Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w88 11/1 kur. 10-14
  • Yehova Ajaza Kila Uhitaji Wangu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Ajaza Kila Uhitaji Wangu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kung’amua Mahitaji ya Kiroho
  • Fursa za Kutaharukisha Zafunguka Wazi
  • Kuvuka Nyika ya Nullarbor
  • Kushiriki au Kutoshiriki?
  • Mwaliko wa ‘Kujitahidi Kufikia’
  • Mkusanyiko Wenye Kusisimua wa Rangoon
  • Vita na Uvamizi wa Wajapani
  • Kurudi Australia
  • Yehova, Tumaini Langu Kutoka Ujana na Kuendelea
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Sehemu ya 3—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • “Mimi Hapa, Nitume Mimi”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • ‘Vuno Limeiva’ Katika Burma
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
w88 11/1 kur. 10-14

Yehova Ajaza Kila Uhitaji Wangu

Kama ilivyosimuliwa na John E. (Ted) Sewell

TULIPOKUWA tukipiga kila hatua kupita kwenye mwitu ule wa Thailand ulio na joto kali sana, mimi niliwaza, ‘Lazima kuwe kuna njia rahisi zaidi za kutoka Bangkok kwenda Burma!’ Nyayo za miguu zikiwa zinauma na nikiwa nimelowana jasho, hangaikio langu kubwa lilikuwa kwamba tungekutana na mmoja wa simba-milia, dubu weusi, au ndovu waliojulikana kuwa wenye kuzurura-zurura katika miitu hiyo​—licha ya nyoka wenye sumu. Kwa nini Frank Dewar na mimi tulikuwa tunafunga safari hii yenye hatari?

Sisi wote wawili tulikuwa wamisionari katika Thailand, na tulikuwa tumetoka sasa tu kupata habari kwamba mkusanyiko wa siku tatu ungefanywa katika Rangoon, Burma, Novemba 26-28, 1938. Pesa zetu haba zilitushurutisha kwenda Rangoon kutoka Bangkok kwa kutumia usafiri ulio wa bei rahisi iwezekanavyo, na sehemu ya safari hiyo ilitutaka tusafiri mwendo mgumu wa kilometa 80 kupitia mwituni.

Tulianza safari kutoka Bangkok kwa garimoshi siku ya Novemba 16, tukahamia basi ndogo, tukavushwa Mto Ping tukiwa katika mtumbwi mkubwa, na ndipo tukaanza mtembeo wetu mrefu wa kupita mwituni. Frank alikuwa amechunguza sana ramani mbalimbali na hatimaye akatuliza macho kwenye njia ambayo ilionekana yenye kufaa zaidi. Hatukuwa na barabara za kufuata​—isipokuwa kijia chembamba tu, kilichofanyizwa na wasafiri, ambacho kilifuatana hasa na kamba ya simu.

Tulitoa asante kwamba wanyama peke yao tulioona walikuwa nyani wengi sana katika miti. Mimea-orkidi iliyo na uzuri wa kuvutisha pumzi ilikuwa kitu cha kupendeza ambacho hatukutarajia. Vivuli vya alasiri vilipokuwa vikirefuka, sisi tukawa na hangaiko juu ya kadiri ya usalama ambao tungekuwa nao kwa kulala katika mwitu huo. Ulikuwa tofauti sana na eneo lenye vichaka la Australia ambako nilikuwa nimelala nje mara nyingi wakati wa usiku. Tulikuwa pia tumeonywa juu ya walanguzi haramu waliojulikana kuwa wenye kunyang’anya na hata kudhuru wasafiri kimwili.

Mioyo yetu ililegea tulipokabiliana uso kwa uso na kikundi cha wanaume wenye sura kali-kali, kila mmoja akiwa na sime kubwa yenye kuning’inia kwenye mshipi wake. Wao walitusimamisha na kutuuliza tulikokuwa tukienda. Tulipoeleza kwamba tulikuwa njiani kwenda kuhudhuria mkusanyiko wa Kikristo katika Rangoon, walitutazama kwa kutoitikadi lakini wakasonga mbele bila kutudhuru.

Muda mfupi baadaye, tulikuta wanaume wawili vijana walioonekana wenye urafiki zaidi. Kwa kutumia maarifa yetu haba juu ya lugha ya Thai, sisi tukawakodi watuongoze mpaka tukafike Burma. Giza lilipokuwa likiingia, tuliwasili kwenye mti mkubwa wenye vidato vya kupanda juu mpaka kwenye jukwaa la mbao miongoni mwa matawi. Hapo ndipo sisi wanne tulilala.

Ilipofika jioni ya siku iliyofuata, tukawa kwenye kijiji kidogo ambako tuliweza kukaa usiku ule kwenye sakafu ya nje ya nyumba iliyojengwa kwa muundo wa hivi hivi. Siku ya tatu, tulifika kijiji cha Mae Sot katika mpaka wa Burma. Hapo sisi tukawaambia waongozi wetu waende salama nasi tukaterema kuwalipa kwa utumishi wao mwema.

Baada ya kuuvuka mto kuingia Burma, tulipanda basi dogo tukasafiri juu ya barabara ya milimani na ndipo tukapanda mashua-mtoni kwenda Moulmein. Sehemu ya mwisho ya safari yetu ya kwenda Rangoon ilikuwa kwa gari-moshi, nayo ilionekana kuwa rahisi sana baada ya ile safari ngumu ya kutembea miguu. Safari nzima ilikuwa imechukua juma moja, lakini ilistahiki jitihada yote ile kufurahia ushirika wa kiroho wa ndugu zetu. Hiyo ilikuwa ithibati moja tu zaidi kati ya zile nyingi zinazoonyesha kwamba Yehova amejaza kila uhitaji wangu. Lakini acha nikuambie jinsi mimi nilivyokuja kuwa katika Thailand.

Kung’amua Mahitaji ya Kiroho

Maisha na desturi zilikuwa zikibadilika wakati mimi nilipozaliwa katika Australia ya Magharibi katika 1910. Vita ya Ulimwengu 1 iliyoanza katika 1914 ilionekana kuharakisha mwendo wa mabadiliko. Ingawa nilikuwa na miaka karibu saba tu, mimi nakumbuka vizuri kwamba Mama alimwandikia barua mbalimbali Baba aliyekuwa ameenda vitani katika Ulaya. Wakati mmoja Mama alisema kwa mimi hivi: “Wajua, Biblia inasema kutakuwako vita na matetesi ya vita.” Yeye hakueleza mengi zaidi ya hilo, lakini mimi nilitaka kujua habari hizo.

Miaka kadhaa baadaye, katika Desemba 1934, wakati mimi nilipokuwa nimepanda farasi nikirudi kwenye shamba ambako nilifanya kazi nilikutana na mmoja aliyekuwa rafiki yangu shuleni naye akaniambia kwamba watu fulani walio Mashahidi wa Yehova walikuwa wamekuja hivi majuzi kutoka Perth. Jamaa yake ilinunua vitabu vyao lakini wakawa wameamua kutovisoma. Kwa kutaka kujua, nikajipatia kitabu Life kutoka kwake.

Nilipokuwa nikisonga mbele nikiwa juu ya farasi yule katika ile hewa ya usiku mwangavu, nuru ya mwezi ilikuwa iking’aa sana hata ikawa naweza kusoma zile herufi za chapa kubwa za kichwa cha kila sura. Nilipofika kwenye shamba, nikaendelea kusoma kwa kutegemea taa ya mafuta. Hapo, kwa mara ya kwanza, nikapata kujua kwamba Mungu ana jina la kibinafsi​—Yehova. Niliingiwa na upendezo mwingi kujua kwamba Mungu ana kusudi zuri ajabu kwa dunia yetu, ndiyo, kwamba dunia itakuwa paradiso ili ifurahiwe na aina ya binadamu iliyo tiifu. Ala, katika kitabu hicho maswali yangu yote yalikuwa yanajibiwa!

Watu wa kwanza niliotaka kuambia walikuwa wazazi wangu, ambao waliishi katika shamba dogo kilometa 138 kutoka hapo. Hiyo ilimaanisha mwendo wa kupanda farasi wa siku moja na nusu. Nilipoambia Mama niliyokuwa nimekuwa nikijifunza, yeye alinishangaza kwa kusema kwamba yeye pia alikuwa akijifunza na kufurahia fasihi ile ile ya Biblia! Nilipokuwa katika ile safari ndefu ya kurudia maskani yangu juma moja baadaye, nilikuwa na mengi ya kufikiria, kwa maana mafunzo yangu yalikuwa yamenionyesha kwamba maarifa na imani siyo mambo pekee ambayo Mungu anataka. Sasa nilijua kwamba ni lazima Mkristo wa kweli afuate Yesu Kristo na kutumikia Yehova yeye binafsi kwa kuhubiria wengine. Kwa hiyo nikapiga moyo konde kujaribu kufanya hivyo kila mwisho-juma tangu hapo na kuendelea.

Fursa za Kutaharukisha Zafunguka Wazi

Ili kutoa ushuhuda katika wilaya yetu ya ukulima iliyotapakaa, nilinunua gari la muundo wa T-Fordi lililokuwa limegeuzwa kuwa lori la matumizi mbalimbali. Nikiwa nimechukua matandiko na mahitaji mengine machache, nilizuru wakulima alasiri yote ya Jumamosi, nikalala ndani ya lori hiyo, halafu nikaendelea kutoa ushuhuda shamba kwa shamba asubuhi ya Jumapili. Mwishoni-mwishoni mwa alasiri nilirudi kwenye maskani yangu.

Katika Aprili 1936 mimi nilionyesha wakfu wangu kwa kubatizwa kwenye mkusanyiko mdogo katika Perth. Moja ya hotuba ilikazia huduma ya wakati wote ya painia. Mimi nilijua sikuwa na wajibu wowote wa Kimaandiko wenye kunizuia nisishiriki katika kazi hiyo ya maana, kwa hiyo katika Desemba 1936, nikaanza kupainia.

Katika mwezi uo huo, mapainia wawili wenye maungo imara, Arthur Willis na Bill Newlands, waliwasili katika Perth kwa lori. Walikuwa wametoka Sydney kwenye pwani ya mashariki miezi tisa mapema na wakawa wamefanya ziara ya kutoa ushuhuda na kupita katikati ya Australia mpaka upande huu mwingine. Unaweza kuwazia taharuki yangu wakati nilipopewa mgawo na Sosaiti nijiunge nao katika safari yao ya kurudi. Wao walinipa mazoezi ya thamani kubwa ambayo sijasahau kamwe.

Kuvuka Nyika ya Nullarbor

Jina Nullarbor linamaanisha “hakuna miti.” Ni elezo linalofaa juu ya nyika kavu, isiyo na miti katikati ya Australia. Katika miaka ya katikati ya 1930 njia ambayo tulipitia ilikuwa safari ya kilometa zipatazo 1,600 za kupita katika barabara iliyoparuzika mno.

Kila usiku tulilala juu ya vitanda vya kukunja, kwa kawaida tukiwa nje kabisa chini ya anga. Katika sehemu hiyo ya nchi mvua ni kidogo na umande ni wa kiasi kidogo mno kana kwamba haupo kabisa. Tulipotulia kila usiku chini ya zile nyota zilizo kama chandarua, zikiwa zinang’aa katika ile hewa safi, isiyochafuzwa, mara nyingi nilikumbushwa juu ya maneno yenye kufungua Zaburi ya 19: “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, na anga laitangaza kazi ya mikono yake.”

Reli yenye kuvuka nyika ya Nullabor inasemwa kuwa ndiyo reli ndefu zaidi ulimwenguni kwa urefu wa kunyooka moja kwa moja. Hiyo inaendelea kwa kilometa 480 bila kujipinda au kujikunja hata kidogo. Sisi tulifurahia kutoa ushuhuda katika makao madogo-madogo ya ulowezi yaliyo kando-kando ya reli ile, na kwa watu wanaoishi kwenye vituo au nyanja za kufugia kondoo. Mashamba ya watu katika sehemu hiyo ya Australia yalikuwa makubwa sana. Mimi nakumbuka kituo kimoja cha zaidi ya kilometa za mraba 4,000 chenye maskani iliyo karibu kilometa 80 kutoka kwenye lango la mbele.

Hatimaye, tuliwasili katika Katoomba katika ile Milima ya Buluu iliyoko mwendo mfupi tu magharibi ya Sydney kwa wakati unaofaa kabisa ili tuhudhurie Ukumbusho siku ya Machi 26,1937. Mgawo wetu wa kusafiri hapa na pale ulikuwa umekuwa wa kufurahika na wenye kuthawabisha kiroho, lakini lilikuwa badiliko la kufurahisha kukaa pale kwa muda pamoja na kundi la watu wa Mungu.

Kushiriki au Kutoshiriki?

Kwenye wakati wa Ukumbusho huo wa 1937, bado kulikuwa na mvurugo kuhusu “kondoo wengine.” (Yohana 10:16) Watu fulani walihisi kwamba kipimo cha imani na bidii ya Kikristo ambacho mtu alionyesha ndicho kingeonyesha kama yeye alikuwa au hakuwa amepokea ule mwito wa kimbingu. Kwa hiyo, kama wengine kadhaa waliokuwa katika mastakimu zinazofanana na zangu, mimi nilishiriki ile mifano. Mwaka uliofuata hesabu fulani ya sisi mapainia tulisumbuka mawazo tena juu ya kushiriki.

Kwa ndani sisi tulikuwa tukitazamia uhai juu ya dunia-paradiso, hata hivyo wengi walihisi kwamba bidii na huduma yetu ya painia ilitoa ithibati ya kwamba tulikuwa wapakwa-mafuta kwa roho. Katika wakati unaofaa kabisa Yehova akatupa sisi jibu kupitia tengenezo lake la kidunia. Katika alasiri ile ile ya Ukumbusho, toleo la Machi 15, 1938 la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) liliwasili. Makala yalo kuu, “Kundi Lake,” ilikuwa funzo lenye maelezo marefu juu ya Yohana 10:14-16. Tuliingiwa na upendezo ulioje kwa sababu ya elezo hilo la wazi lililojibu maswali yetu!

Makala hiyo iliandaa vielelezo juu ya jinsi roho ya Mungu ilivyotenda kazi kwa uweza mwingi juu ya watumishi wake katika nyakati za kale na kusababisha wafanye kazi za uweza mwingi muda mrefu kabla ya ule mwito wa kimbingu kufunguka wazi. Vivyo hivyo, Mungu hutia roho yake juu ya watumishi wake waliojiweka wakfu duniani leo ambao yeye amewapa tumaini la kidunia. Hivyo sisi tulishukuru kuelewa tofauti kati ya kuzaliwa na roho takatifu na kutiwa nishati na roho ya Mungu ili kufanya mapenzi yake.

Mwaliko wa ‘Kujitahidi Kufikia’

Matukio mengine ya kusisimua ya 1938 yalikuwa ziara ya msimamizi wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, Ndugu Rutherford, na ule mkusanyiko kwenye Uwanja wa Michezo Sydney. Mwito ulitokezwa kwenye mkusanyiko ili mapainia wenye nia wakatumikie katika Burma, Malaya, Siam (ambayo sasa ni Thailand) na Java (ambayo sasa ni Indonesia). Hector Oates, Fred Paton, na mimi tuliingiwa na upendezo mwingi wa kupokea migawo ya kwenda Burma.

Mimi nilikuwa sijapata kutoka kwenye fuo za Australia. Hata hivyo, katika muda wa miezi miwili mapainia wengine pamoja na mimi tukawa katika meli tukiwa njiani kuelekea kwenye migawo yetu. Tulifika nchi kavu kule Singapore siku ya Juni 22, 1938, tukalakiwa kwenye gati na Bill Hunter, aliyekuwa tayari akipainia huko. Kila kitu kilionekana kuwa cha kigeni na cha kupendeza sana wakati tulipokuwa tukiona mvalio na desturi za watu wa huko na kusikia lugha ambazo hatungeweza kuelewa.

Ndugu Hunter alinipa mimi barua-simu kutoka Australia iliyobadili mgawo wangu kutoka Burma kwenda Malaya. Fred Paton na Hector Oates wangesonga mbele kwenda Burma bila mimi. Mimi niliterema kupata habari kwamba ningekuwa nikifanya kazi pamoja na wamisionari wawili wenye ujuzi, Kurt Gruber na Willi Unglaube. Hapo awali wao walikuwa wa kutoka Ujeremani lakini wakawa wamekuwa wakitumikia katika Malaya kwa muda fulani.

Baada ya kukaa miezi mitatu katika Malaya, niligawiwa kwenda Thailand. Willi Unglaube angeandamana nami, pamoja na Frank Dewar, ambaye hapo kwanza alikuwa amefanya kazi ya misionari huko. Tuliwasili kwa gari-moshi katika Septemba 1938, tukajitafutia kao la muda, na kuanza katika kazi ya ushuhuda. Tuliwapata Wathai kuwa watu wenye fadhili na saburi tulipokuwa tukimenyana na lugha yao yenye wingi wa maneno ya kujieleza.

Mkusanyiko Wenye Kusisimua wa Rangoon

Ilikuwa kutoka Bangkok, Thailand, kwamba sisi tukafunga ile safari ya jasho kali ya kwenda Rangoon, Burma, iliyoelezwa mapema kidogo. Ilikuwa ndiyo mara ya kwanza mkusanyiko kufanywa katika Burma, na lile Jumba la Jiji lililo la kupendeza lilijaa pomoni likiwa na watu zaidi ya elfu moja kwa ajili ya mhadhara. Ikawa lazima milango ifungwe kwa maana hakukuwa na nafasi zaidi. Kulikuwa na Mashahidi wachache tu katika Burma na nchi za ujirani, kwa hiyo walio wengi kati ya waliokuja kusikia mhadhara huo walikuwa watu waliokuwa wamejibiza yale maelfu ya mialiko ya vikaratasi vya ukaribishaji vilivyogawanywa kabla ya mkusanyiko.

Kwa sisi tuliokuwa tumekuja kutoka migawo ya mbali mbali ya umisionari, hicho kilikuwa kiongezea nishati za kiroho kweli kweli. Lakini mkusanyiko ulipoisha, sisi tulirudia maskani yetu Thailand​—hata hivyo, wakati huu ilikuwa ni kwa kufuata njia rahisi kidogo isiyotaka tutembee kupitia ule mwitu.

Vita na Uvamizi wa Wajapani

Sasa mawingu ya dhoruba ya vita yalikuwa yakielekea Esia ya kusini-mashariki kwa njia yenye kuogofya. Kani za kijeshi za Wajapani zilipokuwa zikijongea kuingia Thailand, kazi ya Mashahidi wa Yehova ilipigwa marufuku. Waingereza wote, Waamerika, na Waholanzi walishurutishwa kukaa katika kambi moja bila kutoka humo muda wote wa vita hiyo. George Powell, painia mmoja aliyekuwa amehama Singapore kuja kujiunga nasi katika Bangkok, alitiwa gerezani pamoja nami. Tulikaa miaka mitatu na miezi minane tukiwa pamoja katika kambi hiyo.

Wakati huo tulipokuwa tumezuiliwa, hatukuweza kupokea fasihi yoyote mpya wala neno kutoka kwa Sosaiti. Lakini tulijionea wenyewe ile ahadi ya mtunga zaburi: “BWANA [Yehova, NW] huwategemeza wote waangukao, huwainua wote walioinama chini.”​—Zaburi 145:14.

Kurudi Australia

Vita ilipoisha katika 1945, mimi nilirudi Australia. Nikiwa na chakula kizuri na hali za maisha zinazofaa zaidi, nilirudia afya yangu njema na nikaweza kuanza kupainia tena. Halafu, katika 1952, nilipewa mgawo niwe kwenye kazi ya kusafiri nikiwa mwangalizi wa mzunguko, na nikafurahia pendeleo hilo kwa miaka 22 iliyofuata. Katika 1957, nilimwoa Isabell, aliyekuwa amekuwa painia kwa miaka 11, tukaendelea katika kazi ya mzunguko tukiwa mume na mke.

Matatizo ya afya yalianza kufanya usafiri wa daima uwe mgumu, kwa hiyo katika 1974 tulitulia tufanye upainia tukiwa katika Melbourne. Mara kwa mara mimi bado hutumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko aliye badala, na hivi majuzi nilikuwa na pendeleo la kushiriki nikiwa mkufunzi kwenye moja ya shule za utumishi wa painia. Katika kazi yote hiyo, mke wangu amekuwa utegemezo wa daima wenye kunitia shangwe. Sasa nikiwa na umri wa miaka 78, nahisi shukrani za kina kirefu kwa Yehova anapoendelea kujaza kila uhitaji wangu.

Nikitazama nyuma kwenye miaka iliyopita, mara nyingi mimi hufikiria jinsi Yehova ametuzoeza sisi, akatusaidia kushinda makosa, na kututia nidhamu ili atutakatishe taka tukiwa watumishi wake. Mimi nakumbuka visa ambapo Mungu ameniandalia mimi njia ya kushinda majaribu yaliyokuwa hayavumiliki kwa uwezo wa kibinadamu. Kumbukumbu hizo ni chanzo cha imara na ni kikumbusho cha daima kwamba kweli kweli Yehova amejaza kila uhitaji.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Picha yangu ya hivi majuzi nikiwa pamoja na mke wangu, Isabell

[Picha katika ukurasa wa 12]

Kutoa ushuhuda katika nyika ya Nullarbor

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki