Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 5/15 kur. 10-15
  • Fikirieni Mifano ya Ustahimilivu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Fikirieni Mifano ya Ustahimilivu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ustahimilivu kwa Ajili ya Jina Lake
  • Ustahimilivu kwa Ajili ya Wanadamu
  • Mfano wa Yesu wa Ustahimilivu
  • Mifano ya Ustahimilivu ya Maandiko ya Kiebrania
  • Fikiria Mfano wa Paulo
  • Yehova Ni Mungu Mstahimilivu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • ‘Jivikeni Wenyewe Ustahimilivu’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Iweni Wastahimilivu Kuelekea Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Ustahimilivu
    Mwimbieni Yehova
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 5/15 kur. 10-15

Fikirieni Mifano ya Ustahimilivu

“Mungu, . . . alivumilia kwa ustahimilivu mwingi vyombo vya hasira kuu vilivyofanywa vistahili uharibifu.”—WARUMI 9:22, NW.

1. (a) Neno la Mungu lililopuliziwa roho latumikiaje kwa manufaa yetu? (b) Kwa habari hii, kwa nini sifa ya ustahimilivu yafikiriwa hapa?

YEHOVA MUNGU, Muumba wetu, alitupa sisi Neno lake, Biblia Takatifu. Inapasa kutumika kama ‘taa ya miguu yetu, na mwanga wa njia yetu.’ (Zaburi 119:105) Neno la Mungu linatusaidia pia tuwe ‘tayari kabisa kwa kila kazi njema.’ (2 Timotheo 3:16, 17, NW) Hivyo njia moja ambayo hilo hututayarisha ni kwa kutupa mifano mizuri ya ustahimilivu. Sifa hiyo ni moja ya matunda ya roho ya Mungu na ni ya lazima ili tupate kibali chake na kupatana na wanadamu wenzetu.—Wagalatia 5:22, 23.

2. Ni nini maana ya neno la Kigiriki ambalo limefasiriwa “ustahimilivu,” na ni nani wa mbele kabisa katika kuonyesha sifa hiyo?

2 Neno la Kigiriki lililotafsiriwa “ustahimilivu” humaanisha kwa halisi “urefu wa roho.” Ustahimilivu umeelezwa kuwa “sifa hiyo ya kujizuia katika kukabiliana na jambo la kukasirisha ambayo hailipizi kisasi upesi au kuadhibu bila kusita.” (Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words, by W. E. Vine, Buku 3, ukurasa wa 12) Kuwa mstahimilivu kuna-maanisha kuzoea kujidhibiti na kutokuwa mwepesi wa hasira. Na ni nani wa mbele kabisa miongoni mwa wale wasio wepesi wa hasira, wenye kuonyesha ustahimilivu? Hapana mwingine ila Yehova Mungu. Hivyo, kwenye Kutoka 34:6, tunasoma kwamba Yehova ni “Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema [fadhili zenye upendo, NW] na kweli.” Kwa kweli, mara nane zaidi katika Maandiko, Yehova asemekana kuwa “si mwepesi wa hasira.”—Hesabu 14:18; Nehemia 9:17; Zaburi 86:15; 103:8; 145:8; Yoeli 2:13; Yona 4:2; Nahumu 1:3.

3. Ni sifa zipi zinazosababisha Mungu kuwa mstahimilivu?

3 Kuwa mstahimilivu, au kutokuwa mwepesi wa hasira ni jambo tu ambalo sisi tungetarajia kabisa kutoka kwa Yehova, kwa kuwa yeye ni mwenye uwezo na hekima zisizo na mwisho, mkamilifu katika haki, na mfano kamili wa upendo. (Kumbukumbu 32:4; Ayubu 12:13; Isaya 40:26; 1 Yohana 4:8) Anadhibiti sifa zake, akiziweka katika usawaziko mkamilifu nyakati zote. Neno lake linafunua nini juu ya kwa nini na jinsi gani ameonyesha ustahimilivu kuelekea wanadamu wasio wakamilifu?

Ustahimilivu kwa Ajili ya Jina Lake

4. Ni kwa sababu zipi nzuri mbili Mungu amedhihirisha ustahimilivu kuelekea watenda dhambi?

4 Kwa nini Yehova ni mstahimilivu? Kwa nini yeye hawaadhibu watenda dhambi mara moja tu? Si kwa sababu ya kutojali au ukosefu wa bidii kwa ajili ya uadilifu. Hapana, bali Yehova si mwepesi wa hasira naye ana sababu nzuri ya kutoadhibu watu upesi. Sababu moja ni ili jina lake lipate kujulishwa. Sababu nyingine ni kwamba wakati ulihitajiwa ili kujibu masuala ya enzi kuu ya Yehova na ukamilifu wa maadili wa ainabinadamu, yaliyozushwa na uasi katika Edeni. Bado sababu nyingine ya ustahimilivu wa Mungu ni kwamba unawapa wenye kukosa nafasi ya kusahihisha njia zao.

5, 6. Kwa nini Yehova alidhihirisha ustahimilivu kuhusiana na uasi wa mwanadamu?

5 Yehova alikuwa mstahimilivu katika kushughulika na wanadamu wawili wa kwanza katika shamba la Edeni. Walipovunja amri yake dhidi ya kula tunda la mti wa ujuzi wa mema na mabaya, mara hiyo tu yeye angaliua wao na malaika mwenye kuasi ambaye alimdanganya Hawa. Hakukuwa na shaka kwamba maoni ya Yehova ya uadilifu na haki yalikuwa yametendewa vibaya, kwamba aliwakasirikia wale waasi watatu. Angalikuwa katika haki zake kikamilifu ikiwa angaliwauwa mara hiyo tu. Mungu alikuwa amemwonya mwanamume wa kwanza, Adamu hivi: “Walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.” (Mwanzo 2:17) Siku ile ile Adamu alipotenda dhambi, Mungu alitaka hesabu kwa wale waasi watatu na akatangaza hukumu ya kifo. Kihukumu, Adamu na Hawa walikufa siku iyo hiyo. Hata hivyo, Muumba wetu mwenye ustahimilivu alikubali Adamu kuishi miaka 930.—Mwanzo 5:5.

6 Mungu alikuwa na sababu nzuri za kuwa mstahimilivu, au kutokuwa mwepesi wa hasira, katika kisa hicho. Kama angaliua waasi hao mara moja tu, hiyo isingalijibu lawama la wazi sana la Ibilisi kwamba Yehova Mungu hastahili kuabudiwa na kwamba hawezi kuwa na watumishi wa kibinadamu ambao watadumisha ukamilifu wao wa maadili kwake zijapokuwa hali mbalimbali. Tena, maswali kama haya yangalibaki bila kujibiwa: Lilikuwa kosa la nani kwamba Adamu na Hawa walitenda dhambi? Je! Yehova aliwaumba kwanza wenye udhaifu kiadili sana hivi kwamba hawakuweza kupinga kishawishi kisha akawaadhibu kwa ajili ya kushindwa kufanya hivyo? Jibu la hayo yote laonekana kutoka kwa usimulizi unaopatikana katika kitabu cha Ayubu, sura za 1 na 2. Kwa kuruhusu jamii ya wanadamu kuongezeka, Yehova aliwaruhusu wanadamu wawe na nafasi za kuthibitisha mashtaka ya Shetani kuwa bandia.

7. Kwa nini Yehova hakumwua Farao mara moja?

7 Yehova alipokuwa karibu kukomboa watu wake, Waisraeli, kutoka kwa utumwa wa Misri, yeye alithibitisha tena kuwa mstahimilivu. Yehova angaliweza kuharibu Farao na jeshi lake mara moja tu. Hata hivyo, badala ya kufanya hivyo, Mungu aliwavumilia kwa wakati fulani. Kwa sababu gani nzuri? Wakati ulipopita, Farao akawa mshupavu zaidi katika kukataa kwake kuacha Waisraeli kuondoka Misri wakiwa watu wa Yehova walio huru. Hivyo alionyesha kwamba alikuwa ‘chombo cha hasira’ kilichostahili uharibifu kwa kumwasi Yehova. (Warumi 9:14-24) Hata hivyo, kulikuwa sababu kubwa zaidi ya Mungu kuwa mstahimilivu katika kisa hicho. Kupitia Musa, alimwambia Farao: “Wakati huu ningekwisha kuunyosha mkono wangu, na kukupiga wewe na watu wako, kwa tauni, nawe ungekatiliwa mbali na kuondolewa katika nchi; lakini, nilikusimamisha wewe kwa sababu ii hii, ili nikuonyeshe uweza wangu, tena kwamba jina langu litangazwe katika dunia yote.”—Kutoka 9:15, 16.

8. Ni kwa sababu gani Mungu hakuwaua Waisraeli wenye kuasi jangwani?

8 Ustahimilivu wa Yehova ulionyeshwa pia kwa sababu nzuri Waisraeli walipokuwa jangwani. Jinsi walivyoijaribu saburi ya Mungu kwa kuabudu ndama wa dhahabu na kwa kushindwa kuzoea imani wakati wapelelezi kumi waliporudi na ripoti mbaya! Mungu hakuwafutilia mbali kuwa watu wake kwa sababu jina na sifa yake vilihusika. Naam, Yehova alidhihirisha ustahimilivu kwa ajili ya jina lake.—Kutoka 32:10-14; Hesabu 14:11-20.

Ustahimilivu kwa Ajili ya Wanadamu

9. Kwa nini Yehova alionyesha ustahimilivu katika siku za Noa?

9 Yehova amekuwa mstahimilivu kwa ajili ya aina ya binadamu tangu Adamu alipokosea wote ambao wangekuwa wazao wake, akiwatendea jambo lisilo la haki kwa kutenda dhambi. Ustahimilivu wa Mungu uliwezesha kosa hilo lisahihishwe kwa kuwa aliruhusu wakati ili wanadamu wenye kutubu waje kupatanishwa naye. (Warumi 5:8-10) Yehova Mungu pia alionyesha ustahimilivu kuelekea wanadamu katika siku za Noa. Wakati huo, “BWANA [Yehova, NW] akaona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani na kwamba kila kusudi analowaza moyoni mwake ni baya tu sikuzote.” (Mwanzo 6:5) Ingawa Mungu angaliweza kufutilia mbali jamii ya wanadamu mara tu alipoona hali hiyo, aliamuru kwamba angeleta mwisho wa hali hiyo katika muda wa miaka 120. (Mwanzo 6:3) Wonyesho huo wa ustahimilivu uliruhusu wakati ili Noa awe na wana watatu, wakue na kuoa, na familia hiyo ijenge safina ili kuokoa nafsi zao na ili kuhifadhi uumbaji wa wanyama. Katika njia hiyo iliwezekana kusudi la Mungu la kwanza kwa dunia kutimizwa.

10, 11. Kwa nini Yehova alikuwa mstahimilivu sana na taifa la Israeli?

10 Ufafanuzi mwingine wa ustahimilivu unatumika hasa kuhusu kushughulika kwa Mungu pamoja na watu wake. Huo ni “saburi yenye kuvumilia mabaya au jambo la kukasirisha, pamoja na kukataa kuacha kuwa na tumaini la kwamba uhusiano uliovurugwa utatengenezeka.” (Insight on the Scriptures, Buku 2, ukurasa wa 262; limechapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.) Hiyo huonyesha sababu zaidi ya Mungu kuwa mstahimilivu kuelekea Waisraeli. Tena na tena waligeukia mbali kutoka kwa Yehova na wakaja kuwa katika utumwa wa mataifa Wasio Wayahudi. Hata hivyo, yeye alionyesha ustahi-milivu kwa kukomboa Waisraeli na kuwapa nafasi ya kutubu.—Waamuzi 2:16-20.

11 Wafalme Waisraeli walio wengi waliongoza raia wao kuingia katika ibada bandia. Je! Mungu alitupilia mbali taifa hilo mara moja? Hapana, hakuacha upesi kuwa na tumaini kwamba uhusiano uliovurugwa utatengenezeka. Badala ya hiyo, Yehova hakuwa mwepesi wa hasira. Akionyesha ustahimilivu, Mungu aliwapa nafasi ya kutubu tena na tena. Tunasoma kwenye 2 Nyakati 36:15, 16 hivi: “BWANA [Yehova, NW], Mungu wa baba zao, akatuma kwao kwa mikono ya wajumbe wake, akiondoka mapema, na kutuma; kwa sababu aliwahurumia watu wake, na makao yake; lakini waliwadhihaki wajumbe wa Mungu, na kuyadharau maneno yake, na kuwacheka manabii wake, hata ilipozidi ghadhabu ya BWANA [Yehova, NW] juu ya watu wake, hata kusiwe na kuponya.”

12. Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanatoa ushuhuda gani juu ya sababu Yehova ni mstahimilivu?

12 Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanaandaa pia ushuhuda kwamba Yehova huonyesha ustahimilivu kusaidia watu wake wenye kukosa. Kwa mfano, mtume Paulo auliza Wakristo wenye kukosa: “Waudharau wingi wa wema wake na ustahimili wake na uvumilivu wake, usijue ya kuwa wema wa Mungu wakuvuta upate kutubu?” (Warumi 2:4) Maneno haya ya Petro ni ya maana iyo hiyo: “Bwana [Yehova, NW] hakawii kuitimiza ahadi yake, kama wengine wanavyokudhani kukawia, bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba.” (2 Petro 3:9) Kwa kufaa zaidi, tunaambiwa ‘tuhesabu uvumilivu wa Bwana wetu kuwa ni wokovu.’ (2 Petro 3:15) Hivyo, tunaona kwamba Yehova ni mstahimilivu, si kwa sababu ya kusisimukia mambo bila kufikiri wala kwa sababu ya uzembe, bali kwa sababu jina na makusudi yake yanahusika na ni mwenye rehema na upendo.

Mfano wa Yesu wa Ustahimilivu

13. Kuna ushuhuda gani mwingine wa Kimaandiko kwamba Yesu Kristo alikuwa mstahimilivu?

13 Wa pili tu kwa mfano wa ustahimilivu unaotolewa na Mungu ni ule wa Mwana wake, Mesiya, Yesu Kristo. Yeye ni mfano mzuri sana wa kujizuia bila kulipa kisasi kwa haraka-haraka ajapokasirishwa.a Kwamba Mesiya angekuwa mstahimilivu kulitabiriwa na nabii Isaya katika maneno haya: “Alionewa, lakini alinyenyekea, wala hakufunua kinywa chake; kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni, na kama vile kondoo anyamazavyo mbele yao wakatao manyoya yake; naam, hakufunua kinywa chake.” (Isaya 53:7) Inayoshuhudia ukweli uo huo ni taarifa ya Petro: “Yeye alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi kwake yeye ahukumuye kwa haki.” (1 Petro 2:23) Jinsi wanafunzi wa Yesu walivyomjaribu kwa mabishano yao ya tena na tena juu ya ni nani aliye mkubwa zaidi! Hata hivyo, jinsi yeye alivyokuwa mstahimilivu na mwenye saburi nao!—Marko 9:34; Luka 9:46; 22:24.

14. Mfano wa Yesu wa kuwa mstahimilivu unapasa kutusukuma kufanya nini?

14 Sisi tunapaswa kufuata mfano ambao Yesu aliweka katika kuwa mstahimilivu. Paulo aliandika hivi: “Na tupige mbio kwa saburi katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu, tukimtazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu [Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu, NW]; ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba [mti wa mateso, NW] na kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu. Kwa kweli mtafakarini sana yeye aliyeyastahimili mapingamizi makuu namna hii ya watendao dhambi juu ya nafsi zao, msije mkachoka, mkizimia mioyoni mwenu.”—Waebrania 12:1-3.

15. Tunajuaje kwamba Yesu alikuwa mstahimilivu na alivumilia majaribu kwa nia?

15 Kwamba Yesu alikuwa mstahimilivu na mwenye kuvumilia majaribu kwa nia inaweza kuonwa katika mwelekeo aliodhihirisha wakati wa kukamatwa kwake. Baada ya kumkemea Petro kwa kuchukua upanga ili kumlinda Bwana wake, Yesu alisema hivi: “Ama wadhani ya kuwa mimi siwezi kumsihi Baba yangu, naye ataniletea sasa hivi zaidi ya majeshi kumi na mawili ya malaika? Yatatimizwaje basi maandiko, ya kwamba hivyo ndivyo vilivyopasa kujiri?”—Mathayo 26:51-54; Yohana 18:10, 11.

Mifano ya Ustahimilivu ya Maandiko ya Kiebrania

16. Maandiko yanatuonyeshaje kwamba Yusufu mwana wa Yakobo alikuwa mstahimilivu?

16 Hata wanadamu wasio wakamilifu, wenye dhambi wanaweza kuonyesha ustahimilivu. Maandiko ya Kiebrania yana mifano ya saburi yenye kuvumilia mabaya inayohusu watu wasio wakamilifu. Kwa mfano, kuna Yusufu, mwana wa Yakobo mzee wa ukoo Mwebrania. Jinsi alivyovumilia kwa saburi mambo yasiyo haki aliyotendewa na ndugu-nusu zake na mke wa Potifa! (Mwanzo 37:18-28; 39:1-20) Yusufu hakuruhusu majaribu hayo yamfanye awe na uchungu. Hilo laonekana wazi wakati alipowaambia ndugu zake hivi: “Msihuzunike, wala msiudhike nafsi zenu, kwa kuniuza huku; maana Mungu alinipeleka mbele yenu kuhifadhi maisha za watu.” (Mwanzo 45:4, 5) Ni mfano mzuri kama nini wa ustahimilivu uliowekwa na Yusufu!

17, 18. Tuna ushuhuda gani wa ustahimilivu katika kisa cha Daudi?

17 Daudi ni mfano mwingine wa mtumishi mwaminifu wa Yehova aliyevumilia mabaya kwa saburi, akionyesha ustahimilivu. Akifuatwa kama mbwa na Mfalme Sauli mwenye wivu, nyakati mbili Daudi angaliweza kulipa kisasi kwa kumwua. (1 Samweli 24:1-22; 26:1-25) Lakini Daudi alimngojea Mungu, kama vile yaweza kuonwa kutokana na maneno yake kwa Abishai: “Aishivyo BWANA [Yehova, NW], BWANA [Yehova, NW] atampiga; au siku yake ya kufa itampata; au atashuka kwenda vitani na kupotea. Hasha! nisiunyoshe mkono wangu juu ya masihi wa BWANA [Yehova, NW]”! (1 Samweli 26:10, 11) Naam, Daudi alikuwa na uwezo wa kukomesha kuwindwa kwake na Sauli. Badala ya hiyo, Daudi alichagua kuwa mstahimilivu.

18 Fikiri pia, kilichotokea wakati Mfalme Daudi alipokuwa akikimbia kutoka kwa mwana wake Absalomu aliyekuwa msaliti. Shimei, Mbenyamini wa nyumba ya Sauli, alimtupia Daudi mawe na kumlaani, akipaaza sauti hivi: “Nenda zako! Nenda zako! Ewe mtu wa damu! Ewe mtu usiyefaa!” Abishai alitaka Shimei auawe, lakini Daudi alikataa kulipa kisasi. Badala ya kufanya hivyo, yeye alidhihirisha sifa ya ustahimilivu tena.—2 Samweli 16:5-13.

Fikiria Mfano wa Paulo

19, 20. Mtume Paulo alijionyeshaje kuwa mstahimilivu?

19 Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, tuna mfano mwingine mzuri wa ustahimilivu unaohusu mwanadamu asiye mkamilifu—mtume Paulo. Alionyesha saburi yenye kuvumilia, ustahimilivu, kuhusiana na adui zake wa kidini na watu mmoja mmoja waliodai kuwa Wakristo pia. Naam, Paulo alidhihirisha ustahimilivu ingawa wengine katika kundi la Korintho walisema hivi: “Nyaraka zake ni nzito, hodari; bali akiwapo mwenyewe mwilini ni dhaifu, na maneno yake si kitu.”—2 Wakorintho 10:10; 11:5, 6, 22-33.

20 Kwa hiyo, ilikuwa kwa sababu nzuri kwamba Paulo waliwaambia Wakorintho hivi: “Katika kila neno tujipatie sifa njema, kama watumishi wa Mungu; katika saburi nyingi, katika dhiki, katika misiba, katika shida; katika mapigo, katika vifungo, katika fitina, katika taabu, katika kukesha, katika kufunga; katika kuwa safi, katika elimu, katika uvumilivu, katika utu wema, katika Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW], katika upendo usio unafiki.” (2 Wakorintho 6:4-6) Kwa habari iyo hiyo, mtume angeweza kumwandikia mfanya kazi mwenzi wake Timotheo hivi: “Umeyafuata mafundisho yangu, na mwenendo wangu, na makusudi yangu, na imani, na uvumilivu, na upendo, na saburi; tena na adha zangu na mateso, . . . naye Bwana aliniokoa katika hayo yote.” (2 Timotheo 3:10, 11) Mtume Paulo alituwekea mfano mzuri kama nini katika kuwa mstahimilivu!

21. Makala inayofuata yaweza kutusaidiaje?

21 Kwa wazi, Maandiko yamejaa mifano mizuri ya ustahimilivu. Yehova na Mwana wake mpendwa ni mifano mikuu. Lakini inatia moyo kama nini kuona kwamba sifa hii imeonyeshwa na wanadamu wasio wakamilifu, kama Yusufu, Daudi, na mtume Paulo! Makala inayofuata imekusudiwa kutusaidia kuiga mifano mizuri kama hiyo.

[Maelezo ya Chini]

a Kuwa mstahimilivu hakumaanishi kuteseka kwa muda mrefu tu. Ikiwa mtu mwenye kuteseka kwa muda mrefu angefadhaika au awe na uchungu kwa sababu ya kutoweza kulipa kisasi, yeye asingekuwa mstahimilivu.

Ungejibuje?

◻ Inamaanisha nini kuwa mstahimilivu?

◻ Yehova amekuwa mstahimilivu kwa sababu zipi hasa?

◻ Yesu alijionyesha kuwa mstahimilivu katika njia zipi?

◻ Kuna uthibitisho gani wa Kimaandiko kwamba ustahimilivu unaweza kuonyeshwa na wanadamu wasio wakamilifu?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Yusufu, Ayubu, Yesu, Daudi, na Paulo, walikuwa mifano ya ustahimilivu

[Picha katika ukurasa wa 13]

Yesu alionyesha ustahimilivu kuelekea wanafunzi wake

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki