Simameni Imara Katika Uhuru wa Kikristo!
Mambo Makuu Kutokana na Wagalatia
YEHOVA ndiye Mungu wa uhuru. (2 Wakorintho 3:17) Mwana wake, Yesu Kristo, alisema hivi: “Mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.” (Yohana 8:32) Na katika kumwiga Kristo, mtume Paulo alihubiri habari njema za uhuru.—Warumi 6:18; 8:21.
Kwa kujulisha rasmi ujumbe huo wenye kutoa uhuru, Paulo alianzisha makundi ya Galatia (mkoa wa Kiroma katika Esia Ndogo) wakati wa ziara yake ya kwanza ya kimisionari (47-48 W.K.). Wagalatia walijua juu ya uamuzi wa baraza lenye kuongoza kwamba tohara si takwa kwa Wakristo. (Matendo 15:22-29) Lakini watetezi wa mawazo ya dini ya Kiyahudi walikuwa wakitafuta kuwaingiza ndani ya utumwa kwa kusisitiza kwamba watahiriwe. Hivyo basi Paulo alikazia uhuru wa Kikristo katika barua aliyowaandikia Wagalatia akiwa Korintho au Antiokia ya Siria karibu 50-52 W.K. Mathalani, yeye alisema hivi: “Kristo alitufanya huru kwa uhuru; basi, simameni, musiingie tena katika kongwa la utumwa.”—Wagalatia 5:1, ZSB.
Paulo Atetea Utume Wake
Kwanza Paulo alionyesha kwamba utume wake ulikuwa kupitia “Yesu Kristo, na Mungu.” (1:1–2:14) Kwa sababu ya ufunuo, Paulo (pamoja na Barnaba na Tito) alienda Yerusalemu kuhusu suala la tohara. Huko Yakobo, Kefa (Petro), na Yohana walitambua kwamba yeye alikuwa ametiwa nguvu kuwa mtume kwa mataifa. Na wakati Petro baadaye alipojitenga na waamini Wasio Wayahudi huko Antiokia kwa sababu ya kuhofu Wakristo Wayahudi wa kutoka Yerusalemu, Paulo alimkaripia.
Kujulishwaje Rasmi Kuwa Waadilifu?
Mtume pia alitoa wazo lenye nguvu kwamba ni kupitia imani tu katika Yesu Kristo kwamba mtu yeyote aweza kujulishwa rasmi kuwa mwadilifu. (2:15–3:29) Wagalatia walipokea roho ya Mungu, si kwa sababu ya kazi za sheria, bali kwa sababu ya kuzikubali habari njema kwa imani. Wana wa kweli wa Abrahamu wana imani, lakini watu mmoja mmoja wanaojaribu kujithibitisha kuwa waadilifu kwa “matendo ya sheria, wako chini ya laana.” Kwa nini? Kwa sababu hawawezi kuishika Sheria kikamilifu. Kwa kweli, Sheria ilifanya makosa yadhihirike nayo ilikuwa “kiongozi kutuleta kwa Kristo.”
Simameni Imara!
Kwa kifo chake, Kristo ‘aliwakomboa waliokuwa chini ya sheria.’ Lakini ni lazima wafuasi wake wasimame imara katika uhuru wa Kikristo. (4:1–6:18) Hivyo Wagalatia walihitaji kukinza mtu yeyote anayejaribu kuwashawishi wakubali nira ya utumwa. Zaidi ya hilo, hawakupaswa kuutumia vibaya uhuru wao bali walipaswa kuepuka “matendo ya mwili” na kuonyesha tunda la roho ya Mungu. Wale wenye kutafuta kuwaleta ndani ya utumwa wa Sheria walitaka “kuonekana ni wazuri kwa mambo ya mwili,” waepuke mnyanyaso, na wawe na kisababishi cha kujisifu. Hata hivyo, Paulo alionyesha kwamba wala tohara wala kutotahiriwa si kitu. Bali, “kiumbe kipya” ndicho kitu. Alisali kwamba amani na rehema iwe juu ya Israeli wa kiroho, wale wa kiumbe kipya.
Barua ya Paulo kwa Wagalatia iliwasaidia wakinze wale wenye kutafuta kuwatumikisha kiroho. Na itusaidie sisi pia kuonyesha tunda la roho na kusimama thabiti katika uhuru wa Kikristo.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 23]
Alama za Chapa: “Tangu sasa mtu asinitaabishe,” akaandika Paulo, “kwa maana ninachukua mwilini mwangu chapa zake Yesu.” (Wagalatia 6:17) Miongoni mwa wapagani fulani wa kale, watumwa walitiwa alama za chapa kuonyesha wenyeji wao ni akina nani. Alama mbalimbali zilifanywa kwa moto au zikachorwa katika mnofu wao. Bila shaka, yale mabaya mengi yaliyofanywa kwenye mwili wa Paulo kwa sababu ya utumishi wake wa Kikristo yaliacha makovu fulani, yakitoa ushuhuda kwa dai lake kuwa ni mtumwa mwaminifu wa Kristo, mmoja aliyenyanyaswa kwa ajili Yake. (2 Wakorintho 11:23-27) Huenda hizi zikawa ndizo “alama za chapa” ambazo Paulo alirejezea, au huenda hata ikawa alikuwa akifikiria maisha aliyoishi akiwa Mkristo, akionyesha tunda la roho ya Mungu na kutekeleza huduma yake.
[Picha]
Watumwa wa Waroma walishurutishwa kutumikia bwana-wakubwa zao, lakini Paulo alikuwa mtumwa mwenye nia na shangwe wa Yesu Kristo