Waliitikia Upendo wa Mungu Bila Ubinafsi
“Na wamshukuru BWANA [Yehova, NW] kwa fadhili zake, na maajabu yake kwa wanadamu.”—ZABURI 107:8.
1. Mtume Yohana anakaziaje sifa ya upendo katika barua yake ya kwanza?
“MUNGU ni upendo.” Jinsi maneno hayo yamejaa maana! Si ajabu mtume Yohana aliona ikihitajiwa kuyarudia katika barua yake ya kwanza. (1 Yohana 4:8, 16) Si kwamba tu Yehova Mungu ni upendo bali pia yeye ni ujazo, au ufananisho, wa upendo.
2. Ni katika njia zipi Mungu alionyesha upendo katika kuumba mwanamume na mwanamke na kuwaandalia?
2 Fikiria upendo ambao Mungu alionyesha kwa jinsi alivyotuumba. Maneno ya Daudi ya uthamini yanafaa sana. Akiwa mtunga zaburi aliyevuviwa, alisema hivi: “Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha.” (Zaburi 139:14) Ili tuweze kuishi katika afya na furaha, Mungu alitufanyia mapendezo yasiyo na mwisho kwa njia ya milango yetu mitano ya maarifa —kuona, kusikia, kuonja, kunusa, na kugusa. Lo, tunaona upendezi wa jinsi gani katika uumbaji ulio kila mahali kutuzunguka! Jinsi zilivyo nzuri zile namna nyingi za mimea na wanyama mbalimbali, bila kutaja marembo ya maumbo na sura za kibinadamu! Pia Mungu aliweka matunda, mboga, na vyakula vingine vyenye kupendeza ndani ya mipaka yetu. (Zaburi 104:13-16) Kwa sababu nzuri, mtume Paulo alikumbusha wakaaji wa Listra ya kale kwamba Mungu “alitenda mema, akiwapeni mvua kutoka mbinguni, na nyakati za mavuno, akiwa-shibisha mioyo yenu chakula na furaha.”—Matendo 14:17.
3. Ni uwezo gani mzuri ajabu ambao Mungu ametupa?
3 Fikiria pia baraka ambazo zashirikiana na maisha yenye furaha ya jamaa. Zaidi ya hilo, waza juu ya mafurahisho ambayo yawezekana sisi kuonea shangwe kwa sababu ya nguvu zetu za akili na maono ya moyoni: kuwazia, kusababu, kukumbuka, kudhamiria, na hasa uwezo wa kuabudu—yote hayo yakituweka juu sana kuliko wanyama; wala hatupaswi kusahau mafurahisho ambayo muziki waweza kutupa sisi. Zawadi hizi na nyinginezo ni maonyesho wazi ya upendo wa Mungu kwetu.
4. Ni maonyesho gani wazi ya upendo wa Mungu ambayo wanadamu wameona kuanzia kukosa kwa wazazi wetu wa kwanza?
4 Hakuna shaka kwamba Adamu na Hawa walionea shangwe mapendezo mengi katika hali yao ya ukamilifu katika bustani ya Edeni. (Mwanzo 2:7-9, 22, 23) Lakini waliposhindwa kuitikia bila ubinafsi shuhuda zote za upendo wa kimungu waliokuwa wakionea shangwe, je! Mungu alitupilia mbali jamii ya kibinadamu? Sivyo hata kidogo! Alifanya haraka uandalizi wa kurekebisha makosa yote yaliyotokana na kosa la wazazi wetu wa kwanza. (Mwanzo 3:15) Pia Yehova alionyesha upendo wazi kwa kuchukuliana kwa subira na wazao wasiokamilika wa Adamu. (Warumi 5:12) Kwa muda gani? Kwa miaka kama 6,000 kufikia sasa! Hasa Mungu ameonyesha upendo katika kushughulika na watumishi wake. Ni ya kweli maneno haya: “BWANA [Yehova, NW], BWANA [Yehova, NW], Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli; mwenye kuwaonea huruma watu elfu elfu, mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi.”—Kutoka 34:6, 7.
5. Yehova alionyeshaje subira yenye upendo katika kushughulika na taifa la Israeli?
5 Ndiyo, ilikuwa kubwa kweli kweli subira ambayo Yehova Mungu alionyesha katika shughuli zake na Waisraeli kuanzia wakati alipowatokeza wakiwa taifa chini ya Mlima Sinai mpaka upotovu wao ulipofanya iwe lazima awatupilie mbali kabisa. Kama vile tunavyosoma kwenye 2 Nyakati 36:15, 16: “BWANA [Yehova, NW], Mungu wa baba zao, akatuma kwao kwa mikono ya wajumbe wake, akiondoka mapema, na kutuma; kwa sababu aliwahurumia watu wake, na makao yake, lakini waliwadhihaki wajumbe wa Mungu, na kuyadharau maneno yake, na kuwacheka manabii wake, hata ilipozidi ghadhabu ya BWANA [Yehova, NW] juu ya watu wake, hata kusiwe na kuponya.” Lakini kulikuwa na wale ambao waliitikia upendo wa Yehova Mungu bila ubinafsi. Ili tuone walifanyaje hivyo, acheni sasa tuchunguze maisha za wengine wa hawa watu mmoja mmoja. Hii itaweka msingi wa kuonyesha jinsi sisi wenyewe twaweza kuitikia upendo wa Mungu katika njia zenye kutumika vizuri sana.
Jinsi Musa Alivyoitikia Bila Ubinafsi
6. Ni katika njia zipi mfano wa Musa ulikuwa wa kutokeza, naye aliona upendo wa Mungu katika vyeo gani?
6 Musa alikuwa mfano wa kutokeza wa mtu aliyeitikia upendo wa Mungu bila ubinafsi. Lo, ni nafasi zilizoje zilizowekwa mbele ya Musa akiwa mwana wa malezi wa binti Farao! Lakini yeye alichagua “kupata mateso pamoja na watu wa Mungu kuliko kujifurahisha katika dhambi kwa kitambo; akihesabu ya kuwa kushutumiwa kwake Kristo ni utajiri mkuu kuliko hazina za Misri.” (Waebrania 11:25, 26) Hata hivyo, makumi kadhaa ya miaka baadaye Musa alitaka kukomboa ndugu zake, Waisraeli, kutoka utumwa wa Kimisri. Lakini wao hawakuthamini jitihada zake, wala haukuwa wakati wa Mungu unaofaa kuwakomboa. (Matendo 7:23-29) Wakati mmoja, kwa sababu ya imani ya Musa na tamaa isiyo na ubinafsi ya kusaidia ndugu zake, Yehova alimtia nguvu kufanya miujiza mingi na kutumikia Waisraeli kwa miaka 40 akiwa nabii, mwamuzi, mpaji-sheria, na mpatanishi Wake. Katika vyeo hivi, Musa aliona visa vingi vya upendo wa Yehova kwake na Waisraeli wenzake.
7. Musa aliitikiaje maonyesho ya upendo wa Mungu?
7 Musa aliitikiaje upendo na fadhili zisizostahiliwa (neema, UV) za Mungu? Je! ‘aliipokea neema ya Mungu bure’ kwa kukosa kusudi lake? (2 Wakorintho 6:1) Sivyo kamwe! Musa aliitikia bila ubinafsi maonyesho ya Yehova ya upendo kuelekea yeye kwa kukaza fikira zake zote kwenye Mungu. Alitegemea Yehova nyakati zote na alikuwa na uhusiano wa kindani pamoja na Mfanyi wake. Mungu alisifu Musa kama nini alipokuwa akikemea Haruni na Miriamu kwa kuchambua ndugu yao! Ndiyo, Yehova alisema na Musa “mdomo kwa mdomo” na akamwacha atazame “umbo la BWANA [Yehova, NW].” (Hesabu 12:6-8) Ingawa Musa alikuwa na mapendeleo mengi, aliendelea kuwa binadamu aliye msikivu kupita wote na kutekeleza amri za Yehova “vivyo hivyo.”—Kutoka 40:16; Hesabu 12:3, NW.
8. Musa alionyeshaje kwamba kwa kweli yeye alikaza fikira zake kwenye Mungu?
8 Pia Musa alionyesha kwamba alikaza fikira zake kwenye Mungu bila ubinafsi kwa hangaiko aliloonyesha kwa jina, sifa, na ibada safi ya Yehova. Hivyo, katika pindi mbili Musa alifanikiwa kusihi Yehova awe na rehema kwa Israeli kwa sababu jina la Mungu lilitiwa ndani. (Kutoka 32:11-14; Hesabu 14:13-19) Waisraeli walipoingia katika ibada-sanamu ya ndama, Musa alionyesha bidii kwa ajili ya ibada safi kwa kupaaza sauti hivi: “Mtu awaye yote aliye upande wa BWANA [Yehova, NW], na aje kwangu.” Baada ya hayo, Musa na wale walio pamoja naye wakaua 3,000 wa waabudu sanamu hao. Halafu, kwa miaka 40 akachukuliana na kikundi cha watu wenye kulalamika na kuasi. Hakika hakuna shaka kwamba Musa aliitikia bila ubinafsi mawonyesho ya upendo wa Mungu, akituwekea mfano mzuri sana sisi leo.—Kutoka 32:26-28; Kumbukumbu 34:7, 10-12.
Itikio Zuri Sana la Daudi
9. (a) Daudi aliitikiaje upendo wa Yehova Mungu? (b) Kama Daudi, sisi tunawezaje kuheshimu Yehova kwa mali?
9 Mtu mwingine wa Biblia aliyeweka mfano mzuri sana wa kuitikia upendo wa Mungu bila ubinafsi alikuwa mtunga zaburi Daudi, mfalme wa pili wa Israeli. Bidii yake kwa ajili ya jina la Yehova ilimsukuma kupigana na Goliathi lile jitu la Kifilisti lenye kudhihaki vikali, naye Mungu akampa Daudi ushindi juu yalo. (1 Samweli 17:45-51) Bidii iyo hiyo ilisukuma Daudi kuleta sanduku la agano Yerusalemu. (2 Samweli 6:12-19) Na je! tamaa ya Daudi ya kujengea Yehova hekalu haikuwa wonyesho mwingine wa bidii na uthamini wake kwa upendo na wema wa Mungu? Bila shaka ilikuwa. Kunyimwa pendeleo hilo hakukuzuia Daudi asitayarishe mradi huo na kuheshimu Yehova kwa kuchanga kibinafsi dhahabu, fedha, na mawe yenye thamani kubwa sana. (2 Sa-mweli 7:1-13; 1 Nyakati 29:2-5) Itikio kama hilo lisilo na ubinafsi kwa upendo wa Mungu linapasa kutusukuma sisi ‘kuheshimu Yehova kwa mali zetu’ kwa kutumia vitu vyetu vya kimwili kuendeleza faida za Ufalme.—Mithali 3:9, 10; Mathayo 6:33.
10. Ni kwa njia gani mwendo wa Daudi unastahili kuigwa?
10 Ingawa Daudi alifanya makosa mazito, muda wote wa maisha yake alithibitika kuwa ‘mtu mwenye kukubalika kwa moyo wa Yehova.’ (1 Samweli 13:14; Matendo 13:22, NW) Zaburi zake zimejaa maonyesho ya uthamini kwa upendo wa Mungu. The International Standard Bible Encyclopædia inasema kwamba Daudi “alikuwa mwingi zaidi na zaidi kwa ushukuru kuliko mwingine yeyote anayetajwa katika Andiko Takatifu.” Mtunga zaburi Asafu alisema kwamba Mungu ‘alimchagua Daudi, mtumishi wake, akamwondoa katika mazizi ya kondoo awachunge Yakobo watu wake, na Israeli urithi wake. Akawalisha kwa ukamilifu wa moyo wake.’ (Zaburi 78:70-72) Kwa kweli, Daudi alikuwa na mwendo unaofaa kuigwa na sisi.
Yesu Kristo, Mfano Wetu Mkamilifu
11, 12. Yesu alionyeshaje kwamba kwa kweli yeye alikaza fikira zake kwenye Mungu?
11 Bila shaka, Yesu Kristo ndiye mfano mzuri kabisa wa Kimaandiko wa binadamu aliyeitikia upendo wa Mungu bila ubinafsi. Huu ulimsukuma Yesu kufanya nini? Kwanza kabisa, alisukumwa kumpa Yehova ujitoaji usiotia mwingine ndani. Hakuna shaka kwamba Yesu alikaza fikira zake zote kabisa kwenye Mungu. Uthamini kwa upendo na wema wa Baba yake wa kimbingu ulimsukuma awe mwanamume wa kiroho kweli kweli. Alikuwa na uhusiano wa karibu, ulio wa kindani pamoja na Mungu. Yesu alikuwa mwanamume wa sala, naye alipenda kuongea na Baba yake wa kimbingu. Tena na tena, tunasoma kwamba Kristo alikuwa akisali. Katika pindi moja alitumia usiku mzima katika sala. (Luka 3:21, 22; 6:12; 11:1; Yohana 17:1-26) Katika kuitikia upendo wa Mungu, Yesu aliishi kulingana na ukweli wa kwamba ‘mtu haishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu [Yehova, NW].’ Kwa uhakika, kufanya mapenzi ya Baba kulikuwa chakula kwake. (Mathayo 4:4; Yohana 4:34) Je! sisi hatupaswi kuitikia upendo wa Mungu hivyo hivyo, tukimpa ujitoaji usiotia mwingine ndani?
12 Kwa kuitikia upendo wa Mungu bila ubinafsi, sikuzote Yesu Kristo alielekeza uangalifu kwa Mungu aliye Baba yake. Mtu fulani alipoita Yesu “Mwalimu mwema,” yeye alikataa na kusema hivi: “Hakuna aliye mwema ila mmoja, naye ndiye Mungu.” (Luka 18:18, 19) Yesu alikazia-kazia kwamba yeye hangeweza kufanya kitu kwa uanzishi wake mwenyewe. Hakukosa kamwe nafasi ya kutukuza jina la Baba yake, na kwa kufaa sana alianza sala yake ya kielelezo kwa ombi hili rasmi: “Jina lako litukuzwe [litakaswe, NW].” Alisali hivi: “Baba, ulitukuze jina lako.” Na muda mfupi kabla ya yeye kufa, Kristo alisema hivi kwa Baba yake: “Mimi nimekutukuza duniani, hali nimeimaliza kazi ile uliyonipa niifanye.” (Mathayo 6:9; Yohana 12:28; 17:4) Hakika, kwa kuitikia upendo wa Mungu, tunapaswa kutafuta kutukuza Yehova, kusali jina lake takatifu litakaswe.
13. Ni jinsi gani upendo wa Mungu ulichochea Yesu kufanya kitendo?
13 Sasa, tafadhali angalia njia ya pili ambayo itikio lisilo na ubinafsi kwa upendo wa Mungu lilisukuma Yesu. Lilimfanya apende uadilifu na kuchukia uovu, kama ilivyotabiriwa kwenye Zaburi 45:7. (Waebrania 1:9) Alikuwa “mtakatifu [mwaminifu-mshikamanifu, NW], asiyekuwa na uovu, asiyekuwa na waa lo lote, aliyetengwa na wakosaji.” (Waebrania 7:26) Yesu alitokeza wito wa ushindani kwa wapinzani wake wenye nia mbaya kwamba wamshtaki juu ya dhambi, lakini hawakuweza kufanya hivyo. (Yohana 8:46) Katika pindi mbili, chuki yake ya uovu ilimfanya asafishe hekalu lisiwe na wanadini wenye pupa. (Mathayo 21:12, 13; Yohana 2:13-17) Na Yesu aliwalaumu vikali namna gani viongozi wanafiki wa kidini, hata kuwaambia kwamba walikuwa wa Ibilisi!—Mathayo 6:2, 5, 16; 15:7-9; 23:13-32; Yohana 8:44.
14. Kwa kuitikia upendo wa Yehova, Yesu alishughulikaje na wanafunzi wake?
14 Njia nyingine bado ambayo upendo wa Yehova ulisukuma Yesu inaweza kuonwa katika shughuli zake na mitume wake na wanafunzi wengine. Jinsi alivyokuwa mwenye upendo, mwenye subira, na ustahimilivu kwao! Ni lazima wawe walimjaribu kwa kumhuzunisha sana na ushindani wao, wakibishana ni nani mkubwa zaidi hata kufikia usiku wenyewe wa kusalitiwa kwake. (Luka 22:24-27) Hata hivyo, sikuzote Yesu alijionyesha kuwa mwenye tabia pole ya moyoni na mnyenyekevu moyoni. (Mathayo 11:28-30) Ni kweli, Yuda alisaliti Yesu, Petro akamkana mara tatu, na mitume wale wengine wakakimbia wakati kikundi chenye ghasia kilipokuja kumkamata. Lakini yeye hakuona uchungu wala kuchukizwa kamwe. Tunajuaje? Ni kwamba, alipojiunga na mitume baada ya ufufuo wake, Yesu hakuwapa kemeo lenye kuwachoma sana kwamba walijiacha washindwe na hofu. Bali, aliwafariji na kuwaimarisha kwa ajili ya utumishi zaidi wa Ufalme.—Yohana 20:19-23.
15. Yesu alihudumiaje mahitaji ya watu ya kimwili bila ubinafsi?
15 Acheni tufikirie njia nyingine bado ambayo Yesu Kristo aliitikia upendo wa Mungu bila ubinafsi. Alifanya hivyo kwa kujitoa dhabihu kwa ajili ya wengine, mpaka kifo cha aibu kubwa na maumivu juu ya mti wa mateso. (Wafilipi 2:5-8) Yesu alihudumia mahitaji ya kimwili ya watu kwa kulisha kimwujiza umati wa watu na kufanya maponyo mengi. (Mathayo 14:14-22; 15:32-39) Sikuzote aliweka mapendezi ya wengine mbele yaliyo yake mwenyewe. Ndiyo sababu angeweza kusema hivi: “Mbweha wana pango, na ndege wa angani wana vioto; lakini Mwana wa Adamu [mwana wa binadamu, NW] hana pa kulaza kichwa chake.” (Mathayo 8:20) Yesu alikuwa mwepesi kuitikia utendaji wa roho ya Mungu ilipotiririka kutoka kwake katika kufanya maponyo ya kimwujiza. Lakini hakujaribu kamwe kufaidika kimwili kwa kutumia nguvu hiyo inayozidi ile ya asili, kama wakati mwanamke mwenye mtiririko wa damu kwa miaka 12 alipogusa vazi lake la nje kwa imani na akaponywa. (Marko 5:25-34) Zaidi ya hilo, Yesu hakutumia kamwe nguvu zinazozidi zile za asili kwa ajili yake mwenyewe.—Linganisha Mathayo 4:2-4.
16. Ni kwa njia zipi Kristo alihudumia uhitaji wa kiroho wa watu?
16 Ingawa Yesu alihudumia mahitaji ya kimwili ya watu bila ubinafsi kwa kuponya magonjwa yao na kuwalisha kimwujiza, kichocheo kikubwa cha huduma yake ya kidunia kilikuwa kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu, kufundisha, na kufanya wanafunzi. Ingawa maponyo yote ya ajabu aliyofanya, hakujulikana kuwa yule Tabibu Mkubwa wala Mfanya Miujiza bali yule Mwalimu Mwema. (Mathayo 4:23, 24; Marko 10:17) Yesu alijitaja kuwa Mwalimu, vilevile wanafunzi wake na hata adui zake walimtaja hivyo. (Mathayo 22:16; 26:18; Marko 9:38) Naye alifundisha kweli zilizoje, kama vile katika Mahubiri yake juu ya Mlima! (Mathayo 5:1–7:29) Lo, mifano yake ilifaa jinsi gani, na hadithi zake zenye mifano ya unabii na unabii mwingine-mwingine ziliamsha upendezi jinsi gani! Si ajabu askari waliotumwa kukamata Yesu katika pindi moja hawakuweza kujipa moyo wa kumshika!—Yohana 7:45, 46.
17. (a) Yesu alituandaliaje kielelezo kikamilifu cha upendo? (b) Ni nini litazungumzwa katika makala inayokuja?
17 Bila shaka, Yesu Kristo alituwekea mfano ulio mkamilifu wa kuitikia bila ubinafsi maonyesho ya Mungu ya upendo kuelekea sisi. Yesu alimpa Baba yake wa kimbingu mahali pa kwanza katika maisha na shauku zake. Alipenda uadilifu kikweli, akashughulika kwa upendo na mitume wake na wanafunzi wengine, na kutumia maisha yake akihudumia mahitaji ya watu ya kiroho na ya kimwili. Mwishowe, Yesu alipamba upeo wa huduma yake kwa kutoa uhai wake kuwa ukombozi. (Mathayo 20:28) Lakini namna gani sisi? Ni kweli, sisi ni wasiokamilika, kama Musa na Daudi. Hata hivyo, kama inavyoonyesha makala inayokuja, kuna njia zinazotumika vizuri ambazo sisi tunaweza kuiga Mfano wetu katika kuitikia bila ubinafsi maonyesho wazi ya upendo wa Mungu.
Wewe Ungejibuje?
◻ Kwa nini inaweza kusemwa kwamba “Mungu ni upendo”?
◻ Musa aliitikiaje maonyesho wazi ya upendo wa Mungu?
◻ Ni katika njia zipi Daudi aliitikia upendo wa Yehova Mungu?
◻ Ni mfano gani ambao Yesu Kristo aliweka katika kuitikia upendo wa Mungu?
[Picha katika ukurasa wa 10]
Wewe unajua jinsi Musa aliitikia upendo wa Mungu?
[Picha katika ukurasa wa 12, 13]
Yesu aliitikia upendo wa Mungu kwa kusaidia wengine kiroho na kimwili na kwa kutoa uhai wake kuwa ukombozi