kulingana na Wagalatia 6:1?
12 Kwanza, katika kesi zinazohusisha tofauti za kibinafsi, huenda ikawezekana watu mmoja mmoja watatue mambo kifaragha. (Mathayo 18:15-17) Kwa kuwa wazee si ‘mabwana-wakubwa juu ya imani yetu,’ hawatazamiwi kujiingiza katika shughuli za kibinafsi sana ambazo hazihusishi kuvunja kwa uzito sheria na kanuni za Biblia. Kwa njia ya asili, ikiwa kuna ushuhuda wa kwamba mtu ‘ameghafilika katika kosa kabla yeye hajajua juu yayo,’ wale walio na sifa za kiroho wanapaswa ‘wajaribu kumrejeza upya mtu kama huy0 kwa roho ya upole.’—Wagalatia 6:1.
13. Maandiko yanaonyeshaje kwamba wazee wanapaswa kutenda kwa kutegemea ushuhuda tu wa kwamba kosa limefanywa, wala si maneno ya kusikia tu?
13 Wazee wanapaswa kutumikia kwa “haki yenyewe,” sikuzote wakiwa wasiopendelea. Kwa hiyo wanapaswa kutenda kwa kutegemea ushuhuda wa kwamba kosa limefanywa wala si maneno ya kusikia tu. Paulo alishauri hivi: “Usikubali mashitaka juu ya mzee, ila kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu.” (1 Timotheo 5:19) Kulingana na kiwango cha Yehova, katika Israeli ya kale mtu aliyeshtakiwa kwa dhambi inayostahili kifo angeuawa ‘kwa midomo ya mashahidi wawili, au mashahidi watatu, si mmoja.’ Tena, kwa wazi mshtakiwa alikuwa na fursa ya kukabiliana na washtaki wake, na ikiwa ushuhuda ulikuwa wa kutosha, ‘mikono ya wale mashahidi ingekuwa juu yake kwanza kwa kumwua.’—Kumbukumbu 17:6, 7.
14. (a) Diotrefe alijaribu kufanya nini kimakosa? (b) Mungu anatazamia nini kuhusu wazee wanaposhughulikia mambo ya hukumu?
14 Ni lazima kuwe na msingi timamu wa Kimaandiko kwa hatua ya hukumu. Tuna nderemo iliyoje kwamba waangalizi wa makundi hawako kama Diotrefe wa karne ya kwanza W.K. mwenye majivuno! Kwa makosa yeye alijaribu “kuwatupa nje ya kundi” wale waliotaka kuwapokea ndugu wasafirio kwa ukaribishaji. Mtume Yohana hakuChukua jambo hili na matendo mengine mabaya kuwa mambo madogo tu bali alionya hivi: “Mimi nikija, mimi nitazikumbuka kazi zake.” (3 Yohana 9, 10) Hivyo, ni lazima halmashauri ya hukumu ya kisasa ihakikishe kwamba kuna msingi wa Biblia kwa hukumu yoyote ya kutenga na ushirika wanayofanya.a Bila shaka, Mungu anawatazamia wazee Wakristo watumie haki wanaposhughulika na wengine. Kweli kweli, wale wanaosimamia shughuli za tengenezo la kidunia la Yehova lazima wawe “watu walio na uwezo, wenye kumcha Mungu, watu wa kweli.”—Kutoka 18:21.
15. Ni daraka gani ambalo sala inapaswa kuwa nalo katika kesi za hukumu?
15 Kila halmashauri ya hukumu ya Kikristo inapaswa itafute msaada wa Yehova kwa sala yenye kuhisiwa moyoni. Mkutano unaofanywa pamoja na ndugu au dada ambaye ameshtakiwa kuwa amefanya kosa zito unapaswa ufUnguliwe na kufungwa kwa sala. Kwa kweli, lingekuwa jambo linalofaa kusali wakati wowote wa mazungumzo ikiwa uhitaji fulani unatokea.—Yakobo 5:13-18.
16. Wazee wanapaswa kushughulikia kesi za hukumu kwa njia gani, na kwa nini?
16 Wazee wanajua kwamba mwamini mwenzi anayeshtakiwa kuwa amefanya kosa ni “kondoo” katika kundi la Mungu na anapaswa kutendewa kwa wororo. (Linganisha Ezekieli 34:7-14.) Kondoo halisi wanahitaji utunzaji mwororo, kwa kuwa ni viumbe waoga-waoga wanaotegemea mchungaji wao kwa ajili ya ulinzi. Kwa hiyo, namna gani kondoo wa mfano katika kundi la mahali penu? Bila shaka wanahisi usalama katika utunzaji wa Mchungaji Mkubwa, Yehova Mungu, na Mchungaji Mwema, Yesu Kristo. Lakini ni lazima wachungaji-wa-chini wa kundi watende katika njia zinazochangia amani ya kindani na hisia ya usalama kwa watumishi wa Yehova walio kama kondoo. Ikiwa wewe ni mchungaji-wa-chini aliye Mkristo, basi, je! ndugu na dada zako wanahisi wakiwa salama na wenye utulivu katika utunzaji wako? Ni kweli kwamba ni lazima wazee washikilie kwa uthabiti sheria na kanuni za Biblia. Lakini Maandiko yanawataka washughulikie kondoo kwa njia yenye upendo na waendeshe kesi za hukumu katika njia ya utulivu, yenye utaratibu, fadhili, na yenye ufikirio.
17. Ni mambo gani ya Kimaandiko ambayo wazee wanapaswa wayakumbuke, hasa wakati wa kesi za hukumu?
17 Kwa kuwa hatujakamilika, “twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi” tunayosema. (Yakobo 3:2) Kila mmoja wetu anahitaji rehema ya Mungu na tunahitaji “dhabihu ya upatanisho” ya Kristo. (1 Yohana l:8–2:2, NW; Zaburi 130:3) Kwa hiyo mchungaji-wa-chini aliye Mkristo anapaswa ajione kwa unyenyekevu. Anapaswa pia akumbuke maneno ya Yesu: “Kama mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni vivyo hivyo.” (Luka 6:31) Hasa shauri hili lapasa kutumiwa wakati wa kesi za hukumu. Wanaume wenye ustahili wa kiroho wanapaswa kujaribu kurekebisha upya Mkristo mwenye kukosa ‘kwa roho ya upole, wakijiangalia wao wenyewe, wakihofu wasije wao pia wakashawishwa.’—Wagalatia 6:1, NW; 1 Wakorintho 10:12.
18. (a) Ni jambo gani ambalo linaweza kutokea ikiwa wazee wangewatendea wengine kwa ukali wakati wa kesi za hukumu? (b) Kulingana na Marko 9:42, wazee na Wakristo wengine wanapaswa wajilinde dhidi ya kufanya nini?
18 Kama wazee wangetendea wengine kwa ukali wakati wa kesi za hukumu, hiyo ingeweza kuwadhuru watu hao mmoja mmoja. Lakini hata dhara la kihisia-moyo au la kimwili lisipotokea, kungeweza kuwa na umizo zito la kiroho, na sifa za waangalizi hao zingeweza pia kutiliwa shaka. (Linganisha Yakobo 2:13.) Kwa sababu hiyo, wakati wa kesi za hukumu na nyakati nyingine zote, wazee wanapaswa wawe wenye fadhili na ni lazima wajilinde dhidi ya kukwaza wengine. Bila shaka, Wakristo wote wanapaswa kuwa waangalifu katika jambo hili, kwa kuwa Yesu alisema: “Na ye yote atakayemkosesha [atakayekwaza, NW] mmojawapo wa wadogo hawa waniaminio, afadhali afungiwe jiwe la kusagia shingoni mwake, na kutupwa baharini.” (Marko 9:42) Jiwe la kusagia lililo mahali pa juu lingekuwa kubwa sana hivi kwamba nguvu ya mnyama ilihitajika kwa ukawaida ili kuligeuza, na hakuna mtu yeyote mwenye kutupwa baharini akiwa amezungushiwa uzito huo shingoni angeweza kuokoka. Hakika, basi, mzee anapaswa kuwa mwangalifu asiwe kwazo ambalo lingeweza kutokeza dhara la kiroho lenye kudumu kwake mwenyewe na kwa mtu mmoja yeyote ambaye angekwazwa hivyo. —Wafilipi 1:9-11.
Endeleeni Kuonyesha Ufikirio Mwororo
19. Ni shauri gani ambalo Petro aliwapa wazee wenzake, na kuliitikia inavyofaa kunamaanisha nini kwa matazamio yao?
19 Mtume Petro alionyesha jinsi waangalizi wenzake wangepaswa kulichunga kundi alipoandika hivi: “Lichungeni kundi la Mungu lililo kwenu, na kulisimamia, si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari kama Mungu atakavyo; si kwa kutaka fedha ya aibu, bali kwa moyo. Wala si kama wajifanyao mabwana juu ya mitaa yao, bali kwa kujifanya vielelezo kwa lile kundi. Na Mchungaji mkuu atakapodhihirishwa, mtaipokea taji ya utukufu, ile isiyokauka.” (1 Petro 5:2-4) Kwa kutumia shauri kama hili tu na kudhihirisha ufikirio mwororo, kwa kundi la kondoo za Mungu, hapo tu ndipo waangalizi wapakwa-mafuta wanaweza kupokea thawabu yao ya kimbingu wakiwa viumbe-roho visivyoweza kufa na ndipo wazee wenye matumaini ya kidunia wanaweza kupokea uhai wa milele katika Paradiso inayokuja ya tufe lote.
20. (a) Ni lazima wachungaji-wa-chini walio Wakristo washughulike na waamini wenzi katika njia gani? (b) Wewe unahisije kuhusu utumishi wenye kielelezo kizuri na utunzaji mwororo wa wazee wenye upendo?
20 Wote wawili Yehova Mungu na Yesu Kristo ni Wachungaji wenye upendo, wenye huruma. Kwa hiyo huku wachungaji-wa-chini walio Wakristo wakiwa wanashikilia kwa uthabiti viwango vya kimungu, ni lazima waonyeshe upendo na huruma wanaposhughulika na waamini wenzao walio kama kondoo Hakika, Mashahidi wote washikamanifu wa Yehova wanathamini kwa kina kirefu utumishi wenye kielelezo kizuri wa wazee hao wenye kujidhabihu ambao wanalinda amana yao na kulitendea kundi la kondoo za Mungu kwa wororo. Uthamini huo, pamoja na staha inayofaa, unaweza kuonyeshwa kwa kuwatii wale ambao wanatoa uongozi miongoni mwetu.
[Maelezo ya Chini]
a Mtu anaweza kuomba rufani ya uamuzi wa kumtenga ikiwa anaamini kwamba kosa zito limefanywa katika kuhukumu.
Wazo Lako Ni Nini?
◻ Yesu Kristo alionyeshaje kwamba ukatili hauna nafasi miongoni mwa wafuasi wake?
◻ Wazee wanapaswa kufanya nini wanapopokea maagizo kutoka kwa Baraza Linaloongoza?
◻ Kulingana na Isaya 32:1, 2, wazee wanapaswa wawe vyanzo vya nini?
◻ Maandiko yanaonyeshaje kwamba wazee hawapaswi kutenda kwa kusikia tu?
◻ Wachungaji-wa-chini walio Wakristo wanapaswa walitendeeje kundi la kondoo?
[Picha katika ukurasa wa 18]
Sala yenye kuhisiwa moyoni ni ya muhimu wakati halmashauri ya hukumu inapokutana pamoja na mwamini mwenzi