Kukopesha Wakristo Wenzetu Pesa
PEDRO na Carlos walikuwa rafiki wazuri.a Walikuwa Wakristo wenzi, na familia zao zilifurahia ushirikiano mchangamfu pamoja. Kwa hiyo Carlos alipohitaji pesa kwa ajili ya biashara yake, Pedro hakusita kujitolea kumkopesha pesa hizo. “Kwa kuwa sisi tulikuwa rafiki wazuri,” aeleza Pedro, “Sikuona ubaya wa hilo.”
Hata hivyo, baada ya miezi miwili tu, biashara ya Carlos ilifilisika, na malipo yakakoma. Pedro akapata kujua kwa mshangao wake kwamba Carlos alikuwa ametumia sehemu kubwa ya pesa alizokuwa amekopa kulipa madeni yasiyokuwa ya kibiashara na kulipia mtindo-maisha wenye gharama nyingi. Jambo hilo halikusuluhishwa kwa kumtosheleza Pedro hata baada ya mwaka mmoja wa ziara na barua. Akiwa mwenye kuvunjika moyo, Pedro aliwaendea wenye mamlaka na kumfanya Carlos—rafiki yake aliye ndugu wa Kikristo—afungwe gerezani.b Je! hatua hiyo ilifaa kuchukuliwa? Tutaona.
Kutopatana na kutoelewana juu ya mikopo ya pesa mara nyingi ndivyo visababishi vya kuharibika kwa urafiki miongoni mwa watu kotekote ulimwenguni. Nyakati nyingine huenda hata kikawa kisababishi cha mzozo kati ya Wakristo wenzi. Katika nchi nyingi mikopo ya benki ni migumu kupata, kwa hiyo ni kawaida kwa watu wenye uhitaji wa fedha kuwaendea rafiki na watu wa ukoo. Hata hivyo, jambo la kuhuzunisha lililowapata Pedro na Carlos, linaonyesha kwamba kanuni za Biblia zisipofuatwa kwa uangalifu na mkopi na mkopeshi pia, matatizo mazito yaweza kutokea. Basi, ni njia gani inayofaa kushughulikia maombi ya mkopo kwa Mkristo mwenzetu?
Kuhesabu Gharama za Kukopa
Biblia hupinga kukopa kusiko kwa lazima. “Msiwiwe na mtu cho chote, isipokuwa kupendana,” ahimiza mtume Paulo. (Warumi 13:8) Kwa hiyo kabla ya kuchukua deni, hesabu gharama ya kufanya hivyo. (Linganisha Luka 14:28.) Je! kuna uhitaji kweli kweli kukopa pesa? Je! inahusu riziki yako ili kutunza familia yako? (1 Timotheo 5:8) Au kadiri fulani ya pupa inahusika—labda tamaa ya kuishi kwa ustarehe zaidi?—1 Timotheo 6:9, 10.
Jambo jingine lenye umaana ni kama kuchukua deni kutakushurutisha ufanye kazi kwa muda wa saa nyingi zaidi na labda kuacha mikutano na utumishi wa shambani. Pia, je, waweza kweli kweli kuingiza pesa za mtu mwingine hatarini? Vipi ikiwa biashara au shughuli hiyo inafilisika? Kumbuka kwamba, “asiye haki hukopa wala halipi.”—Zaburi 37:21.
‘Kusema Kweli’ kwa Wakopeshi
Baada ya kufikiria mambo kama hayo, huenda bado ukaona kwamba mkopo wa kibiashara unahitajiwa. Ikiwa hauwezi kupatikana kupitia njia za kilimwengu, si vibaya kwa lazima, kumwendea Mkristo mwenzako, kwa kuwa ni jambo la kawaida kuwageukia rafiki wakati wa uhitaji, kama Yesu alivyoonyesha kwenye Luka 11:5. Hata hivyo ni lazima mtu ajitahidi ‘kusema kweli.’ (Waefeso 4:25) Eleza kwa unyofu mambo yote yanayohusika—kutia na hatari, hata zile zinazoonekana kutoweza kutokea. Na usiudhike ikiwa yule ambaye huenda atakukopesha anakuuliza maswali mengi ya moja kwa moja ili aweze kuwa na uhakika kwamba anaelewa mambo yote kwa usahihi.c
Je! ingekuwa kusema kweli kukopa kwa sababu moja na kisha kutumia pesa hizo kwa sababu nyingine? La. Mwenye benki wa Amerika ya Kilatini aeleza hivi: “Benki yaweza kutangua pesa ulizonazo kwenye benki na kama hukulipa deni yako mara hiyo hiyo, wangepata amri ya mahakama kutwaa mali zako.” Ikiwa pesa zinakopeshwa kwa kusudi la kuongeza faida ya biashara, kuzitumia kwa kusudi jingine kwa kweli kunamwondolea mkopeshi uhakikishio wake kwamba deni hilo laweza kulipwa. Ni kweli, huenda usiogope kisasi cha kisheria unapokopa kutoka kwa Mkristo mwenzako. Hata hivyo, “akopaye ni mtumwa wake akopeshaye,” nawe una wajibu wa kumtendea kwa kufuata haki.—Mithali 22:7.
Kutumia Kanuni ya Kidhahabu Katika Biashara
Yesu alisema hivi: “Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Ni muhimu kama nini kwamba kanuni hiyo ifuatwe sikuzote tunapofanya biashara na mwamini mwenzetu! Kwa mfano, ungeitikiaje kwa tendo ikiwa ndugu angekataa ombi lako la mkopo? Je! ungehisi kwamba amesaliti urafiki wenu? Au, ungeheshimu haki yake ya kukataa ombi lako, ukifahamu kwamba huenda akahitaji pesa zake, au huenda akakadiri hatari kuwa zenye uzito zaidi ya jinsi wewe unavyoziona? Huenda akashuku kwa unyofu uwezo wako wa kushughulikia pesa hizo kwa njia yenye matokeo. Katika hali kama hiyo, yaelekea sana kwamba kukataa kwake kwaweza kuwa jambo linalofaa na lenye upendo pia.—Mithali 27:6.
Rafiki akikubali kukukopesha pesa, ni lazima habari zote ndogo ndogo ziandikwe, kutia ndani kiasi ambacho kimekopwa, jinsi pesa hizo zitakavyotumiwa, ni mali zipi ziwezazo kuwa amana kwa mkopo huo, na jinsi zitakavyolipwa na wakati gani. Katika hali fulani ni jambo la hekima hata kuwa na wakili kufanya au kuangalia mkataba huo na kuuweka katika faili ya wenye mamlaka. Kwa vyovyote vile, mkataba ukiishawekwa sahihi, “maneno yenu yawe Ndiyo, ndiyo; Siyo, siyo.” (Mathayo 5:37) Usikose kuthamini hisani ya rafiki yako kwa kutochukua kwa uzito wajibu wako kwake kama vile ungefanya kwa benki.
Wakopeshi Waangalifu
Vipi ikiwa unajiwa kwa ajili ya mkopo? Mengi yatategemea hali zinazohusika. Kwa mfano, ndugu Mkristo huenda akapatwa na angamio la kifedha, ambalo si kosa lake. Ukiwa na uwezo kufanya hivyo, upendo wa Kikristo utakusukuma ‘umpe mahitaji ya mwili.’—Yakobo 2:15, 16.
Lingekuwa jambo lisilo la upendo kama nini kufaidika na msiba wa ndugu kwa kumtoza faida katika hali kama hiyo! Yesu alisihi hivi: “Wapendeni adui zenu, tendeni mema, na kukopesha [bila kutoza faida, NW] msitumaini kupata malipo.”—Luka 6:35; linganisha Mambo ya Walawi 25:35-38.
Lakini, vipi ikiwa unaombwa tu fedha kwa kuinua biashara iliyofilisika au kupata mkopo? Kwa ujumla, mambo kama hayo yanafaa kushughulikiwa kuwa biashara za kupata faida. Biblia husihi kwa wazi kujihadhari, ikihimiza hivi: “Usiwe mmoja wao wapanao mikono; au walio wadhamini kwa deni za watu.”—Mithali 22:26.
Hali ikiwa hivyo, ni lazima kwanza uamue kama kwa kweli waweza kutoa pesa za kutosha kwa biashara hiyo. Biashara hiyo ikifilisika au mkopi asiweze kulipa deni kwa wakati, je utapatwa na angamio la kifedha? Ikiwa unaweza kukopesha pesa za kutosha na faida itapatikana, wewe una haki pia ya kushiriki katika faida hiyo kwa kutoza faida ya kiasi kwa mkopo wako. (Linganisha Luka 19:22, 23.) Mithali 14:15 huonya hivi: “Mjinga huamini kila neno; bali mwenye busara huangalia sana aendavyo.” Wanabiashara wengine ambao kwa kawaida ni waangalifu wametenda bila hadhari wanapofanya biashara na Wakristo wenzao. Uvutano wa malipo ya faida ya juu umewavuta wengine kwenye biashara za ovyoovyo ambazo katika hizo wamepoteza pesa zao na pia urafiki wao pamoja na Wakristo wenzao.
Kwa kupendeza, wenye benki mara nyingi hufikiria mambo matatu ili kukadiri jinsi mkopo uwezavyo kuwa wenye hatari: (1) tabia ya mtu anayeomba mkopo huo, (2) uwezo wake wa kulipa, na (3) hali zilizopo katika aina yake ya biashara. Je! isingeonyesha “hekima yenye kutumika” kukadiri mambo vivyo hivyo unapofikiria kukopesha mtu pesa zako ambazo umechuma kwa juhudi nyingi?—Mithali 3:21, NW.
Kwa mfano, ndugu mwenye kukuomba pesa hizo ana sifa gani? Je, yeye ajulikana kuwa mwaminifu na mwenye kutegemeka au mwenye kutojali na asiye thabiti? (Linganisha 1 Timotheo 3:7.) Ikiwa anataka kupanua biashara yake, je, ameisimamia kwa mafanikio hadi wakati huu? (Luka 16:10) Ikiwa sivyo, msaada wenye kutumika wa jinsi ya kusimamia pesa zake huenda ukawa wenye kumsaidia kwa muda mrefu kuliko kumkopesha pesa ambazo huenda zikatumiwa vibaya.
Jambo jingine lingekuwa uwezo wa ndugu wa kulipa. Anachuma pesa ngapi? Ana madeni gani? Ni jambo la kiakili tu kwamba akueleze mambo wazi. Hata hivyo, upendo wa Kikristo wapaswa uonyeshwe. Kwa mfano, huenda ukataka mali za ndugu huyo ziwezazo kuuzwa kuwa amana ya mkopo huo. Sheria ya Musa ilikataza kutwaa ama riziki ya mtu ama mali zake za msingi kuwa amana ya mkopo. (Kumbukumbu la Torati 24:6, 10-12) Hivyo, ndugu Mwamerika wa Kusini ambaye ni mfanya biashara asema aweza kukopesha nusu tu ya kiasi cha mali za ndugu ziwezazo kuuzwa. “Nami sioni vifaa vya kazi yake au nyumba yake kuwa mali ziwezazo kuuzwa,” yeye aeleza. “Kwa hakika singependa kumwondosha ndugu yangu nyumbani kwake kwa lazima na kutwaa nyumba yake ili kuzipata pesa zangu.”
Mwisho, wapaswa ufikirie kihalisi hali za biashara za ujumla mahali uishipo. Tunaishi katika “siku za mwisho,” wakati watu ni “wenye kupenda fedha, . . . wasaliti.” (2 Timotheo 3:1-4) Ingawa rafiki na ndugu yako aweza kuwa mnyofu, washiriki wake wa biashara, waajiriwa wake, na wenye kununua kwake huenda wasiwe wanyofu. Akiwa Mkristo, hawezi kutumia rushwa na uwongo—njia za hila ambazo huenda washindani wake wakatumia kwa faida yao. Jambo la kufikiriwa pia ni hasara za “wakati na tukio lisilotazamiwa.” (Mhubiri 9:11, NW) Thamani ya mali yaweza kuanguka kwa ghafula. Ongezeko la bei za bidhaa lenye kuzidi kwa kasi laweza kuharibu biashara au kufuta thamani ya mkopo wako. Wizi, aksidenti, kuharibu vitu ovyo, na majeraha pia ni mambo halisi ya biashara yasiyopendeza. Wapaswa ufikirie mambo hayo yote kabla ya kufanya uamuzi wako.
Kushindwa
Nyakati nyingine, zijapokuwa hadhari zote, Mkristo hawezi tu kulipa mkopo wake. Kanuni ya Kidhahabu yapasa imsukume awasiliane kwa kawaida na mdai wake. Labda kiasi kidogo kidogo kinawezekana kwa muda fulani. Hata hivyo, Mkristo hapaswi kufikiri kwamba malipo hayo madogo madogo yanampa udhuru wa kutofanya dhabihu kweli kweli ili kutimiza wajibu wake mbalimbali. (Zaburi 15:4) Mdeni aliye Mkristo ana wajibu pia wa kuonyesha upendo. Ikiwa anahisi kwamba ameshughulikiwa kwa udanganyifu, aweza kutumia lile shauri kwenye Mathayo 18:15-17.
Kuhusisha mamlaka za kilimwengu, kama Pedro alivyofanya katika habari iliyotajwa mwanzoni, si jambo lenye kupendekezwa mara nyingi. Mtume Paulo asema hivi: “Je! mtu wa kwenu akiwa na daawa juu ya mwenzake athubutu kushitaki mbele ya wasio haki, wala si mbele ya watakatifu? . . . Je! ndivyo, kwamba kwenu hakuna hata mtu mmoja mwenye hekima, awezaye kukata maneno ya ndugu zake? Bali mwashitakiana, ndugu kwa ndugu, tena mbele yao wasioamini. Basi imekuwa upungufu kwenu kabisa kwamba mnashitakiana ninyi kwa ninyi. Maana si afadhali kudhulumiwa? Maana si afadhali kunyang’anywa mali zenu?”—1 Wakorintho 6:1-7.
Huenda zikawako hali—kama zile zinazohusu washiriki wa biashara wasio waamini, watoaji bidhaa wa kilimwengu, au mambo ya bima—zinazoonekana kuhitaji suluhisho katika mahakama ya kilimwengu au na wakala wa kiserikali. Lakini katika hali zilizo nyingi, Mkristo angekubali kupatwa na hasara ya kifedha kuliko kulisababishia kundi aibu ambayo ingeletwa kama angemshtaki ndugu juu ya mkopo usioweza kulipwa.
Katika hali zilizo nyingi matokeo mabaya kama hayo yaweza kuepukwa. Jinsi gani? Kabla ya kukopesha au kukopa kutoka kwa ndugu, fahamu hatari zinazoweza kutokea. Tumia uangalifu na hekima. Zaidi ya yote, “mambo yenu yote,” kutia na mambo ya biashara, “na yatendeke katika upendo.”—1 Wakorintho 16:14.
[Maelezo ya Chini]
a Majina yamebadilishwa.
b Bado katika nchi fulani ufilisi na kutolipa mikopo kwa kawaida hutokeza sana-sana kifungo cha gerezani.
c Wengine wamekopa kiasi kidogo kidogo kutoka kwa wakopeshi wengi. Kila mkopeshi, akiwa hapati mambo ya hakika juu ya hali kamili, huenda akafikiri kwamba mkopi ataweza kulipa kwa urahisi.