Je! Wewe Utanufaika na Fadhili Zisizostahiliwa?
“KADIRI nilivyozidi kujifunza juu ya viwango vya Mungu katika Biblia, ndivyo nilivyohisi nikizidi kupungukiwa ustahiki wa kuwa na upendeleo na baraka yake,” akasema Frank. Kupendezwa kwake na Biblia kulikuwa kumeamshwa alipokuwa gerezani kwa sababu ya makosa ya dawa za kulevya. Alisoma nakala ya kitabu Kweli Iongozayo kwenye Uzima wa Milele,a akahisi uhakika wa kwamba kiliyoyasema yalikuwa ukweli, na, baada ya kuachiliwa gerezani, akapashana habari na Mashahidi wa Yehova ili ajifunze mengi zaidi kuhusu Biblia.
Kwa nini kujifunza Biblia kulimfanya aihisi hakuwa na ustahiki? Kwa sababu mtindo wa maisha yake ya zamani ulikuwa umevunja nyingi za kanuni za Mungu. Utumizi mbaya wa dawa za kulevya, utumizi mbaya wa kileo, na tabia nyingine mbalimbali zenye kushusha tabia ni mambo yaliyokuwa yameshusha sana hadhi yake hivi kwamba katika pindi moja polisi mmoja alisema kwake hivi: “Tafadhali niambie anwani ya nyumbani kwako ni ipi. Nitakalo tu kujua ni mahali nitapeleka maiti yako ukifa!”
Ingawa hivyo, kilichofanya ahisi zaidi kutokuwa na ustahiki ni kwamba ajapojaribu namna gani, aliona ikiwa vigumu sana kushinda tabia hizi zilizoimarika sana za ukosefu wa usafi. Kwa kielelezo, kushikwa sana na zoea la vileo lenye kushusha tabia kulikaribia kumshinda. “Tena na tena mimi nikawa nimeshindwa vibaya kabisa na nikashuka moyo sana,” akasema. “Karibu nikate tamaa kabisa kuhusu hali yangu mwenyewe, nikihisi kwamba mimi ni mtu bure asiye na tumaini.”
Huenda ikawa wengine hapo zamani hawakuwa kama Frank. Hata hivyo, huenda bado wakawa wana hisia za kwamba hawatoshelei. Huenda ikawa hivyo kwa sababu wao hujiwekea viwango vilivyo juu kupita kiasi wajaribupo kuishi kulingana na madai ya Mungu. Washindwapo, huhisi wakiwa na hatia. “Hatia yaweza kusumbua sana kama jinamizi la usiku,” aeleza Dakt. Claire Weekes katika kitabu chake Self-Help for Your Nerves, “hasa kwa wale wanaojaribu kujiwekea kiwango cha juu.” Mkristo aweza kufanya nini akiathiriwa na hisia hizo za utostahiki?
Thamini Fadhili Zisizostahiliwa
“Jambo moja lililonisaidia sana,” akasema Frank, “lilikuwa kuthamini vile Biblia husema kwenye Waebrania 4:15, 16.” Hapo mtume Paulo atukumbusha kwamba Yesu ni msaidiaji mwenye kujali ambaye aweza “kuhurumia udhaifu wetu mbalimbali” na ambaye amefanya iwezekane sisi ‘tujipatie rehema na kupata fadhili zisizostahiliwa ili kuwa na msaada wakati ufaao.”
Je! ungependa ufunguo wa kushinda hisia za utostahiki? Ndio huu: Kumbuka kwamba Yehova Mungu na Yesu Kristo wajua kwamba sisi ni dhaifu kwa sababu ya kutokamilika tulikorithi. Wao waelewa kwamba hatuwezi kutimiza kikamilifu viwango vya uadilifu. (Zaburi 51:5; Warumi 3:23; 5:12, 18; Yakobo 3:2) Kwa hiyo hawatarajii kwetu mambo yazidiyo yale tuwezayo kutoa. Wao hutafuta mema yetu, si udhaifu wetu mbalimbali. Mtunga zaburi aliuliza hivi: “Bwana [Yehova, NW], kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama?” (Zaburi 130:3) Waweza kuthamini kwamba hakuna yeyote kati yetu angeweza. Hata hivyo, kupitia dhabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo Yehova aweza kutupa sisi msimamo safi zijapokuwako hali zetu za kutokamilika. (1 Yohana 2:2; 4:9, 10) Twaweza kupata “msamaha wa mikiuko yetu”—na hivyo tusaidiwe kushinda hisia zozote za utostahiki—“kulingana na mali za fadhili zisizostahiliwa zake.”—Waefeso 1:7, NW.
Fikiria mambo kwa njia hii. Watu ambao hupenda kazi za sanaa hujitahidi sana ili warudishe michoro au sanaa nyinginezo zilizoharibiwa sana. Kwa kielelezo, wakati mtu fulani mwenye bunduki alipoharibu katuni ya Leonardo da Vinci yenye thamani ya pauni milioni 20 (karibu dola milioni 32 za United States) katika Jumba la Michoro ya Kitaifa katika London, Uingereza, hakuna mtu aliyedokeza kwamba kwa kuwa sasa mchoro huo ulikuwa umeharibiwa, wapasa kutupiliwa mbali. Kazi ya kurudisha kazi hiyo ya ustadi yenye miaka 487 ilianza mara ile. Kwa nini? Kwa sababu ilikuwa ya thamani kubwa machoni pa wapenda sanaa.
Je! wewe huna ustahiki mwingi kuliko mchoro wa chaki na makaa? Hakika hivyo ndivyo ulivyo machoni pa Mungu—hata kama umeharibiwa namna gani na udhambi wa kurithi. (Zaburi 72:12-14; Mathayo 20:28) Yehova Mungu, Muumba stadi asilia wa jamaa ya kibinadamu, atafanya mambo ambayo yahitajiwa kabisa ili awarudishe kwenye ukamilifu washiriki wa jamaa hiyo walio na nia ya kuitikia utunzi wake wenye upendo.—Linganisha Matendo 3:21; Warumi 8:20-22.
Itikia Fadhili Zisizostahiliwa
Fuata kielelezo cha mtume Paulo. Yeye alithamini sana fadhili za Mungu katika kumsamehe kwa rehema makosa yake ya zamani na pia katika kutegemeza daima pambano lake la kushinda udhaifu mbalimbali wenye kurudirudi. (Warumi 7:15-25; 1 Wakorintho 15:9, 10) Paulo alisahihisha mwendo wake wa maisha na pia ‘akaupigapiga ngumi mwili wake na kuuongoza kama mtumwa’ ili abaki katika mwendo wenye kukubaliwa na Mungu. (1 Wakorintho 9:27, NW) Hakuacha mwili wake, pamoja na mibetuko yao yenye dhambi ya kimwili na kihisia-moyo, imwongoze yeye kama mtumwa.
Pokea fadhili zisizostahiliwa za Mungu, na uziache zikuongoze kwenye toba. (Warumi 2:4; 2 Wakorintho 6:1) Ikiwa makosa ya wakati uliopita yakusumbua, yarekebishe halafu uamini uhakikisho wa Yehova kwamba amekusamehe. (Isaya 1:16-18; Matendo 2:38) Ukighasiwa na udhaifu mbalimbali wenye kuendelea-endelea, zidi kupigana nao. Sali kwa uzito uombe msaada wa Yehova kuushinda, na huku pia ukitegemea rehema yake. (Zaburi 55:22) Kutokana na mambo aliyojionea mwenyewe, Frank ashauri hivi: “Wakati mtu fulani ashindwapo pindi kwa pindi katika pigano lake dhidi ya tabia fulani mbaya, hapaswi kuiona kama ushinde wa kabisa kabisa, bali kama kipingamizi cha muda.” Wengine wakiongezea matatizo yako kwa kudai mengi kuliko yale uwezayo kutoa, kumbuka kwamba wewe unajaribu kufurahisha Mungu, si wanadamu.—Wagalatia 1:10.
Katika pigano lako la kufanya yaliyo sawa, linda dhidi ya “vitendo vya kiufundi” vya Shetani, vile ambavyo vingeweza kuitwa “kengo ovu za Ibilisi.” (Waefeso 6:11, Reference Bible, kielezo-chini; Today’s English Version) Fikiria “kengo ovu” mbili atakazotumia kujaribu kukunyang’anya manufaa za fadhili zisizostahiliwa.
“Kengo Ovu” za Shetani
Ibilisi hutumia hisia za utostahiki kujaribu kukuvuta mbali na Mungu. Shetani ndiye chimbuko la dhambi iliyokuharibu palepale mwanzoni. Sasa huenda akajaribu kukutia moyo uhisi kwamba hustahiki machoni pa Mungu, kama vile Bildadi alivyojaribu kumfanya Ayubu. (Ayubu 25:4-6; Yohana 8:44) Ni mapigano mengi kama nini yamekuwa ya ushinde kwa sababu askari-jeshi waliingia piganoni wakiwa tayari wamedhoofika moyo! Kwa hiyo, usiache Shetani akudhoofishe moyo. (Waefeso 6:10-13) Kuwa na habari juu ya mbinu za Shetani kwapasa kukuchochee upigane kwa nguvu hata zaidi ili kufanya yaliyo sawa.—2 Wakorintho 2:11.
Ikiwa pindi kwa pindi wewe huhuzunishwa na kasoro za aina moja au nyingine, hakikisha kwamba ‘humezwi kwa kuhuzunika kupita kiasi.’ (2 Wakorintho 2:7, NW) Dakt. Claire Weekes alielezea elekeo la watu fulani kuacha makosa ya wakati uliopita yawalemee hisia: “Kuacha hatia ya zamani ipoozeshe kitendo cha sasa ni maisha yenye kuharibu.”—Ona Matendo 3:19.
Kama sisi tungeweza kutimiza matakwa yote ya Mungu kikamilifu, zingekuwa ni fadhili zenye kustahiliwa kwamba yeye atupe baraka ambazo ameahidi. Lakini Yehova Mungu na Yesu Kristo wanatuonyesha fadhili “zisizostahiliwa.” Kamusi A Greek-English Lexicon of the New Testament, iliyotungwa na J. H. Thayer, yafafanua maana ya neno lililotumiwa na mtume Paulo kuaridhia sifa hii ya Mungu: “Neno hilo [khaʹris] lina wazo la fadhili ambazo huweka juu ya mtu kitu ambacho hakustahili.” Hakuna kazi zetu ambazo zaweza kuchuma baraka ya Mungu. Ni fadhili zisizostahiliwa, kama Paulo asemavyo. Ikiwa kwa weupe wa moyo unafanya yote uwezayo katika mipaka ya uwezo wake ili kutimiza wajibu wako mbalimbali kwa Mungu, furahia kufanya hivyo. Yehova hakuombi mengi zaidi ya hayo.
Hata hivyo, uwe na habari juu ya nyingine za “kengo ovu” za Shetani. Yeye huongoza vibaya watu fulani wafikiri kwamba wao waweza kutumia fadhili zisizostahiliwa za Mungu kwa faida zao wenyewe, kwamba waweza kuchezea rehema yake. Kwa upendo Yehova husamehe udhaifu wetu mbalimbali, lakini hiyo haimaanishi twaweza kuacha kung’ang’ana nao. Paulo aliaridhia habari ya watu fulani waliokuwa ‘wamekanyaga-kanyaga Mwana wa Mungu na kwa madharau wakaitia kasirani kali ile roho ya fadhili zisizostahiliwa.’ (Waebrania 10:29, NW) Watu hawa hawakuwa wameonyesha staha yoyote kwa kanuni za uadilifu na wakapuuza sheria za Mungu kimadharau, wakijiweka katika hali ya kutoweza kurudi. Yuda ndugu-nusu wa Yesu, aliyeiona hatari iliyotokezwa na mabaradhuli hao wa Shetani, aliandika hivi: “Watu fulani wamejipenyeza ndani [kwenye makundi], . . . watu wasioogopa Mungu, wakigeuza fadhili zisizostahiliwa za Mungu wetu ziwe udhuru wa mwenendo mlegevu.”—Yuda 4, NW.
Huenda Shetani akapumbaza watu hao wafikiri kwamba kwa kiasi fulani waweza kuingilia makosa halafu waombe Mungu asamehe dhambi yao. Lakini Yehova hatasamehe watu hao wenye kuvunja kimakusudi sheria zake. Yeye ni “mwingi wa fadhili-upendo” kwa wale wenye kujitahidi kumtumikia kwa kadiri wawezavyo wajapokuwa na hali zao za kutokamilika. “Lakini kwa vyovyote hatatoa achilio la adhabu” wakati istahiliwapo.—Kutoka 34:6, 7, NW.
Waweza Kunufaika na Fadhili Zisizostahiliwa
Inafariji kujua kwamba Yehova hakuoni wewe katika hali yako ya kutokamilika, yenye kuharibika-haribika tu. Yeye ajua vile wewe uwezavyo kuwa wakati nguvu za urudishaji za dhabihu ya ukombozi ya Yesu zitumiwapo kikamili. Kwa hiyo, mpelekee Yehova sala kwa uhakika kama alivyofanya mtunga zaburi Daudi. “Nionyeshe upendeleo, O Mungu,” akasema Daudi, “kulingana na fadhili-upendo zako. Kulingana na wingi wa rehema zako futilia mbali miruko-mipaka yangu. Nioshe kosa langu kabisa kabisa, na unisafidi mimi hata dhambi yangu. Kwa maana mimi mwenyewe najua miruko-mipaka yangu, na dhambi yangu iko mbele yangu daima. Sitiri uso wako kutoka kwenye dhambi zangu, na pangusia mbali makosa yangu yote. . . . Moyo uliovunjika na kupondeka, O Mungu, wewe hutaudharau.”—Zaburi 51:1-3, 9, 17, NW.
Miruko-mipaka na makosa yako huenda vikawa mbele yako daima. Nyakati fulani huenda ukahisi kama yule mwana mfujaji aliyeelezwa na Yesu. Mwanamume kijana huyu aliporudi nyumbani baada ya kuponda urithi wake kiaibu katika mahali pa kigeni, alitoa mshangao huu kwa baba yake: “Mimi sistahiki tena kuitwa mwana wako”! (Luka 15:21, NW) Hata hivyo, mwanamume kijana huyu alikuwa na mtazamo ufaao. Hakukataa fadhili za baba yake wala hakujaribu kuzichezea. Kwa hiyo baba yake alimpokea kwa upendo arudi kati ya watu wa nyumba yake. (Luka 15:20-24) Yehova hufurahi kufanya hivyo hivyo leo kwa ajili ya watu wenye dhambi ambao hujaribu kufanya penzi lake bila mchezo.—Zaburi 103:8-14; Isaya 55:7.
Frank hakuruhusu hisia za utostahiki zimlemee. Aliitikia fadhili zisizostahiliwa za Mungu, na sasa atumikia akiwa mtumishi wa huduma katika kundi moja la Mashahidi wa Yehova. Yeye asema kwamba, “sasa mimi huruka kwa shangwe nifikiriapo ambacho Yehova Mungu na Yesu Kristo wametufanyia na bado watatufanyia!”
[Maelezo ya Chini]
a Kimetangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.