Maisha na Huduma ya Yesu
Mbele ya Sanhedrini, Halafu kwa Pilato
USIKU unakaribia mwisho. Petro amekana Yesu kwa mara ya tatu, na washiriki wa Sanhedrini wamemaliza kesi yao ya bandia na wametawanyika. Hata hivyo, wanakutana tena asubuhi ya Ijumaa mara tu kunapopambazuka, wakati huu wakiwa kwenye Jumba la Sanhedrini yao. Inaelekea kusudi lao ni kufanya ionekane eti kesi yao ya usiku ilifuata uhalali wa sheria. Yesu anapoletwa mbele yao, wanasema hivi, kama vile walivyofanya usiku: “Kama wewe ndiwe Kristo, tuambie.”
“Nijapowaambia, hamtasadiki kabisa,” Yesu anajibu. “Tena, nikiwauliza, hamtajibu.” Hata hivyo, kwa moyo mkuu Yesu anaelekeza kwenye utambulishi wake, akisema: “Tangu sasa Mwana wa Adamu [Mwana wa binadamu, NW] atakuwa ameketi [akiketi, NW] upande wa kuume wa Mungu Mwenyezi.”
“Basi, wewe ndiwe Mwana wa Mungu?” wote wanataka kujua.
“Ninyi mwasema kwamba mimi ndiye,” Yesu anajibu.
Kwa wanaume hawa ambao wameazimia kuua, jibu hili linatosha. Wanaliona kuwa kufuru. “Tuna haja gani tena ya ushuhuda?” wanauliza. “Maana, sisi wenyewe tumesikia maneno ya kinywa chake.” Hivyo basi wanamfunga Yesu, wanamwongoza kutoka hapo, na kumpa kwa gavana Mroma Pontio Pilato.
Yudasi, msaliti wa Yesu, amekuwa anatazama hatua za mambo hayo. Anapoona kwamba Yesu amelaaniwa vikali, anahisi majuto. Hivyo yeye anaendea wakuu wa makuhani na wanaume wazee kurudisha vile vipande 30 vya fedha, akieleza hivi: “Nalikosa nilipoisaliti damu isiyo na hatia.”
“Basi, haya yatupasani sisi? Yaangalie haya wewe mwenyewe”! wanajibu bila moyo wa huruma. Hivyo basi Yuda anatupa vile vipande vya fedha hekaluni na kwenda zake na kujaribu kujinyonga. Hata hivyo, inaonekana kwamba tawi ambalo Yuda anafungilia kamba linakatika, na mwili wake unaporomoka kwenye miamba iliyoko chini, ambako unapasuka msamba.
Wakuu wa makuhani hawana uhakika wafanye nini na vile vipande vya fedha. “Si halali kuviweka katika sanduku ya sadaka,” wanakata shauri, “kwa kuwa ni kima cha damu.” Hivyo basi, baada ya kushauriana, kwa pesa hizo wananunua shamba la mfinyanzi ili kuzika wageni. Hivyo shamba hilo linakuja kuitwa “konde la damu.”
Bado ni mapema asubuhi wakati Yesu anapopelekwa kwenye jumba la gavana. Lakini Wayahudi ambao wameandamana naye wanakataa kuingia kwa sababu wanaamini kwamba huo uhusiano wa kindani pamoja na Wasio Wayahudi utawatia unajisi. Hivyo basi ili kuruhusu maoni yao, Pilato anakuja nje. “Ni mashitaka gani mnayoleta juu ya mtu huyu?” anauliza.
“Kama huyu asingekuwa mtenda mabaya, tusingemleta kwako,” wanajibu.
Akitaka kuepuka kuhusika, Pilato anajibu hivi: “Haya! mtwaeni ninyi, mkamhukumu kwa ile torati yenu!”
Wakifunua azimio lao la uuaji, Wayahudi wanadai hivi: “Sisi hatuna ruhusa ya kuua mtu.” Kwa kweli, kama wangeua Yesu wakati wa Sikukuu ya Kupitwa, inaelekea ingeleta msukosuko wa watu wote, kwa kuwa wengi wanaheshimu Yesu sana. Lakini wakiweza kufanya Waroma wamwue kwa shtaka la kisiasa, hiyo itaelekea kuwaondolea daraka mbele ya watu.
Hivyo basi viongozi wa kidini, bila kutaja kesi yao ya mapema ambamo walilaani Yesu vikali juu ya kukufuru, sasa wanatunga mashtaka tofauti. Wanafanyiza lile shtaka lenye sehemu tatu: “Tumemwona huyu akipotosha taifa letu, na kuwazuia watu wasimpe Kaisari kodi, akisema kwamba yeye mwenyewe ni Kristo, mfalme.”
Lile shtaka la kwamba Yesu adai kuwa mfalme ndilo linahangaisha Pilato. Kwa hiyo, yeye anaingia tena katika jumba, aita Yesu aende alipo, na kuuliza: “Je! Wewe ni Mfalme wa Wayahudi?” Ndiyo kusema, je! umevunja sheria kwa kujijulisha wazi kuwa mfalme kwa kupinga Kaisari?
Yesu anataka kujua ni mengi kadiri gani ambayo tayari Pilato amesikia juu yake, hivyo basi anauliza hivi: “Wewe wasema hivi kwa nafsi yako, au watu wengine walikuambia habari zangu?”
Pilato anadai hana maarifa yoyote juu yake na ana tamaa ya kujua mambo ya uhakika. “Ama! Ni Myahudi mimi!” anajibu. “Taifa lako na wakuu wa makuhani ndio waliokuleta kwangu. Umefanya nini?”
Yesu hajaribu kwa njia yoyote kupiga chenga suala hilo, ambalo ni la kuwa na ufalme. Jibu ambalo Yesu anatoa sasa bila shaka linashangaza Pilato. Luka 22:66–23:3; Mathayo 27:1-11; Marko 15:1; Yohana 18:28-35; Matendo 1:16-20.
◆ Sanhedrini inakutana tena asubuhi kwa kusudi gani?
◆ Yuda anakufaje, na ni jambo gani linafanywa na vile vipande 30 vya fedha?
◆ Kwa sababu gani Wayahudi wanataka Waroma waue Yesu, kuliko wao wenyewe kumwua kama walivyokuwa wamejaribu kufanya katika pindi za mapema?
◆ Ni mashtaka gani ambayo Wayahudi wanafanyia Yesu?