Barua ya Paulo kwa Wagalatia—Ujumbe wa Habari Njema
BAADA ya salamu za utangulizi mtume Paulo aliwaandikia hivi Wagalatia: “Nastaajabu kwa kuwa mnamwacha upesi hivi yeye aliyewaita . . . na kugeukia injili [habari njema] ya namna nyingine.” Halafu muda mfupi baadaye akapaza sauti akisema: “Enyi Wagalatia msio na akili, ni nani aliyewaloga?”—Wagalatia 1:6; 3:1.
Kwa sababu gani Paulo aliudhiwa sana na Wagalatia? Wao walikuwa akina nani, na Paulo alikutanaje nao? Ni ujumbe gani wa habari njema aliowapa? Na ni kwa njia gani ujumbe huo una mafaa kwetu sisi leo?
Watu Wenyewe na Tatizo Lao
Wagalatia walikuwa hasa watu wa mchanganyiko wa Wahindi na Wanaulaya wenye asili ya Kelti waliotoka Gauli. Lakini wengine wao walikuwa pia watu wa mataifa mengine. Mkoa wa Kiroma wa Galatia ulikuwa na miji isiyopungua minne inayotajwa na maandishi ya Biblia: Ikonio, Listra, Derbe na Antiokia katika Pisidia. Hiyo ilitembelewa na Paulo wakati wa safari yake ya kwanza ya umisionari, na makundi yalianzishwa katika sehemu hizo. (Matendo 13:14–14:23) Kijana Timotheo alikuwa mmoja wa Wakristo Wagalatia wa kwanza.—Matendo 16:1, 2.
Baada ya safari ya Paulo ya kwanza ya umisionari ya kupitia Galatia, baraza yenye kuongoza ya mitume na wanaume wazee ilikutana katika Yerusalemu mwaka wa 49 WK na kufanya uamuzi wa kwamba tohara si takwa kwa Wakristo. (Matendo 15:1-29) Baada ya mkutano huo Paulo na Sila waliyapelekea makundi ya Galatia sehemu hiyo ya zile habari njema.—Matendo 16:1-6.
Walakini, muda mfupi baada ya hapo Paulo alishangaa sana kusikia kwamba watu fulani katika Galatia walikuwa wakisisitiza kwamba ni lazima Wakristo watahiriwe. Watu hao walikuwa waendelezaji wa dini ya Kiyahudi waliokuwa wakijaribu kuwafanya Wakristo wa mataifa yasiyo ya Kiyahudi wajifuatishe na mambo ya sheria ya Musa. Walikuwa pia wakiharibu mamlaka ya Paulo ya kuwa mtume.
Kwa hiyo Paulo aliwaandikia Wagalatia ili ashughulike na hali hiyo yenye kusikitisha, akiwahimiza warudiwe na fahamu zao. Ama aliiandika barua hiyo akiwa bado katika safari yake ya pili ya umisionari, labda akiwa katika Korintho, ama muda mfupi tu baada ya kufika katika Antiokia ya Shamu. Basi, huenda ikawa kwamba barua hiyo iliandikwa mapema sana, kwa mfano wakati wa vuli ya mwaka wa 50 WK au baadaye sana katika mwaka wa 52 WK.
Paulo anawaambia Wagalatia kwamba hao waendelezaji wa dini ya Kiyahudi wanajaribu kuzipotosha habari njema. Na, kama Paulo anavyosema, habari njema hizo zinahusu Kristo Yesu. Ndiyo, ni habari njema juu ya uhuru ambao Kristo analeta—uhuru wa kutoka katika utumwa wa sheria ya Musa. Basi Paulo anarudia mara mbili kuonya kwamba mtu ye yote, hata awe ni malaika kutoka mbinguni, akitangaza kuwa habari njema kitu kinachoyazidi mambo aliyoyatangaza kuwa habari njema “na alaaniwe.”—Wagalatia 1:7-9.
Basi, je! barua ya Paulo inatimiza jambo gani? Kwanza, inathibitisha waziwazi mamlaka yake ya kuwa mtume. Pili, inauunga mkono kwa uthabiti uamuzi wa baraza yenye kuongoza juu ya tohara. Tena inatofautisha kazi za mwili na tunda la roho, ikikaza fikira kwenye kazi zinazopendeza Mungu.
Paulo Anatetea Utume Wake
Pale pale mwanzoni Paulo anaelekeza fikira kwenye mamlaka yake, akisema: “Paulo, mtume, si mtume wa wanadamu, wala kutumwa na mwanadamu, bali na Yesu Kristo, na Mungu Baba . . . injili [habari njema] hiyo niliyowahubiri, nawajulisha ya kuwa siyo ya namna ya kibinadamu. Kwa kuwa sikuipokea kwa mwanadamu wala sikufundishwa na mwanadamu, bali kwa ufunuo wa Yesu Kristo.”—Wagalatia 1:1, 11, 12; Matendo 22:6-16.
Paulo anasimulia kifupi namna hapo kwanza alivyokuwa mashuhuri katika dini ya Kiyahudi, lakini baada ya kuongolewa kwake na Kristo kwa mwujiza, akaenda kuzitangaza habari njema katika Arabia na Dameski. Halafu Paulo anaeleza habari za kutembelea Yerusalemu akiwa na Petro muda wa siku kumi na tano (mwaka wa 36 WK). Miaka kumi na minne baada ya hapo, katika mwaka wa 49 WK, ndipo Paulo aliporudi Yerusalemu kwa ajili ya mkutano wa kulizungumza shauri la tohara. (Wagalatia 1:13-24) Anawaita “ndugu za uongo” wale waendelezaji wa dini ya Kiyahudi waliokuwa wakisogeza mbele wazo la tohara, wakijaribu ‘kuwatia utumwani’ Wakristo waaminifu. Lakini yeye akasema: “Hata saa moja hatukujitia chini yao, ili kwamba kweli ya Injili ikae pamoja nanyi.”—Wagalatia 2:1-5.
Tunapofikiria jambo hili, kwa uhakika tunaona kwamba Paulo alituwekea mfano mwema wa unyenyekevu. Ingawa yeye alikuwa mtume aliyechaguliwa na Yesu Kristo kibinafsi, aliziweka habari njema alizokuwa akihubiri chini ya baraza yenye kuongoza, akaitambua mamlaka ya baraza hiyo. Je! sisi leo tunaonyesha heshima inayofaa kwa wanaume waliowekwa na Baraza Linaloongoza na kuwaonyesha ushirikiano katika kuzihubiri habari njema?
Baadaye Paulo alishikilia sana mamlaka yake ya kiutume kwa kumpinga mtume Petro uso kwa uso. Alifanya hivyo kwa sababu Petro alikuwa ameacha kula pamoja na Wakristo Mataifa kwa sababu ya kuogopa wanadamu. Akifunua wazi kosa la Petro, Paulo alimwuliza hivi: “Ikiwa wewe uliye Myahudi wafuata desturi za Mataifa, wala si za Wayahudi, kwa nini unawashurutisha Mataifa kufuata desturi za Wayahudi?”—Wagalatia 2:11-14.
Imara Ni Kuu Kuliko Kazi za Sheria
Akiwahimiza Wagalatia warudiwe na fahamu zao, Paulo anauliza hivi: “Je! mlipokea [roho] kwa matendo ya sheria, au kwa kusikia kunakotokana na imani?” Kwa kuwa jibu ni wazi, anauliza: “Baada ya kuanza katika [roho], mnataka kukamilishwa sasa katika mwili?” Anawakumbusha juu ya Abrahamu ambaye, ingawa hakuwa chini ya sheria, ‘alimwamini Mungu akahesabiwa haki.’ Sheria iliongezwa baadaye ili kudhihirisha makosa. Kwa kweli iliwahukumia kifo wale waliojaribu kuishika. Lakini, kama Paulo anavyoeleza, Kristo alikufa kama mlaaniwa ili wafuasi wake waweze kufunguliwa katika sheria na kuishi kulingana na imani. Hata hivyo, sheria ilitimiza kusudi lenye mafaa la kuwa ‘kiongozi [mwalimu] kuwaleta kwa Kristo.’—Wagalatia 3:1-29.
Kwa kuwa Wagalatia wamepokea uana wa kiroho na uhuru kupitia Kristo, Paulo anauliza sababu yao ya kutaka kurudia utumwa kwa sheria, wakiadhimisha siku na miezi na majira na miaka. Anasema kwamba waendelezaji wa dini ya Kiyahudi “wanawatafuta ninyi kwa juhudi, si kwa njia nzuri, bali wanataka kuwafungia ninyi msihusiane nami.” Walakini, Paulo anaonyesha hangaiko lake lenye upendo, akisema: “Mimi niko tena katika maumivu ya kuzaa mtoto mpaka Kristo aumbike ndani yenu.”—Wagalatia 4:1-20, NW.
Ndipo Paulo anapotumia mfano kutofautisha utumwa kwa kazi za sheria na uhuru wa kweli wa Kikristo. Kijakazi wa Abrahamu, Hagari (Hajiri), anafananisha agano la torati na ‘analingana na Yerusalemu wa sasa: kwa kuwa anatumika utumwani pamoja na watoto wake.’ Kwa upande mwingine, Sara anafananisha agano la Kiabrahamu, naye analingana na ‘Yerusalemu wa juu ambaye ni mwungwana, naye ndiye mama yetu sisi.’ Kama vile Ishmaeli alivyomtesa Isaka, ndivyo Wayahudi walivyokuwa wakiwapinga Wakristo wa kweli, watoto wa yule mwanamke mwungwana (aliye huru).—Wagalatia 4:21-31.
Simama Imara Katika Uhuru wa Kikristo
Kwa kutegemea mfano uliotangulia kutajwa, Paulo anatoa kitia-moyo hiki: “Katika ungwana huo Kristo alituandika huru; kwa hiyo simameni, wala msinaswe tena chini ya kongwa la utumwa.” Paulo anakazia kwamba mtu akitahiriwa, kutahiriwa kwake hakutakuwa na faida. Mtu anayetahiriwa atakuwa katika wajibu wa kuishika sheria nzima na hivyo akose kupata haki (uadilifu) kwa imani. Basi kwa kuchukizwa na hali hiyo Paulo anatamka hivi: “Laiti hao wanaowatia mashaka wangejikata nafsi zao [au, “wangejikatisha viungo vyao vya uume waache kuwa wanaume,” NW].”—Wagalatia 5:1-12.
Ingawa Wakristo wamepata uhuru, kuna hatari ya kwamba uhuru huo unaweza kutumiwa vibaya kutosheleza tamaa za mwili usio mkamilifu. Kwa hiyo Paulo anatokeza hadhari hii: “Maana ninyi, ndugu, mliitwa mpate uhuru; lakini uhuru wenu usiwe sababu ya kuufuata mwili, bali tumikianeni kwa upendo. Maana torati yote imetimilika katika neno moja, nalo ni hili, Umpende jirani yako kama nafsi yako.”—Wagalatia 5:13, 14.
Hata hivyo Paulo anaonyesha kwamba tuna pambano kali la daima kati ya kutimiza tamaa za kimwili na kutembea kulingana na roho. Anatofautisha kazi za mwili na tunda la roho. Kazi za mwili “ni uasherati, uchafu, mwenendo mpotovu . . . na mambo kama hayo. . . . Kwa upande mwingine, tunda la roho ni upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujiweza.” Paulo anaonyesha kwamba Wakristo wanaotembea kwa utaratibu kulingana na roho wanahitaji pia kuepuka kuwa “wenye kujivuna, kuchochea ushindani mtu na mwenzake, kuoneana kijicho mtu na mwenzake.”—Wagalatia 5:15-26, NW.
Kazi Zenye Faida
Katika sura ya mwisho, Paulo anazitaja kazi zenye faida ambazo Mkristo anaweza kufanya, kama vile kusaidia kurudisha mtu mwenye kukosa na kuchukuliana mizigo. Mtu akipanda kulingana na mwili, Paulo anaeleza kwamba atavuna uharibifu kutokana na mwili wake. Lakini akipanda kulingana na roho atavuna uzima wa milele kutokana na roho. Kwa hiyo Wagalatia wanahimizwa hivi: “Tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio.” Halafu, katika kumalizia, Paulo anaonyesha makusudi waliyo nayo wale wenye kuendeleza dini ya Kiyahudi, wanaowataka watahiriwe. Kusudi ni kwamba “wapate kuona fahari katika miili yenu.” Lakini Paulo anasema ataona fahari (atajisifu) katika “[mti wa mateso] wa Bwana wetu Yesu Kristo” wala si katika kitu kingine.—Wagalatia 6:1-14.
Kwa kweli, barua ya Paulo kwa Wagalatia ni yenye kutokeza katika kupambana kithabiti na masuala yaliyokuwako nyakati zake. Faida tutakazopata kutokana nayo leo zinategemea kadiri yetu ya kuyafuata mashauri mazuri yaliyomo.
[Ramani katika ukurasa wa 21]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Korintho
Antiokia
GALATIA
Ikonio
Listra
Derbe
Antiokia
SHAMU
Bahari ya Kati