Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w89 12/15 uku. 15
  • Yehova Ndiye Msaidiaji Wangu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Ndiye Msaidiaji Wangu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Katika Uhitaji wa Kutaka Msaada wa Yehova
  • Upendo wa Kidugu kwa Vitendo
  • Uwe Mwenye Ukaribishaji-Wageni
  • Wakumbuke Wale Wenye Kunyanyaswa
  • Lazima Ndoa Iheshimiwe
  • Kuridhika na Mambo ya Sasa
  • Mtumaini Yehova
  • Toeni Dhabihu Ambazo Zampendeza Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Azimia Kuendeleza ‘Upendo Wako wa Kindugu’!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
  • Toa Ushahidi kwa Ajili ya Yehova na Usichoke
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Wakati Msiba wa Ulimwengu Ukaribiapo—‘Mfikirie Yesu’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
w89 12/15 uku. 15

Yehova Ndiye Msaidiaji Wangu

“Mwe wenye moyo mkuu na kusema: ‘Yehova ndiye msaidiaji wangu; mimi sitaogopa. Mwanadamu aweza kunifanya nini?’”—WAEBRANlA 13:6, NW.

1, 2. (a) Mtunga zaburi na mtume Paulo walionyesha uhakika gani katika Yehova? (b) Ni maswali gani ambayo yazuka?

YEHOVA MUNGU ni chanzo kisichoshindwa cha msaada. Mtunga zaburi alijua jambo hili kutokana na mambo yaliyompata naye angeweza kusema: “Yehova yuko upande wangu, mimi sitaogopa. Mwanadamu wa dunia aweza kunifanya nini?” (Zaburi 118:6, NW) Mawazo ya moyoni yaliyo kama hayo yalielezwa na mtume Paulo alipowaandikia Wakristo Waebrania barua yake iliyovuviwa kimungu.

2 Yaelekea akinukuu maneno ya mtunga zaburi kutoka Septuagint ya Kigiriki, Paulo aliwaambia waabudu wenzi Waebrania: ‘Mwe wenye moyo mkuu na kusema: “Yehova ndiye msaidiaji wangu; mimi sitaogopa. Mwanadamu aweza kunifanya nini?”’ (Waebrania 13:6, NW) Kwa nini mtume aliandika kwa njia hii? Nasi twaweza kujifunza nini kutokana na habari zenye kuzunguka mstari huu?

Katika Uhitaji wa Kutaka Msaada wa Yehova

3. (a) Yehova alithibitika kuwa Msaidiaji wa Paulo chini ya hali gani? (b) Kwa nini Wakristo Waebrania hasa walihitaji Yehova awe Msaidiaji wao?

3 Paulo alikuwa shahidi mwenye kujidhabihu aliyekuwa na ushuhuda wa kuthibitisha kwamba Yehova alikuwa Msaidiaji wake. Mungu alimsaidia mtume alipokabili magumu mengi. Paulo alikuwa amewekwa gerezani, akachapwa, na kupigwa kwa mawe. Alivunjikiwa merikebu na pia akapatwa na hatari nyingine nyingi katika safari zake akiwa mhudumu Mkristo. Alijua sana kutoa jasho, kukosa usingizi usiku, njaa, kiu, na hata uchi. “Baghairi ya mambo ya nje,” akasema, “yako yanijiayo kila siku, ndiyo maangalizi ya makanisa [makundi, NW] yote.” (2 Wakorintho 11:24-29) Paulo aliwahangaikia hivyo Wakristo Waebrania. Siku za Yerusalemu zilikuwa zimepunguzwa, na ndugu na dada Wayahudi wa mtume huyo waliokuwa Yudea wangekabili mitihani mikubwa ya imani. (Danieli 9:24-27; Luka 21:5-24) Kwa hiyo wangehitaji kuwa na Yehova akiwa Msaidiaji wao.

4. Ni mawaidha gani ya msingi yatolewa katika barua yote waliyoandikiwa Waebrania?

4 Akifungua barua yake kwa Wakristo Waebrania, Paulo alionyesha kwamba msaada wa kimungu ungepatikana tu ikiwa wangemsikiliza Mwana wa Mungu, Yesu Kristo. (Waebrania 1:1, 2) Habari hii ilikuzwa katika barua hiyo. Mathalani, ili ategemeze shauri lake, mtume aliwakumbusha wasomaji wake kwamba Waisraeli waliadhibiwa kwa kutotii katika jangwa. Wakristo hao Waebrania hawangeepuka adhabu ikiwa wangeyakataa yale ambayo Mungu aliwaambia kupitia Yesu na wawe waasi-imani wakishikilia Sheria ya Musa ambayo ilikuwa imewekwa kando kupitia dhabihu ya Kristo!—Waebrania 12:24-27.

Upendo wa Kidugu kwa Vitendo

5. (a) Barua waliyoandikiwa Waebrania yaandaa shauri gani jingine? (b) Paulo alisema nini kuhusu upendo?

5 Barua waliyoandikiwa Waebrania iliwapa shauri wale waliotazamiwa kuwa warithi wa Ufalme wa kimbingu kuhusu jinsi ya kufuata Kiolezo chao, Yesu Kristo, ‘kutoa utumishi mtakatifu wakiwa na hofu na kicho cha kimungu,’ na kumfanya Yehova awe Msaidiaji wao. (Waebrania 12:1-4, 28, 29, NW) Paulo aliwahimiza waamini wenzi wakutane kwa ukawaida na ‘kuchochea mmoja na mwenzake kwenye upendo na kazi nzuri.’ (Waebrania 10:24, 25, NW) Sasa akatoa shauri hivi: “Acheni upendo wenu wa kidugu uendelee.”—Waebrania 13:1, NW.

6. Ni katika maana gani Yesu aliwapa wafuasi wake “amri mpya” kuhusu upendo?

6 Yesu alitaka wafuasi wake wawe na upendo huo, kwa kuwa yeye alisema: “Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo. Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:34, 35) Hii ilikuwa “amri mpya” katika maana ya kwamba ilitaka mengi zaidi ya Sheria ya Musa, ambayo ilisema: “Umpende jirani yako kama nafsi yako.” (Walawi 19:18) “Amri mpya” ilitaka mengi kuliko mtu kumpenda jirani yake kama ajipendavyo mwenyewe. Ilitaka upendo wa mtu kujidhabihu kufikia kuutoa uhai wake kwa ajili ya mtu fulani. Maisha na kifo cha Yesu vilitolea kielelezo upendo wa namna hiyo. Tertullian alitaja kijuu-juu alama hii ya utambulishi aliponukuu maneno ya walimwengu kuhusu Wakristo na kusema: “‘Tazama,’ wao husema, ‘jinsi wanavyopendana mmoja na mwenzake . . . na jinsi walivyo tayari kufiana mmoja na mwenzake.’”—Apology, sura 39, 7.

7. Upendo wa kidugu ulionekanaje wazi baada ya Pentekoste 33 W.K.?

7 Upendo wa kidugu ulionekana wazi miongoni mwa wanafunzi wa Yesu baada ya Pentekoste 33 W.K. Ili waamini wengi waliobatizwa karibuni tu wa kutoka sehemu za mbali waweze kukaa katika Yerusalemu muda mrefu zaidi na kujifunza mengi juu ya uandalizi wa Mungu kwa ajili ya wokovu kupitia Kristo, “wote walioamini walikuwa mahali pamoja, na kuwa na vitu vyote shirika, wakiuza mali zao, na vitu vyao walivyokuwa navyo, na kuwagawia watu wote kama kila mtu alivyokuwa na haja.”—Matendo 2:43-47; 4:32-37.

8. Kuna uthibitisho gani kwamba upendo wa kidugu umo miongoni mwa Mashahidi wa Yehova leo?

8 Upendo wa kidugu wa namna hiyo umo miongoni mwa Mashahidi wa Yehova katika wakati wetu. Mathalani, baada ya Vita ya Ulimwengu 2, upendo huo uliwasukuma watu wa Mungu wafanye kampeni ya miaka miwili na nusu ya kutoa msaada. Mashahidi katika Kanada, Sweden, Switzerland, United States, na mabara mengine walichanga nguo na pesa za kununulia waamini wenzao chakula katika nchi zilizokumbwa na vita, za Austria, Ubelgiji, Bulgaria, China, Chekoslovakia, Denmark, Uingereza, Finland, Ufaransa, Ujeremani, Ugiriki, Hangari, Italia, Uholanzi, Norowei, Ufilipino, Polandi, na Romania. Hiki ni kielelezo tu, kwa kuwa hivi karibuni watumishi wa Mungu wamewaonyesha upendo wa namna hiyo Wakristo waliojeruhiwa na matetemeko ya dunia katika Peru na Meksiko, dhoruba katika Jameika, na maafa kama hayo katika sehemu nyingine. Katika njia hii na nyingine nyingi, watu wa Yehova ‘huacha upendo wao wa kidugu uendelee.’

Uwe Mwenye Ukaribishaji-Wageni

9. (a) Ni sifa gani ya kimungu yatajwa kwenye Waebrania 13:2? (b) Watu fulani ‘walikaribishaje malaika’ pasipo kujua?

9 Ndipo Paulo akataja sifa nyingine ambayo hudhihirishwa na wale wenye kumfuata Kristo, ‘wakitoa utumishi mtakatifu wakiwa na hofu na kicho cha kimungu,’ na kumfanya Yehova awe Msaidiaji wao. Yeye alihimiza hivi: “Msisahau kuwafadhili wageni [ukaribishaji-wageni, NW]; maana kwa njia hii wengine wamewakaribisha malaika pasipo kujua.” (Waebrania 13:2) Ni nani ambao ‘waliwakaribisha malaika’ pasipo kujua? Basi, mzee wa ukoo Abrahamu alikaribisha malaika watatu. (Mwanzo 18:1-22) Wawili wao waliondoka, na Loti mpwa wake akaalika wageni hawa wawili kwenye nyumba yake katika Sodoma. Hata hivyo, kabla hawajaenda kupumzika, nyumba ya Loti ilizingirwa na wanaghasia, “vijana kwa wazee.” Walidai kwamba Loti awatoe wageni wake kwa makusudi yasiyo ya adili, lakini yeye akakataa katakata. Ijapokuwa Loti hakujua mwanzoni, alikuwa amekaribisha malaika, ambao walimsaidia yeye pamoja na binti zake waepuke kifo wakati ‘Yehova aliponyesha juu ya Sodoma na juu ya Gomora kiberiti na moto toka mbinguni.’—Mwanzo 19:1-26.

10. Wakristo wakaribishaji-wageni hupata shangwe ya kuwa na mibaraka gani?

10 Wakristo wakaribishaji-wageni hupata shangwe ya kuwa na mibaraka mingi. Wao husikia maono yenye kujenga yakisimuliwa na wageni wao na kunufaika na ushirika wao wenye kuthawabisha kiroho. Gayo alipongezwa kwa kuwapokea waamini wenzi kwa ukaribishaji-wageni, “tena wakiwa ni watu asiowajua,” sawa na vile wengi wa watu wa Yehova hukaribisha waangalizi wasafirio sasa. (3 Yohana 1, 5-8, NW) Kuwa mkaribishaji-wageni ni sifa moja ya kuwekwa rasmi kuwa mzee. (1 Timotheo 3:2; Tito 1:7, 8) Pia yastahili kuangaliwa kwamba Yesu aliahidi mibaraka ya Ufalme kwa watu mmoja mmoja wa mfano wa kondoo ambao waliwatendea mema “ndugu” zake wapakwa-mafuta.—Mathayo 25:34-40.

Wakumbuke Wale Wenye Kunyanyaswa

11. Kwa nini shauri la Waebrania 13:3 lilifaa?

11 Wale wanaotamani kupata msaada wa Yehova na ‘kutoa utumishi mtakatifu wakiwa na hofu na kicho cha kimungu’ ni lazima wasisahau waamini wenzi wanaoteseka. Paulo alielewa magumu waliyovumilia Wakristo waliotendwa vibaya. Mapema wakati fulani, wanafunzi walikuwa wametawanyika kwa sababu ya mnyanyaso, na mfanya-kazi mwenzake Timotheo alikuwa ndipo amefunguliwa kutoka gerezani. (Waebrania 13:23; Matendo 11:19-21) Wamisionari Wakristo walikuwa wakisafiri pia na kufanyiza makundi mapya au kujenga kiroho yale yaliyokuwako. Kwa kuwa wengi wa akina ndugu na dada waliokuwako wakati huo walikuwa Wasio Wayahudi, huenda Wakristo fulani Waebrania wakawa hawakuwahangaikia vya kutosha. Basi, shauri hili lilifaa: “Wakumbukeni hao waliofungwa kana kwamba mmefungwa pamoja nao; na hao wanaodhulumiwa, kwa vile ninyi nanyi mlivyo katika mwili.”—Waebrania 13:3.

12. Twaweza kutumiaje shauri la kuwakumbuka waamini wenzetu wenye kutendwa vibaya?

12 Waebrania walikuwa ‘wamewaonea huruma wale waliokuwa katika vifungo’ lakini hawakupaswa kusahau hao waabudu wenzi waaminifu, wawe walikuwa Wayahudi au Wasio Wayahudi. (Waebrania 10:34) Lakini namna gani sisi? Twaweza kuonyeshaje kwamba twawakumbuka Wakristo wenye kutendwa vibaya? Katika visa fulani huenda ikafaa tuandike barua ya kuomba rufani kwa wenye mamlaka serikalini kwa jitihada ya kusaidia waamini wenzi waliofungwa gerezani kwa sababu ya imani yao katika mabara ambamo kazi ya kuhubiri Ufalme imepigwa marufuku. Hasa twapaswa kuwakumbuka katika sala zetu, hata kuwataja wengine kwa jina, ikiwezekana. Mnyanyaso wao hutuathiri kwa kina kirefu, na Yehova husikiliza maombi yetu ya bidii kwa ajili yao. (Zaburi 65:2; Waefeso 6:17-20) Ingawa hatumo katika chumba kimoja cha gereza, ni kana kwamba tumefungwa pamoja nao na twaweza kutoa msaada na kitia-moyo. Kwa uhakika Wakristo waliozaliwa kwa roho huwahurumia wapakwa-mafuta wenye kutendwa vibaya. (Linganisha 1 Wakorintho 12:19-26.) Vilevile wao huhangaikia waandamani wao wenye kunyanyaswa walio na matumaini ya kidunia, ambao pia hutendwa ubaya wa aina mbalimbali mikononi mwa wanyanyasi. Yafaa kuwa na hisia-mwenzi hiyo, kwa kuwa sisi sote tungali katika mwili wa kibinadamu na twaweza kupata mateso na mnyanyaso tukiwa waabudu wa Yehova.—1 Petro 5:6-11.

Lazima Ndoa Iheshimiwe

13. Kwa maana halisi, Paulo alisema nini kwenye Waebrania 13:4?

13 Kufuata kielelezo cha Kristo na ‘kutoa utumishi mtakatifu tukiwa na hofu na kicho cha kimungu’ kwapasa kuathiri hangaiko letu kwa wengine katika njia nyingi. Akiisha kusema kwamba ‘ninyi nanyi mmo katika mwili,’ Paulo alitaja uhusiano wenye upande wa kimwili, ambao ulitoa fursa ya kuwafikiria wengine kwa njia ifaayo. (Waebrania 13:3) Aliwapa Wakristo Waebrania onyo hili la upole: “Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi; kwa maana waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu.” (Waebrania 13:4) Shauri hili lafaa kama nini, kwa kuwa ukosefu wa adili katika ngono ulikuwa umeenea katika Milki ya Roma! Wakristo wa siku hizi wahitaji pia kutii maneno haya kwa sababu viwango vya maadili ya ulimwengu ni vya hali ya chini na kwa sababu ya uhakika wa kwamba kila mwaka maelfu hutengwa na ushirika wa kundi kwa ukosefu wa adili katika ngono.

14. Kwa nini ungesema kwamba ndoa inaheshimika?

14 Miongoni mwa wale ambao hawakuiona ndoa kwa staha walikuwa Waesene wa wakati wa Paulo. Kwa kawaida wao walikuwa waseja waliofungwa na nadhiri ya kuepuka ndoa, kama makasisi fulani leo ambao hufikiria kimakosa kwamba nadhiri ya useja ni takatifu kuliko kifungo cha ndoa. Hata hivyo, kwa yale ambayo Paulo aliwaambia Wakristo Waebrania, yeye alionyesha waziwazi kwamba ndoa inaheshimika. Kuheshimiwa kwayo kulionekana wazi wakati Naomi alipowatolea ombi hili binti wakweze waliokuwa wajane, Ruthu na Orpa: “Yehova na afanye zawadi kwa ajili ya nyinyi, na nyinyi pateni mahali pa pumziko kila mmoja katika nyumba ya mume wake.” (Ruthu 1:9, NW) Katika mahali pengine, Paulo mwenyewe alionyesha kwamba ‘nyakati za mwisho wengine wangejitenga na imani, wakiwazuia watu wasioe.’—1 Timotheo 4:1-5.

15. Ni nani waliotajwa kuwa waasherati na wazinzi kwenye Waebrania 13:4, na Mungu angewahukumuje?

15 Waebrania ambao walikuwa katika Sheria wakati mmoja lakini wakaingizwa katika agano jipya waliijua amri hii: “Usizini.” (Kutoka 20:14) Lakini wao walikuwa katika ulimwengu wenye kukosa adili na walihitaji onyo: “Malazi yawe safi; kwa maana waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu.” Walio miongoni mwa waasherati hao ni watu wasiofunga ndoa wenye kufanya ngono. Wazinzi hasa ni watu mmoja mmoja waliofunga ndoa wenye kujamiiana na wale ambao si wenzi wao, wakichafua kitanda chao wenyewe cha ndoa. Kwa kuwa wazoeaji wasiotubu wa uasherati na uzinzi wastahili hukumu kali ya Mungu, hawataruhusiwa kuingia katika Yerusalemu Mpya ya kimbingu wala kushangilia uhai milele katika dunia chini ya utawala wa Ufalme. (Ufunuo 21:1, 2, 8; 1 Wakorintho 6:9, 10) Onyo hili la kutochafua kitanda cha ndoa lapasa pia kuwafanya Wakristo waliofunga ndoa waepuke kufanya pamoja na wenzi wao mwenendo wa ngono ambao ni wenye kuchafua, ingawa hakuna ubaya wowote wa kuwa na uhusiano wa kimwili wenye vitendo vya usiri ufaao katika ndoa.—Ona Mnara wa Mlinzi, Januari 1, 1984, kurasa 3-7.

Kuridhika na Mambo ya Sasa

16, 17. Ni nini kilichosemwa kwenye Waebrania 13:5, na kwa nini Waebrania walihitaji shauri hili?

16 Tutaridhika tukifuata Kiolezo wetu na ‘kutoa utumishi mtakatifu tukiwa na hofu na kicho cha kimungu,’ tukiwa na uhakika kwamba Yehova ni Msaidiaji wetu. Kujihusisha sana katika ufuatiaji wa vitu vya kimwili kwaweza kuwa kishawishi kikubwa. Lakini Wakristo hawapaswi kutumbukia ndani yacho. Waebrania waliambiwa hivi: “Msiwe na tabia ya kupenda fedha; mwe radhi na vitu mlivyo navyo; kwa kuwa yeye mwenyewe amesema, Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa.” (Waebrania 13:5) Kwa nini Waebrania walihitaji shauri hili?

17 Labda Waebrania walihangaikia pesa mno kwa sababu walikumbuka “njaa kubwa” iliyokuwako katika utawala wa Kaisari Klaudio (41-54 W.K.). Njaa hiyo ilikuwa mbaya sana hivi kwamba Wakristo waliokuwa katika sehemu nyingine waliwapelekea msaada ndugu zao katika Yudea. (Matendo 11:28, 29) Kulingana na mwanahistoria Myahudi Yosefo, njaa hiyo iliendelea kwa miaka mitatu au zaidi, ikisababisha umaskini wenye kulemea katika Yudea na Yerusalemu.—Antiquities of the Jews, XX, 2, 5; 5, 2.

18. Shauri lililo kwenye Waebrania 13:5 laandaa somo gani kwetu sisi?

18 Je! hapa pana somo kwa ajili yetu? Ndiyo, kwa maana hata tuwe maskini namna gani, haitupasi kupenda pesa au kuzihangaikia mno. Badala ya kuwa na wasiwasi kuhusu usalama wa kimwili, labda hata kuwa wenye kutamani sana, twapaswa ‘tuwe radhi na vitu tulivyo navyo.’ Yesu alisema: “Endeleeni, basi, kutafuta kwanza ufalme na uadilifu [wa Mungu], na vitu vingine hivi vyote vitaongezwa kwenu nyinyi.” (Mathayo 6:25-34, NW) Pia alionyesha kwamba twapaswa kukazia fikira juu ya kuwa ‘tajiri kwa Mungu’ kwa sababu ‘uzima wetu haumo katika wingi wa vitu tulivyo navyo.’ (Luka 12:13-21) Basi, ikiwa kupenda pesa kunatisha hali yetu ya kiroho, acheni tutii shauri la Paulo kwa Waebrania na pia tukumbuke kwamba “utawa [ujitoaji kimungu, JW] pamoja na kuridhika ni faida kubwa.”—1 Timotheo 6:6-8.

Mtumaini Yehova

19. Mungu alimpa Yoshua uhakikishio gani, nao wapasa kutuathirije?

19 Tukiwa wafuasi wa Yesu wanaotafuta ‘kutoa utumishi mtakatifu wakiwa na hofu na kicho cha kimungu,’ ni lazima tusitumaini pesa bali tutumaini Baba yetu wa kimbingu, ambaye msaada wake ni wa muhimu. Hata tuwe twakabili matatizo gani, twapaswa kukumbuka uhakikishio wake: “Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa.” (Waebrania 13:5) Hapa Paulo alitaja kijuu-juu maneno ya Mungu kwa Yoshua: “Sitakupungukia wala sitakuacha.” (Yoshua 1:5; linganisha Kumbu-kumbu 31:6, 8.) Yehova hakumwacha kamwe Yoshua, na Yeye hatatuacha sisi tukimtumaini Yeye.

20. (a) Ni nini andiko la mwaka wa 1990? (b) Twapaswa tuendelee kufanya nini bila woga?

20 Msaada wa Mungu usioshindwa utakaziwa miongoni mwa Mashahidi wa Yehova katika miezi iliyo mbele, kwa kuwa andiko lao la mwaka 1990 lasomwa hivi: ‘Mwe wenye moyo mkuu na kusema: ‘Yehova ndiye msaidiaji wangu.’ “Maneno haya yapatikana kwenye Waebrania 13:6, NW, ambapo Paulo alinukuu mtunga zaburi na akawaambia Waebrania hivi: “Ili tuwe wenye moyo mkuu na kusema: ‘Yehova ndiye msaidiaji wangu; mimi sitaogopa. Mwanadamu aweza kunifanya nini?”’ (Zaburi 118:6, NW) Ijapokuwa twanyanyaswa, hatuogopi, kwa kuwa wanadamu hawawezi kufanya zaidi ya yale ambayo Mungu aruhusu. (Zaburi 27:1) Hata tukilazimika kufa tukiwa tumeshika uaminifu wa kimaadili, tuna tumaini la ufufuo. (Matendo 24:15) Basi na tuendelee kumfuata Kiolezo wetu katika ‘kutoa utumishi mtakatifu tukiwa na hofu na kicho cha kimungu,’ tukiwa na uhakika kwamba Yehova ni Msaidiaji wetu.

Wewe Ungeitikiaje?

◻ Kwa nini Wakristo Waebrania hasa walihitaji msaada wa Yehova?

◻ Watu wa Yehova ‘wameachaje upendo wao wa kidugu uendelee’?

◻ Kwa nini kuwa wakaribishaji-wageni?

◻ Twaweza kufanya nini ili tuonyeshe kwamba twakumbuka waamini wenzi wenye kutendwa vibaya?

◻ Kwa nini ni lazima ndoa iendelezwe ikiwa yenye kuheshimika?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki