Maswali Kutoka kwa Wasomaji
◼ Je! yule mwanamke kijana Myahudi Esta alifanya ngono isiyo ya adili na mfalme Mwajemi ili apate upendeleo wake na hivyo apate faida fulani fulani?
Huenda watu fulani wakawa walikata shauri hivyo kutokana na uripoti wa kilimwengu, lakini maandishi yenye kutegemeka katika Biblia yanapinga wazo hili.
Mwanahistoria Myahudi Flavius Josephus anatoa ripoti ya kilimwengu kwamba malkia Mwajemi Vashti alikataa kwenda mbele ya mume wake, Ahasuero. Basi ikawa kwamba, mfalme, yaonekana ni Xerxes 1 wa karne ya tano K.W.K., akamkataa Vashti kwa hasira na kukubali kuwe na utafutaji wa malkia mpya katika milki yote. Mabikira vijana walio wazuri walikusanywa na kwa muda mrefu wakatendewa kwa njia yenye kuwafanya wawe wazuri zaidi.
“Halafu, wakati [towashi wa mfalme] alipofikiri kwamba mabikira walikuwa wamepata utunzaji wa kutosha . . . na sasa walifaa kuingia katika kitanda cha mfalme, alituma mmoja kila siku ili alale na mfalme, ambaye, baada ya kufanya ngono naye, alimwagiza arudi mara moja kwa yule towashi. Lakini, Esta alipomjia, alifurahishwa naye halafu, akiisha kumwonea mapenzi, akamfanya mke wake wa sheria na kufanya arusi yao.”—Jewish Antiquities, Kitabu 11, 184-202, kilichotafsiriwa na Ralph Marcus, (Kitabu 11, sura 6, mafungu 1, 2, kama kilivyotafsiriwa na William Whiston).
Usimulizi huu wa kilimwengu ungeweza kuongoza mtu afikiri kwamba mabikira hao walishiriki katika ngono isiyo ya adili pamoja na mfalme na kwamba tofauti ya pekee katika kisa cha Esta ilikuwa kwamba ukosefu wake wa adili uliongoza kwenye ndoa na kuwa kwake malkia. Hata hivyo, Biblia inatutolea habari zilizo sahihi na zenye kutosheleza zaidi.
Baada ya kueleza juu ya kufanyiwa matendo ya kuwafanya wazuri zaidi, Biblia inasema hivi: “[Kwa masharti haya, NW] mwanamwali huingia hivyo kwa mfalme . . . Huenda jioni [yeye mwenyewe, NW], na asubuhi hurudi nyumba ya pili ya wanawake, mikononi mwa Shaashgazi, msimamizi wake mfalme, mwenye kuwalinda masuria. Wala haingii tena kwa mfalme, isipokuwa amempendeza mfalme, naye akaitwa kwa jina.”—Esta 2:13, 14.
Maandiko yanasema kwamba Esta “alipelekwa” kwenye “nyumba ya wanawake” kwa ajili ya ule muda mrefu ulioagizwa wa kuwafanya wawe wazuri zaidi: “Basi Esta alipelekwa kwa mfalme Ahasuero . . . Mfalme akampenda Esta kuliko wanawake wote, naye akapata neema na kibali machoni pake kuliko mabikira wote; basi akamtia taji ya kifalme kichwani pake, akamfanya awe malkia badala ya Vashti.”—Esta 2:8, 9, 16, 17.
Je! umeona kutokana na usimulizi huo wa Biblia ni wapi wanawake walipopelekwa baada ya wao kushinda pamoja na mfalme usiku? Kwenye ‘nyumba ya pili ya wanawake, mikononi mwa mwenye kuwalinda masuria’ (wanawake wa kupangishwa). Hivyo basi wao walikuwa wamepata kuwa masuria. Mordekai, mwandikaji wa kitabu cha Biblia cha Esta, alikuwa Mwebrania, na miongoni mwa watu wake huko nyuma, suria alikuwa na msimamo wa kijamii wa kuwa mke wa pili. Sheria ya kimungu iliruhusu kwamba mwanamume Mwisraeli angeweza kuchukua msichana wa kigeni aliyetekwa wakati wa vita, naye angekuwa suria wake, au mke wa pili, akiwa na haki mbalimbali na ulinzi wa kisheria. (Kumbukumbu 21:10-17; linganisha Kutoka 21:7-11.) Watoto waliozaliwa kwa huyo suria wa kisheria walikuwa wa halali na wangeweza kupata urithi. Wana 12 wa Yakobo, waliokuwa mababa wa zamani wa makabila 12 ya Israeli, walikuwa wazao wa wake zake na masuria wa kisheria.—Mwanzo 30:3-13.
Utaratibu wa kufuata ulikuwa kwamba baada ya mabikira hao kuwa pamoja na yule mfalme Mwajemi, walienda kwenye nyumba ya masuria. Hii inaonyesha kwamba walipata kuwa wake zake za pili.
Namna gani Esta? Biblia haisemi kwamba alilala pamoja na mfalme na hivyo akapata upendeleo wake. Haielezi juu ya kupelekwa kwake kwenye nyumba ya masuria, bali inasema hivi tu: “Basi Esta alipelekwa kwa mfalme Ahasuero, katika nyumba ya kifalme . . . Mfalme akampenda Esta kuliko wanawake wote.” Kumbuka kwamba mapema kidogo, bila kukubali kutoa hali yake ya nguvu za wema na ubikira kwa kufanya ngono, yeye alipata “neema [fadhili-upendo, NW]” ya “Hegai mwenye kuwalinda wanawake.” Zaidi ya hilo: “Huyu Esta alikuwa amepata [alikuwa akipata, NW] kibali machoni pa wote waliomwona.” (Esta 2:8, 9, 15-17) Hivyo basi Esta alimvutia mfalme kwa wazi na kupata heshima yake, kama vile alivyokuwa amepata heshima ya wengine.
Tunaweza kutoa asante kama nini kwa kuwa na mambo ya uhakika na muono-ndani ambao Biblia inatutolea! Ingawa sisi tuko maelfu ya miaka mbali na matukio hayo, hivyo sisi tuna sababu ya kuwa na uhakika kwamba Esta alitenda kwa nguvu za kutenda wema kikweli na kupatana na kanuni za kimungu.