Yehova—“Mtu Mfanya Kiume wa Vita”
VIKOSI vyenye ustadi sana vya jeshi la Misri vilikuwa vimefutwa kabisa kabisa. Kwenye Bahari Nyekundu, miili ya waendeshaji gari-farasi na wapanda-farasi walikuwa wakitupwa huku na huku kwa mawimbi, na vifaa vya kijeshi vikawa takataka iliyojaa ufuoni. Wakiongozwa na Musa, wanaume wa Israeli walichachawa (walirukaruka kwa furaha) katika kuimba wimbo wa ushindi: “Nitamwimbia BWANA [Yehova, NW], kwa maana ametukuka sana; farasi na mpanda farasi amewatupa baharini. BWANA [Yehova, NW] ni mtu wa vita [mtu mfanya kiume wa vita, NW], BWANA [Yehova, NW] ndilo jina lake.”—Kutoka 15:1, 3.
Ushindi wa Yehova kwenye Bahari Nyekundi ulikuwa kwa kweil wonyesho wa uwezo wake mkubwa zaidi vitani. Israeli walikuwa wameondoka Misri katika mpango wa kivita lakini bila uwezo mwingi wa kupigana. Kwa nguzo ya wingu iliyokuwa nguzo ya moto usiku, Yehova aliwaongoza kutoka Ramesesi hadi “kwenye mpaka wa ile jangwa” huko Ethamu. (Kutoka 12:37; 13:18, 20-22) Kisha Yehova akamwambia Musa: “Waambie wana wa Israeli, kwamba warudi na kupiga kambi yao mbele ya Pi-hahirothi, kati ya Migdoli na bahari, kukabili Baal-sefoni . . . Naye Farao atasema katika habari za wana wa Israeli, Wametatanishwa katika nchi, ile jangwa imewazuia wasitoke. . . . naye atafuata nyuma yao.” (Kutoka 14:1-4) Kwa kutii, Israel waligeuka kabisa kurudi wakatembea kwenda Pi-hahirothi. Wapelelezi wa Farao waliripoti ule ulioonekana kuwa mchafuko, na kama ilivyotabiriwa, Farao akakusanya jeshi lake ili wafuatie.—Kutoka 14:5-9.
Mtego—Kwa Israeli au kwa Farao?
Wakiwa wamefungiwa ndani ya milima kila upande, bahari ikiwa mbele yao, na Wamisri nyuma yao, Waisraeli wenye kuogopa walionekana kuwa katika mtego, kwa hilo walimwomba Mungu msaada. Akiwakusanya watu tena, Musa aliwaambia hivi: “Msiogope, simameni tu, mkauone wokovu wa BWANA [Yehova, NW] atakaowafanyia leo; kwa maana hao Wamisri mliowaona leo hamtawaona tena milele. BWANA [Yehova, NW] atawapigania ninyi, nanyi mtanyamaza kimya.” (Kutoka 14:10-14) Kwa ukweli kulingana na ahadi hiyo, “ile nguzo ya wingu ikaondoka hapo mbele yao, ikasimama nyuma yao; ikafika kati ya jeshi la Misri na jeshi la Israeli . . . na hawa hawakukaribia hawa usiku kucha.”—Kutoka 14:15-20.
Kama Yehova alivyoelekeza, Musa aliinua fimbo yake juu ya bahari “akaifanya irudi nyuma” ili Waisraeli waweze kuponyoka. Na muujiza wenye kustaajabisha sana ukatokea! (Kutoka 14:16, 21) Upepo wenye nguvu kutoka mashariki ukaanza kugawanya maji ya Bahari Nyekundu, ukifanya njia ya kupitia iliyokuwa kubwa vya kutosha ili taifa zima—watu milioni tatu walio thabiti—lipite kwa mpango wa kivita. Kwa upande wa kushoto na wa kulia wa safu hiyo ya Waisraeli, maji ‘yaliyogandamana’ yalisimama kama kuta kubwa mbili.—Kutoka 15:8.
Waisraeli, wakisaidiwa na ile nuru kutoka kwa nguzo ya moto, waliponyoka kwa kupitia bahari iliyokaushwa kwa upepo. Kufikia asubuhi, Waisraeli wa mwisho walikuwa wametokea kwenye ufuo ule mwingine. “Na wale Wamisri wakawafuatia, wakaingia ndani kati ya bahari, farasi zote za Farao, na magari yake, na wapanda farasi wake.” Wakimbizi walikuwa wameingia ndani ya mtego!—Kutoka 14:23.
“[Yehova] akalifadhaisha jeshi la Wamisri. Akayaondoa magurudumu ya magari yao, hata yakaenda kwa uzito.” Musa sasa akaunyoosha mkono wake juu ya bahari, “bahari ikarudi kwa nguvu zake.” Kuta za maji zilianguka zikaanza kuwagharikisha Wamisri. Walijaribu kukimbia, wapi, “BWANA [Yehova, NW] akawakukutia mbali hao Wamisri kati ya bahari.” Hakuna hata mmoja aliyeokoka! Kwa kushangilia Waisraeli walimwimbia Yehova wimbo wao wa ushindi.—Kutoka 14:24–15:3; Zaburi 106:11.
Yehova Apigania Yoshua
Yehova alithibitika kuwa “mtu mfanya kiume wa vita” katika vita vinginevyo. Mojawapo ilikuwa vita huko Ai. Shambulio la kwanza juu ya mji huo halikufaulu kwa sababu ya kosa zito la Akani. Jambo hilo liliposahihishwa, Yehova akampa Yoshua maagizo ya kivita.—Yoshua 7:1, 4, 5, 11-26; 8:1, 2.
Usiku Yoshua aliweka oteo nyuma ya mji huo upande wao wa magharibi, kwa kutii maagizo ya Yehova. Kikosi chake kikuu kilisongezwa kaskazini kwenye bonde lililokuwa nje tu ya Ai nacho kilionekana kuwa tayari kwa shambulio la mbele. Wanaume wa Ai walivutwa ndani ya mtego. Wakiwa bado wamesisimushwa na kufanikiwa kwao katika pigano lililotangulia, wakakimbia nje ya mji kwa ujasiri dhidi ya Waisraeli. Wakijifanya kuwa wanakimbia, Waisraeli walirudi nyuma “kwa njia ya nyika,” wakiwavuta adui mbali hata zaidi kutoka Ai.—Yoshua 8:3-17.
Kwa wakati uliofaa kabisa, Yehova akamwambia Yoshua hivi: “Unyoshe huo mkuki ulio nao mkononi mwako, uuelekeze upande wa Ai; kwa kuwa nitautia mkononi mwako.” Kwa ishara hiyo, waoteaji wakashambulia mji, wakitumia upanga na moto. Vikosi vya adui vilivyokuwa nje, walipoona moshi, wakavunjika moyo kabisa. Akiacha kukimbia na kuanza kushambulia, Yoshua akatega adui kati ya vikosi vyake viwili. Huo ulikuwa ushindi wa kibinadamu? Hapana. Waisraeli walishinda kwa sababu, kama vile Yoshua baadaye alivyowaambia: “BWANA [Yehova, NW], Mungu wenu, ndiye aliyewapigania ninyi.”—Yoshua 8:18-27; 23:3.
Pigano Kishoni
Uwezo mkubwa zaidi wa Yehova vitani ulionyeshwa tena kwenye bonde la Kishoni, karibu na Megido. Mfalme wa Kanaani Yabini alikuwa ameonea Israeli kwa miaka 20. Jeshi lake, chini ya amri ya Sisera, lilikuwa na magari-vita 900 pamoja na miundu ya chuma kwenye magurudumu yayo—jeshi lililoonekana kutoshindika katika siku hizo.—Waamuzi 4:1-3.
Hata hivyo, kupitia Debora nabii wa kike, Yehova alimwamuru Mwamuzi Baraka akusanye mashujaa wa vita elfu kumi juu ya mlima Tabori kupigana na vikosi vya Yabini. Sisera akatenda haraka kwa kuona ongezeko hilo la wanajeshi, akienda kasi kutoka Haroshethi hadi bonde lenye mto la Kishoni, kati ya Mlima Tabori na Megido. Alisababu bila shaka kwamba huko kwenye nchi tambarare, askari wa miguu wa Israeli wasio na silaha za kutosha hawangekuwa na uwezo wowote dhidi ya magari-vita yake. Lakini hakutazamia kupigana na Adui wa kimbingu.—Waamuzi 4:4-7, 12, 13.
Yehova akamwagiza Baraka aondoke kutoka sehemu za juu za Tabori zilizo salama na kuingia nchi tambarare ya bonde, akivivuta vikosi vya Sisera vitani. Kisha Yehova akapiga! Furiko la ghafula likafanya uwanda wa vita uwe kinamasi (mahali penye tope), likizuia mwendo wa vikosi vya Sisera. Katika hali ya woga wa ghafula uliotokea, askari wa miguu wa Israeli waliweza kuwashinda kabisa adui zao kwa urahisi. “Jeshi lote la Sisera likaanguka kwa makali ya upanga; hakusalia hata mtu mmoja.” Maji ya Kishoni yaliyofurika yalitopeza magari-vita ya Kikanaani na huenda ikawa yaliondolea mbali baadhi ya maiti.—Waamuzi 4:14-16; 5:20, 21.
Ushindi Dhidi ya Gogu na Umati Wake
Matukio hayo ya kale yaliandaa viishara vya ushindi wa Yehova ulio mkubwa zaidi ambao bado utakuja. Lenye kuonekana kuwa linakaribia sana ni pigano ambalo litatukia “katika miaka ya mwisho.” Kulingana na unabii wa Ezekieli, Gogu, kifananisho cha “mtawala wa ulimwengu huu,” Shetani Ibilisi, atatayarisha jeshi shambulizi la kimataifa. Ataelekeza vikosi vyake kuvamia “milima ya Israeli” ya kifananisho, yaani, hali ya kiroho iliyoinuliwa ya “Israeli wa Mungu” wa Kikristo.—Ezekieli 38:1-9, NW; Yohana 12:31, NW; Wagalatia 6:16.
Ni nini kinachoshawishi Gogu kufanya shambulio hilo la kishindo juu ya watu wa Mungu? Unabii huo unaelekeza kwenye hali yao yenye amani ya kufanikiwa kiroho. Gogu asema hivi: “Nitapanda juu, niiendee nchi yenye vijiji visivyo na maboma; nitawaendea watu wanaostarehe, wanaokaa salama, wote wakikaa pasipo kuta, ambao hawana makomeo wala malango. ili kuteka mateka, na kuwinda mawindo . . . ya watu . . . waliopata ng’ombe na mali.”—Ezekieli 38:10-12.
Kwa ujumla, watu wa Yehova si wenye mali kwa njia ya kimwili. Hata hivyo, wametokeza mali nyingi za kiroho zikiwa tokeo la kazi yao ya kuhubiri ulimwenguni pote. “Mkutano mkubwa . . . wa kila taifa” umekusanywa, sasa ukiwa na idadi ya watu zaidi ya milioni nne. (Ufunuo 7:9, 10) Mali kweli kweli! Shetani—akiwa na hasira nyingi juu ya kufanikiwa huko kwa kiroho—ajaribu kuangamiza kabisa watu wa Mungu.
Lakini kwa kuja juu ya udongo wa Israeli wa kifananisho, kwa kweli, Gogu ashambulia Yehova Mungu mwenyewe. “Ghadhabu yangu itapanda katika mianzi ya pua yangu,” asema Yehova, atakayelipiza kisasi kwa ajili ya watu wake. Majeshi ya Gogu yatafifia katika mchafuko. “Upanga wa kila mtu utakuwa juu ya ndugu yake.” Kisha Yehova aachilia nguvu zake za uharibifu—“mvua ifurikayo, na mvua ya mawe makubwa sana, na moto na kiberiti.” Kama vile katika Bahari Nyekundu, katika Ai, na katika Kishoni, kwa mara nyingine Yehova atapigania watu wake na kutukuza jina lake. “Nitajitukuza, na kujitakasa, na kujidhihirisha, mbele ya macho ya mataifa mengi; nao watajua ya kuwa mimi ndimi BWANA [Yehova, NW].”—Ezekieli 38:18-23.
Rekodi ya kihistoria ya mapigano ya Yehova katika nyakati za kale inatutolea sababu ya kuwa na uhakika kabisa katika ushindi huo wa wakati ujao wakati wa “dhiki kubwa.” (Mathayo 24:21, 22) Yehova akiwa mwenye kudhibiti mambo sikuzote, aweza kushinda adui zake katika kuwaza na aweza kugeuza hali kwa ajili ya wokovu wa watu wake. Kwa kweli, itathibitika kuwa kama Isaya alivyotoa unabii: “BWANA [Yehova, NW] atatokea kama shujaa; ataamsha wivu kama mtu wa vita; atalia, naam, atapiga kelele; atawatenda adui zake mambo makuu.” (Isaya 42:13) Machoni pa Mashahidi wake, milele atakuwa YEHOVA, YULE “MTU MFANYA KIUME WA VITA”!—Kutoka 15:3 NW.
[Ramani katika ukurasa wa 25]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Njia ya Kutoka katika Misri
GOSHENI
Memfisi
Ramesesi
Sukothi
Migdoli
Pi-hahirothi
Ethamu
[Picha katika ukurasa wa 26]
Hapa, katika eneo la Ai, Yehova aliongoza Yoshua na watu Wake kwenye ushindi wa kushangaza
Maji ya Kishoni yaliinuka kwa haraka, yakichangia ushinde wa adui za Yehova
[Hisani]
Picha: Pictorial Archive (Near Eastern History) Est