Yehova, Tumaini Langu Kutoka Ujana na Kuendelea
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA BASIL TSATOS
Ulikuwa mwaka wa 1920; mahali palikuwa vilima vya Arkadia katika mji wenye kupendeza wa Peloponnisos, Ugiriki. Nilikuwa kitandani, nikiwa mgonjwa mahututi na yale mafua ya Kihispania yaliyohofiwa sana yaliyokuwa yakiukumba ulimwengu.
KILA mara kengele ya kanisa ilipolia, niling’amua kwamba ilitangaza kifo cha mgonjwa mwingine. Je! mimi ningefuata? Kwa furaha, nilipona, lakini mamilioni hawakupona. Ingawa wakati huo nilikuwa na miaka minane tu, ningali nakumbuka waziwazi ono hilo lenye kuhofisha.
Mahangaiko ya Kiroho ya Mapema
Muda mfupi baadaye, Babu yangu alikufa. Baada ya maziko, nakumbuka Mama akijiunga na dada yangu na mimi kwenye roshani ya nyumba yetu. Bila shaka akijaribu kutuliwaza, alisema hivi kwa sauti ya chini: “Basi, watoto, ni lazima sisi sote tuzeeke na kufa.”
Ingawa alisema maneno hayo kwa uanana sana, maneno yake yalinisumbua. ‘Inahuzinisha kama nini! Ni jambo lisilo la haki kama nini!’ nikawaza. Sote wawili tulichangamka Mama alipoongeza hivi: “Lakini, Bwana anapokuja tena, atawafufua wafu, na hatutakufa tena!” Lo, hilo lilifariji!
Kutoka wakati huo na kuendelea nilikuja kupendezwa sana na kupata kujua wakati hasa ambapo hilo lingetukia. Niliwauliza watu wengi, lakini hakuna aliyeweza kuniambia, wala, hakuna aliyeonekana hata kupendezwa kuzungumzia jambo hilo.
Siku moja nilipokuwa na miaka 12 hivi, baba yangu alipokea kitabu kimoja kutoka kwa kaka yake aliyeishi United States. Kilikuwa na kichwa The Harp of God, kilichochapishwa na Watch Tower Bible and Tract Society. Nilitazama ukurasa wa yaliyomo, na macho yangu yalichangamka nilipoona sura “Kurudi kwa Bwana Yetu.” Niliisoma kwa kupendezwa sana, lakini nilikata tamaa kwa sababu mwaka haukutolewa kwa kuja huko. Hata hivyo, kitabu hicho kilionyesha kwamba (kurudi huko) kulikuwa karibu.
Upesi nilianza kwenda shule ya upili nikajihusisha sana na masomo yangu. Lakini mara kwa mara, mjomba wangu katika Amerika alipeleka nakala za Mnara wa Mlinzi nilizofurahia kusoma. Pia, kila Jumapili, nilihudhuria shule ya Jumapili, ambako mara nyingi askofu angekuja na kuongea na sisi.
Katika Jumapili moja hasa, askofu alikuwa amekasirika sana akasema: “Wageni wanalijaza jiji letu na vichapo vya uzushi.” Kisha akatoa nakala ya Mnara wa Mlinzi akapaaza sauti hivi: “Yeyote wenu akipata vichapo kama hivi nyumbani, avilete kanisani, nami nitavichoma.”
Sauti yake ilinisumbua, lakini roho yake ya kulipiza kisasi ilinisumbua zaidi. Kwa hiyo, sikutii ombi lake. Hata hivyo, nilimwandikia mjomba wangu nikamwomba asipeleke vichapo vingine vya Watch Tower. Hata hivyo, niliendelea kufikiria sana jambo kuhusu kuja kwa Kristo.
Hamu ya Kiroho Yakua
Likizo ya kiangazi ilipokuja, nilitoa sanduku yangu kufunganya nguo zangu. Hapo chini palikuwa vijitabu vitatu vilivyochapishwa na Watch Tower Society. Sikuwa nimeviona kabla ya hapo. Kimoja kiliitwa Where Are the Dead?
‘Hiki chaonekana kuwa chenye kupendeza,’ nikawaza. Ingawa nilikumbuka onyo la askofu, niliamua kuvisoma vijitabu hivyo kwa uangalifu ili kupata makosa ambayo nilifikiri vilikuwa navyo. Nilichukua kalamu nikaanza utafiti wangu kwa uangalifu. Kwa mshangao wangu, kila jambo katika vijitabu hivyo lilionekana lenye kufaa, na kila taarifa ilikuwa na maandiko yaliyotajwa ili msomaji aweze kuichunguza Biblia.
Kwa kuwa hatukuwa na Biblia, nilitaka kujua kama maandiko yaliyotajwa yalikuwa yametumiwa vibaya kufaana na kusudi la waandishi. Kwa hiyo nilimwandikia mjomba wangu nikamwomba anipelekee nakala ya Biblia nzima. Alifanya hivyo upesi. Niliisoma kutoka Mwanzo hadi Ufunuo mara mbili, na ingawa kulikuwa mengi ndani yayo ambayo sikuweza kuelewa, nilisisimuliwa na vitabu vya Danieli na Ufunuo. Nilitaka kuyaelewa yale mambo ambayo vitabu hivyo vilitabiri, lakini hakuna yeyote hapo ambaye angeweza kunisaidia.
Niliacha shule katika 1929, na upesi baadaye mjomba wangu katika Amerika akanipelekea tena nakala za Mnara wa Mlinzi. Nilianza kuzifurahia zaidi na zaidi nikamwomba anipelekee kwa ukawaida. Nilianza pia kuongea na wengine juu ya tumaini kwa wakati ujao ambalo nilikuwa nikijifunza kutoka katika magazeti. Lakini wakati huo maisha yangu yakabadilika sana.
Maendeleo ya Kiroho Katika Burma
Ndugu za mama yangu walikuwa wamehamia Burma (sasa Myanmar), na familia ikaamua kwamba kama ningejiunga nao, ujuzi wangu ungeongezeka na labda kunifungulia fursa za biashara. Mashariki ilikuwa imenipendeza sikuzote, kwa hiyo nilisisimuka kuwa na taraja la kwenda huko. Katika Burma, niliendelea kupokea Mnara wa Mlinzi kutoka kwa mjomba wangu, lakini sikukutana kamwe kibinafsi na mmoja wa Wanafunzi wa Biblia, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo.
Siku moja nilisisimuka kupata tangazo katika Mnara wa Mlinzi la vitabu Light, mabuku mawili yaliyoeleza kitabu cha Biblia cha Ufunuo. Kwa kuongezea, nilipata kujua kwamba utendaji wa Wanafunzi wa Biblia katika Burma ulitunzwa na tawi la India la Watch Tower Society, katika Bombay. Mara moja niliandika kuomba vitabu Light, pia nikaomba kwamba Wanafunzi wa Biblia katika India watumwe wahubiri katika Burma.
Vitabu hivyo viliwasili upesi kwa posta, na juma moja hivi baadaye, Wanafunzi wa Biblia wenyeji wa Burma walinitembelea. Nilifurahi kujifunza kwamba kulikuwa kikundi kidogo chao mahali nilikokuwa nikiishi katika Rangoon (sasa Yangon), jiji kuu la Burma. Walinialika kuhudhuria funzo la Biblia lao la kawaida na pia kushiriki nao katika kuhubiri nyumba kwa nyumba. Nilisita kidogo mwanzoni lakini upesi nikaanza kufurahia kushiriki ujuzi wa Biblia na Wabuddha, Wahindu, na Waislamu, pamoja na Wakristo kwa jina tu.
Kisha tawi la India likawatuma wahudumu wawili wa wakati wote (waitwao mapainia), Ewart Francis na Randall Hopley kuja Rangoon. Wote wawili walikuwa wametoka Uingereza awali lakini walikuwa wametumikia katika India kwa miaka kadhaa. Walinitia moyo sana, na katika 1934, nilibatizwa kwa ufananisho wa wakfu wangu kwa Yehova.
Ushahidi Wenye Moyo Mkuu
Baadaye tawi la India liliwatuma mapainia wengine kuja Burma. Wawili kati yao, Claude Goodman na Ron Tippin, walitembelea stesheni ya gari-moshi wakasema na Sidni Coote, mkuu wa stesheni. Alikubali vitabu, akavisoma kabisa, na kuanza kumwandikia dada yake mwenye umri mkubwa zaidi aliyeolewa, Daisy D’Souza, katika Mandalay. Yeye pia alipata vitabu hivyo kuwa vyenye kupendeza akaomba mengine.
Daisy, aliyekuwa amezoea Ukatoliki, alikuwa mtu mwenye moyo mkuu usio wa kawaida. Alianza kuwatembelea majirani wake na kuwaambia yale aliyokuwa akijifunza. Na alipotembelewa na padri wa parishi, aliyemwuliza ni kwa nini alikuwa ameacha kuhudhuria kanisa, Daisy alimwonyesha kwamba Biblia haiungi mkono mambo aliyokuwa akifundisha, kama vile helo inayowaka moto.
Mwishoni, padri huyo akamwuliza hivi: “Baada ya miaka hii yote ya kuwaambia juu ya helo inayowaka moto, ninaweza kuwaambiaje kwamba hakuna mahali kama hapo? Hakuna atakayetaka kuja kanisani.”
“Ikiwa wewe ni Mkristo mwenye kufuatia haki,” Daisy akaitikia, “utawafundisha kweli, ijapokuwa matokeo.” Kisha akaongeza hivi: “Ikiwa hutafanya hivyo, mimi nitafanya!” Naye akafanya hivyo.
Dick na Daisy na binti zao wawili wenye umri mkubwa zaidi walibatizwa katika Rangoon wakati uleule nilipobatizwa. Miaka mitatu baadaye, katika 1937, nilimwoa binti yao wa pili, Phyllis.
Kuponyoka Kwenda India
Majeshi ya Japani yalishambulia Burma wakati wa Vita ya Ulimwengu 2, na Rangoon ikatekwa katika Machi 8, 1942. Raia wageni walilazimika waondoke upesi kwenda India. Mamia walijaribu kuponyoka kupitia misitu, lakini wengi walikufa njiani. Ilitukia kwamba nilimjua binafsi yule ofisa aliyesimamia shughuli za kuondoka, kwa hiyo niliweza kupata tikiti za kusafiri kwenye mojawapo meli za mwisho za kubebea mizigo kuondoka Rangoon kwenda Kalkutta. Kuacha nyumba yetu na mali zetu nyingi kwa haraka hivyo ulikuwa wakati wenye huzuni kwetu. Burma ilikaliwa na Wajapani kutoka 1942 hadi 1945.
Tulikuwa na fedha kidogo tulipofika India, na kupata kazi ya kuajiriwa hakukuwa rahisi. Hilo lilitokeza mtihani wa imani. Nilikutana na ofisa mmoja Mwingereza aliyenitolea kazi yenye faida isiyo ya kupigana katika vita, lakini ilihusisha kutumikia nikiwa sehemu ya jeshi. Kwa msaada wa Yehova, niliweza kukataa toleo hilo na hivyo kudumisha dhamiri safi ya Kikristo. (Isaya 2:2-4) Tulihisi mkono wa Yehova wenye upendo katika njia nyinginezo pia.
Tulikaa New Delhi, jiji kuu la India, ambako ilikuwa karibu haiwezekani kupata makao. Hata hivyo, tulipata nyumba kubwa katikati mwa jiji. Ilikuwa na sebule kubwa yenye mwingilio yao yenyewe, na chumba hicho kilitumikia kikiwa Jumba la Ufalme kwa miaka chache iliyofuata kwa Kutaniko la Delhi la Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, kwa sababu ya marufuku yaliyowekwa katika 1941 juu ya vichapo vyote vya Watch Tower Society katika India, hatukuweza kupata fasihi ya Biblia.
Jinsi Marufuku Yalivyoondolewa
Jumapili moja katika 1943, wale waliokuwa wakihudhuria mahubiri kwenye makanisa ya Delhi walipokea kikaratasi kilichotiwa sahihi na makasisi 13 wa makanisa tofauti-tofauti. Kilionya hivi: “RAIA WA DELHI JIHADHARINI NA MASHAHIDI WA YEHOVA.” Shtaka lilikuwa kwamba tulikuwa tumepigwa marufuku katika India kwa sababu za kisiasa.
Upesi, kwa kibali cha ofisi ya tawi katika Bombay, tulichapisha na kugawanya kikaratasi kilichowafunua makasisi. Kwa kuwa nilikuwa mwangalizi msimamizi, jina langu na anwani yangu ilichapishwa chini ya kikaratasi hicho chenye maneno makali. Upesi baadaye, polisi walipompata Margrit Hoffman na mimi tukigawanya nakala za kikaratasi hicho, tulikamatwa na kutiwa gerezani. Hata hivyo, upesi takaachiliwa kwa dhamana.
Baadaye, alipokuwa katika huduma, Margrit alitembelea nyumba ya Bwana Srivastava, waziri mashuhuri katika baraza la mawaziri la kaimu wa India. Bwana Srivastava alimpokea kwa ukaribishaji-wageni, na wakati wa mazungumzo, alimwambia kwamba fasihi yetu ilikuwa imepigwa marufuku isivyo haki katika India. Siku hiyo ilitukia kwamba Margrit alikutana pia na mbunge kutoka jimbo la Madras. Alikuwamo jijini ili kuhudhuria kikao cha bunge. Margrit alimtajia ukosefu wa haki wa marufuku iliyowekwa juu ya fasihi yetu, naye aliahidi kutokeza swali hilo kwenye mkutano uliokuwa ukija.
Wakati huo, nilikuwa nikifanya kazi nikiwa tabibu wa kurekebisha viungo vya mwili kwenye hospitali ya hapo. Basi, ilitukia kwamba Bwana Srivastava alipata jeraha, na hospitali ikanituma nione kama utabibu wa kurekebisha viungo vya mwili ungeweza kumsaidia. Nilimpata Bwana Srivastava kuwa mtu mwenye kupendeza, na tulipozungumza, nilitaja kwa kutukia tu kwamba Bi Hoffman na mimi tulikuwa tumeachiliwa kutoka gerezani kwa dhamana. Nilieleza ni kwa sababu ya msongo wa makasisi kwamba fasihi yetu ya Biblia ilikuwa imepigwa marufuku kwa misingi ya kisiasa lakini kwamba hatukuwa wanasiasa hata kidogo. Mwakilishi wetu wa tawi, Edwin Skinner, nikaendelea kusema, alikuwa ametoa maombi ya kuwa na mahojiano ili kueleza msimamo wetu, lakini alikuwa amekatazwa.
Siku chache baadaye, Bwana Srivastava aliniambia mimi: “Bw. Jenkins [yule ofisa wa serikali aliyekuwa hapendezwi na kazi yetu] atastaafu katika siku chache, na mahali pake patachukuliwa na Bwana Francis Mudie. Mwombe Bw. Skinner aje, nami nitamjulisha kwa Bwana Francis.”
Bwana Srivastava alipanga mkutano huo kama vile alivyokuwa ameahidi. Wakati wa mkutano huo, Bwana Francis Mudie alimwambia Ndugu Skinner: “Siwezi kukuahidi jambo lolote, lakini nitachunguza jambo hilo.” Kwa kuwa bunge ingefunguliwa siku chache baadaye, Ndugu Skinner alibaki ili aone matokeo. Kama alivyoahidi, mbunge kutoka Madras alisimama akauliza: “Je! ni kweli kwamba vichapo vya Watch Tower Bible and Tract Society vimepigwa marufuku kwa sababu za kisiasa?”
“La, marufuku iliwekwa kwa sababu za hadhari,” Bwana Francis Mudie akajibu, “lakini sasa serikali imeamua kuiondoa marufuku.”
Huo ulikuwa wakati wenye kusisimua kama nini kwetu tuliposikia habari hiyo! Juma moja baadaye ofisi ya tawi katika Bombay ilipokea barua iliyothibitisha kuondolewa kwa marufuku.
Kurudi Burma Yenye Kukumbwa na Vita
Utawala wa Uingereza ulirudi Burma baada ya Vita ya Ulimwengu 2, kisha sisi Mashahidi kumi tulirudi Rangoon miezi michache baadaye. Tulifurahi kuwaona tena wale Mashahidi wenyeji wachache waliobaki. Nchi ilikuwa katika hali yenye kusikitisha. Utumishi mbalimbali wa umma, kutia na umeme na usafiri wa umma, haukupatikana. Kwa hiyo tulinunua gari aina ya jeep kutoka kwa jeshi tukalitumia vizuri tukiwapeleka watu mikutanoni ambayo tulikuwa tumepanga upesi baada ya kurudi kwetu.
Mtu mmoja mwenye kupendezwa alitutolea uwanja, na kwa msaada wa watu wenye fadhili katika eneo hilo, tulijenga Jumba la Ufalme lenye ukubwa unaofaa. Lilijengwa kwa nguzo za mianzi yenye nguvu, kuta za mianzi iliyosokotwa, na paa iliyoezekwa. Hapo, katika Aprili 1947, Nathan H. Knorr, aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Society wakati huo, na katibu wake, Milton G. Henschel, walitoa hotuba wakati wa ziara yao katika Rangoon. Wakati huo, tulikuwa na Mashahidi 19 kwa ujumla katika Burma yote. Lakini hotuba ya watu wote ya Ndugu Knorr, iliyofanywa kwenye Thieta ya New Excelsior, ilihudhuriwa na watu 287!
Twaenda Kukaa Australia
Katika Januari 4, 1948, Burma ilipewa uhuru kutoka kwa Uingereza, na Wazungu wengi waliona inafaa kuondoka nchi hiyo. Baada ya kufikiria jambo hilo kwa sala, Phyllis na mimi tukaamua kumchukua binti yetu na kuhamia Australia. Tulikaa katika Perth, jiji kuu la Australia Magharibi.
Kuondoka Burma tena, na wakati huu kabisa, ulikuwa wakati wenye huzuni sana kwetu. Mara kwa mara, tulisikia habari kutoka kwa wapendwa walio huko, tukafurahi kujua kwamba kazi ya Ufalme ilikuwa ikisonga mbele kwa utaratibu katika nchi hiyo.
Kuanzia 1978, kwa miaka minne tulifurahia kutumikia makutaniko yote yenye kusema Kigiriki katika majiji makuu ya Australia. Hilo lilimaanisha kusafiri sana, kwa kuwa ni zaidi ya mwendo wa kilometa 4,200 kutoka pwani ya magharibi hadi pwani ya mashariki ya nchi hii kubwa. Baada ya muda fulani, hali-hewa, inayotofautiana sana kutoka jimbo moja hadi jingine, ilichangia kudhoofika kwa afya yetu. Kwa hiyo tulikaa katika Perth, ambako ninaendelea kutumikia nikiwa mzee katika mojawapo makutaniko 44 ya jiji hilo.
Kadiri miaka imepita, uwezo wangu wa kuona umedhoofika zaidi, na kusoma limekuwa jambo gumu. Hata hivyo, ijapokuwa matatizo ya afya, mioyo yetu ingali michanga. Sote wawili tunangojea kwa uhakika ile siku yenye furaha ambapo wote wanaomhofu Yehova wataona mwangaza wa upendeleo wake ‘likiwazukia, lenye kuponya katika mbawa zake; nasi tutatoka nje, na kucheza-cheza kama ndama wa mazizini.’—Malaki 4:2.a
[Maelezo ya Chini]
a Katika Desemba 13, 1992, wakati masimulizi haya ya maisha yalipokuwa yakikamilishwa, Ndugu Tsatos alilala usingizi katika kifo.
[Picha katika ukurasa wa 24]
Familia yangu pamoja na Ndugu Henschel na Ndugu Knorr huko Burma (Myanmar) katika 1947
[Picha katika ukurasa wa 25]
Basil Tsatos na mke wake, Phyllis, katika Australia