Je! Wewe Wathamini Yale Ambayo Mungu Amefanya?
“Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba [mti wa mateso, NW] wake kila siku, anifuate.”—LUKA 9:23.
SISI twawiwa na Mungu uhai wetu. Kama yeye asingaliumba ainabinadamu, tusingalizaliwa kamwe. Lakini Mungu hakuumba uhai tu. Alitufanya sisi kwa njia ambayo tungeweza kuonea shangwe vitu vingi: ladha ya chakula, ujotojoto wa nuru ya jua, mvumo wa muziki, hewa safi ya siku ya masika, wororo wa upendo. Hata zaidi, Mungu alitupa sisi akili na tamaa ya kujifunza mengi juu yake. Aliivuvia Biblia, ambayo hutupa sisi mwongozo timamu, hutuonyesha kuishi maisha zenye furaha zaidi, na hutuandalia tumaini la kuishi milele katika ulimwengu mpya wake wenye uadilifu. Pia Mungu huandaa roho takatifu yake, tegemezo la kundi la kwetu, na wanaume na wanawake wazee wenye upendo wawezao kutusaidia tubaki imara katika utumishi wake.—Mwanzo 1:1, 26-28; 2 Timotheo 3:15-17; Waebrania 10:24, 25; Yakobo 5:14, 15.
2 Zaidi ya yote hayo, Mungu alituma Mwana wake mwenyewe aliye mzaliwa wa kwanza atuambie mengi zaidi juu ya yale ambayo Baba atarajia kwetu na aandae “uachilio kwa njia ya ukombozi” kwa ajili ya kila mtu ambaye ataukubali. (Waefeso 1:7; Warumi 5:18, NW) Mwana huyo, Yesu Kristo, alisema hivi: “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Wokovu ambao ukombozi huo ulifanya uwezekane ni wa thamani bora kabisa hivi kwamba kwa vyovyote hakuna njia ambayo mtu yeyote angeweza kufanya matendo ya kuuchuma, kwa uhakika si kazi zilizofanywa hapo kwanza chini ya Sheria ya Musa. Hivyo, Paulo aliandika hivi: “Mwanadamu hahesabiwi haki kwa matendo ya sheria, bali kwa imani ya Kristo Yesu.”—Wagalatia 2:16; Warumi 3:20-24.
Imani na Kazi
3 Wokovu huja kwa imani, lakini imani na uthamini kwa yote ambayo Mungu amefanya vyapasa kutusukuma kwenye kitendo. Vyapasa kutuchochea tufanye mambo yaonyeshayo imani yetu. Yakobo ndugu-nusu ya Yesu aliandika hivi: “Imani, isipokuwa ina matendo, imekufa nafsini mwake.” Zaidi ya hilo alisema hivi: “Nionyeshe imani yako pasipo matendo, nami nitakuonyesha imani yangu kwa njia ya matendo yangu.” Yakobo alionyesha wazi kwamba hata roho waovu “waamini na kutetemeka,” lakini ni wazi kwamba roho waovu hawafanyi kazi za kimungu. Kwa upande mwingine, Abrahamu alikuwa na vyote viwili imani na kazi. “Imani ilitenda kazi pamoja na matendo yake, na ya kwamba imani ile ilikamilishwa kwa njia ya matendo yale.” Yakobo alirudia hivi: “Imani pasipo matendo imekufa.”—Yakobo 2:17-26.
4 Pia Yesu alionyesha umaana wa matendo yafaayo, akisema hivi: “Nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni.” “Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba [mti wa mateso, NW] wake kila siku, anifuate.”a ‘Tukijikana’ wenyewe, twaacha mengi ya machaguo yetu ya kibinafsi. Twatambua kwamba twawiwa na Mungu kila kitu, kwa hiyo twajitoa kwake tukiwa watumwa wake, tukitafuta kujifunza na kufanya mapenzi yake, kama alivyofanya Yesu.—Mathayo 5:16; Luka 9:23; Yohana 6:38.
Maisha Zaathiriwa
5 Petro alionyesha wazi kwamba “damu ya thamani” ya Kristo, iliyotolewa kwa ajili yetu, ni ya thamani izidiyo sana hivi kwamba kuithamini kwetu kwapasa kuonekane wazi katika njia nzima ya maisha yetu. Mtume aliorodhesha mambo mengi ambayo uthamini wetu wapasa utuharakishe kuyafanya. Alishauri hivi: “Wekeni mbali ubaya wote.” “Fanyizeni tamanio la la maziwa yasiyotoholewa ya lile neno.” ‘Tangazeni kotekote matukufu ya yule mmoja aliyeita nyinyi kutoka gizani kuingia katika nuru yake ya ajabu.” “Geukeni kutoka lililo baya na mtende lililo jema.” “Fanyeni utetezi mbele ya kila mmoja adaiye kutoka kwenu sababu ya tumaini lililo ndani yenu.” “Ishini sehemu ya wakati [wenu] uliobaki katika mnofu, si kwa ajili ya tamaa za wanadamu tena, bali kwa ajili ya mapenzi ya Mungu.”—1 Petro 1:19; 2:1, 2, 9; 3:11, 15; 4:2, NW.
6 Wakristo wa karne ya kwanza waliishi kulingana na imani yao. Hiyo iliwabadili mwelekeo wa maoni na nyutu zao, ikiwachochea wapatanishe maisha zao na mapenzi ya Mungu. Waliteseka kwa kuhamishwa, kupigwa mawe, kuchapwa-chapwa, kutiwa gerezani, na hata kuuawa kuliko kuvunja imani yao. (Matendo 7:58-60; 8:1; 14:19; 16:22; 1 Wakorintho 6:9-11; Waefeso 4:22-24; Wakolosai 4:3; Filemoni 9, 10) Tasito mwanahistoria maarufu Mroma, aliyezaliwa karibu 56 W.K., asema kwamba Wakristo ‘walihukumiwa miali na wakachomeka, ili wawe mmuliko wakati wa usiku, wakati nuru ya mchana ilipokuwa imekwisha.” Na bado hawakuyumba-yumba!—The Annals, Kitabu cha 15, fungu la 44.
7 Katika makundi fulani huenda ukakuta watu ambao wamehudhuria mikutano kwa miaka mingi. Wao hupenda tengenezo la Yehova, wana fikira ya kwamba watu wake ndio watu bora kabisa waliopata kukutana nao, tena wao hutoa maelezo mazuri juu ya ukweli, na kutetea ukweli kwa watu wa nje. Lakini kitu fulani huwafungia njia, kitu fulani hufanya wasitesite. Wao hawajachukua kamwe ile hatua nzuri ambayo wale 3,000 waliichukua siku ya Pentekoste, ile ambayo Mwethiopia mwenye kuamini aliulizia, au ile ambayo Anania alimhimiza Sauli aichukue mara tu mnyanyasi huyo wa hapo kwanza alipokwisha kung’amua kwamba kwa kweli Yesu alikuwa ndiye Mesiya. (Matendo 2:41; 8:36; 22:16) Ni kitu gani kinachokosekana kwa watu wa jinsi hiyo leo? Kwa nini hawajaichukua hatua ambayo Biblia huiita “ombi lifanywalo kwa Mungu kwa ajili ya dhamiri njema”? (1 Petro 3:21, NW) Ukikuta kwamba wewe mwenyewe umo katika hali hiyo—kuujua ukweli lakini kusitasita kuuchukulia hatua—ione makala hii kuwa imetayarishwa kwa upendo maalumu kwa ajili yako.
Kushinda Vipingamizi Vizuiavyo Ubatizo
8 Ni kitu gani kingeweza kuwa chakufungia njia? Makala iliyotangulia ilionyesha kwamba huenda watu fulani wakaona funzo la kibinafsi kuwa tatizo. Mungu alitupa sisi akili nzuri ajabu, naye hututarajia tuzitumie kumtumikia. Watu fulani ambao hata hawakuwa wamejifunza kusoma walijitoa kufanya jambo hilo la jasho ili wajifunze mengi zaidi juu ya Mungu na makusudi yake. Namna gani wewe? Ikiwa wewe tayari wajua kusoma, je! wewe hujifunza kikweli, kama walivyofanya Waberoya, ‘wakichunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku’ ili waone kama mambo haya ndivyo yalivyo? Je! umepeleleza “upana na urefu na kina” cha ukweli? Je! umechimba kwa kina kirefu ndani ya Neno la Mungu? Je! umetafuta kujua jinsi hilo lilivyo jambo la kusisimua sana? Je! kweli wewe una njaa asilia, kwa ajili ya ukweli?—Matendo 17:10, 11; Waefeso 3:18.
9 Nyakati fulani watu husitasita kwa sababu ya tatizo halisi au la kuwaziwa tu ambalo wamekuwa wanalo pamoja na mtu fulani katika kundi. Je! mtu fulani amekuudhi kwa uzito? Basi fuata mwongozo uonyeshwao na maneno ya Yesu: “Nenda ukafunue kosa lake kati yako wewe na yeye peke yenu.” (Mathayo 18:15, NW) Huenda ukashangaa kupata kwamba mtu huyo hata hakujua kwamba wewe uliudhika. Lakini hata akijua, huenda bado ‘ukampata ndugu yako,’ kama vile Yesu alivyosema. Huenda pia ukamsaidia aepuke kukwaza mtu mwingine. Zaidi ya hilo, ufikiriapo hilo, wewe unatumikia nani kwa kweli—mtu huyo au Mungu? Je! upendo wako kwa Mungu ni haba sana hivi kwamba ungeacha kosa la binadamu asiyekamilika livuruge upendo wako Kwake?
10 Huenda dhambi ya siri ikazuia mtu asibatizwe. Hilo lingeweza kuwa jambo lililotukia wakati uliopita, au huenda kikawa ni kigezo kibaya kinachoendelea. Ikiwa hili ni tatizo kwako, je! huu sio wakati wa kusahihisha jambo hilo? (1 Wakorintho 7:29-31) Wengi wa watu wa Yehova wamelazimika kufanya mabadiliko katika maisha zao. Biblia husema: “Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu zifutwe, zipate kuja nyakati za kuburudishwa kwa kuwako kwake Bwana [Yehova, NW].”—Matendo 3:19.
11 Hata liwe ni jambo gani ulilofanya wakati uliopita, waweza kutubu, ubadilike, na uombe msamaha wa Mungu. “Basi, vifisheni viungo vyenu vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya, mawazo mabaya, na kutamani . . . [vueni] kabisa utu wa kale, pamoja na matendo yake; mkivaa utu mpya, unaofanywa upya upate ufahamu sawasawa na mfano wake yeye aliyeuumba.” Wewe waweza kupatanisha maisha yako na njia zake, uone shangwe ya dhamiri safi, na uwe na tumaini la uhai wa milele katika ulimwengu mpya wake wenye uadilifu. Je! huo hauhalisi jitihada yoyote ile?—Wakolosai 3:5-10; Isaya 1:16, 18; 1 Wakorintho 6:9-11; Waebrania 9:14.
12 Je! utumizi wa tumbako, utumizi mbaya wa vileo, au uzoelevu wa dawa za kulevya wakuzuia usiwe na dhamiri safi? Je! mazoea hayo yenye kutisha uhai hayaonyeshi ukosefu wa staha kwa zawadi nzuri ajabu ya Mungu ya uhai? Ikiwa mazoea hayo yakuzuia, hakika huu ndio wakati wa kuyasahihisha. Je! mazoea haya ni ya bei moja na uhai wako? Paulo alisema: “Na tujitakase nafsi zetu na uchafu wote wa mwili na roho, huku tukitimiza utakatifu katika kumcha Mungu.” Je! wewe wazithamini njia safi na adilifu za Mungu kwa kadiri ya kutosha kufanya hivyo?b—2 Wakorintho 7:1.
Vitu vya Kimwili
13 Ulimwengu wa leo hutanguliza mafanikio na “wonyesho mshaufu wa mali za maisha za mtu” mbele ya karibu kila kitu kinginecho. Lakini Yesu alifananisha “mahangaiko ya mfumo huu wa mambo na uwezo mdanganyifu wa mali” na “miiba” ambayo hulisonga neno la Mungu. Pia aliuliza hivi: “Atafaidiwa nini mtu akiupata ulimwengu wote, na kupata hasara ya nafsi yake?”—1 Yohana 2:16, NW; Marko 4:2-8, 18, 19; Mathayo 16:26.
14 Yesu alionyesha kwamba Mungu alipanga ili nyuni wapate chakula na maua yachanue kwa uvutio. Halafu akauliza hivi: “Bora ninyi mara nyingi kuliko ndege! . . . Je! [Mungu] hatawatendea ninyi zaidi?” Kwa hekima, Yesu alituambia tuache ‘kusumbukia’ vitu vya kimwili. Alisema hivi: “Utafuteni [kwa uendelevu, NW] ufalme wa Mungu, na hayo mtaongezewa.” Alionyesha wazi kwamba twapaswa kuweka mambo ya kimbingu kwanza kwa sababu ‘hazina yetu ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wetu.’—Luka 12:22-31; Mathayo 6:20, 21.
Utumishi wa Kimungu kwa Msaada wa Mungu
15 Je! wewe huelekea kutatizika kuwapa wengine ushahidi? Je! haya husababisha usitesite? Ikiwa ndivyo, ni jambo la maana kukumbuka kwamba Wakristo wa karne ya kwanza walikuwa na aina ile ile ya hisia tulizo nazo leo. Mungu hakuchagua wengi wenye hekima na uwezo, bali alichagua “mambo mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima.” (1 Wakorintho 1:26-29) Viongozi wa kidini wenye uwezo walipinga watu hawa ‘wa kikawaida’ na kuwaagiza waache kuhubiri. Wakristo hao walifanya nini? Walisali. Walimwomba Mungu ujasiri, naye akawapa. Tokeo ni kwamba, ujumbe wao ulijaaa Yerusalemu na baadaye ukatikisa ulimwengu mzima!—Matendo 4:1-4, 13, 17, 23, 24, 29-31; 5:28, 29; Wakolosai 1:23.
16 Hivyo, kuhofu wanadamu hakupasi kamwe kutuzuie kutumikia Mungu. Waebrania sura ya 11 hutuambia juu ya “wingu kubwa la mashahidi” waliohofu Mungu, si wanadamu. Twapaswa kuonyesha imani kama hiyo. Mtume aliandika hivi: “Kwa kuwa tunazungukwa na wingu kubwa la mashahidi namna hii, na tuweke kando kila mzigo mzito, na dhambi ile ituzingayo kwa upesi; na tupige mbio kwa saburi katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu.”—Waebrania 12:1.
17 Mungu aweza kuandalia watumishi wake msaada mkubwa ajabu. Muumba wa ulimwengu wote mzima alimwambia Isaya hivi: “Wao wamngojeao BWANA [Yehova, NW] watapata nguvu mpya; watapanda juu kwa mbawa kama tai; watapiga mbio, wala hawatachoka; watakwenda kwa miguu, wala hawatazimia.”—Isaya 40:31.
18 Mashahidi wenye moyo mkuu na furaha ambao wewe huwaona katika kundi la kwenu ni kisehemu kidogo tu cha watumishi zaidi ya milioni tatu na nusu ambao ni wenye bidii duniani pote. Wao hushangilia kuwa na sehemu katika kazi ambayo Yesu Kristo mwenyewe alitabiri kwa maneno haya: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia nzima yote inayokaliwa kwa ajili ya ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakuja.” Ikiwa kushiriki katika kuhubiri Ufalme huwa tatizo kwako hata ingawa wastahili kufanya hivyo, kwa nini usiombe Shahidi afanyaye vema katika huduma aende nawe mkashiriki katika kazi ya kuhubiri? Kwa kweli Mungu huandaa “uwezo upitao ulio wa kawaida,” na huenda wewe ukashangaa kugundua jinsi utumishi huu wa kimungu ulivyo wenye shangwe sana.—Mathayo 24:14; 2 Wakorintho 4:7, NW; ona pia Zaburi 56:11; Mathayo 5:11, 12; Wafilipi 4:13.
19 Yesu hutarajia wale wathaminio ujumbe wa Ufalme wauchukulie hatua. Alisema hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru nyinyi.”—Mathayo 28:19, 20, NW.
20 Je! kuthamini kwako baraka za Mungu, “damu ya thamani” ya Yesu, na lile tumaini zuri sana la uhai wa milele kwakusukuma uchukue hatua? (1 Petro 1:19) Je! wewe umepatanisha maisha yako na matakwa ya Mungu ya uadilifu? Je! wewe hushiriki kwa ukawaida kufanya wanafunzi? Je! umejikana na kuweka maisha yako wakfu kwa Mungu? Jibu la maswali yote hayo likiwa ni ndiyo ya uhakika kabisa, huenda ukawa ni wakati wa kuuliza mmoja wa wazee katika kundi ambalo wewe wahudhuria swali lile lile ambalo Mwethiopia mwenye kuamini alimwuliza Filipo: “Nini kinachonizuia nisibatizwe?”—Matendo 8:36.
[Maelezo ya Chini]
a The Jerusalem Bible hufasiri hilo kuwa “ajikatae katakata.” Fasiri ya J. B. Phillips husema “aache kabisa haki yote aliyo nayo mwenyewe.” The New English Bible husema “ajiache nyuma.”
b Ili upate habari juu ya kuacha mazoea ya jinsi hiyo, ona Mnara wa Mlinzi, Februari 1, 1981 (Kiingereza), kurasa 3-12; Desemba 1, 1973 (Kiswahili), kurasa 542-549; na Amkeni!, Julai 8, 1982 (Kiingereza), kurasa 3-12; Mei 22, 1981 (Kiingereza), kurasa 3-11. Hayo yaweza kupatikana maktabani kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova la kwenu.
Je! Wewe Wakumbuka?
◻ Tuna sababu gani maalumu za kuwa wenye shukrani kwa Mungu?
◻ Imani na uthamini vyapasa kutuchochea tufanye nini?
◻ Ni matatizo gani ambayo huenda yakatuzuia kumtii Mungu, nasi tungeweza kufanya nini nayo?
◻ Watu wasiobatizwa bado waweza kujiuliza maswali gani?
[Maswali ya Funzo]
1. Ni nini baadhi ya zawadi nzuri ajabu ambazo Mungu ameandaa?
2. (a) Ni kitu gani cha kutokeza zaidi ambacho Mungu ameandaa? (b) Je! twaweza kuchuma wokovu kupitia kazi?
3. Yakobo alisema nini juu ya imani na kazi?
4. Yesu alisema wale watakao kumfuata wapaswa kufanya nini?
5. (a) Petro alionyesha ni nini kipasacho kuathiri njia yetu nzima ya maisha? (b) Alipendekeza kazi gani nzuri?
6. (a) Wakristo wa karne ya kwanza walionyeshaje imani yao? (b) Jambo hilo lapasa kutuwekea kielelezo gani?
7. Huenda watu fulani wakajikuta katika hali gani?
8. Ikiwa wewe hujapata kamwe kuwa mwanafunzi mwema, ingekuwa hekima ufuate mwendo gani sasa?
9. Ni jambo gani lifaalo kufanywa ikiwa una tatizo na mtu fulani katika kundi?
10, 11. Wapaswa kufanya nini ikiwa dhambi fulani ya siri imekuwa ikifanya usitesite?
12. Wapaswa kufanya nini ikiwa tumbako, utumizi mbaya wa vileo, au dawa zenye uzoelevu zakuzuia kuwa na dhamiri safi?
13, 14. (a) Maandiko yasema nini juu ya miradi ya kufuatia vitu vya kimwili? (b) Kwa nini ni jambo la maana kuweka mambo ya kimbingu kwanza?
15. Kielelezo cha Wakristo wa karne ya kwanza chatupa sisi kitia-moyo gani kizuri?
16. Twajifunza nini kutokana na “wingu kubwa la mashahidi” wasimuliwao katika Waebrania sura ya 11?
17. Ni kitia-moyo gani ambacho Mungu alitoa kupitia Isaya?
18. Wewe ungewezaje kushinda woga ili ushiriki kuhubiri Ufalme?
19. Ni kazi gani ya kufundisha ambayo Yesu aliamuru wafuasi wake wafanye?
20. Ikiwa wewe unasonga mbele kiroho, ni swali gani ambalo huenda likafaa karibuni?
[Sanduku katika ukurasa wa 18]
‘Mimi ni aina gani ya “udongo”’?
Yesu alitoa kielezi cha mtu aliyeenda nje kupanda mbegu. Mbegu fulani zilianguka kando ya njia zikaliwa na ndege. Nyingine zilianguka juu ya mahali penye miamba pasipo na udongo mwingi. Zilichipuka, lakini jua lilipopanda juu, zikanyauka na kufa. Bado mbegu nyingine zilianguka miongoni mwa miiba zikasongwa. Yesu alisema kwamba vikundi vitatu hivi viliwakilisha: kwanza, mtu “alisikiapo neno la ufalme asielewe nalo”; pili, mtu alikubaliye neno lakini aondoshwa na joto la “dhiki au udhia [mnyanyaso, NW]”; na tatu, mtu ambaye “shughuli za dunia, na udanganyifu wa mali hulisonga lile neno.”
Lakini pia Yesu alieleza juu ya mbegu nyingine iliyoanguka juu ya udongo mzuri. Alisema: “Huyo ndiye alisikiaye lile neno, na kuelewa nalo; yeye ndiye azaaye matunda.”—Mathayo 13:3-8, 18-23.
Ingefaa kujiuliza hivi: ‘Mimi ni “udongo” wa aina gani?’
[Sanduku katika ukurasa wa 19]
Walifia imani yao
Je! wewe wajua mtu yeyote ambaye huona ni afadhali kufa kuliko kuvunja imani yake? Maelfu ya Mashahidi wa Yehova wamefanya hivyo. Katika The Nazi State and the New Religions: Five Case Studies in Non-Conformity, Dakt. Christine E. King aliandika hivi: “Mmoja kati ya kila Mashahidi wawili Wajeremani alitiwa gerezani, mmoja katika wanne alipoteza uhai wake.”
Mabaya ya kuogofya sana katika kambi yalipoisha mwishowe katika 1945, “hesabu za Mashahidi zilikuwa zimeongezeka na hakuna uridhiano uliokuwa umefanywa.” Katika The Nazi Persecution of the Churches, J. S. Conway aliandika hivi juu ya Mashahidi: “Hakuna farakano [dhehebu] jingine lililokaribia kuonyesha azimio lile lile kwa kukabiliana na mwogofyo kamili wa Magestapo.”
Mashahidi wa Yehova hawakunyanyaswa kwa sababu ya siasa wala rangi ya ngozi. Bali, sababu kamili ya kuteseka kwao ilikuwa upendo wao kwa Mungu na kukataa kwao kutenda kinyume cha dhamiri zao zilizozoezwa na Biblia.