Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 4/15 kur. 21-23
  • Ukopeshaji wa Pesa na Upendo wa Kikristo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ukopeshaji wa Pesa na Upendo wa Kikristo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kurudishiwa Pesa kwa Malipo
  • Kukopesha kwa Kutazamia Faida
  • Nafasi za Kuonyesha Upendo
  • Kukopesha na Kukopa Kati ya Marafiki
    Amkeni!—1999
  • Kukopesha Wakristo Wenzetu Pesa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Je, Nimwombe Ndugu Yangu Mkopo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Je, Nikope Pesa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 4/15 kur. 21-23

Ukopeshaji wa Pesa na Upendo wa Kikristo

MUDA fulani uliopita, binti ya mkulima mmoja alikuwa mgonjwa sana. Alihitaji sana matibabu, lakini mkulima huyo alikuwa maskini na hakuweza kupata pesa za kupeleka binti yake kwa daktari. Katika mji ambamo waliishi—kama ilivyo katika miji mingi ya nchi hiyo—kulikuwa na mkopesha-pesa aliyekopesha kwa kiwango cha sita kwa tano, cha faida. Mtu angekopa dola tano halafu mwezi uliofuata alipe sita. Kwa utayari mkopeshaji alimtolea mkulima pesa alizozihitaji sana, lakini bila shaka mwezi ambao ungefuata mkulima huyo angelazimika kuanza kumlipa pesa zake pamoja na faida.

Wewe ungekuwa na maoni gani juu ya mpango huo? Je! ingekuwa sawa Mkristo akopeshe watu pesa ambazo zitalipwa pamoja na faida chini ya hali kama hizo?

Mtume Yohana aliwaambia Wakristo wenzake kwamba haiwapasi ‘kuwazuilia huruma’ ndugu zao wenye uhitaji. (1 Yohana 3:17) Nayo sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli ilisema hivi waziwazi: “Usimfumbie mkono wako nduguyo maskini; lakini mfumbulie mkono wako kwa kweli, umkopeshe kwa kweli yatoshayo haja yake katika ahitajiayo.”—Kumbukumbu la Torati 15:7,8.

Kwa hiyo, yule mkopesha-pesa alifanya vema kutoa pesa za matibabu ya yule msichana mgonjwa. Lakini kuna sehemu nyingine ya sheria ambayo Israeli walipewa. Ilisema hivi: “Ukimkopesha mtu aliye maskini, katika watu wangu walio pamoja nawe; usiwe kwake mfano wa mwenye kumdai [usiwe kwake kamwe kama mtozaji wa faida kubwa sana, NW ] ; wala hutamwandikia faida.” (Kutoka 22:25) Kwa sababu gani Wayahudi hawangeweza kukopeshana kwa njia ya kutozana faida?

Kumbuka kwamba hapo kwanza hesabu kubwa ya Wayahudi walikuwa wakulima, si wafanya biashara. Ikiwa mkulima mwenye kufanya kazi katika shamba aliloachiwa na mababu aliomba mkopo, ilielekea sana kuwa ni kwa sababu alikuwa ameingia katika uhitaji. Sheria ilikuwa na maoni ya kwamba mwenye kuomba mkopo alikuwa “maskini,” wala si mtu asiye maskini. Labda yeye alipatwa na tukio lisilotazamiwa, labda akakosa kupata mazao, au kwa sababu fulani akawa anahitaji pesa za kumsukuma mpaka wakati ule mwingine wa mavuno. Kudai faida chini ya hali kama hizo kungekuwa ni kujifaidi kutokana na taabu ya ndugu yako. Lingekuwa jambo la kutokuonyesha upendo, na Waisraeli waliamriwa hivi: “Umpende jirani yako kama nafsi yako.”—Mambo ya Walawi 19:18.

Ingawa leo Wakristo hawako chini ya sheria hiyo ya kale, bado wana wajibu wa kupendana. Yesu alisema: “Mpende jirani yako kama unavyojipenda wewe mwenyewe! ” (Matayo 22:39, HNWW) Kwa hiyo, Mkristo pia hapaswi kutaka ajipatie faida kutokana na matukio mabaya yaliyopata ndugu yake kwa kudai alipwe kwa faida wakati ndugu yake anapoingia katika uhitaji na kuomba mkopo.

Uhakika ni kwamba, katika nyakati za magumu, Wakristo wanasaidiana katika mambo mengine, hata zaidi ya mikopo tu. Wanatoa zawadi. Katika karne ya kwanza Paulo na Barnaba waliagizwa wachukue upaji uliokuwa umetolewa na Wakristo wa Asia Ndogo wapelekee ndugu zao katika Yudea ambao walikuwa wakitaabishwa na njaa. (Matendo 11:29,30) Vivyo hivyo, leo, wakati wote msiba unapopiga, Wakristo wanapeleka zawadi za kusaidia ndugu zao.

Katika roho iyo hiyo, Yesu alihimiza hivi: “Usijiepushe na yeye ambaye anataka kukuomba bila faida.” (Mathayo 5:42, NW ) Hivyo Mkristo anayaona magumu ya muda ya ndugu yake kuwa nafasi ya kuonyesha upendo. Ana wajibu wa kumsaidia kwa kadiri anavyoweza, hata kufikia kiasi cha kumpa zawadi au mikopo isiyo ya kulipwa kwa faida. Bila shaka, kama yule mkopeshaji aliyetangulia kutajwa angalikuwa akitumia kanuni za Kikristo, hata yeye angalikuwa na maoni hayo pia.

Kurudishiwa Pesa kwa Malipo

Mwenye kukopa ana wajibu wa kulipa. Paulo aliwapa Wakristo onyo hili la upole: “Msiwe na deni kwa mtu ye yote, isipokuwa tu deni la kupendana.” (Waroma 13:8, HNWW) Kwa hiyo, inampasa mwenye kukopa ajue kwamba ana wajibu wa kulipa deni alilo nalo upesi iwezekanavyo. Yeye asifikiri kwamba, kwa sababu mtu yule aliyemkopesha pesa ni tajiri kuliko yeye, hakuna uhitaji wa kumrudishia pesa zake. Vivyo hivyo asitazamie Mkristo mwenzake, kama vile daktari au mwana-sheria, amfanyie utumishi fulani wa kibinafsi bila ya kumrudishia Mkristo huyo malipo kwa utumishi aliomfanyia.

Yesu alisema: “Ukisema, ‘Ndiyo’, basi, iwe ‘Ndiyo’; ukisema, ‘Siyo’, basi, iwe kweli ‘Siyo’.” (Matayo 5:37, HNWW) Ndiyo kusema, Mkristo ana wajibu wa kutimiza ahadi yake. Ikiwa amekopa pesa na kuahidi kuzirudisha, au kama anaingia katika deni kwa njia nyingine, anapaswa afanye yote awezayo alipe deni hilo. Ili kumsaidia afanye hivyo, na kuhakikisha hakuna kutokuelewana kati ya wo wote wanaohusika, ni jambo la hekima kuwa na kumbukumbu la maandishi, yenye kuonyesha kiasi chenyewe, namna kitakavyorudishwa, na hivyo hivyo.

Kukopesha kwa Kutazamia Faida

Je! nyakati zote ni jambo lisilo la upendo kuomba faida? Si lazima iwe hivyo. Inastahili kuangaliwa kwamba, ingawa Wayahudi hawakupaswa kuwaomba Waisraeli wenzao faida, mambo yalikuwa tofauti kwa wageni wasio Waisraeli. “Mgeni waweza kumkopesha kwa riba [faida, NW ] ,” ndivyo sheria ilivyosema. (Kumbukumbu la Torati 23:20) Kwa sababu gani kuwe na tofauti hiyo? Kwa sababu mgeni katika Israeli angeelekea kuwa ni mfanya biashara, na labda mkopo ambao angepewa ungekuwa wa makusudi ya kufanyia biashara. Kwa hiyo, ilifaa kabisa kwamba mwenye kumkopesha pesa ashiriki kupata faida zo zote ambazo zingepatikana, na angeweza kufanya hivyo kwa kuomba alipwe kwa faida.

Yesu hakutokeza katazo lo lote kuhusu kanuni ya kukopesha pesa kwa kutazamia faida. Alionyesha hivyo katika mmoja wa mifano yake. Alieleza habari ya kabaila (tajiri) aliyeenda zake kwa muda na kuachia watumwa wake pesa zake. Aliporudi aliwaita wafanye hesabu, kisha akakuta kwamba walio wengi kati ya watumwa walikuwa wameziweka pesa kwa wawekaji nazo zikapata faida. Watumwa hao walisifiwa. Lakini, mtumwa mmoja hakuwa ameweka pesa alizopewa kwa wawekaji; kwa hiyo hakuwa na faida ya kuonyesha. Hata hakuwa ameziweka katika banki—maana yake kukopesha banki pesa hizo zitumiwe katika biashara—na kujipatia faida. Mtumwa huyo alikemewa na bwana wake. —Luka 19:11-24.

Namna gani leo? Wanawake wawili Wakristo walikuwa na mpango wa kibiashara. Mmoja alikuwa akikopesha mwenzake kila siku kiasi cha pesa kinacholingana na dola 20 hivi (kama shilingi 260). Halafu huyo mwenye kukopeshwa alikuwa akinunua chakula kisha anakiuza sokoni. Kufikia mwisho wa siku huyu wa pili alikuwa na dola kama 25 (shilingi 325 hivi), kisha yeye alimrudishia mwenye kumkopesha dola (kama shilingi 273), halafu dola 4 (shilingi 52) zinakuwa zake mwenyewe. Katika nchi hiyo si ajabu mtu kupata mshahara wa dola 4 kwa siku moja.

Katika sehemu nyingine ya ulimwengu, mwanamume Mkristo alikuwa akiendesha biashara ya jamaa. Kwa sababu hali ya mambo ya kiufundi ilikuwa ikipata maendeleo, alijua kwamba baada ya muda mfupi biashara hiyo ingekwisha. Lakini kulikuwa na nafasi ya kuanzisha shughuli ya upande mwingine. Tatizo la pekee ni kwamba alihitaji pesa zaidi. Kwa hiyo akaomba mkopo kwa Mkristo mwenzake, kisha akaahidi kulipa kila mwezi kiasi fulani cha faida.

Je! wo wote kati ya mipango hiyo ulipingana na roho ya sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli kusema kwamba hawakupaswa kuombana faida? Hata kidogo! Ikiwa mtu hana uhitaji wa haraka, bali anataka kupata mkopo—labda kwa sababu za kuufanyia biashara—hakuna sababu inayofanya mkopeshaji asipaswe kuomba faida. Aombe faida ya kiasi gani? Kati ya mambo mengine, hiyo ingetegemea namna ya mkopo unaotolewa, kiasi ambacho kila anayehusika anakubali, na pia ingetegemea sheria ya nchi. Katika ule mpango wa kwanza ambao umetajwa sasa hivi, huenda faida ya asilimia (%) 5 ikaonekana kuwa kubwa sana. Lakini mwenye kukopeshwa kwa kweli alikuwa akijipatia faida ya asilimia 25 na alifurahi kugawana kiasi fulani cha faida hiyo pamoja na aliyemkopesha.

Bila shaka, matatizo yakitokea baadaye, halionekani kuwa jambo la akili mwenye deni alalamike akisema kwamba kiasi cha faida anayotozwa ni cha juu mno, ikiwa yeye alikubali kulipa kwa kujitolea na kwa hiari yake mwenyewe. Hapa tena, ni jambo la hekima kuweka katika maandishi masharti ambayo wamekubaliana juu ya mkopo, ili kuepuka kutokuelewana baadaye.

Nafasi za Kuonyesha Upendo

Wakati mapatano ya namna hiyo yanapofanyika bila kutokeza matatizo, yanaweza kufaidi kila mmoja. Lakini huu ni ulimwengu wenye mashaka-mashaka, na mara nyingi mambo yanakwenda vingine. Kwa mfano, ingekuwaje kama yule bibi aliyetangulia kutajwa ambaye alikopa dola 20 kila siku angenyang’anywa pesa hizo? Au ingekuwaje kama katika mpango wa kibiashara kati ya wale wanaume wawili biashara yenyewe haikufanikiwa kama walivyotumainia kisha mwenye kukopeshwa akashindwa kulipa faida aliyoahidi?

Biblia haitoi sheria zo zote juu ya namna matatizo hayo yanavyopasa kushughulikiwa, lakini ule wajibu ungali unahusika: “Mpende jirani yako kama unavyojipenda wewe mwenyewe! ” (Matayo 22:39, HNWW) Ikiwa watu wote wawili wanaohusika wanasawazisha hangaiko la kweli kwa faida za kila mmoja pamoja na roho ya hekima iliyo na mafaa, nao waichukue hali hiyo kwa njia inayofaa na kukubali mapendekezo yanayolingana na akili nzuri, basi kwa kawaida mambo yanaweza kumalizwa kwa njia nzuri.

Kwa uhakika, mtume Paulo hakupendekeza kwamba Wakristo wapeleke ndugu zao mahakamani kwa sababu zinazohusu pesa. Yeye alisema: “Basi imekuwa upungufu kwenu kabisa kwamba mnashitakiana ninyi kwa ninyi. Maana si afadhali kudhulumiwa? Maana si afadhali kunyang’anywa mali zenu? ”—1 Wakorintho 6:7.

Mkristo aliyekopeshwa pesa ambaye ‘si mwenye pupa ya pato la udanganyifu’ anapaswa atake kweli kweli kulipa deni alilo nalo. (1 Timotheo 3:8, NW ) Biblia inatuambia kwamba “mwovu anakopa, wala halipi.” (Zaburi 37:21) Hata kama magumu yasiyokuwa yametazamiwa yametokea, bado yeye hataki kutiwa katika jamii moja na ‘waovu.’ Anapaswa atake kuwa mtu ‘asiye na deni kwa mtu ye yote,’ isipokuwa deni la upendo. (Waroma 13:8, HNWW) Kwa hiyo, anapaswa atende kwa njia yenye kuheshimika wala asitafute vinafasi vya kuponyoka kwa kutumia sheria ili asitimize wajibu unaompasa.

Kwa upande mwingine, mkopeshaji anapaswa kuwa na kiasi katika matazamio yake. Anatambua kwamba kutoa mikopo kunatia ndani uwezekano wa kuweza kupata hasara fulani-fulani. Kwa hiyo, hapaswi kumkazakaza mwenye deni kwa njia itakayomfanya ashindwe kuvumilia mikazo yake. Huenda ikawa kwamba mkopeshwa anashindwa kurudisha pesa kwa sababu tu hajazipata. Wakristo wengi walio katika hali za namna hiyo wameonyesha kwamba wao si ‘wenye kupenda fedha’ kwa kurefusha kipindi cha kurudishiwa pesa zao, au kukubali kufikia uamuzi unaofaa kulingana na akili nzuri. (1 Timotheo 3:3) Wengine wamefuta kabisa deni lenyewe.

Kutajwa kwa matatizo yanayoweza kutokea katika ukopaji na ukopeshaji wa pesa kunatokeza ulizo jingine: “Je! kweli ni lazima pesa zikopwe? ” Biblia haikatazi kukopa pesa inapokuwa lazima kufanya hivyo. Lakini mara nyingi si lazima. Nyakati nyingi “tamaa ya macho” inataka vitu ambavyo mfuko hauna uwezo wa kuvipata, na watu wanakopa pesa wanunue vitu vya raha tu ambavyo hawavihitaji kweli kweli. (1 Yohana 2:16) Mwishowe inakuwa lazima pesa zenyewe zilipwe. Kwa hiyo Biblia inaonya hivi ikitoboa mambo wazi: “Akopaye ni mtumwa wake akopeshaye.”—Mithali 22:7.

Lakini, wakati kukopesha na kukopa kunapokuwa lazima kati ya Wakristo, mara nyingi jambo hilo linatokeza nafasi ya kuonyesha sifa za Kikristo. Kwa mfano, tamaa ya unyofu ya kutaka kutimiza wajibu ambao mtu anao, pia hangaiko lenye kina kirefu la kutaka kuona wengine wakiwa na hali njema na kuepuka kupenda fedha, ni mambo yatakayotusaidia tuhakikishe kwamba ukopeshaji wa pesa unafanywa kwa upendo wa Kikristo. Kwa njia hiyo amri hii ya Kibiblia itafuatwa kwa utii: “Mambo yenu yote na yatendeke katika upendo.”—1 Wakorintho 16:14.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki