Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w90 1/1 kur. 28-31
  • Kushangilia Mavuno Katika India

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kushangilia Mavuno Katika India
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuamua Kuhusu Mwendo wa Maisha
  • Shamba Jipya Lililo Kubwa Sana
  • Wakati wa Vita ya Ulimwengu 2
  • Sababu za Kushangilia
  • Yehova, Tumaini Langu Kutoka Ujana na Kuendelea
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Kujua Yaliyo Sawa na Kuyatenda
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Imani ya Familia Yajaribiwa
    Amkeni!—2004
  • Wamishonari Wangesafiri Hadi Wapi Upande wa Mashariki?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
w90 1/1 kur. 28-31

Kushangilia Mavuno Katika India

Kama ilivyosimuliwa na F. E. Skinner

KWANGU mimi lilikuwa jambo lililokaribia kutoaminika​—mikusanyiko 21 katika lugha 10, wahudhuriaji zaidi ya 15,000 wakijifunza maana ya haki ya kimungu, na 545 wakibatizwa kufananisha upendo wao kwa yule Mungu mkubwa wa haki, Yehova! Kwa wale Mashahidi wa Yehova 9,000 walio katika India, hili lilikuwa jambo kubwa la 1989. Lakini kwangu hasa kilikuwa kisababishi cha kushangilia. Kwa nini? Kwa sababu ingalikuwa vigumu mimi kuwazia matukio makubwa jinsi hiyo nilipokanyaga udongo wa India mara ya kwanza katika Julai 1926. Wakati huo walikuwako wahubiri wa ujumbe wa Ufalme walio wachache kuliko 70 katika nchi nzima. Lo, ni mgawo ulioje ambao mwenzangu na mimi tulipokea miaka zaidi ya 63 iliyopita!

Jinsi Nilivyokuja India

Katika Mei 1926 mimi nilihudhuria mkusanyiko mkubwa katika London, Uingereza, na mara baada ya hapo nikarudi nyumbani kwangu katika Sheffield. Siku kadhaa baadaye, nikiisha kuingia nyumbani kutoka huduma ya shambani, nilipata simu ya barua ikiningojea. Ilisomeka hivi: “Jaji Rutherford ataka kukuona.”

Ndugu Rutherford, msimamizi wa pili wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, alikuwa amekuja kutoka New York kwa ajili ya mkusanyiko huo wa hivi majuzi, naye alikuwa angali London. Asubuhi iliyofuata nikiwa katika safari ya kurudi London kwa gari-moshi, nilikuwa nikijiuliza, ‘Hii ina maana gani?’ Kwenye ofisi ya tawi, nilipelekwa kwa Ndugu Rutherford, naye akaniuliza: “Je! kuna sehemu ya ulimwengu ambayo ungeona ikiwa vigumu kwako kufanya kazi?”

“Sivyo,” mimi nikajibu.

“Ungependa kwenda India?”

“Wataka niende lini?” nikajibu bila kusitasita. Hivyo, majuma matatu baadaye, George Wright na mimi tukawa mashuani kuelekea India. Nilikuwa na umri wa miaka 31, na sikuwa na shaka akilini na moyoni mwangu kuhusu nililotaka kufanya na maisha yangu.

Kuamua Kuhusu Mwendo wa Maisha

Kufikia 1918 vita ya ulimwengu ya kwanza ilikuwa imekwisha, na ndiyo sasa tu mimi nilikuwa nimemaliza miaka minne katika jeshi la Uingereza. Nilipendezwa na upigaji foto na uenezaji habari kupitia redio, na fursa nzuri za kibiashara zilikuwa wazi kwangu. Pia, nilikuwa nikifikiria ndoa. Hata hivyo, wakati ule ule, nikawa ndiyo ninapata uelewevu wa mambo ambao ulikuwa ukibadili lengo la maisha yangu ambalo nilikuwa nikilikazia fikira zote.

Baba yangu alikuwa amekubali fungu moja la Studies in the Scriptures, na kolpota mmoja, kama vile mapainia walivyoitwa wakati huo, alianza kujifunza Biblia na jamaa yetu. Mwanamke huyo alikuwa amekuwa mwalimu wa shule. Baada ya muda, kikundi cha wanaume vijana wa umri wangu wakawa wakienda nyumbani kwake kila Jumamosi kupata kikombe cha chai na funzo la Biblia. Mwanamke huyo alirudia-rudia kutuambia tujifanye kupatikana tutumiwe na Yehova, akisema hivi: “Msikatae kamwe mgawo.” Pia alinitia mimi moyo nibaki nikiwa mseja.

Kwa muda fulani niling’ang’ana na fikira zangu kuhusu jambo ambalo ningefanya. Maneno ya Yesu kwa yule mtawala tajiri kijana kwenye Mathayo 19:21 yalinisaidia: “Ukitaka kuwa mkamilifu, enenda ukauze ulivyo navyo, uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha njoo unifuate.” Mimi nilitoa barua ya kujiuzulu nikalipa shirika nililokuwa nikilifanyia kazi, na kabla miezi mitatu haijamalizika nikawa kolpota. Jambo hili, pamoja na uamuzi wa kubaki mseja, lilinistahilisha kupokea mgawo huo wenye thamani kubwa wa kwenda India karibu miaka minne baadaye.

Shamba Jipya Lililo Kubwa Sana

George Wright na mimi tuligawiwa kufanya uangalizi wa kazi ya kuhubiri Ufalme si katika India tu bali pia katika Burma (ambayo sasa ni Myanmar) na Ceylon (ambayo sasa ni Sri Lanka). Baadaye, Persia (Uajemi, ambayo sasa ni Iran) na Afghanistan ziliongezwa. Eneo la India lilikuwa haba kidogo kuliko lile la United States, lakini idadi ya wakaaji ilikuwa kubwa zaidi kwa mara kadhaa. Lilikuwa bara lenye vyakula, desturi, na lugha tofauti-tofauti, likiwa na watu wenye imani mbalimbali za kidini​—Wahindu, Waislamu, Waparsisi, Wajaini, Wasikhi (Makalasinga), na Wabuddha, na pia Wakatoliki na Waprotestanti.

Kazi ya kuhubiri ilikuwa imeanza India katika 1905, nayo ilipokea kichocheo kikubwa wakati Charles T. Russell, msimamizi wa kwanza wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, alipozuru katika 1912. Mahoji ya Russell pamoja na A. J. Joseph, mwanafunzi mchanga wa Biblia mwenye bidii, yaliongoza kwenye mpango wa kudumu wa utendaji mwendelevu wa kuhubiri. Joseph alitafsiri fasihi za Biblia katika ulimi wake wa kienyeji wa Malayalam na akasafiri na kuhutubu mahali pengi, hususa katika India ya kusini. Leo, karibu nusu ya wahubiri wa India huishi katika eneo hili ambamo Malayalam hunenwa, ingawa ni karibu asilimia 3 tu ya wakaaji wa India ambao huishi humo. Eneo hili, ambalo hapo zamani lilikuwa Travancore na Cochin, likawa Mkoa wa Kerala katika 1956.

George Wright na mimi tulibadilishana zamu za kuhudumia ofisi ya Bombay na kwenda nje kufanya ziara za kazi ya ziada ya kuhubiri. Tulitumia kikamili reli, farasi, na mikokoteni yenye kuvutwa na mafahali wa India. Baadaye tulitumia gari. Wakati huo wazo lilikuwa kuacha fasihi tu na kualika watu kwenye mahali pa mkutano kwa ajili ya funzo la kikundi. Tulikaza fikira nyingi zaidi juu ya wenye kunena Kiingereza waliojiita Wakristo.

Hapo kwanza, mimi nilipewa majina na anwani za waandikishaji wote wa Mnara wa Mlinzi. Sana-sana hawa walikuwa watu wa reli au wa telegrafu. Mimi nilizuru kila mmoja wao nikatafute upendezi wa kweli. Kwa miaka mingi nilikuwa nikienda Punjab kaskazini mwa India katika Januari na kuzuru kutoka Lahore hadi Karachi. Kwa kuwa matungamo ya watu yalipinga Biblia, vijiji vilivyokuwa na wenye kujiita Wakristo vilikuwa vichache na vilitenganishwa na mwendo mkubwa.

Ndugu mmoja alikuwa akisafiri pamoja nami akiwa mkalimani, nasi tuliishi na kula pamoja na watu. Wanavijiji waliishi katika nyumba zilizojengwa kwa matope yaliyookwa kwa jua, kukiwa na paa zilizoezekwa au zilizojengwa kwa mbao. Walilalia vyaripoi, vitanda vidogo vya miguu minne vilivyojengwa kwa fremu ya mbao vikiwa na kamba zilizokingamana. Mara nyingi wakulima wangekalia vyaripoi vyao Biblia ikiwa mkononi, huku wakivuta buruma (kiko) lenye kishikio cha urefu wa meta 0.5 hadi 1, wakifungua andiko hili na hili tulipokuwa tukiwaeleza kweli za Biblia. Mikutano yenye kufanywa nje ya nyumba ilithibitika kuwa ya kufaa sana, kwa kuwa sehemu kubwa ya mwaka haikuwa na mvua. Ingawa Wazungu walio wengi walijiona mno wasiweze kuhudhuria mikutano ya jinsi hiyo, Wahindi wangekusanyika mahali popote.

Tulijaribu kutangaza chapa ya fasihi katika lugha nyingi kwa kadiri ilivyowezekana. Kijitabu World Distress katika lugha ya Kikanari kilifanikiwa sana. Kilisukuma mhariri wa kichapo cha kidini cha pindi kwa pindi katika lugha ya Kanari atualike tutoe makala ziandikwe kwenye karatasi-habari yake, na kwa muda fulani, sisi tulitoa habari mfululizo za kitabu Deliverance baada ya kila majuma mawili.

Katika miaka ya kuanzia 1926 hadi 1938 kazi kubwa sana ya kuhubiri ilifanywa na mapainia wenye idili. Sisi tulisafiri maelfu ya kilometa, na fasihi nyingi sana zikagawanywa, lakini ongezeko lilikuwa la kiasi. Kufikia 1938 walikuwako mapainia 18 tu na wahubiri 273 katika makundi 24 yaliyotapakaa sehemu zote za India.

Wakati wa Vita ya Ulimwengu 2

Vita ya Ulimwengu 2 ilifoka katika 1939, na bado sisi tukaendelea na kuhubiri kwetu. Kwa uhakika, mapema katika 1940 kazi ya kutoa ushahidi barabarani ilianzishwa. Hata dada zetu Wahindi walishiriki, na hilo ni jambo zuri ajabu kwa kulinganishwa na desturi za kienyeji. Miaka kadhaa baadaye mwanafunzi wa Biblia alimwambia hivi Shahidi aliyemwomba ashiriki kazi ya jinsi hiyo: “Mimi ni mwanamke Mhindi, na siwezi kuonekana nikiongea na mwanamume barabarani kwa sababu ningefedheheshwa katika ujirani mzima. Siwezi kunena na mwanamume barabarani hata kama yeye ni mtu wa ukoo.” Hata hivyo, dada zetu Wakristo katika India wamekuwa wahudumu wa peupe walio na bidii.

Katika miaka hiyo ya mapema, mikusanyiko ilipangwa pia. Asubuhi zilitolewa ziwe za utumishi wa shambani, nao sana-sana ulikuwa wa kutembea kilometa nyingi tukiambia wakaaji na wapita-njia kuhusu ile mikutano ya peupe. Zaidi ya 300 walihudhuria mmoja wa mikutano hii, huku vipindi vikifanywa chini ya uvuli wa jengo la mianzi na makuti. Lakini haikuwapo manufaa kubwa ya kutaja wazi wakati wa kuanza, kwa kuwa ni watu wachache waliokuwa na saa. Wao walikuja wakati tu walipohisi wakitaka kuja, na mikutano ilianza wakati wasikilizaji wa kutosha walipokuwa wamekusanyika. Watu wa kuchelewa-chelewa waliendelea kuwasili-wasili huku mkutano ukiendelea.

Kwa kawaida programu iliendelea mpaka saa nne usiku, halafu wengi wakalazimika kutembea kilometa nyingi ili wafike nyumbani. Kulipokuwa na mbalamwezi, hapo mambo yalikuwa mazuri zaidi; kulikuwa na baridi nzuri na ya kuonewa shangwe. Ikiwa hakukuwa na mwezi, watu waliokota tawi la mtende wakalisokota kulifanya tochi. Ilipowashwa, tochi hiyo iliwaka wekundu usio mwangavu. Nuru zaidi ilipotakwa, tochi hiyo ilizungushwa-zungushwa hewani mpaka ikatoa miali ya moto. Hiyo ilitoa nuru ya kutosha ili kuona njia kwenye ardhi iliyoparuzwa.

Karibu na wakati huu serikali ilipiga marufuku uingizaji wa fasihi za Sosaiti katika India na Ceylon. Mashine yetu ndogo ya uchapaji katika Travancore ilishikwa, na serikali kuu ikatoa agizo lenye kukataza uchapaji wa fasihi zetu. Baadaye, katika 1944, mmoja wa ndugu zetu mwenye kutibu watu kwa kuwakanda mwili alikuwa akimtibu Sir Srivastava, waziri katika Baraza la Mawaziri wa Vaisiroi, naye akatokezewa ile habari ya marufuku.

“Haya basi, usiwe na wasiwasi,” ndugu yetu akaambiwa. Sir Srivastava akamweleza kwamba Bw. Jenkins (waziri mmoja aliyekuwa hapendelei kazi yetu) angestaafu karibuni na rafiki mwema wa Sir Srivastava angechukua mahali pake. “Mwombe Bw. Skinner aje kule,” Sir Srivastava akatia moyo, “nami nitamjulisha kwa Sir Francis Mudie,” mwenye kuchukua mahali pa Jenkins. Hatimaye, mimi nikaitwa; nikanena na Bw. Mudie, na marufuku ikaondolewa rasmi Desemba 9, 1944.

Sababu za Kushangilia

Kisababishi kikubwa cha kushangilia kilikuja katika 1947 wakati wamisionari wa kwanza waliozoezwa Gileadi walipowasili India. Kuwasili kwao kulisadifiana na wakati wenye umaana mkubwa katika historia ya India, kwa maana mwaka huo huo, siku ya Agosti 15, uhuru ulipatikana kutoka kwenye utawala wa Uingereza. Taifa lilipogawanyika kuwa India ya Wahindu na Pakistan ya Waislamu, machinjo yenye umwagaji damu yalitukia. Ijapokuwa hivyo, wahitimu wawili wa Gileadi walitumwa Pakistan, ambalo siku ya Agosti 14 lilikuwa limekuwa taifa huru. Muda si muda wamisionari kumi zaidi wakawa wakifanya kazi katika India yenyewe, na wengi zaidi wakawasili kusaidia katika miaka iliyofuata.

Moyo wangu ulishangilia zaidi wakati taratibu za kitengenezo zilipoanzishwa. Kazi ya mzunguko ilianza katika 1955 wakati ndugu Dick Cotterill, mhitimu mmoja wa Gileadi, alipowekwa rasmi awe mwangalizi wa mzunguko wa kwanza. Alitumikia kwa uaminifu mpaka kifo chake katika 1988. Halafu, katika 1960, tukawa na mpango wetu wa kwanza wa mwangalizi wa wilaya aliye wa kawaida, jambo ambalo lilisaidia sana mizunguko. Baada ya 1966 hakuna wamisionari zaidi wa kigeni walioruhusiwa kuingia nchini. Lakini muda si muda kazi ya painia wa pekee ikafunguka, na mapainia Wahindi wenye kustahili wakapelekwa kwenye sehemu nyingi za India. Leo, kuna karibu 300 katika kazi hii.

Haikuwa mpaka 1958 ndipo mwishowe tukafika wahubiri 1,000 wa Ufalme. Lakini hapo mwendo uliongezeka, na sasa tuna zaidi ya 9,000. Zaidi ya hilo, hudhurio letu la 24,144 la Ukumbusho wa 1989 laonyesha kwamba watu wengi zaidi wenye kupendezwa wanatafuta msaada. Sasa Sri Lanka ni tawi tofauti. Ni shangwe kama nini kuona kwamba wao wameongezeka kutoka wahubiri wawili tu katika 1944 wakapita sana 1,000 leo, lijapokuwako lile pigano lenye kuendelea katika nchi yao.

Ukuzi wa hesabu ya wahubiri umemaanisha ukuzi wa tawi letu pia. Baada ya kukaa miaka 52 katika Bombay yenye pirika-pirika nyingi, makao makuu yetu yalihamishwa 1978 yakapelekwa mji wa karibu wa Lonavla. Mimi sikuwazia kamwe kwamba tungekuwa na vifaa vya hali ya juu kama zile kompyuta za MEPS na mashine kubwa ya uchapaji fasihi wa rangi mbili katika lugha nyingi za Kihindi. Leo, sisi tunatokeza Mnara wa Mlinzi katika lugha 9 na fasihi nyinginezo katika lugha 20 tofauti-tofauti.

Kwa uwazi, zile siku za tawi letu lenye wanaume wawili zilikwisha zamani. Sasa sisi tuna jamaa ya Betheli yenye washirika zaidi ya 60! Nikiwa na umri wa miaka 95, mimi nafurahi kuwa ningali katika utumishi wa wakati wote kwenye ofisi ya tawi na kutumikia nikiwa mshirika wa Halmashauri ya Tawi la India. Na hasa nasisimuka kuwa shahidi mwenye kuiona kazi ya mavuno katika siku za mwisho hizi. Hilo ni jambo la kushangilia kweli kweli.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki