Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Kulingana na Wagalatia 6:8, ‘yeye apandaye kwa mwili wake, katika mwili wake atavuna uharibifu; bali yeye apandaye kwa roho, katika roho atavuna uzima wa milele.’ Ni “roho” gani inayomaanishwa hapa, na hivyo twaweza kuvunaje uhai?
Maneno ya Kiebrania na Kigiriki yanayotafsiriwa “roho” yana maana mbalimbali, kama vile: (1) kani ya utendaji ya Mungu, (2) kani ya uhai iliyo katika wanadamu au wanyama, (3) kani ya akilini inayomsukuma mtu, na (4) mtu wa roho au malaika. Ile ya kwanza—kani ya utendaji ya Mungu—ndiyo maana tupatayo katika Wagalatia 6:8.
Ili kupata habari inayotusaidia kuelewa, ona Wagalatia 3:2, ambapo twapata utumizi wa kwanza wa neno “roho” katika kitabu cha Wagalatia. Paulo aliuliza Wakristo hivi: ‘Je! mlipokea roho kwa matendo ya sheria, au kwa kusikia kunakotokana na imani?’ Halafu katika Wagalatia 3:5, alihusianisha “roho” hiyo na kule kufanya kazi zenye nguvu. Kwa hiyo “roho” aliyokuwa akitaja ilikuwa roho takatifu, kani ya utendaji isiyoonekana ya Mungu.
Baadaye, kwenye Wagalatia 5:16, Paulo alitofautisha roho na mwili. Twasoma hivi: ‘Basi nasema, Enendeni kwa roho, wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili.’ Kwa kusema “tamaa za mwili” yeye alimaanisha tamaa za kimwili zenye dhambi. Hivyo, katika Wagalatia 5:19-23, yeye aliorodhesha “matendo ya mwili” kwa kuyatofautisha na ‘matunda ya roho.’
Sasa, kwenye Wagalatia 6:8, ni lazima yule mtu “apandaye kwa mwili wake” awe yule anayejiacha aongozwe na tamaa za kibinadamu zenye dhambi, akijitia katika “matendo ya mwili.” Huenda yeye akapatwa na matokeo yenye kufisidi ya mwenendo huo, na ikiwa habadiliki, kwa kweli hatapata uhai ama katika Ufalme wa Mungu ama chini yao.—1 Wakorintho 6:9, 10.
Tukiwa Wakristo waliojitoa twatamani ‘kupanda kwa roho ya Mungu.’ Hiyo yatia ndani kuishi katika njia inayoruhusu roho takatifu itende kazi bila kuzuiwa maishani mwetu, ikitusaidia kudhihirisha matunda yayo. Twapaswa kukumbuka hayo tunapoamua kile ambacho tutasoma au programu za televisheni tutakazotazama. Twapanda kwa roho tunaposikiliza kwa uangalifu katika mikutano ya kutaniko na kujitahidi kutumia shauri la wazee waliowekwa kwa roho.—Matendo 20:28.
Kwa kupendeza, Wagalatia 6:8 lamalizia kwa kutoa uhakikisho kwamba tupandapo kwa roho takatifu, tutaweza ‘kuvuna uzima wa milele katika roho.’ Ndiyo, kwa msingi wa fidia ya Kristo, Mungu atatoa uhai usio na mwisho kupitia utendaji wa roho takatifu.—Mathayo 19:29; 25:46; Yohana 3:14-16; Warumi 2:6, 7; Waefeso 1:7.