Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 5/1 kur. 28-31
  • “Mimi Hapa, Nitume Mimi”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Mimi Hapa, Nitume Mimi”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Uchaguo Uliofanywa Mapema Maishani
  • Kwenda Hadi Singapore
  • Mgawo Wangu Katika Shanghai
  • Hong Kong na Kisha Burma
  • Kurudi Australia
  • Kurudi Mahali Ambapo Hayo Yote Yalianza
  • Nimepata Shangwe Maishani kwa Kufanya Mapenzi ya Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Singapore—Kito cha Asia Kilichopoteza Mng’ao
    Amkeni!—1997
  • Yehova Ajaza Kila Uhitaji Wangu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Yehova, Tumaini Langu Kutoka Ujana na Kuendelea
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 5/1 kur. 28-31

“Mimi Hapa, Nitume Mimi”

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA WILFRED JOHN

Walinzi wa kijeshi wenye silaha kutoka Burma walitushambulia kutoka pande zote za mto. Wakiwa na singe zilizo tayari na bunduki zikiwa zimelengwa, walitembea ndani ya maji yaliyofika viunoni pao wakatuzunguka chini ya daraja la barabara kuu.

MWENZANGU nami tuliogopa sana. Hayo yote yalihusu nini? Ingawa hatukuielewa lugha, tulikuja kuelewa punde—kwamba tulikuwa tumekamatwa. Tukiwa na taulo tu viunoni petu, tulisindikizwa bila heshima hadi kituo cha polisi cha karibu tukahojiwa na ofisa aliyesema Kiingereza.

Huo ulikuwa 1941, wakati wa vita ya ulimwengu ya pili, na tulidhaniwa kuwa mahaini. Baada ya sisi kueleza kazi yetu ya kuhubiri ya Kikristo kwa njia iliyomridhisha ofisa, alituambia kwamba tuliokoka shambulio hilo kidogo tu. Alisema washtakiwa wengi walipigwa risasi, bila kuulizwa maswali. Tulimshukuru Yehova tukafuata shauri la ofisa huyo la kutotangatanga karibu na madaraja wakati ujao.

Nilipataje kuwa katika hali kama hiyo katika Burma (sasa Myanmar)? Acheni nieleze na kuandaa habari fulani juu ya malezi yangu mwenyewe.

Uchaguo Uliofanywa Mapema Maishani

Nilizaliwa Wales katika 1917 na nilipokuwa na miaka sita nilihamia New Zealand pamoja na wazazi wangu na ndugu yangu mchanga zaidi, nilikokulia kwenye shamba la Baba yangu lenye ng’ombe wa maziwa. Siku moja yeye alileta nyumbani vitabu kadhaa vya zamani ambavyo alikuwa amenunua kwenye duka la kuuzia vitu vilivyotumiwa. Miongoni mwao mlikuwa mabuku mawili ya Studies in the Scriptures, yaliyotangazwa na Watch Tower Bible and Tract Society. Hivyo vilikuja kuwa mali za mama yangu zenye kuthamaniwa zaidi, na kama vile mama wa Timotheo, Eunike, yeye alikaza ndani yangu tamaa ya kutumia ujana wangu katika kutumikia faida za Ufalme wa Yehova.—2 Timotheo 1:5.

Katika 1937, nilikabili chaguo mbili: kuchukua usimamizi wa shamba la baba yangu lenye ng’ombe wa maziwa au kumwambia Yehova kama vile nabii wa Mungu Isaya alivyomwambia, “Mimi hapa, nitume mimi.” (Isaya 6:8) Nilikuwa kijana, mwenye afya nzuri, na sikuwa na madaraka. Nilikuwa nimeishi maisha ya shambani na niliyafurahia. Kwa upande ule mwingine, sikuwa na ujuzi wowote wa kuwa mhudumu wa wakati wote, au painia. Ningechagua mwendo gani—kufanya kazi shambani au kutumikia nikiwa painia?

Wasemaji kutoka ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Australia walikuwa chanzo cha kitia-moyo. Walitembelea eneo letu katika New Zealand wakanihimiza nitumie ujana wangu wenye thamani nikimtumikia Mungu. (Mhubiri 12:1) Nilizungumzia jambo hilo pamoja na wazazi wangu, nao wakakubaliana na hekima ya kutanguliza mapenzi ya Mungu. Pia nilitafakari juu ya maneno ya Yesu Kristo katika Mahubiri yake ya Mlimani: “Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.”—Mathayo 6:33.

Nilikuwa nimefanya uchaguo wangu! Kwa kuwa wakati huo hakukuwako tawi la Mashahidi wa Yehova New Zealand, nilialikwa kutumikia kwenye tawi la Australia katika Sidni. Hivyo, katika 1937, nilipanda meli kwenda Australia kuwa mhudumu wa wakati wote wa Yehova Mungu.

‘Nitapokea mgawo upi?’ nikajiuliza. Hata hivyo, tatizo lilikuwa nini? Kwa kweli, nilikuwa nimemwambia Yehova, ‘Mimi hapa. Nitumie popote utakapo.’ Kwa miaka miwili nilisaidia katika kutengeneza vinanda vya santuri vilivyotumiwa na Mashahidi wa Yehova siku hizo ili kuwachezea wenye nyumba hotuba za Biblia zilizorekodiwa. Hata hivyo, kazi niliyozoezwa hasa kufanya kwenye tawi ilikuwa kazi ya depo ya fasihi.

Kwenda Hadi Singapore

Katika 1939, nilipokea mgawo kwenda Mashariki ya Mbali—kutumikia kwenye depo ya Sosaiti katika Singapore. Depo hiyo ilitumikia ikiwa kitovu cha kupokea na kusafirishia fasihi kutoka Australia, Uingereza, na United States hadi nchi nyingi katika Esia.

Singapore lilikuwa jiji lenye lugha nyingi ambako tamaduni za Mashariki na Ulaya zilikuwa zimechanganyika. Lugha ya Malay ilikuwa ndiyo njia ya kawaida ya kuwasiliana, na ili kuhubiri nyumba kwa nyumba, sisi wageni tulilazimika kujifunza lugha hiyo. Katika lugha nyingi, tulikuwa na zile zilizoitwa kadi za ushuhuda. Hizo zilikuwa na utoaji mfupi wa ujumbe wa Ufalme uliokuwa umechapishwa juu yazo.

Mwanzoni nilijifunza kwa moyo ile kadi ya ushuhuda ya lugha ya Malay halafu nikaongeza polepole msamiati wangu wa lugha hiyo. Lakini tulibeba pia fasihi ya Biblia katika lugha nyinginezo nyingi. Kwa kielelezo, kwa wakaaji Wahindi tulikuwa na vichapo katika Kibengali, Kigujarati, Kihindi, Kimalayalam, Kitamil, na Kiurdu. Kukutana na watu wa vikundi vingi vya lugha jinsi hiyo kulikuwa ono jipya kwangu.

Nakumbuka vema lile tangazo lenye kuhofisha la Septemba 1939, julisho rasmi la vita katika Ulaya. Tulijiuliza, ‘Je! itaenea na kuhusisha Mashariki ya Mbali?’ Ilionekana kwangu kuwa utangulizi wa Har–Magedoni—nilidhani ilikuwa imefika kwa wakati ufaao barabara! Nilihisi uradhi kwamba nilikuwa nikitumia ujana wangu kikamili na ifaavyo.

Pamoja na kazi yangu kwenye depo, nilishiriki kikamili katika mikutano ya kundi na huduma ya shambani. Mafunzo ya Biblia yaliongozwa, na baadhi ya watu waliitikia na kujitiisha kwa ubatizo wa maji. Walipelekwa kwenye ufuo mmoja wa bahari uliokuwa karibu na kuzamishwa ndani ya maji yenye ujoto ya bandari ya Singapore. Hata tuliamua kuwa na kusanyiko, tulizungusha mialiko kimya-kimya miongoni mwa wenye kupendezwa. Kwa shangwe yetu, karibu 25 walikuja kwa lile tulilofikiria lingekuwa kusanyiko letu la mwisho kabla ya Har–Magedoni.

Mawasiliano kati ya matawi ya Sosaiti yalizuiwa sana na vita hiyo. Kwa kielelezo, depo yetu ya Singapore ilipokea taarifa fupi kwamba mapainia watatu Wajerumani walikuwa karibu kufika Singapore wakati fulani kwenye meli isiyotajwa jina wakiwa njiani kwenda mgawo usiotambulishwa. Majuma machache baadaye waliwasili wakatumia muda wa saa kumi zenye kusisimua pamoja nasi. Ingawa lugha ilikuwa tatizo, tuliweza kuelewa kwamba mgawo wao ulikuwa Shanghai.

Mgawo Wangu Katika Shanghai

Mwaka mmoja baadaye mimi pia nilipokea mgawo wa kutumikia Shanghai. Sikupewa jina lolote la barabara, nilipewa tu namba ya sanduku la posta. Baada ya kuhojiwa kikamili kwenye ofisi ya posta, niliweza kujitambulisha vya kutosha ili kuweza kupewa mahali pa makao ya Sosaiti. Hata hivyo, mwenye nyumba hiyo Mchina aliniarifu kwamba tawi lilikuwa limehama, na kwamba mahali lilipohamia hapakujulikana.

‘Nifanyeje sasa?’ nikajiuliza. Nilitoa sala kimya-kimya ya kupata mwongozo. Nilipotazama juu, niliona wanaume watatu, waliokuwa warefu kidogo kuliko wenyeji kwa ujumla na walioonekana tofauti na wenyeji kwa kadiri fulani. Walionekana sana kama wale Wajerumani watatu waliotua Singapore kwa muda wa saa chache zilizopita upesi. Upesi, nikaingia njiani mwao.

“Naomba radhi, tafadhali,” nikagugumiza kwa msisimuko. Walitua wakanikazia macho kwa njia ya kutaka kujua habari zaidi wakiwa na macho ya kutafuta-tafuta. “Singapore. Mashahidi wa Yehova. Mwanikumbuka?” nikauliza.

Baada ya dakika chache, walijibu: “Ja! Ja! Ja!” Tulikumbatiana mara moja, na machozi ya shangwe yakatiririka usoni pangu. Kati ya mamilioni ya watu, ilikuwaje kwamba wanaume hao watatu, wapate kupitia mahali hapo wakati huo mahususi? Nilisema tu, “Asante, Yehova.” Familia tatu za Kichina, Wajerumani hao watatu, na mimi tulikuwa ndio Mashahidi pekee katika Shanghai wakati huo.

Hong Kong na Kisha Burma

Baada ya kutumikia katika Shanghai kwa miezi michache, nilipewa mgawo kwenda Hong Kong. Wakati yule ambaye angekuwa mwenzi wangu wa upainia kutoka Australia aliposhindwa kuwasili, nilikuwa peke yangu, Shahidi pekee katika koloni hiyo. Tena, nililazimika kujikumbusha mwenyewe kwamba nilikuwa nimemwambia Yehova, “Mimi hapa. Nitume mimi.”

Utendaji wangu ulielekezwa hasa kwa Wachina waliosema Kiingereza, hata hivyo lilikuwa tatizo kwangu kupita malango ya makao, kwa kuwa watumishi waliowekwa huko walisema Kichina tu. Kwa hiyo nilijifunza Kichina kidogo katika lahaja zayo mbili zinazotumiwa zaidi. Hiyo ikafaulu! Ningewaendea watumishi hao walinzi, na kuonyesha kadi yangu ya biashara, na kusema maneno machache katika Kichina, na kisha nikapelekwa ndani kwa kawaida.

Wakati mmoja nilipokuwa nikitembelea shule moja, nilifuata utaratibu huo nikijaribu kusema na mwalimu mkuu. Mwalimu mdogo alikutana na mimi katika sebule. Nilimfuata kupitia madarasa kadhaa, nikaitikia ishara za watoto za kuonyesha staha, nikajitayarisha kujulishwa kwa mwalimu mkuu. Mwalimu huyo alibisha mlango, akaufungua, na kunitolea ishara ya kuingia. Kwa mshangao wangu wenye hasira, alikuwa amenipeleka chooni kwa hisani! Ilionekana kwamba Kichina changu kilikuwa kimeeleweka vibaya na kwamba, kama vile mwalimu mkuu alivyoniambia baadaye, nilikuwa nimedhaniwa kimakosa kuwa mkaguzi wa mabomba ya maji safi na ya maji machafu.

Baada ya miezi minne ya utendaji, niliarifiwa na polisi wa Hong Kong kwamba kazi yetu ya kuhubiri ilikuwa imepigwa marufuku na kwamba ningehitaji ama kuacha kuhubiri, ama kuondoshwa nchini. Nilichagua kuondoshwa nchini kwani nafasi ya kuhubiri ilikuwa ingali wazi kwingineko. Nilipokuwa Hong Kong, nilikuwa nimeangusha vitabu 462 na nilikuwa nimesaidia wengine wawili washiriki katika huduma.

Kutoka Hong Kong, nilipewa mgawo kwenda Burma. Huko nilifanya upainia na kusaidia katika kazi ya depo katika Rangoon (sasa Yangon). Mojayapo maono yenye kupendeza zaidi lilikuwa lile la kuhubiri katika miji na vijiji vilivyotawanyika kwenye njia kuu kutoka Rangoon hadi Mandalay na mbali zaidi hadi mji Lashio kwenye mpaka wa China. Mwenzi wangu wa upainia na mimi tulikazia jumuiya ya wenye kusema Kiingereza, tukipata mamia kadhaa ya maandikisho ya Consolation (sasa ni gazeti Amkeni!). Baadaye, barabara hiyo kuu kutoka Rangoon hadi Mandalay ingekuja kujulikana kuwa Burma Road, njia ambayo kupitia hiyo ugavi mbalimbali wa kivita kutoka Amerika uliingizwa China.

Kutembea kupitia mavumbi ambayo mara nyingi yalifikia vifundo vya miguu kulitufanya tuhisi uhitaji wa kuoga vizuri. Hilo liliongoza kwenye lile tukio lililosimuliwa mwanzoni, lile la kukamatwa tulipokuwa tukioga katika mto mmoja chini ya daraja. Punde baadaye utendaji wa kijeshi na ugonjwa ukatulazimisha turudi Rangoon. Niliweza kubaki Burma mpaka 1943, wakati utendaji wa vita uliozidishwa uliponilazimisha kurudi Australia.

Kurudi Australia

Wakati uleule, utendaji wa Mashahidi wa Yehova ulikuwa umepigwa marufuku katika Australia. Hata hivyo, marufuku iliondolewa upesi, na hatimaye nikaalikwa kufanya kazi kwenye ofisi ya tawi. Baadaye, katika 1947, nilimwoa Betty Moss, aliyekuwa amefanya kazi kwenye tawi la Sosaiti katika Australia. Baba na mama ya Betty walikuwa mapainia, na waliwatia moyo yeye na kaka yake Bill wafanye upainia kuwa kazi-maisha zao. Betty alianza kufanya upainia siku aliyomaliza shule, akiwa na miaka 14. Nilidhani tungepatana vema, kwani yeye pia, kwa kweli, alikuwa amemwambia Yehova, “Mimi hapa. Nitume mimi.”

Baada ya sisi kuwa tumefunga ndoa kwa mwaka mmoja, nilialikwa kwenye kazi ya mzunguko, nikitembelea makundi ya Mashahidi wa Yehova. Kufanya kazi katika maeneo ya mashambani ya Australia kulikuwa kazi ngumu. Mara nyingi mafuriko ya ghafula yalitokeza matatizo ya usafiri, hasa kwenye barabara za udongo zenye utelezi. Halijoto za kiangazi ziliongezeka hadi digrii 43 sentigredi chini ya kivuli. Tukiwa tunaishi katika hema, tuliona vipindi vya kiangazi vyenye kuunguza kuwa na joto jingi mno karibu lisiweze kuvumilika na vipindi vya baridi kuwa baridi mno.

Ilikuwa shangwe kutumikia nikiwa mwangalizi wa wilaya kulipokuwa wilaya mbili tu katika Australia. Donald MacLean alitumikia wilaya moja, na mimi nilitumikia ile nyingine. Halafu tulikuwa tunabadilishana wilaya. Ni jambo la kusisimua kusoma juu ya makundi yaliyoko sasa mahali tulipotumikia wakati mmoja. Kwa hakika mbegu za kweli ya Biblia zimemea na kuzaa!

Kurudi Mahali Ambapo Hayo Yote Yalianza

Katika 1961, nilikuwa na pendeleo la kuhudhuria darasa la kwanza la shule ya mishonari ya Gileadi baada yayo kuhamia Brooklyn, New York. Kabla ya hapo, nilikuwa nimepokea mialiko mingine ya shule hiyo lakini sikuweza kukubali kwa sababu za afya. Mwishoni mwa mtaala huo wa miezi kumi, nilialikwa kukubali New Zealand kuwa mgawo wangu.

Kwa hiyo tangu Januari 1962, Betty na mimi tumekuwa hapa New Zealand, mojayapo mabara yaliyoko sehemu ya chini ya dunia. Mara nyingi inaitwa mojayapo lulu (visiwa vyenye kupendeza sana) za Pasifiki. Kwa njia ya kitheokrasi, imekuwa shangwe kutumikia katika kazi ya mzunguko na ya wilaya pia. Kwa muda wa miaka 14 ambayo imepita, tangu Aprili 1979, tumekuwa tukifanya kazi kwenye ofisi ya tawi ya New Zealand.

Sasa Betty na mimi tumo katika miaka yetu ya katikati ya 70, na kati yetu tuna miaka 116 ya mfululizo katika utumishi wa Ufalme wa wakati wote. Betty alianza kufanya upainia katika Januari 1933, na mimi katika Aprili 1937. Shangwe zetu zimekuwa nyingi huku tukiwa tumewatazama watoto na wajukuu wetu wa kiroho wakifanya tulivyofanya tulipokuwa vijana, yaani, kutii shauri la Mhubiri 12:1: “Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako.”

Limekuwa pendeleo lililoje kutumia karibu maisha zetu zote tukihubiri habari njema za Ufalme wa Mungu na kufanya wanafunzi, kama vile Bwana wetu Yesu Kristo alivyoamuru! (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Tunafurahi sana kwamba tuliitikia mwaliko wa Mungu kama vile nabii Isaya alivyoitikia zamani za kale, “Mimi hapa. Nitume mimi.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki