Kukusanyika Pamoja na Wapendao Uhuru wa Kupewa na Mungu
MASHAHIDI WA YEHOVA ni watu wa kipekee katika njia nyingi sana. Wao pekee ndio husema “lugha iliyo safi.” (Sefania 3:9) Ni wao tu walio na umoja, wakiwa na alama ya kutofautisha ya upendo iliyoelezwa na Yesu Kristo. (Yohana 13:35) Na ni wao pekee wanaoonea shangwe uhuru ambao Yesu Kristo alisema ungeletwa na kweli, kama irekodiwavyo kwenye Yohana 8:32: “Mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.”
Maneno hayo ambayo Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, alielekezea wanafunzi wake, yamethibitika kuwa ya kweli. Na yanathaminiwa sasa zaidi ya wakati mwingine wowote na Mashahidi wa Yehova wale wote waliohudhuria “Wapendao Uhuru” Mikusanyiko ya Wilaya. Programu ya mkusanyiko imekazia kwao sehemu mbalimbali za uhuru wao, jinsi wapasavyo kuutumia, daraka la kutoa hesabu linaloandamana na uhuru wao, na jinsi walivyobarikiwa kuwa watu huru.
Mikusanyiko hiyo ya wakati unaofaa na yenye kutumika ilianza katika Kizio cha Kaskazini Juni 7, 1991, katika Los Angeles, California, U.S.A. Programu ilianza saa 4:20 asubuhi kwa utoaji wa muziki, uliofuatwa na wimbo na sala. Hotuba ya kufungua ilikuwa utoaji wenye nguvu na wa moja kwa moja wenye msingi wa Yakobo 1:25. Kulingana na The Jerusalem Bible, mstari huo husomeka hivi: “Mtu anayeangalia kwa makini sheria kamilifu ya uhuru na kufanya hilo kuwa zoea lake—si kusikiliza na kisha kusahau, bali kuizoea kwa bidii—atakuwa na furaha katika kila kitu anachofanya.” Sawa na vile tunavyojitazama kwenye kioo ili kuona mahali tunapohitaji kufanya maendeleo katika sura yetu, ndivyo tunavyohitaji kuendelea kutazama katika sheria kamilifu ya Mungu iliyo ya uhuru ili tujifunze ni wapi tunapohitaji kufanya mabadiliko katika utu wetu. Na twapaswa kuendelea kukichungulia kioo hicho.
Ndipo ikaja hotuba ya mwenyekiti, “Karibuni, Enyi Nyote Mpendao Uhuru.” Mashahidi wa Yehova hupenda uhuru, na wanataka wabaki wakiwa huru. Msemaji alinukuu wenye mamlaka wa kisheria walioonyesha kwamba hakuwezi kuwa uhuru wowote bila sheria. Naam, Wakristo hawako huru kufanya vile wapendavyo bali wako huru kufanya mapenzi ya Yehova. Wanataka kuutumia uhuru wao kikamili wala si kuutumia vibaya. Mashahidi wa Yehova wameonea shangwe uhuru zaidi hasa tangu 1919. Msemaji aliufuatisha mkazo juu ya uhuru katika vichwa vya mkusanyiko na vichapo vya Kikristo. Wakusanyikaji wote wangejifunza zaidi juu ya uhuru wa kupewa na Mungu na jinsi ya kuutumia.
Maelezo hayo ya wakati unaofaa yalifuatwa na mahoji ya wapendao uhuru walioshangilia kuwako kwenye mkusanyiko. Mikusanyiko ya jinsi hiyo ni nyakati za kushangilia, sawa na vile sikukuu tatu za Israeli za kila mwaka zilivyothibitika kuwa zenye shangwe nyingi. Mahoji kadhaa yalithibitisha kwamba mikusanyiko ni nyakati za shangwe zenye kujenga kiroho.
Kisha ikaja ile hotuba ya msingi, “Kusudi na Utumizi wa Uhuru Wetu Tuliopewa na Mungu.” Kutokana na hutoba hiyo wakusanyikaji walijifunza kwamba Yehova pekee ndiye aliye na uhuru kamili kwa sababu yeye ndiye Mamlaka ya Juu Zaidi na ndiye mweza yote. Hata hivyo, kwa ajili ya jina lake na kwa manufaa ya viumbe vyake, yeye huzuia uhuru wake nyakati nyingine kwa kutokuwa mwepesi wa hasira na kwa kuzoea kujidhibiti. Viumbe vyake wote wenye akili wana uhuru wa kadiri, kwani wako chini ya Yehova na wanazuiwa na sheria zake za kimwili na za kiadili. Yehova amewapa uhuru ili wafurahie lakini hasa ili waweza kumletea heshima na shangwe kwa kumwabudu. Kwa sababu ya kutumia uhuru wao vizuri, Mashahidi wa Yehova wamepata sifa nzuri ulimwenguni pote kwa ajili ya mwenendo mzuri na bidii katika huduma yao.
Ijumaa Alasiri
“Unashughulika na Kazi Zisizo na Uhai au na Utumishi wa Yehova?” ndicho kilichokuwa kichwa chenye kuamsha fikira cha hotuba iliyofungua pindi ya Ijumaa alasiri. Kazi zisizo na uhai hutia ndani si zile za mnofu tu bali pia nyinginezo zisizo hai kiroho, za ubatili na zisizofaa—kama vile mipango ya kuchuma pesa nyingi. Kuhusu hilo, ni muhimu tujichunguze wenyewe kwa unyofu ili tuone ikiwa tunaweka Ufalme kwanza maishani.
Ikiwa na lengo lile lile ilikuwa hotuba iliyofuata, “Kutekeleza Utume Wetu Tukiwa Wahudumu wa Mungu.” Msemaji alionyesha kwamba Wakristo hawapaswi wajiridhishe wenyewe na utumishi usiotoka moyoni au na kufikia saa zilizowekwa. Wanapaswa watake kuwa wenye matokeo katika sehemu zote za huduma ya Kikristo. Mambo hayo yalikazwa zaidi akilini mwa wasikilizaji kupitia onyesho na mahoji. Wote walihimizwa watimize huduma yao kikamili kadiri wawezavyo.
Katika hotuba “Watu Huru Lakini Wanaotakwa Watoe Hesabu,” msemaji alikazia kwamba ingawa watu wa Yehova huthamini sana uhuru ambao kweli imewaletea, wanapaswa wakumbuke kwamba daraka la kutoa hesabu linaandamana nao. Wanapaswa watumie uhuru wao, si kuwa udhuru wa mwenendo mbaya, bali kwa sifa ya Yehova. Wakiwa Wakristo, wanatakwa watoe hesabu kwa “mamlaka iliyo kuu” na wanapaswa pia washirikiane na wazee wa kundi. (Warumi 13:1) Isitoshe, wanatakwa watoe hesabu kwa ajili ya mavazi, mapambo, na mwenendo wao. Hawapaswi kamwe kusahau kwamba “kila mtu miongoni mwetu atatoa habari zake mwenyewe [hesabu, NW] mbele za Mungu.”—Warumi 14:12; 1 Petro 2:16.
Kisha yakafuata mazungumzo ya uhitaji wa Wakristo wote kuwa “Wasio na Hofu Mwisho wa Ulimwengu Huu Ukaribiapo.” Ingawa ainabinadamu ina hofu juu ya lile litakaloletwa na wakati ujao, Wakristo wanahitaji kuwa bila hofu ili watekeleze huduma yao. Kuwa bila hofu ni tokeo la kumtumaini Yehova, kwani kadiri Mkristo azidivyo kuhofu kutompendeza Mungu, ndivyo atakavyo hofu viumbe kwa kadiri ndogo zaidi. Kukariri kwa akili maandiko yenye kufariji kwaweza kuimarisha mtu kutokuwa na hofu. Ili kuwa wenye nguvu kiroho na wasio na hofu, watumishi wa Mungu wanahitaji pia watumie vizuri nafasi zote za kushirikiana na waamini wenzao. Kila mtu ahitaji pia akumbuke daraka ambalo sala hutimiza katika kuwa bila hofu. Kwa kubaki wasio na hofu, Wakristo watadumisha uhusiano mwema pamoja na Yehova Mungu.
Programu ya siku ya kwanza ilimalizia kwa drama yenye kuagiza sana Tumewekwa Huru ili Kuendeleza Ibada ya Kweli. Ilionyesha jinsi familia ya ki-siku-hizi ilivyojifunza somo kutokana na Ezra na kikundi chake cha 7,000, waliojinyima ili warudi Yerusalemu. Liliwezesha kila mmoja achunguze mambo apaswayo kupa umaana wa kwanza na kuona jinsi angeweza kuongeza mapendeleo yake ya utumishi. Drama hiyo ilikuwa na masomo kwa wazee na vijana pia.
Jumamosi Asubuhi
Baada ya programu ya muziki, wimbo, sala, na mazungumzo ya andiko la Biblia la kila siku, jambo kuu la programu ya Jumamosi asubuhi lilikuwa mfululizo wenye kichwa “Uhuru Wenye Daraka Katika Kikundi cha Familia.” Katika sehemu ya kwanza, “Jinsi Akina Baba Wanavyoweza Kumwiga Yehova,” akina baba walishauriwa juu ya njia mbalimbali ambazo katika hizo wanaweza kumwiga Baba yetu wa kimbingu. Timotheo ya Kwanza 5:8 hutaka kwamba waandae si kimwili tu bali kiroho pia. Wanamwiga Yehova kwa kuwa walimu wema wa familia yao na kwa kutoa nidhamu yenye upendo kama inavyohitajiwa. Mambo hayo yalitolewa kielezi kwa mahoji kadhaa.
“Fungu la Mke la Kuunga Mkono” ilikuwa sehemu iliyofuata ya mfululizo huo. Ilianza kwa kukazia kwamba mke ana cheo chenye fahari katika familia ya Kikristo, kile cha kuwa muungaji mkono. Hilo lataka nini kwake? Kwamba ajitiishe mwenyewe inavyofaa, bila kusonga mumewe kamwe afanye lile ambalo yeye pekee atakalo. Anahitaji kutunza vyema wajibu wake mbalimbali kwa mume na watoto wake, naye aweza kupata uradhi wa kweli kwa kuweka nyumba yake ikiwa safi na nadhifu. Na akiwa mhudumu Mkristo, huenda akawa na nafasi nyingi za kushiriki katika utumishi wa shambani. Hoji moja pamoja na familia lilikazia hekima ya shauri la Kimaandiko la jinsi hiyo.
Vijana walielekezewa fikira katika sehemu “Watoto ambao Husikiliza na Kujifunza.” Kwa kuzoeza watoto wao kusikiliza na kujifunza, wazazi humletea Yehova heshima na huonyesha upendo kwa ndugu zao wa kiroho na kwa wazao wao wenyewe. Kifungo imara kitakuwako kati ya wazazi na watoto ikiwa watatumia wakati unaofaa pamoja. Ni lazima wazazi wawe tayari kujibu maswali ya watoto wao na kuchochea kiu yao ya kupata maarifa. Tena, mahoji yalionyesha jinsi hilo laweza kufanywa.
Ndipo likaja lile shauri jema “Endelea Kujiweka Huru Umtumikie Yehova.” Hilo lafanywaje? Kwa kuendelea kujiweka huru kutoka kufuatia kazi-maisha za kilimwengu, vipendezi vyenye kutumia wakati mwingi, na miradi ya kufuatia vitu vya kimwili. Yesu na mtume Paulo waliweka mifano myema kwa kuwa wenye kujidhabihu. Watu wa Yehova wanahitaji kudumisha jicho sahili, lenye kukaziwa juu ya masilahi ya Ufalme. Kwa habari ya kupata vitu vya kimwili, ni jambo la hekima zaidi kuweka pesa akibani sasa na kununua baadaye kuliko kununua sasa na kulipa baadaye. Ni lazima vijana wajilinde dhidi ya kuwazia-wazia juu ya raha za ngono na kazi-maisha za kilimwengu. Hoji moja ya painia asiyeoa lilionyesha mibaraka yanayotokea wakati mtu anapoendelea kujiweka huru kumtumikia Yehova.
Programu ya Jumamosi asubuhi ilimalizia kwa hotuba “Ingia Katika Uhuru kwa Wakfu na Ubatizo.” Wataka kubatizwa walikumbushwa kwamba ingawa uumbaji ulikuwa umeingizwa katika utumwa kwa uasi wa Adamu, Mkombozi mwenye nguvu, Yesu Kristo, alifungua njia kwenye uhuru kwa dhabihu yake. Msemaji alionyesha lile lililohusika katika kuwekwa huru ili kufanya mapenzi ya Mungu na akakazia wajibu mbalimbali na mibaraka ambayo ingekuwa ya wale wanaobatizwa.
Jumamosi Alasiri
Programu ya Jumamosi alasiri ilianza kwa swali lenye kuchunguza yaliyo moyoni “Wewe Watafuta Faida ya Nani?” Ulimwengu huangaza roho ya kujitafutia faida iliyo ya Ibilisi. Hata hivyo, Wakristo wapaswa kuiga roho ya kujidhabihu ya Yesu Kristo. Yeye aliweka mfano mwema kama nini! Aliacha utukufu wa kimbingu na kisha akadhabihu uhai wake wa kibinadamu kwa faida yetu. Hali ngumu zinazoonyesha ni faida ya nani tunayotafuta hutokea kunapokuwako kutoelewana kati ya Wakristo katika mambo ya kibiashara au ya kifedha, kunapokuwako migongano ya utu, na kadhalika. Mambo kama hayo hujaribu upendo wa Kikristo. Lakini kwa kutafuta faida ya wengine, mtu kwa hakika atatambua baraka kubwa zaidi ya kutoa, naye atapata kibali cha Yehova.
Kisha kikafuata kichwa chenye kuhusiana kwa ukaribu na kichwa kilichotangulia “Kutambua na Kushinda Udhaifu wa Kiroho.” Hotuba hiyo ilikazia uhitaji wa kutambulisha ishara za udhaifu wa kiroho na kisha kutenda kwa uamuzi thabiti katika pigano la kushinda Shetani na mitego yake. Ni lazima watumishi wa Yehova wasitawishe upendo mwingi kwa Yehova na kulichukia lililo baya. Hilo lataka kwamba wapate kumjua Yehova kupitia funzo la Biblia la kawaida la kibinafsi na la familia linalofaa. Ni lazima waepuke namna zote za vitumbuizo vinavyotukuza jeuri na ukosefu wa maadili katika ngono. (Waefeso 5:3-5) Sala na hudhurio la kawaida mikutanoni ni za msingi pia ili kufanikiwa katika kushinda udhaifu wa kiroho.
Labda yenye kuzungumziwa sana faraghani zaidi ya hotuba nyingine yoyote iliyotolewa kwenye mkusanyiko ni ile yenye kichwa “Je! Ndoa Ndiyo Ufunguo wa Kupata Furaha?” Vijana wengi hufikiria hivyo! Lakini msemaji alielewesha wazi kwamba kuna viumbe wa roho wasiohesabika wanaofurahi ingawa hawajaoa, sawa na Wakristo wengi waliojiweka wakfu ambao ni wenye furaha sana ingawa hawajafungwa nira katika ndoa. Isitoshe, wenzi wengi wa ndoa hawana furaha, kama ionyeshwavyo na kiwango cha juu cha talaka. Mtu anahitaji tu afikirie mibaraka mingi ambayo Wakristo wote waliojiweka wakfu huonea shangwe, ili atambue kwamba ingawa ndoa yaweza kuwa baraka, sio ufunguo wa kupata furaha.
Ndipo ukaja mfululizo wenye kichwa “Uhuru wa Kikristo Katika Siku Zetu.” Msemaji wa kwanza alizungumzia “Pande za Uhuru Wetu wa Kikristo.” Hizo hutia ndani uhuru kutoka katika mafundisho bandia ya kidini kama vile Utatu, kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu, na mateso ya milele. Halafu kuna uhuru kutoka katika utumwa wa dhambi. Ingawa Wakristo si wakamilifu, wako huru na mazoea mabaya kama vile uvutaji sigareti, kucheza kamari, ulevi, na kufanya ngono ovyoovyo. Kuna uhuru pia kutoka katika hali ya kukosa tumaini, kwani wana tumaini jangavu la Paradiso linalowasukuma waambie wengine juu yalo.
Msemaji aliyefuata aliuliza swali “Je! Wewe Binafsi Unathamini Sana Uhuru Huo?” Kuthamini sana humaanisha kuona kitu kuwa chenye thamani nyingi, kukitunza kwa uangalifu. Ili kufanya hivyo, ni lazima mtumishi wa Mungu ajilinde dhidi ya kushawishwa aruke mipaka ya uhuru wa Kikristo. Uhuru wa ulimwengu ni uwongo wenye kudanganya, kwani matokeo yake ni utumwa wa dhambi na uharibifu.
Msemaji wa mwisho katika mfululizo huo alisema juu ya habari “Wapendao Uhuru Simameni Imara.” Ili kufanya hivyo, ni lazima Wakristo washikamane kwa ukaribu na wazazi wao wa kimbingu, Yehova na tengenezo lake lililo kama mke. Watu wa Yehova hawawezi kujiruhusu wakengeushwe na propaganda za uasi-imani; ni lazima wakatae wale wanaokuja wakiwa na makusudio ya ukosefu wa adili. Ili kusimama imara katika uhuru wa kimungu, ni lazima Wakristo ‘waishi kwa roho.’—Wagalatia 5:25.
Hotuba ya mwisho ya siku hiyo ilikuwa yenye kufurahisha kweli kweli. Ilikuwa na kichwa “Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi.” Yesu Kristo ndiye aliyekuwa mtu mkuu zaidi, kwani aliathiri uhai wa aina ya kibinadamu kwa nguvu zaidi ya majeshi, manowari, mabunge, na wafalme wote wakiwa pamoja. Yeye alikuwa Mwana wa Mungu, aliyekuwa mbinguni kabla ya kuja duniani. Yesu alimwiga Baba yake wa kimbingu vizuri sana katika yale aliyosema na kufundisha na jinsi alivyoishi hivi kwamba angeweza kusema: “Aliyeniona mimi amemwona Baba.” (Yohana 14:9) Yesu alionyesha vizuri kama nini kwamba “Mungu ni upendo”! (1 Yohana 4:8) Baada ya kuzungumzia sana sifa za Yesu, msemaji alionyesha kwamba mfululizo wa makala zenye kichwa “Maisha na Huduma ya Yesu” zilikuwa zimetangazwa katika Mnara wa Mlinzi tangu Agosti 1985. Kwa kuitikia maombi mengi, Sosaiti sasa ilikuwa ikitoa kitabu kipya Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi. Kina sura 133 nacho kimechapishwa kwa rangi kamili. Habari katika mfululizo huo imehaririwa, na yote imeunganishwa pamoja katika kurasa 448 za kitabu hicho. Kwa kweli, siku hiyo ya mkusanyiko iliisha kukiwa na shangwe nyingi mno!
Jumapili Asubuhi
Mapema katika pindi ya Jumapili asubuhi ukaja mfululizo “Kutumika Tukiwa Wavuvi wa Watu.” Hotuba “Kuvua Samaki—Halisi na wa Ufananisho” iliwekea msingi hotuba zilizofuata. Msemaji alionyesha kwamba baada ya Yesu kusababisha uvuvi samaki wa kimuujiza, aliwaalika wavuvi wahusika wawe wavuvi wa watu. Kwa wakati fulani, Yesu aliwazoeza wanafunzi wake kuwa wavuvi wa watu, na kuanzia Pentekoste 33 W.K., walikuwa na mafanikio katika kuwasaidia wanaume na wanawake wengi sana kuwa wanafunzi.
Msemaji aliyefuata alishughulikia mfano wa juya (wavu) unaorekodiwa kwenye Mathayo 13:47-50. Alionyesha kwamba wavu wa ufananisho ulitia ndani Wakristo wapakwa-mafuta na Jumuiya ya Wakristo pia, wale wa pili kwa sababu ya kazi yao ya kutafsiri, kutangaza, na kugawanya Biblia, ingawa juhudi zao zilikusanya samaki wengi sana wasiofaa. Hasa tangu 1919 ndipo kumekuwako kazi ya kutawanya, samaki wasiofaa wakitupwa, hali wale wanaofaa wakikusanywa katika makundi yenye mfano wa vyombo ambavyo vimesaidia kulinda na kuhifadhi Wakristo wa kweli kwa ajili ya utumishi wa kimungu.
Hotuba ya tatu, “Kuvua Watu Katika Maji ya Tufe Lote,” ilikazia wajibu wa Wakristo wote waliojiweka wakfu wa kushiriki katika uvuvi wa ulimwenguni pote. Sasa zaidi ya 4,000,000 wanashiriki katika kazi hiyo katika zaidi ya nchi 200, na katika miaka ya hivi karibuni wengi zaidi ya 230,000 wamekuwa wakibatizwa kila mwaka. Watu wote wa Yehova walisihiwa wafanyie maendeleo stadi zao za kuvua, na “wavuvi” kadhaa wenye kufanikiwa zaidi walihojiwa.
Katika hotuba iliyofuata, yenye kichwa “Kuendelea Kukesha Katika ‘Wakati wa Mwisho,’” msemaji alitaja misaada saba mmoja baada ya mwingine ya kusaidia watu wa Mungu wakeshe: kupigana vita na makengeusho, kusali kwa bidii, kutangaza onyo juu ya mwisho wa mfumo huu wa mambo, kujichunguza, kutafakari juu ya unabii mbalimbali uliotimizwa, na kuzingatia akilini kwamba wokovu wao umekaribia zaidi ya wakati walipokuwa waamini.
Programu ya asubuhi ilimalizia kwa mazungumzo juu ya “Nani Atakayeponyoka ule ‘Wakati wa Taabu’?” Msemaji alionyesha jinsi unabii wa Yoeli ulivyokuwa na utimizo wa kadiri fulani katika nyakati za kimitume, jinsi ulivyokuwa ukitimizwa zaidi sasa, na jinsi utakavyokuwa na utimizo kamili katika wakati ujao ulio karibu.
Jumapili Alasiri
Programu ya alasiri ilianza na hotuba ya watu wote, “Kukaribisha kwa Shangwe Ulimwengu Mpya wa Mungu wa Uhuru!” iliyoendeleza kichwa cha mkusanyiko cha uhuru. Ilionyeshwa kwamba Neno la Mungu hutabiri ulimwengu mpya ambapo kutakuwako uhuru kutoka katika uonevu unaosababishwa na sehemu za dini bandia, siasa, uchumi, na za rangi. Kutakuwako pia uhuru kutoka katika dhambi na kifo. Afya kamilifu itarudishwa ili watu waweze kuishi milele kwa furaha katika dunia-paradiso. Hivyo, wapendao uadilifu wana sababu zote za kumsifu Mtengenezaji wa ulimwengu mpya kwa kupaza sauti hivi: “Asante, Yehova, kwa ajili ya uhuru wa kweli hatimaye!”
Hotuba ya watu wote ilifuatwa na jambo jipya katika mikusanyiko ya wilaya—mazungumzo ya somo la juma la Mnara wa Mlinzi. Kisha mkusanyiko ukafikia mwisho kwa hotuba yenye kusisimua na himizo “Wapendao Uhuru, Endeleeni Kusonga Mbele.” Msemaji alishughulika kwa ufupi na mambo makuu ya kichwa cha mkusanyiko cha uhuru. Alikazia jinsi watu wa Yehova walivyo na furaha kwa sababu ya uhuru wao, akataja njia moja moja ambazo katika hizo Wakristo wamefanya maendeleo, na akawasihi waendelee kusonga mbele kwa umoja ili wavune mibaraka zaidi. Alimalizia kwa maneno haya: “Tufanyapo hivyo, Yehova na aendelee kubariki kila mmoja ili tuendelee kusonga mbele tukiwa wapendao uhuru.”
“Viumbe vyote pia vilitiishwa chini ya ubatili; si kwa hiari yake, ila kwa sababu yake yeye aliyevitiisha katika tumaini; kwa kuwa viumbe vyenyewe navyo vitawekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata viingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.” (Warumi 8:20, 21)
[Picha katika ukurasa wa 25]
Mhudhuriaji mchanga kwenye mkusanyiko katika Prague, Chekoslovakia
[Picha katika ukurasa wa 26]
1.Wataka kubatizwa wakielekea kwenye mahali pa ubatizo katika Prague, Chekoslovakia
2. Kubatizwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova katika Tallin, Estonia
3. Vichapo vipya vililetea shangwe wakusanyikaji katika Usolye-Sibirskoye, Siberia
4. Kutoa “New World Translation of the Holy Scriptures katika lugha za Chek na Slovak kwenye mkusanyiko katika Prague