Mwungamano ni Hakika Kupitia Kristo
Mambo Makuu Kutokana na Waefeso
MAPEMA katika 52 W.K., mtume Paulo alihubiri katika Efeso. Jiji hili lenye utajiri wa kibiashara la Esia Ndogo lilikuwa pia kitovu cha dini bandia. Lakini Ukristo ulisitawi huko baada ya Paulo kurudi Efeso, yaelekea kufikia kipupwe cha 52/53 W.K. Alitoa hotuba za kila siku katika jumba la shule na kutoa ushahidi wa nyumba kwa nyumba wakati wa kukaa kwake kwa miaka mitatu hivi. —Matendo 19:8-10; 20:20, 21, 31.
Alipokuwa amefungwa gerezani katika Roma karibu 60-61 W.K., Paulo aliwaandikia Wakristo Waefeso. Mwungamano pamoja na Yesu Kristo na kupitia yeye ndicho kichwa cha barua yake. Kwa uhakika, ina marejezo 13 yatajayo ‘katika [mwungano na, NW] Kristo,’ zaidi ya barua nyingine yoyote aliyoiandika Paulo. Kama Waefeso, sisi twaweza kunufaika na maneno ya Paulo juu ya daraka litimizwalo na Kristo, tukiepuka ukosefu wa adili na kukinza majeshi ya roho waovu.
Mwungamano Ni Kusudi la Mungu
Kwanza, Paulo alieleza jinsi Mungu angeleta mwungamano kupitia Kristo. (1:1-23) Yehova alikusudia kukukusanya vitu vyote mbinguni na duniani pamoja tena kwa njia ya “madaraka” (“usimamizi,” NW). Kupitia Kristo, Mungu angewaungamanisha pamoja naye wale waliochaguliwa kwa maisha ya kimbingu na wengine ambao wangeishi duniani. Leo, Mungu ameungamanisha wapakwa mafuta na “umati mkubwa,” na ‘kujumlishwa kwa vitu vyote duniani’ kutaendelea mpaka wale walio katika makaburi ya ukumbusho wasikie sauti ya Yesu na kutoka. (Ufunuo 7:9; Yohana 5:28, 29, NW) Yatupasa tushukuru kwa jambo hili, hata kama vile Paulo alivyosali kwamba Waefeso wangethamini uandalizi wa Mungu kwa ajili yao.
Ndipo uangalifu ulielekezwa kwa Wakristo Wasio Wayahudi, waaliokuwa wamekufa katika dhambi. (2:1–3:21) Kwa njia ya Kristo, Sheria ilitanguliwa na msingi ukawekwa ili Wayahudi na Wasio Wayahudi waungamane na kuwa hekalu kwa ajili ya Mungu ili akae ndani yalo kwa roho. Usimamizi wa Paulo ulikuwa wa kujulisha siri takatifu kwamba Wasio Wayahudi wapate kuingia katika mwungano pamoja na Kristo, ambaye kupitia kwake wao waweza kumfikia Mungu kwa uhuru wa kusema. Paulo asali tena kwa ajili ya Waefeso, wakati huu akiomba kwamba Yehova asababishe wathibitishwe imara na imani na upendo.
Mambo Yenye Kuendeleza Mwungamano
Paulo alionyesha kwamba Mungu ameandaa mambo yenye kuungamanisha. (4:1-16) Miongoni mwa haya mna ule mwili mmoja wa kiroho ambao ni kundi. Mwili huu hufanya kazi katika mwungamano chini ya ukichwa wa Kristo. Naye huandaa zawadi katika wanaume ili kusaidia wote wafikie umoja katika imani.
Pia Yehova hufanya iwezekane kuonyesha sifa za Kikristo ambazo huendeleza mwungamano. (4:17–6:9) Wakiisha kuvaa “utu mpya,” Wakristo huepuka ukosefu wa kumcha Mungu kama usemi usio wa adili. Wao hutembea kwa hekima, huonyesha staha kwa Kristo, na hudhihirisha ujitiisho ufaao.
Kwa kuongezea, Mungu huwezesha Wakristo wakinze majeshi ya roho waovu yanayotafuta kuvunja mwungamano wetu. (6:10-24) Silaha za kiroho kutoka kwa Mungu huandaa ulinzi huo. Hivyo basi acheni tuzitumie na kusali kwa bidii ya moyoni, tukitia waamini wenzi katika dua zetu.
Ni shauri zuri kama nini ambalo Paulo aliwapa Waefeso! Na tulitii kwa kuepuka ukosefu wa adili na kukinza majeshi ya roho waovu. Na acheni tuthamini kwa kina kirefu mwungamano ambao twauonea shangwe kupitia Yesu Kristo.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 24]
Makombora Yanayowaka Moto: Silaha za kiroho zatia ndani “ngao kubwa ya imani” ya kuzima au kumaliza madhara ya ‘makombora yanayowaka moto’ ya Shetani. (Waefeso 6:16, NW) Makombora fulani yaliyotumiwa na Waroma yalikuwa matete yenye shimo ndani yakiwa na chombo cha chuma chini ya ncha iliyojazwa mafuta yenye kuwaka moto. Yalifyatuliwa kutoka kwenye pinde zisizofyatuka kasi sana ili kuepuka kuuzima moto huo, na kuyamwagilia maji kuliuongezea tu ukali wa mwali ule. Lakini ngao kubwa ziliwalinda askari na mishale hiyo, kama vile imani katika Yehova huwezesha watumishi wake “kuyazima makombora yote yanayowaka moto ya mwovu.” Ndiyo, imani hutusaidia tukinze mambo kama mashambulio yenye kufanywa na roho waovu na pia vishawishi vya kufanya mabaya, kufuatia njia ya maisha ya kutafuta vitu vya kimwili, na kujiacha kushindwa na hofu na shaka.