Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
◻ MTUME Yohana alisema: “Tusipende kwa neno, wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.” (1 Yohana 3:18) Yesu alisema kwamba ‘tupende jirani yetu kama nafsi yetu.’ (Mathayo 22:39) Kuonyesha upendo kwa tendo huupendekeza ukweli, kama vile lionyeshavyo ono linalofuata kutoka Uingereza.
Pauline alipozuru mama yake, aliyekuwa na multiple sclerosis (ugonjwa wenye kupoozesha maungo) nyakati zote hakukuwa na mtu mwingine yeyote huko. Lakini katika pindi hii, alipokuwa akiiingia nyumba, angeweza kusikia mashine ya kufulia ikifanya kazi na mtu fulani akitumia fagio-umeme kwenye ghorofa ya nyumba hiyo. “Kuna nini, kuna nani huku?” akamwuliza mama yake. Mama yake akamweleza kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wamekuja mlangoni pake, wakaona shida yake, na kukaa kidogo wamsaidie. Baada ya wao kufanya kazi ya nyumba na kutayarisha mlo, waliketi na kusema: “Je! uko tayari?” “Tayari kwa kitu gani?” akauliza Pauline. Mama yake alimweleza kwamba alikuwa amekubali kufanya funzo la Biblia. Pauline akasita-sita kukaa, lakini kwa kuwa alikuwa amekuja mwendo mrefu, akauliza kama ingekuwa sawa yeye ajiunge katika funzo hilo. Alilionea shangwe sana hata akapanga kuja siku iyo hiyo kila juma ili aweze kuhudhuria kwa ukawaida. Hatimaye, rafiki mmoja aliandamana naye, na sasa wote wawili wamebatizwa. Kutokana na funzo hili la asili, sasa washiriki kumi wa jamaa iyo hiyo ni Mashahidi wa Yehova! Ndiyo, kweli huo ulikuwa msaada “kwa tendo”!
Pasta Katika New Guinea Aitikia Ukweli
◻ Katika siku ya Yesu makuhani fulani walikubali fundisho la Yesu. Makasisi wenye mioyo ya kufuata haki leo hufanya hivyo pia, kama ionyeshwavyo na ono moja kutoka nyanda za juu za New Guinea, lililoripotiwa na mwangalizi wa mzunguko. Yeye asimulia hivi: “Mwanamume kijana mwenye elimu nyingi, pasta wa Kipentekoste, alikuwa akijenga kanisa dogo karibu sana na Jumba la Ufalme. Ndugu mmoja kutoka kundi hilo alimtolea ushahidi, naye akaonekana mwenye urafiki. Muda mfupi baada ya hapo, nilizuru kundi hilo nikakaa pamoja na ndugu huyo kwenye barabara hiyo chini kidogo tu kutoka kwenye nyumba ya pasta. Jioni ya kwanza baada ya mimi kuwasili, mwanamume huyu kijana alikuja kwenye mlango wetu akiwa na Biblia, pamoja na kikundi kikubwa cha kutoka kundi lake. Wote walitaka kuusikia ujumbe wa Ufalme. Yeye aliuliza maswali mengi, na mazungumzo yakaendelea vizuri hadi usiku. Kila jioni ya ziara yangu, yeye na wapendezwa wengine walikuja kujibiwa mengi zaidi ya maswali yao. Mimi nikamwalika kwenye kusanyiko la mzunguko juma lililofuata, naye akahudhuria kwa kuandamana na ndugu aliyekuwa amemtolea ushahidi mara ya kwanza. Mwanamume huyu aliendelea na funzo lake la Biblia, ameacha Kanisa la Kipentekoste, na sasa ni mhubiri wa kawaida wa habari njema.”
Kwa kweli, ni mapenzi ya Mungu “kwamba namna zote za watu waokolewe na kuja kwenye maarifa yaliyo sahihi ya ukweli.”—1 Timotheo 2:4, NW.