Ni Nani Anayeweza Kuiva Rafiki ya Mungu?
WEWE unaweza kuwa rafiki ya Mungu. Miaka yapata 4,000 iliyopita, mwanamume Abrahamu aliweka imani katika Yehova Mungu. Jambo hili lilihesabiwa kwake kuwa uadilifu, na mzee huyo wa ukoo akaja kuitwa “rafiki ya Yehova.” (Yakobo 2:23, NW) Kwa hiyo ikiwa wewe una imani katika Yehova, unaweza pia kuwa rafiki ya Mungu.
Yaelekea marafiki wataalikwa kwenye mlo wakiwa wageni. Kwa kweli, sehemu ya Zaburi 23 inayojulikana sana inamwakilisha Mungu akiwa mkaribisha-wageni mwenye neema. Inasema: “Wewe [Yehova] unapanga meza mbele yangu mimi mbele ya wale wanaonionyesha mimi uhasama. . . . Kikombe changu kimejazwa vizuri.”—Zaburi 23:5, NW.
Katika pindi nyingine, mtunga zaburi yule yule—Mfalme Daudi wa Israeli ya kale—aliuliza: “Ee Yehova, ni nani atakuwa mgeni katika hema yako? Ni nani. atakaa katika mlima wako mtakatifu?” (Zaburi 15:1, NW) Kwa njia ya kitamathali, hii inamaanisha kumkaribia Yehova katika sala na ibada inayokubalika. Lo, ni pendeleo kubwa wee! Binadamu wasiokamilika wanawezaje kwa kadiri iwezekanayo kustahili kuwa rafiki na wageni wa Mungu?
Zaburi ya 15 inajibu swali hili. Inataja matakwa kumi hususa kwa wale wanaotaka kuwa rafiki na wageni wa Mungu. Acha tufikirie matakwa haya moja kwa moja, tukianzia mstari 2, (NW).
“Yeye anayetembea bila hitilafu na anayezoea uadilifu”
Wazao wa Abrahamu walisitawi sana kwa sababu Abrahamu hakuwa na hitilafu kiadili katika kutembea mbele za Yehova. (Mwanzo 17:1, 2) Nyakati nyingine “kutembea” kunamaanisha kufuatia mwendo fulani katika maisha. (Zaburi 1:1; 3 Yohana 3, 4) Kwa rafiki na wageni wa Mungu, haitoshi kuwa wa dini fulani, kufurahia majengo yayo yenye mapambo, na kushiriki katika desturi za kawaida. Si wote wanaosema “Bwana, Bwana” au kujulisha rasmi kwamba wanajua Mungu wataona shangwe ya kupata mibaraka ya Ufalme wake. (Mathayo 7:21-23; Tito 1:16) Rafiki za Yehova ‘wanatembea bila hitilafu’ machoni pake na ‘wanazoea uadilifu’ kulingana na viwango vyake.—Mika 6:8.
Hii inaondolea mbali aina yoyote ya ukosefu wa ufuataji haki, ukosefu wa adili katika ngono, na ufisadi. Mungu mwenyewe anatuambia sababu, akisema hivi: “Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu.” (1 Petro 1:16) Je! dini yako inashikamana na viwango vya juu vya Mungu, hata kuwatenga na ushirika wale wanaokataa kujipatanisha na matakwa yake? Je! unasisitizia kwamba wewe mwenyewe na jamaa yako mfuate mwenendo wa uadilifu? Ikiwa ndivyo, utatimiza takwa linalofuata kwa ajili ya rafiki na wageni wa Mungu.
“Na kunena ukweli katika moyo wake”
Ikiwa tunataka urafiki wa Mungu, hatuwezi kusema uwongo au kutumia maneno ya ujanja huku tukiwa na moyo maradufu. (Zaburi 12:2) Lazima ‘tunene ukweli katika moyo wetu,’ si kuwa nao katika midomo yetu tu. Ndiyo, tunapaswa kuwa wafuataji haki kindani na ni lazima tutoe ushuhuda wa “imani isiyo na unafiki.” (1 Timotheo 1:5) Watu fulani husema uwongo au hunena maneno ambayo ni nusu-kweli ili walinde heshima yao. Wengine wanadanganya katika mitihani ya shule au wanasema uwongo kuhusu mapato yao ili walipe kodi kidogo. Matendo kama haya yanaonyesha ukosefu wa kupenda yaliyo ya kweli. Lakini usema-kweli na matendo ya unyoofu hutoka ndani hasa ya mioyo ya rafiki za Mungu. (Mathayo 15:18-20) Wao si wenye hila wala si wadanganyifu.—Mithali 3:32; 6:16-19.
Mtume Paulo aliandika hivi: “Msiambiane uongo, kwa kuwa mmevua kabisa utu wa kale, pamoja na matendo yake; mkivaa utu mpya.” (Wakolosai 3:9, 10) Ndiyo, wale ambao kwa kweli wanasema kweli katika moyo wao wanajivika “utu mpya.” Je! wewe unafuata haki kabisa katika maoni uliyo nayo juu yako mwenyewe na juu ya wengine, huku ukinena ukweli katika moyo wako? Ikiwa unafanya hivyo, hilo linapasa kuathiri yale unayosema juu ya wengine.
“Yeye hajachongea kwa ulimi wake”
Ili takwa hili litimizwe na wageni wa Mungu, ni lazima tusinene kamwe mambo ya kudhuru wengine. (Zaburi 15:3, NW) Kitenzi cha Kiebrania kinachofasiriwa “kuchongea” kimetolewa katika neno la “wayo” na linamaanisha “kukanyaga kwa wayo” na hivyo “kuzurura.” Waisraeli waliamriwa hivi: “Usiende huko na huko katikati ya watu wako, kama mchongezi; wala usisimame kinyume cha damu ya jirani yako; mimi ndimi Bwana [Yehova, NW].” (Walawi 19:16; 1 Timotheo 5:13) Tukimchongea mtu fulani, kumnyang’anya jina lake zuri, hatuwezi kuwa rafiki za Mungu.
Daudi alijulisha wazi hivi: “Amsingiziaye jirani yake kwa siri, huyo nitamharibu [nitamnyamazisha, NW].” (Zaburi 101:5) Sisi pia tunaweza kunyamazisha wachongezi tukikataa kuwasikiliza. Na jambo zuri ni kutosema jambo lolote juu ya mtu akiwa hayupo ambalo hatungeweza kusema akiwapo. Ni jambo zuri kudhibiti ulimi wetu kwa njia hiyo. Hata hivyo, ni jambo muhimu kama nini kudhibiti vitendo vyetu pia!
“Yeye hajatenda jambo lolote baya kwa mwandamani wake”
Maneno ya Yesu yanastahili kuangaliwa hapa: “Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Ili tupate upendeleo wa Mungu, ni lazima tuepuke kutenda lililo baya. Mtunga zaburi alisema: “Enyi mmpendao Bwana [Yehova, NW], uchukieni uovu; huwalinda nafsi zao watauwa wake, na kuwaokoa na mkono wa wasio haki.” (Zaburi 97:10) Kwa hiyo ikiwa tunataka urafiki na msaada wa Mungu, ni lazima tukubali viwango vyake.
Kujiepusha na lililo baya kunatia ndani kutomkosea yeyote katika shughuli za kibiashara au katika njia nyinginezo. Katika neno na tendo, ni lazima tusitende jambo lolote ambalo litaumiza mwandamani wetu, bali twapaswa tuwe tunamtendea mambo mema. Hili linaweza kugusa kila upande wa maisha. Kwa kielelezo, tunapoendesha gari, tunaweza kuonyesha hisani kwa kuwaachia watembea-miguu haki ya kupita barabarani. Tunaweza kusaidia wazee-wazee, kuwatia moyo wenye kukata tamaa, kuwafariji wenye kihoro. Kwa habari hii, Yehova anaweka kielelezo cha kwanza. Kama alivyosema Yesu, Mungu “huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki.” (Mathayo 5:43-48) Linalofanana na kuwatendea wengine mema ni kujipatanisha na kile ambacho mtunga zaburi anataja baadaye.
“Na hakuna aibu ambayo yeye amechukua dhidi ya mfahamiani wake wa usiri”
Sisi sote tunafanya makosa, na tunakuwa wenye shukrani kama nini wakati rafiki wanapochagua kuachilia makosa yetu madogo madogo! Tungeudhika ikiwa rafiki yetu wa usiri angefunulia wengine udhaifu wetu mdogo lakini wenye kuaibisha. Watu wengine wanafanya hivyo ili wapotoshe fikira kutoka makosa yao wenyewe au wajifanye waonekane kuwa wakubwa kuliko wengine. Lakini matendo kama haya hayawafai wale wanaotaka kuwa rafiki za Mungu.
“Afunikaye kosa hutafuta kupendwa; bali yeye akashifuye neno hutenga rafiki,” inasema Mithali 17:9. Bila shaka, hatupaswi kujaribu kuficha makosa mazito. (Walawi 5:1; Mithali 28:13) Lakini ikiwa tunataka kuwa rafiki za Mungu, ‘hatutakubali’ au kupokea hadithi zenye kuaibisha juu ya wafahamiani wanyoofu kuwa za kweli. (1 Timotheo 5:19) Rafiki za Yehova wanasema mema kuhusu watumishi wa Mungu badala ya kueneza uvumi juu yao, wakiongezea yale ambayo tayari wanayavumilia kutokana na mabaya yenye kuaibisha wanayonenewa na watu wasiomcha Mungu. Rafiki na wageni wa Mungu wanalinda mashirika yao pia, kwa kuwa Daudi anaongezea hivi katika mstari 4, NW:
“Katika macho yake yeyote anayedharaulika hukataliwa hakika”
Kwa kutafuta manufaa ya kibinafsi, watu fulani wanaandamana na matajiri au watu mashuhuri hata kama ni wenye ufisadi. (Linganisha Yuda 16.) Lakini hatuwezi kuwa rafiki za Yehova ikiwa tunashirikiana na waovu. Tunapaswa kuchukia uovu sana hivi kwamba hatutaki kuwa na uenzi pamoja na wale wanaouzoea. (Warumi 12:9) Yehoramu Mfalme wa Israeli alikuwa mbaya sana hivi kwamba nabii Elisha alimwambia: “Kama Bwana [Yehova, JVW] wa majeshi aishivyo, ambaye nimesimama mbele zake, kama singemwangalia uso wake Yehoshafati mfalme wa Yuda, singekutazama, wala kuonana nawe.” (2 Wafalme 3:14) Ili tuwe rafiki za Mungu, lazima tutii onyo la Paulo: “Mazungumzo [mashirika, W] mabaya huharibu tabia njema.”—1 Wakorintho 15:33.
Ikiwa tunathamini urafiki wa Yehova, basi, tutakataa kushirikiana na watenda mabaya. Tutaendesha shughuli zinazohitajiwa tu pamoja nao. Tutachagua rafiki zetu kwa sababu ya uhusiano mwema walio nao pamoja na Mungu, wala si kwa sababu ya msimamo wao katika ulimwengu. Tutachagua rafiki kwa hekima ikiwa tuna hofu ya kumcha Mungu. Kwa habari hii, angalia takwa la saba la kutimizwa na wageni wa Mungu.
“Lakini wale wanaomhofu Yehova yeye huwaheshimu”
Ili tuwe marafiki na wageni wa Mungu, ni lazima tumhofu yeye. Inasema Mithali 1:7, NW: “Kumhofu Yehova ndio mwanzo wa marifa.” “Kumhofu Yehova” ni nini? Ni kicho chenye staha kwa Mungu na hofu nyingi inayofaa ya kutomchukiza yeye. Hii inatokeza maarifa ya kweli, nidhamu yenye kuokoa uhai, na hekima ya kimbingu ambayo ni mwongozo hakika.
Wale wanaomhofu Yehova wanashikamana na viwango vyake vya uadilifu hata kama hili linatokeza dhihaka. Kwa kielelezo, wengi wa nadhihaki wakati wale wanaomhofu Mungu wanapofanya kazi kwa bidii, wanapofuata haki kazini, au wanapotafuta kuwasaidia wengine kiroho. Lakini mtu mmoja mmoja anayemcha Mungu anawaonaje watu hawa wanyoofu? ‘Yeye anawaheshimu wale wanaomhofu Yehova,’ akiwastahi sana, hata kama kufanya hivyo kunamaanisha kuaibishwa pa. moja nao. Je! wewe una staha ya namna hii kwa wale wanaomhofu Mungu? Akitaja takwa jingine la kupata upendeleo wa kimungu, mtunga zaburi anaongezea hivi:
“Yeye ameapa kwa lililo baya kwa ajili yake mwenyewe, na bado yeye halibadili”
Kanuni iliyo hapa ni ile ya kutimiza ahadi zetu, kama Mungu anavyofanya. (1 Wafalme 8:56; 2 Wakorintho 1:20) Hata kama baadaye tunapata kwamba kufanya lile tuliloahidi ni kugumu sana, hatupaswi kubadili nia yetu na kuruka ahadi yetu. Hapa maandishi ya Septuagint ya Kigiriki, Peshitta ya Kisiria, na Vulgate ya Kilatini yanasema, “amemwapia jirani yake.” Tukiapa kufanya jambo fulani au kutoa nadhiri inayofaa, tunapaswa tuitimize. (Mhubiri 5:4) Bila shaka, tukipata kujua kwamba jambo fulani tuliloahidi kufanya halipatani na Maandiko, hatupaswi kulifanya.
Yoshua hakuvunja agano lake pamoja na Wagibeoni hata alipopata kujua baadaye kwamba walikuwa wamemdanganya ili alifanye. (Yoshua 9:16-19) Kwa hiyo tunapaswa kuwa wanaume, wanawake, na vijana wanaoshikilia neno lao. Tusiwaahidi wengine mambo kisha tuwaache katika shida wakati fursa nyingine zenye kuvutia sana zinapotokea kwetu. Yesu alisema: “Bali maneno yenu yawe Ndiyo, ndiyo; Siyo, siyo.” (Mathayo 5:37) Hasa wale ambao wamejitoa wakfu kwa Yehova wanapaswa kupiga moyo konde ili waishi kulingana na ahadi yao ya kumtumikia milele wakiwa Mashahidi wake. Zaidi ya kutimiza ahadi zetu, tunapaswa kuwa waangalifu katika mambo ya kifedha, kama Daudi anavyoonyesha kwenye Zaburi ya 15, mstari 5, NW.
“Pesa zake yeye hajatoa apate faida”
Pesa ambazo zinakopeshwa kwa makusudi ya kibiashara zinaweza kwa kufaa kulipiwa kwa faida. Lakini hapa Daudi alimaanisha ‘kuwatolea pesa’ walio maskini sana. Sheria ya Musa ilieleza: “Ukimkopesha mtu aliye maskini, katika watu wangu walio pamoja nawe; usiwe kwake mfano wa mwenye kumdai; wala hutamwandikia faida.” (Kutoka 22:25; Walawi 25:35, 36) Nehemia alipowapata walio maskini sana wakiteseka wakiwa majeruhi wa wala-riba, yeye alikomesha unyonyaji huo.—Nehemia 5:1-13.
Kwa neno “faida,” Daudi alitumia neno la Kiebrania linalotokana na jingine linaloonyesha “kuuma.” Hili linadokeza kwamba wala-riba wenye pupa walikuwa wakinyafua maskini na kiasi kidogo walichokuwa nacho. Kwa uwazi, ni afadhali zaidi kuwasaidia wanaokumbwa na umaskini bila kutazamia kulipwa chochote. Yesu alisema jambo linalofanana na hili aliposema: “Ufanyapo chakula cha mchana au cha jioni, . . . waite maskini, vilema, viwete, vipofu, nawe utakuwa heri [mwenye furaha, NW], kwa kuwa hao hawana cha kukulipa; kwa maana utalipwa katika ufufuo wa wenye haki.” (Luka 14:12-14) Mtu anayetaka kuwa rafiki na mgeni wa Mungu hangetaka kamwe kujifaidi isivyofaa na maskini wa jirani yake na angejipatanisha na lile ambalo mtunga zaburi anaendelea kutaja.
“Na yeye hakuchukua rushwa dhidi ya asiye na hatia”
Rushwa ina uvutano wenye kufisidi. Waisraeli waliamriwa hivi: “Usitwae rushwa; kwa kuwa rushwa hupofusha macho ya wenye akili, na kugeuza daawa ya wenye haki.” (Kumbukumbu 16:19) Ni jambo ovu hasa kuchukua rushwa ili kumwumiza “asiye na hatia,” labda kwa kubadili ushuhuda wa mahakama. Yuda Iskariote alikuwa mbaya kama nini kukubali rushwa ili amsaliti Yesu asiye na hatia!—Mathayo 26:14-16.
Tunaweza kujiona wenyewe tukiwa bila hitilafu katika jambo hili. Lakini je! tumepata kujaribu kujiondoa katika hali inayofadhaisha kwa kutoa pesa? Nabii Samweli hakukubali kamwe “rushwa” au hongo. (1 Samweli 12:3, 4) Sisi sote lazima tujiendeshe katika njia hiyo ikiwa tutakuwa rafiki na wageni wa Mungu.
“Yeye ambaye anatenda mambo haya hatafanywa kamwe atikisike”
Baada ya elezo layo lenye mambo kumi kuhusu mtu mnyoofu, Zaburi ya 15 inamalizia kwa maneno ambayo yametangulia. Haya yanaweza kutufanya tuchanganue dini yetu. Ikiwa ndiyo imani ya kweli, yapaswa itufundishe (1) kutembea bila hitilafu na kuzoea uadilifu, (2) kunena ukweli hata katika moyo, (3) kuepuka kuwachongea wengine, na (4) kuepuka kutenda jambo lolote baya. Dini inayokubalika kwa Mungu (5) itatuzuia tusiwaaibishe wafahamiani wanyoofu na (6) itatufanya tuepuke ushirika pamoja na watu wenye kudharaulika. Imani ya kweli itatuchochea (7) tuwaheshimu wale wanaomhofu Yehova, (8) tutekeleze yale ambayo tumeahidi kufanya ikiwa yanafaa, (9) kuwapa walio maskini bila kutaka faida, na, (10) kutochukua rushwa kamwe dhidi ya mtu asiye na hatia.
Daudi hasemi kwamba mtu yeyote anayesoma, kusikia, kusema, au hata kuamini mambo haya “hatafanywa kamwe atikisike.” Jambo hili litampata tu mtu yule “ambaye anatenda mambo haya.” Imani pasipo matendo ya kuitegemeza imekufa na haitokezi kibali cha kimungu. (Yakobo 2:26) Wale wanaotenda mambo mazuri yanayotajwa katika Zaburi ya 15 hawatatikisika, kwa kuwa Yehova atawalinda na kuwategemeza.—Zaburi 55:22.
Bila shaka, kuna mengi zaidi yanayohusika katika ibada safi kuliko mambo haya kumi ambayo yametajwa katika Zaburi ya 15. Baadaye wafuasi wa Yesu walijifunza mambo mengine juu ya kuabudu Mungu “katika roho na kweli.” (Yohana 4:23, 24) Wewe pia unaweza kujifunza, kwa kuwa watu wanaotenda mambo haya wapo leo. Kushiriki pamoja na hawa Mashahidi wa Yehova kwa ukawaida na funzo la Biblia kutajenga tumaini la uhai katika paradiso ya kidunia ambamo unaweza kuwa mgeni na rafiki ya Mungu milele.