“Nuru Imekuja Ulimwenguni”
“Hii ndiyo hukumu; ya kuwa nuru imekuja ulimwenguni, na watu wamependa giza kupita nuru.”—YOHANA 3:19, ZSB.
1. Kwa nini kila mtu apaswa kufikiria hukumu ya Mungu?
WATU walio wengi leo hawana wasiwasi mwingi kuhusu hukumu ya Mungu. Wengine hudhani kwamba Mungu atawapa hukumu yenye kupendeleka ikiwa wanaenda kanisani kwa ukawaida na kama hawadhuru majirani wao kwa vyovyote. Kwa wengi, mafundisho ya Jumuiya ya Wakristo juu ya helo yenye moto na purgatori yamefanya wazo la hukumu ya kimungu lisisadikike. Lakini ubaridi ulioenea sana na uwongo wa Jumuiya ya Wakristo hauwezi kubadili uhakika wa kwamba kila binadamu atahukumiwa na Mungu hatimaye. (Warumi 14:12; 2 Timotheo 4:1; Ufunuo 20:13) Na mengi yatategemea hukumu hiyo. Wale watakaohukumiwa kwa kupendeleka watapokea zawadi ya Mungu ya uhai wa milele, hali wale watakaohukumiwa kwa kutopendeleka watapokea mishahara kamili ya dhambi: kifo.—Warumi 6:23.
2. Hukumu ya Mungu inategemea nini?
2 Hivyo, Wakristo wa kweli wanafikiria hu-kumu ya Mungu, na wao wanatamani kwa bidii kumpendeza. Wanaweza kufanyaje hivyo? Kwenye Yohana 3:19, Yesu alitupatia ufunguo. Asema, ZSB: “Hii ndiyo hukumu; ya kuwa nuru imekuja ulimwenguni, na watu wamependa giza kupita nuru; kwa sababu matendo yao yalikuwa mabaya.” Naam, hukumu ya Mungu itategemea kama tunapenda nuru badala ya giza.
“Mungu ni Nuru”
3. Giza ni nini, na nuru ni nini?
3 Katika maana ya kiroho, giza linahusisha ukosefu wa maarifa na hali ya kutokuwa na tumaini iliyomo katika milki ya Shetani—ingawa mara nyingi Shetani hujifanya kuwa “malaika wa nuru.” (2 Wakorintho 4:4; 11:14; Waefeso 6:12) Kwa upande mwingine, nuru inahusisha ufahamu na mnurisho unaotoka kwa Yehova Mungu. Paulo alisema juu ya nuru hiyo alipoandika hivi: “Kwa kuwa Mungu aliyesema, Nuru itang’aa toka gizani, ndiye aliyeng’aa mioyoni mwetu, atupe nuru ya elimu ya utukufu wa Mungu katika uso wa Yesu Kristo.” (2 Wakorintho 4:6) Nuru ya kiroho inatambulishwa kwa ukaribu sana na Yehova Mungu hivi kwamba mtume Yohana aliandika hivi: “Mungu ni nuru.”—1 Yohana 1:5; Ufunuo 22:5.
4. (a) Yehova amefanya nuru ipatikaneje? (b) Tunaweza kuonyeshaje upendo wa nuru?
4 Yehova amefanya nuru ipatikane kupitia neno lake, linalopatikana leo kwa wingi katika njia ya maandishi katika Biblia Takatifu. (Zaburi 119:105; 2 Petro 1:19) Hivyo, mtunga zaburi alikuwa kweli kweli akionyesha upendo wake wa nuru alipoandika hivi: “Sheria yako naipenda mno ajabu, ndiyo kutafakari kwangu mchana kutwa. Nafsi yangu imezishika shuhuda [vikumbusho vyako, NW] zako, nami nazipenda mno.” (Zaburi 119:97, 167) Je! wewe huipenda nuru kwa kadiri ambayo mtunga zaburi kwa wazi aliipenda? Je! wewe husoma Neno la Mungu kwa ukawaida, ukilitafakari, na kujikaza sana kutumia yale linayosema? (Zaburi 1:1-3) Ikiwa ndivyo, wewe unatafuta kupokea hukumu yenye kupendeleka kutoka kwa Yehova.
“Mimi Ni Nuru ya Ulimwengu”
5. Nuru ya kimungu inakazia juu ya nani?
5 Nuru yenye kutoa uhai kutoka kwa Yehova inakazia kwenye utu wa Yesu Kristo. Katika utangulizi wa Gospeli ya Yohana, twasoma hivi: “Ndani yake ndimo ulimokuwa uzima, nao ule uzima ulikuwa nuru ya watu. Nayo nuru yang’aa gizani, wala giza halikuiweza.” (Yohana 1:4, 5) Kwa kweli, Yesu ana ushirikiano wa karibu sana na nuru hivi kwamba anaitwa “Nuru halisi, amtiaye nuru kila mtu.” (Yohana 1:9) Yesu mwenyewe alisema hivi: “Muda nilipo ulimwenguni, mimi ni nuru ya ulimwengu.”—Yohana 9:5.
6. Ni lazima mtu afanye nini ili kupata hukumu yenye kupendeleka iongozayo kwenye uhai wa milele?
6 Kwa hiyo, wale wapendao nuru humpenda Yesu nao wana imani katika yeye. Bila rejezeo kwa Yesu haiwezekani kupata hukumu yenye kupendeleka. Naam, ni kwa kumtegemea tu akiwa njia iliyowekwa na Mungu ya wokovu kwamba tunaweza kupata hukumu yenye kupendeleka. Yesu alisema hivi: “Amwaminiye [Yeye anayejizoeza imani katika, NW] Mwana yuna uzima wa milele; asiyemwamini [asiyejizoeza imani katika, NW] Mwana hataona uzima, bali ghadhabu ya Mungu inamkalia.” (Yohana 3:36) Lakini inamaanisha nini kujizoeza imani katika Yesu?
7. Imani katika Yesu inamaanisha imani katika nani mwingine?
7 Kwanza, Yesu mwenyewe alisema hivi: “Yeye aniaminiye [ajizoezaye imani katika, NW] mimi, haniamini [hajizoezi imani katika, NW] mimi [tu] bali [pia] yeye aliyenipeleka. Naye anitazamaye mimi amtazama [pia] yeye aliyenipeleka. Mimi nimekuja ili niwe nuru ya ulimwengu, ili kila mtu aniaminiye [ajizoezaye imani katika, NW] mimi asikae gizani.” (Yohana 12:44-46) Wale wampendao Yesu na kujizoeza imani katika yeye ni lazima pia wawe na upendo wenye kina kirefu na imani katika Yehova, Mungu na Baba ya Yesu. (Mathayo 22:37; Yohana 20:17) Wowote watumiao jina la Yesu katika ibada yao lakini wakosa kumpa Yehova heshima iliyo kuu zaidi hawaonyeshi upendo wa kweli wa nuru.—Zaburi 22:27; Warumi 14:7, 8; Wafilipi 2:10, 11.
“Wakili Mkuu” wa Mungu
8. Nuru ya kimungu ilikaziaje juu ya Yesu hata kabla ya kuzaliwa kwake akiwa binadamu?
8 Kujizoeza imani katika Yesu kunamaanisha pia kukubali kikamili daraka lake katika makusudi ya Yehova. Umaana wa daraka hilo ulitokezwa wakati malaika alipomwambia Yohana hivi: “Kutoa ushahidi kwa Yesu ndiko kunakovuvia kutoa unabii.” (Ufunuo 19:10, NW; Matendo 10:43; 2 Wakorintho 1:20) Kutoka unabii wa kwanza kabisa katika Edeni, unabii mbalimbali wote uliopuliziwa kimungu hatimaye huhusisha Yesu na mahali pake katika kutimiza makusudi ya Mungu. Vivyo hivyo, Paulo aliwaambia Wakristo wa Galatia kwamba agano la Sheria lilikuwa “kiongozi kutuleta kwa Kristo.” (Wagalatia 3:24) Agano la Sheria hilo la zamani lilibuniwa ili kulitayarisha taifa kwa ajili ya kuja kwa Yesu akiwa Mesiya. Kwa hiyo hata kabla ya kuzaliwa kwake akiwa binadamu, nuru kutoka kwa Yehova ilikazia juu ya Yesu.
9. Kupenda nuru kumehusisha nini tangu 33 W.K.?
9 Katika 29 W.K., Yesu alijitoa mwenyewe kwenye ubatizo akapakwa mafuta kwa roho takatifu, hivyo akawa Mesiya aliyeahidiwa. Katika 33 W.K. alikufa akiwa mtu mkamilifu, akafufuliwa, akapaa mbinguni, na huko akatoa thamani ya uhai wake kwa ajili ya dhambi zetu. (Waebrania 9:11-14, 24) Mfululizo huo wa mambo ulitia alama wakati wenye umaana wa Mungu kushughulika na wanadamu. Yesu sasa akawa “Wakili Mkuu wa uhai,” ‘Wakili Mkuu wa wokovu,’ “Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu.” (Matendo 3:15; Waebrania 2:10; 12:2; Warumi 3:23, 24, NW) Tangu 33 W.K. na kuendelea, wapendao nuru wametambua, na kukubali kwamba isipokuwa Yesu “hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo.”—Matendo 4:12.
10. Kwa nini ni jambo la maana sana kusikiliza maneno ya Yesu na kuyatii?
10 Kujizoeza imani katika Yesu kunamaa-nisha pia kumkubali kuwa “Neno” na “Mshauri wa ajabu.” (Yohana 1:1; Isaya 9:6) Yale asemayo Yesu huonyesha kweli ya kimungu sikuzote. (Yohana 8:28; Ufunuo 1:1, 2) Kumsikiliza ni jambo la uhai ama kifo. Yesu aliwaambia Wayahudi wa siku yake hivi: “Yeye alisikiaye neno langu na kumwamini yeye aliyenipeleka yuna uzima wa milele; wala haingii hukumuni, bali amepita kutoka mautini kuingia uzimani.” (Yohana 5:24) Katika karne ya kwanza W.K., wale waliofuata maneno ya Yesu waliokolewa kutoka giza la ulimwengu wa Shetani wakaja kwenye uhai. Walitangazwa rasmi kuwa waadilifu wakiwa na tazamio la kuwa warithi wenzi pamoja naye katika Ufalme wake wa kimbingu. (Waefeso 1:1; 2:1, 4-7) Leo, kutii maneno ya Yesu kunawafungulia wengi njia ya kutangazwa rasmi kuwa waadilifu wakiwa na tazamio la kuokoka Har–Magedoni na kupata uhai mkamilifu wa kibinadamu katika ulimwengu mpya.—Ufunuo 21:1-4; linganisha Yakobo 2:21, 25.
“Kichwa Juu ya Vitu Vyote”
11. Yesu alipewa mamlaka gani ya juu katika 33 W.K.?
11 Baada ya kufufuliwa kwake, Yesu alifunulia wafuasi wake sehemu nyingine ya nuru. Alisema hivi: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” (Mathayo 28:18) Hivyo Yesu alikuwa ameinuliwa kwenye cheo chenye fahari zaidi katika tengenezo la Yehova la ulimwengu wote mzima. Paulo aeleza zaidi asemapo hivi: “[Mungu] aliotenda katika Kristo, wakati alipomufufua toka wafu, na kumukalisha kwa mukono wake wa kuume katika pahali pa mbingu, juu sana kuliko utawala wote na mamlaka na nguvu na usultani, na kila jina linalotajwa, si katika ulimwengu huu tu, lakini vilevile katika ule utakaokuja; na ameweka vitu vyote chini ya miguu yake, akamuweka awe kichwa juu ya vitu vyote kwa kanisa [kundi, NW]; lililo mwili wake.” (Waefeso 1:20-23, ZSB; Wafilipi 2:9-11) Tangu 33 W.K., kuipenda nuru kumetia ndani kukiri cheo hicho cha juu cha Yesu.
12. Wakristo wapakwa-mafuta wamekubali nini kwa furaha tangu mwanzoni, na wao wameonyeshaje hilo kwa njia ya matendo?
12 Hatimaye, ainabinadamu yote italazimika kukiri mamlaka ya juu ya Yesu. (Mathayo 24:30; Ufunuo 1:7) Hata hivyo, wapendao nuru, wameitambua kwa furaha tangu mwanzoni. Washiriki wapakwa-mafuta wa kundi la Kikristo hukubali Yesu kuwa “kichwa cha mwili, yaani, cha kanisa [kundi, NW].” (Wakolosai 1:18; Waefeso 5:23) Wanapokuwa sehemu ya mwili huo, ‘wanaokolewa katika nguvu za giza, na kuhamishwa na kuingizwa katika ufalme wa Mwana wa pendo lake.’ (Wakolosai 1:13) Tangu wakati huo na kuendelea, wanajitahidi kufuata mwongozo wa Yesu katika kila sehemu ya maisha yao, na katika wakati wetu wamewafunza “kondoo wengine” kufanya vivyo hivyo. (Yohana 10:16) Kukiri mwongozo wa Yesu ni takwa kuu ili kupokea hukumu yenye kupendeleka.
13. Yesu alianza kutumia mamlaka ya Ufalme wakati gani, na ni nini kimefuatia hapa duniani?
13 Alipopaa mbinguni katika 33 W.K., Yesu hakutumia mamlaka yake ya juu kikamili. Ingawa alikuwa Kichwa cha kundi la Kikristo, alingojea wakati uliofaa ili kutumia mamlaka kamili juu ya ainabinadamu kwa ujumla. (Zaburi 110:1; Matendo 2:33-35) Wakati huo ukaja katika 1914, Yesu alipotawazwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu na “siku za mwisho” za ulimwengu huu zikaanza. (2 Timotheo 3:1) Tangu 1919, kukusanywa kwa wapakwa-mafuta waliobaki kumeendelea kufikia mwisho wake. Tangu 1935 hasa, Yesu amekuwa akigawanya ainabinadamu katika “kondoo” watakaourithi ‘ufalme waliowekewa tayari,’ na “mbuzi,” ‘watakaokwenda zao kuingia katika adhabu ya milele.’—Mathayo 25:31-34, 41, 46.
14. Umati mkubwa umeonyeshaje upendo wa nuru, na ni nini kitakachotokea kwao?
14 Kwa furaha, kondoo wamethibitika kuwa wengi katika hizi siku za mwisho. Umati mkubwa wao ukihesabiwa kuwa mamilioni umetokea kwenye mandhari ya ulimwengu kutoka “kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha.” Kama waandamani wao, wapakwa-mafuta, hawa wenye mfano wa kondoo hupenda nuru. “Wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo,” na wao hupaza sauti kubwa: “Wokovu una Mungu wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo.” Kwa sababu ya hiyo, umati mkubwa wakiwa kikundi watapokea hukumu yenye kupendeleka. Washiriki walo “wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu,” wakiokoka uharibifu wa wale wapendao giza kwenye Har–Magedoni.—Ufunuo 7:9, 10, 14.
“Watoto wa Nuru”
15. Vitendo vyetu vinaonyeshaje ujitiisho wetu kwa Mfalme, Yesu Kristo?
15 Lakini, wapendao nuru wawe ni wapakwa-mafuta au kondoo wengine waweza kujitiishaje kwa njia yenye kupendeleka kwa Yesu akiwa yule aliyetawazwa na Mungu kuwa Mfalme na hakimu mtendaji? Njia moja ni kwa kujaribu kuwa aina ya watu ambao Yesu hukubali. Alipokuwa duniani Yesu alionyesha uthamini wa sifa kama vile unyofu wa moyo, bidii ya moyo wote, na uchangamfu kwa kweli, naye mwenyewe alionyesha mfano mzuri wa sifa hizo. (Marko 12:28-34, 41-44; Luka 10:17, 21) Kama tunatamani hukumu yenye kupendeleka, ni lazima tusitawishe sifa kama hizo.
16. Kwa nini ni muhimu kuondolea mbali matendo ya giza?
16 Hiyo ni kweli hasa kwa kuwa giza la ulimwengu wa Shetani linazidi kuwa nzito mwisho ukaribiapo. (Ufunuo 16:10) Kwa hiyo maneno Paulo aliyowaandikia Warumi yanafaa sana: “Usiku umeendelea sana, mchana umekaribia; basi na tuyavue matendo ya giza, na kuzivaa silaha za nuru. Kama ilivyohusika na mchana na tuenende kwa adabu; si kwa ulafi na ulevi, si kwa ufisadi na uasherati, si kwa ugomvi na wivu.” (Warumi 13:12, 13) Uhai wa milele ukiwa zawadi kutoka kwa Mungu, ukweli wa imani yetu na upendo wetu wa nuru unathibitishwa na vitendo vyetu. (Yakobo 2:26) Hivyo, hukumu tunayopokea itategemea kwa kadiri kubwa tunavyozoea matendo mazuri na kuepuka matendo maovu.
17. ‘Kuvaa Bwana Yesu Kristo’ kunamaanisha nini?
17 Baada ya kutoa shauri lake kwenye Warumi 13:12, 13, mtume Paulo amalizia kwa kusema hivi: “Vaeni Bwana Yesu Kristo, wala msiuangalie mwili, hata kuwasha tamaa zake.” (Warumi 13:14) ‘Kuvaa Bwana Yesu Kristo’ kunamaanisha nini? Kunamaanisha kwamba Wakristo wapaswa kumfuata Yesu kwa ukaribu, ni kama kujivika mfano wake na mwelekeo wake, wakijitahidi kuwa wenye mfano wa Kristo. “Kwa sababu ndio mlioitiwa,” akasema Petro, “maana Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, akawaachia kielelezo, mfuate nyayo zake.”—1 Petro 2:21.
18. Ni mabadiliko gani makubwa huenda yakahitajiwa ikiwa tunatamani kupokea hukumu yenye kupendeleka?
18 Mara nyingi hiyo inahusisha mabadiliko makubwa katika maisha ya Mkristo. “Kwa maana zamani ninyi mlikuwa giza,” akasema Paulo, “bali sasa mmekuwa nuru katika Bwana; enendeni kama watoto wa nuru; kwa kuwa tunda la nuru ni katika wema wote na haki na kweli.” (Waefeso 5:8, 9) Wowote wazoeao matendo ya giza si wapenda nuru na hawatapokea hukumu yenye kupendeleka isipokuwa wakifanya badiliko.
“Ninyi Ni Nuru ya Ulimwengu”
19. Mkristo aweza kuangaza nuru kwa njia zipi tofauti-tofauti?
19 Hatimaye, kupenda nuru kunamaanisha kuangaza nuru hiyo ili wengine waweze kuiona na kuvutwa kwayo. “Ninyi ni nuru ya ulimwengu,” akasema Yesu. Na aliongeza hivi: “Nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni.” (Mathayo 5:14, 16) Matendo mazuri ya Mkristo hutia ndani kuonyesha kila aina ya wema na uadilifu na kweli, kwa kuwa mwenendo mzuri kama huo huandaa ushahidi wenye nguvu kwa ajili ya kweli. (Wagalatia 6:10; 1 Petro 3:1) Yanatia ndani hasa kuongea na wengine juu ya kweli. Leo, hiyo inamaanisha kushiriki katika kampeni ya ulimwenguni pote ya kuhubiri “habari njema ya ufalme . . . katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote.” Inamaanisha pia, kuwatembelea tena kwa subira waliopendezwa, kujifunza Biblia pamoja nao, na kuwasaidia, wao pia, watokeze matendo ya nuru.—Mathayo 24:14; 28:19, 20.
20. (a) Nuru inang’aa kwa kadiri gani leo? (b) Ni mibaraka gani ya kutajirisha inayoonewa shangwe na wale wanaoitikia nuru?
20 Katika siku yetu, kwa sababu ya utendaji wa kuhubiri wenye bidii wa Wakristo waaminfu, habari njema inasikiwa katika nchi zaidi ya 200, na nuru inang’aa zaidi ya wakati mwingine wowote. Yesu alisema hivi: “Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, yeye anifuataye hatakwenda gizani kamwe, bali atakuwa na nuru ya uzima.” (Yohana 8:12) Ni shangwe kama nini kushiriki katika utimizo wa ahadi hiyo! Maisha zetu zimetajirika zaidi kwa kuwa sasa hatuhitaji tena kunyong’onyea gizani mwa ulimwengu wa Shetani. Na matazamio yetu ni ya ajabu kweli kweli tunapotazamia hukumu yenye kupendeleka kutoka kwa Hakimu aliyewekwa na Yehova. (2 Timotheo 4:8) Lingekuwa jambo lenye kuhuzunisha kama nini, kama tukiwa tumekwisha ingia kwenye nuru, tungepeperuka gizani tena na kupokea hukumu isiyofaa! Katika makala ifuatayo, tutazungumzia jinsi tunavyoweza kubaki imara katika imani.
Waweza Kueleza?
◻ Hukumu ya Mungu inategemea nini?
◻ Yesu ana daraka gani lenye maana kuhusiana na makusudi ya Mungu?
◻ Tunaonyeshaje kwamba tunajitiisha kwa Yesu akiwa yule aliyetawazwa na Yehova kuwa Mfalme?
◻ Tunaweza kujithibitishaje wenyewe kuwa “watoto wa nuru”?
◻ Katika giza la ulimwengu huu, nuru inang’aaje zaidi ya wakati mwingine wowote?
[Picha katika ukurasa wa 10]
Hatimaye, ainabinadamu yote italazimika kukiri mamlaka ya Yesu
[Picha katika ukurasa wa 12]
Tunaonyesha tunapenda nuru tunapoiangaza kwa wengine